Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wasaidieni Kondoo Waliopotea

Wasaidieni Kondoo Waliopotea

Wasaidieni Kondoo Waliopotea

“Shangilieni pamoja nami, kwa sababu nimempata kondoo wangu aliyekuwa amepotea.”—LUKA 15:6.

1. Yesu ameonyesha jinsi gani kwamba yeye ni mchungaji mwenye upendo?

YESU KRISTO, Mwana mzaliwa-pekee wa Yehova, anaitwa “mchungaji mkuu wa kondoo.” (Ebr. 13:20) Maandiko yalitabiri kuja kwake na yalionyesha kwamba alikuwa Mchungaji wa pekee aliyejitahidi kuwatafuta “kondoo waliopotea” wa Israeli. (Mt. 2:1-6; 15:24) Zaidi ya hayo, kama vile mchungaji halisi anavyoweza kuwa tayari kufa ili kulinda kondoo wake, Yesu alikufa akiwa dhabihu ya fidia kwa ajili ya watu walio kama kondoo ambao wangefaidika kupitia dhabihu yake.—Yoh. 10:11, 15; 1 Yoh. 2:1, 2.

2. Ni mambo gani ambayo huenda yamewafanya Wakristo fulani kuwa wasiotenda?

2 Inasikitisha kwamba watu fulani ambao walionekana kuwa wanathamini dhabihu ya Yesu na wakajiweka wakfu kwa Mungu hawashirikiani tena na kutaniko la Kikristo. Pengine kuvunjika moyo, matatizo ya afya, au mambo mengine yalipunguza bidii yao na hivyo wakawa wasiotenda. Hata hivyo, ni katika kundi la Mungu tu ndipo wanapoweza kupata amani na furaha iliyotajwa na Daudi katika Zaburi ya 23. Kwa mfano, Daudi aliimba hivi: “Yehova ni Mchungaji wangu. Sitakosa chochote.” (Zab. 23:1) Wale walio katika kundi la Mungu hawakosi maandalizi yoyote ya kiroho, lakini kondoo waliopotea wanayakosa. Ni nani anayeweza kuwasaidia? Msaada unaweza kutolewa jinsi gani? Kwa kweli, tunaweza kufanya nini ili kuwasaidia warudi katika kundi?

Ni Nani Anayeweza Kusaidia?

3. Yesu alionyesha jinsi gani kile ambacho kinahitajiwa ili kuokoa kondoo wa malisho ya Mungu?

3 Jitihada nyingi zinahitajiwa ili kuokoa kondoo waliopotea wa malisho ya Mungu. (Zab. 100:3) Yesu alitoa mfano kuhusu jambo hilo aliposema hivi: “Mtu akiwa na kondoo 100 na mmoja apotee, je, hatawaacha wale 99 milimani na kuondoka kwenda kumtafuta yule anayepotea? Naye akimpata, hakika ninawaambia ninyi, yeye humshangilia huyo zaidi kuliko wale 99 ambao hawakupotea. Vivyo hivyo Baba yangu aliye mbinguni hatamani kwamba mmoja wa wadogo hawa aangamie.” (Mt. 18:12-14) Ni nani anayeweza kuwasaidia watu walio kama kondoo waliopotea?

4, 5. Wazee wanapaswa kuwa na mtazamo gani kuhusu kundi la Mungu?

4 Ili wazee Wakristo wawasaidie kondoo waliopotea, ni lazima wakumbuke kwamba kundi la Mungu ni kutaniko la watu waliojiweka wakfu kwa Yehova—ndiyo, ni ‘kundi lenye thamani la malisho ya Mungu.’ (Zab. 79:13) Kondoo hao wapendwa wanahitaji kutunzwa kwa upendo, hivyo ni lazima wachungaji wenye upendo wamjali kila kondoo. Kufanya ziara za uchungaji zenye urafiki kunaweza kuwasaidia sana kondoo hao. Mchungaji anapowatia moyo kwa upendo, hilo linaweza kuwajenga kiroho na kuchochea tamaa yao ya kurudi katika kundi.—1 Kor. 8:1.

5 Wachungaji wa kundi la Mungu wana daraka la kuwatafuta kondoo waliopotea na kujitahidi kuwasaidia. Mtume Paulo aliwakumbusha wazee Wakristo wa jiji la kale la Efeso kuhusu madaraka yao ya uchungaji aliposema hivi: “Jiangalieni ninyi wenyewe na kundi lote, ambalo roho takatifu imewaweka ninyi rasmi kuwa waangalizi kati yake, kulichunga kutaniko la Mungu, ambalo alilinunua kwa damu ya Mwana wake mwenyewe.” (Mdo. 20:28) Vivyo hivyo, mtume Petro aliwapa wanaume wazee watiwa-mafuta himizo hili: “Lichungeni kundi la Mungu lililo chini ya uangalizi wenu, si kwa kulazimishwa, bali kwa kupenda; wala si kwa kupenda pato lisilo la haki, bali kwa hamu; wala si kama kwa kupiga ubwana juu ya wale ambao ni urithi wa Mungu, bali kuwa vielelezo kwa kundi.”—1 Pet. 5:1-3.

