Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Uwe na Maoni Yanayopatana na Maandiko Kuhusu Matibabu

Uwe na Maoni Yanayopatana na Maandiko Kuhusu Matibabu

Uwe na Maoni Yanayopatana na Maandiko Kuhusu Matibabu

“Lazima umpende Yehova Mungu wako . . . kwa akili yako yote na kwa nguvu zako zote.”—MARKO 12:30.

1. Mungu alikusudia nini alipowaumba wanadamu?

YEHOVA MUNGU alipowaumba wanadamu hakukusudia wawe wagonjwa na kufa. Adamu na Hawa hawakuwekwa katika bustani ya Edeni, au paradiso ya raha, ili ‘wailime na kuitunza’ kwa miaka 70 au 80 tu, bali milele. (Mwa. 2:8, 15; Zab. 90:10) Kama wenzi hao wawili wangebaki waaminifu kwa Yehova na kujinyenyekeza kwa upendo chini ya enzi yake kuu, hawangekuwa wagonjwa, hawangedhoofika, wala kufa kamwe.

2, 3. (a) Kitabu cha Mhubiri kinafafanua uzee jinsi gani? (b) Ni nani aliyesababisha kifo kupitia Adamu, na madhara yake yatakomeshwa jinsi gani?

2 Kitabu cha Mhubiri sura ya 12 kinafafanua vizuri sana “siku zenye msiba” za wanadamu wasio wakamilifu wanaozeeka. (Soma Mhubiri 12:1-7.) Nywele nyeupe zinalinganishwa na maua ya “mti unaozaa lozi.” Miguu inalinganishwa na “wanaume wenye nguvu” ambao wanainama na kutetemeka. Uwezo wa kuona unaozidi kupungua unalinganishwa na mabibi wanaochungulia madirishani wakitafuta mwangaza lakini wanaona giza. Meno yaliyong’oka yanalinganishwa na ‘wanawake wanaosaga ambao wameacha kufanya kazi kwa sababu wamekuwa wachache.’

3 Bila shaka, Mungu hakukusudia wanadamu wawe na miguu dhaifu, uwezo dhaifu wa kuona, na fizi ambazo hazina meno. Zaidi ya hilo, kifo ambacho wamerithi kutoka kwa Adamu ni kati ya “kazi za Ibilisi” ambazo Mwana wa Mungu atakomesha kupitia Ufalme wake wa Kimasihi. Mtume Yohana aliandika hivi: “Kwa kusudi hili Mwana wa Mungu alifunuliwa, yaani, ili azivunje kazi za Ibilisi.”—1 Yoh. 3:8.

Ni Kawaida Kuhangaikia Afya kwa Kiasi

4. Kwa nini watumishi wa Yehova wanahangaikia afya yao kwa kiasi, lakini wanatambua nini?

4 Watumishi fulani wa Yehova leo wanapambana na matatizo ya afya na ya kuzeeka ambayo yanawakumba wanadamu wenye dhambi. Ni jambo la kawaida na hata lenye faida kuhangaikia afya yetu kwa kiasi tunapokabili matatizo hayo. Bila shaka, tunataka kumtumikia Yehova ‘kwa nguvu zetu zote,’ sivyo? (Marko 12:30) Hata hivyo, ingawa tungependa kuwa na afya nzuri iwezekanavyo, tunapaswa kuona mambo kihalisi na kutambua kwamba ni vigumu kuzuia uzee au kuepuka kabisa magonjwa yote.

5. Tunajifunza nini kutokana na jinsi ambavyo watumishi waaminifu wa Mungu wamekabiliana na magonjwa?

5 Watumishi wengi waaminifu wa Yehova wamekabiliana na magonjwa. Mfano mmoja ni Epafrodito. (Flp. 2:25-27) Pia, Timotheo, ambaye alitumikia kwa ushikamanifu pamoja na mtume Paulo, alisumbuliwa mara kwa mara na ugonjwa wa tumbo. Hivyo, Paulo alipendekeza atumie “divai kidogo.” (1 Tim. 5:23) Paulo pia alikabiliana na “mwiba katika mwili,” labda alikuwa na ugonjwa wa macho au ugonjwa mwingine ambao haungeweza kutibiwa wakati huo. (2 Kor. 12:7; Gal. 4:15; 6:11) Paulo alimsihi sana Yehova amwondolee ‘mwiba huo katika mwili.’ (Soma 2 Wakorintho 12:8-10.) Mungu hakuondoa kimuujiza ‘mwiba huo katika mwili’ wa Paulo. Badala yake, Mungu alimpa nguvu za kuvumilia. Hivyo, Yehova alionyesha nguvu zake kupitia udhaifu wa Paulo. Je, tunajifunza jambo lolote kutokana na Paulo?

Usihangaikie Afya Kupita Kiasi

6, 7. Kwa nini hatupaswi kuhangaikia afya yetu kupita kiasi?

6 Kama unavyojua, Mashahidi wa Yehova wanakubali msaada wa madaktari na matibabu mbalimbali. Kwa kawaida, gazeti letu la Amkeni! linazungumzia masuala mbalimbali kuhusu afya. Na ingawa hatupendekezi matibabu fulani, tunathamini msaada tunaopata kutoka kwa wataalamu wa matibabu walio tayari kutusaidia. Bila shaka, tunatambua kwamba hatuwezi kuwa na afya kamilifu sasa. Kwa hiyo, tunajua kwamba ni jambo la hekima kutohangaikia afya yetu kupita kiasi au kila mara. Tunapaswa kuwa na mtazamo tofauti na wa watu ‘wasio na tumaini,’ ambao wanafikiri kwamba uhai ni huuhuu tu na hivyo wanatafuta matibabu yoyote yale wakijaribu kutibu magonjwa yao. (Efe. 2:2, 12) Tumeazimia kutopoteza kibali cha Yehova tunapojaribu kuokoa uhai wetu wa sasa, kwa kuwa tunasadiki kwamba tukiendelea kuwa waaminifu kwa Mungu, ‘tutaushika imara uzima ulio wa kweli,’ uzima wa milele katika mfumo mpya alioahidi.—1 Tim. 6:12, 19; 2 Pet. 3:13.

7 Kuna sababu nyingine inayotufanya tusihangaikie afya yetu kupita kiasi. Kuhangaikia afya yetu kupita kiasi kunaweza kutufanya tuwe na ubinafsi. Paulo alionya kuhusu hatari hiyo alipowahimiza Wafilipi ‘waendelee kuangalia, si faida za kibinafsi za mambo yao wenyewe tu, bali pia faida za kibinafsi za wengine.’ (Flp. 2:4) Hakuna ubaya wa kujihangaikia ipasavyo, hata hivyo, kuwajali kikweli ndugu zetu na pia watu tunaowahubiria “habari njema ya ufalme” kutatuzuia tusihangaikie hali yetu ya kimwili kupita kiasi.—Mt. 24:14.

8. Huenda