6. Kwa nini kondoo wa Mungu wanahitaji kutunzwa na wachungaji hasa leo?

6 Wachungaji Wakristo wanahitaji kumwiga yule “mchungaji mwema,” Yesu. (Yoh. 10:11) Alihangaikia sana kondoo wa Mungu na akakazia umuhimu wa kuwatunza alipomwambia Simoni Petro ‘achunge kondoo Wake wadogo.’ (Soma Yohana 21:15-17.) Kondoo wanahitaji kutunzwa hasa leo, kwa kuwa Ibilisi amezidisha jitihada zake za kuvunja utimilifu wa wale waliojiweka wakfu kwa Mungu. Shetani anatumia udhaifu wa kimwili na anautumia pia ulimwengu ili kujaribu kuwashawishi kondoo wa Yehova watumbukie katika dhambi. (1 Yoh. 2:15-17; 5:19) Kwa kuwa wale wasiotenda wanaweza kushambuliwa kwa urahisi, wanahitaji kusaidiwa ili wafuate shauri la ‘kutembea kwa roho.’ (Gal. 5:16-21, 25) Ili tuwasaidie kondoo hao tunahitaji kumtegemea Mungu kupitia sala, tunahitaji mwongozo wa roho yake, na kutumia Neno lake kwa ustadi.—Met. 3:5, 6; Luka 11:13; Ebr. 4:12.

7. Ni jambo la maana kadiri gani kwa wazee kuwachunga kondoo walio chini ya utunzaji wao?

7 Mchungaji katika Israeli la kale alitumia fimbo au bakora ndefu iliyopindika ili kuliongoza kundi lake. Kondoo walipoingia au kutoka katika zizi, ‘walipita chini ya bakora’ hiyo na kuhesabiwa na mchungaji. (Law. 27:32; Mika 2:12; 7:14) Vivyo hivyo, mchungaji Mkristo anahitaji kujua hali ya kundi la Mungu lililo chini ya utunzaji wake. (Linganisha na Methali 27:23.) Ndiyo sababu uchungaji ni kati ya mambo ya maana ambayo baraza la wazee linazungumzia. Hilo linatia ndani kufanya mipango ya kusaidia kondoo waliopotea. Yehova mwenyewe alisema kwamba atawatafuta kondoo wake na kuwatunza. (Eze. 34:11) Kwa hiyo, Mungu anafurahi wazee wanapochukua hatua kama hizo ili kuwasaidia kondoo waliopotea warudi katika kundi.

8. Wazee wanaweza kufanya mambo gani ili kuwapa kondoo uangalifu wa pekee?

8 Mchungaji wa kundi la Mungu anapomtembelea mwamini mwenzake ambaye ni mgonjwa, mgonjwa huyo anaweza kuchangamka na kutiwa moyo. Inakuwa hivyo pia wakati kondoo ambaye ni mgonjwa kiroho anapopewa uangalifu wa pekee. Wazee wanaweza kusoma maandiko, kuzungumzia habari fulani zilizochapishwa, kuzungumzia mambo makuu ya mikutano, kusali pamoja na asiyetenda, na kadhalika. Wanaweza kumweleza kwamba washiriki wa kutaniko watafurahi kumwona akianza tena kuhudhuria mikutano ya kutaniko. (2 Kor. 1:3-7; Yak. 5:13-15) Kumtembelea, kumpigia simu, au kumwandikia barua kunaweza kumtia moyo sana! Kumsaidia kondoo aliyepotea kunaweza pia kuongeza shangwe ya mchungaji Mkristo mwenye huruma.

Jitihada za Pamoja

9, 10. Kwa nini unaweza kusema kwamba si wazee tu wanaopaswa kumjali kondoo aliyepotea?

9 Tunaishi katika nyakati hatari na zenye shughuli nyingi, hivyo huenda tusitambue kwamba mwamini mwenzetu anapeperushwa kutoka katika kutaniko. (Ebr. 2:1) Hata hivyo, kondoo wa Yehova ni wenye thamani sana machoni pake. Kila mmoja wao ni mwenye thamani, kama vile kila sehemu au kiungo cha mwili wa mwanadamu kilivyo chenye thamani. Hivyo, sote tunahitaji kuwajali ndugu zetu na kutunzana kikweli. (1 Kor. 12:25) Je, una mtazamo kama huo?

10 Ingawa wazee wanaongoza katika jitihada za kuwatafuta na kuwasaidia kondoo waliopotea, si waangalizi Wakristo tu wanaopaswa kuwajali waamini wenzao waliopotea. Wengine pia wanaweza kushirikiana na wachungaji hao. Tunaweza na tunapaswa kuwatia moyo na kuwasaidia kiroho ndugu na dada zetu wanaohitaji kusaidiwa kurudi katika kundi. Tunaweza kufanya nini ili kuwasaidia?

11, 12. Unaweza kupata pendeleo gani la kumsaidia mtu anayehitaji msaada wa kiroho?

11 Nyakati nyingine, wazee wanaweza kufanya mipango ili wahubiri wa Ufalme wenye uzoefu wajifunze Biblia pamoja na watu wasiotenda ambao wangependa kusaidiwa. Kusudi la jitihada hizo ni kuamsha tena ‘upendo waliokuwa nao mwanzoni.’ (Ufu. 2:1, 4) Waamini hao wenzetu wanaweza kujengwa na kutiwa nguvu kiroho kwa kuchunguza habari zilizochapishwa ambazo hawakupata wakati ambapo hawakuwa wakishirikiana na kutaniko.

12 Wazee wakikuomba ujifunze pamoja na mwamini mwenzako anayehitaji msaada wa kiroho, sali ili Yehova aongoze na kubariki jitihada zako. Ndiyo, “mkabidhi Yehova mwenyewe kazi zako nayo mipango yako itafanywa imara.” (Met. 16:3) Tafakari kuhusu maandiko ya Biblia na hoja zenye kuimarisha imani ambazo unaweza kutumia unapozungumza pamoja na wale wanaohitaji msaada wa kiroho. Tafakari kuhusu mfano bora wa mtume Paulo. (Soma Waroma 1:11, 12.) Paulo alitamani sana kuwaona Wakristo huko Roma ili awape zawadi fulani ya kiroho kusudi wafanywe imara. Pia, alitazamia sana kutiana moyo nao. Je, hatupaswi kuwa na mtazamo huo tunapojitahidi kuwasaidia kondoo walioliacha kundi la Mungu?

13. Unaweza kuzungumzia mambo gani pamoja na mtu asiyetenda?

13 Katika mazungumzo yenu, unaweza kuuliza, “Ulipata kweli jinsi gani?” Msaidie mtu huyo asiyetenda kukumbuka mambo yaliyomletea shangwe zamani na umtie moyo kuzungumzia mambo aliyoyafurahia katika mikutano, mahubiri, na makusanyiko. Zungumzieni mambo yenye kufurahisha ambayo huenda mmefurahia pamoja katika utumishi wa Yehova. Zungumzia shangwe unayopata kwa kumkaribia Yehova. (Yak. 4:8) Mweleze jinsi unavyothamini njia ambayo Mungu anatumia kututunza tukiwa watu wake, hasa kwa kutupa faraja na tumaini katika dhiki zetu.—Rom. 15:4; 2 Kor. 1:3, 4.

14, 15. Huenda ikafaa kuwakumbusha wasiotenda kuhusu baraka gani walizokuwa nazo?

14 Inaelekea sana kwamba itafaa kumkumbusha yule asiyetenda baraka fulani ambazo alipata aliposhirikiana kwa ukaribu na kutaniko. Kwa mfano, alibarikiwa kwa kulijua zaidi Neno la Mungu na makusudi yake. (Met. 4:18) Alipokuwa ‘akitembea kwa roho,’ inaelekea ilikuwa rahisi zaidi kwake kupinga vishawishi vya kutenda dhambi. (Gal. 5:22-26) Kwa sababu hiyo alikuwa na dhamiri safi, na hilo lilimwezesha kusali kwa Yehova na kupata ‘amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote ambayo inalinda mioyo yetu na nguvu zetu za akili.’ (Flp. 4:6, 7) Kumbuka hoja hizo, onyesha kwamba unamjali kikweli, na usikose kamwe kumtia moyo kwa upendo ndugu au dada yako wa kiroho arudi katika kundi.—Soma Wafilipi 2:4.

15 Tuseme wewe ni mzee na unafanya ziara ya uchungaji. Unaweza kuwatia moyo wenzi wa ndoa wasiotenda wakumbuke wakati ambapo walijifunza kweli ya Neno la Mungu kwa mara ya kwanza. Kweli ilikuwa nzuri ajabu, ilieleweka wazi, iliridhisha, na iliwaweka huru kiroho! (Yoh. 8:32) Mioyo yao ilijaa shukrani kwa sababu ya mambo ambayo walikuwa wakijifunza kumhusu Yehova, upendo wake, na makusudi yake bora! (Linganisha na Luka 24:32.) Wakumbushe kwamba Wakristo waliojiweka wakfu wanafurahia uhusiano wa karibu pamoja na Yehova na pendeleo zuri la sala. Fanya yote unayoweza kuwatia moyo wasiotenda wakubali tena “habari njema yenye utukufu ya Mungu mwenye furaha,” Yehova.—1 Tim. 1:11.

Endeleeni Kuwaonyesha Upendo

16. Eleza mfano unaoonyesha kwamba jitihada za kuwasaidia wengine kiroho zina manufaa.

16 Je, kweli mapendekezo hayo yanafanya kazi? Ndiyo. Kwa mfano, kijana mmoja aliyeanza kuwa mhubiri wa Ufalme akiwa na umri wa miaka 12 alikuwa asiyetenda alipofikia umri wa miaka 15. Hata hivyo, baadaye alianza kutenda na amekuwa katika utumishi wa wakati wote kwa miaka zaidi ya 30. Alipona kiroho hasa kwa sababu alisaidiwa na mzee Mkristo. Alithamini sana msaada wa kiroho aliopokea!

17, 18. Ni sifa gani ambazo zitakuwezesha kumsaidia mtu aliyeacha kushirikiana na kundi la Mungu?

17 Upendo ndio unaowachochea Wakristo kuwasaidia wasiotenda warudi katika kutaniko. Yesu alisema hivi kuhusu wafuasi wake: “Ninawapa ninyi amri mpya, kwamba mpendane; kama vile ambavyo nimewapenda ninyi, ninyi nanyi mpendane vivyo hivyo. Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo kati yenu wenyewe.” (Yoh. 13:34, 35) Ndiyo, upendo ni sifa inayowatambulisha Wakristo wa kweli. Je, Wakristo ambao wameacha kutenda hawapaswi kuonyeshwa upendo kama huo? Bila shaka wanapaswa kuonyeshwa upendo huo! Lakini, ili kuwasaidia, tunahitaji sifa fulani za Kikristo.

18 Ili umsaidie mtu fulani ambaye ameacha kushirikiana na kundi la Mungu, unahitaji kuonyesha sifa gani? Zaidi ya upendo, huenda ukahitaji kuonyesha huruma, fadhili, upole, na ustahimilivu. Ikitegemea hali, huenda ukahitaji pia kuwa mwenye kusamehe. Paulo aliandika hivi: “Jivikeni upendo mwororo wenye huruma, fadhili, unyenyekevu wa akili, upole, na ustahimilivu. Endeleeni kuvumiliana na kusameheana kwa hiari ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika juu ya mwingine. Kama vile Yehova alivyowasamehe ninyi kwa hiari, nanyi fanyeni vivyo hivyo pia. Lakini, zaidi ya mambo haya yote, jivikeni upendo, kwa maana huo ni kifungo kikamilifu cha muungano.”—Kol. 3:12-14.

19. Kwa nini si kazi bure kujitahidi kuwasaidia kondoo waliopotea warudi katika kundi la Kikristo?

19 Habari inayofuata itazungumzia kwa nini watu fulani wanaacha kushirikiana na kundi la Mungu. Pia, itaonyesha jinsi ambavyo wale wanaorudi wanaweza kutarajia kupokewa. Unapojifunza habari hiyo na kutafakari kuhusu funzo hili, uwe na hakika kwamba jitihada zozote zile unazofanya ili kuwasaidia watu walio kama kondoo warudi katika kundi la Kikristo si za bure. Katika mfumo huu wa mambo, watu wengi wanatumia maisha yao yote kujirundikia mali, lakini uhai wa mtu mmoja ni wenye thamani kuliko pesa zote ulimwenguni. Yesu alikazia jambo hilo katika mfano wake kuhusu kondoo aliyepotea. (Mt. 18:12-14) Kumbuka hilo unapofanya jitihada za haraka na za moyo wote za kuwasaidia kondoo wapendwa wa Yehova waliopotea warudi katika kundi.

Ungesema Nini?

• Wachungaji Wakristo wana daraka gani kuelekea kondoo waliopotea?

• Unaweza kufanya nini ili kuwasaidia wale ambao kwa sasa hawashirikiani na kutaniko?

• Ni sifa gani ambazo zitakuwezesha kuwasaidia wale walioacha kushirikiana na kundi?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 10]

Wachungaji Wakristo wanajitahidi kwa upendo kuwasaidia wale ambao wameacha kushirikiana na kundi la Mungu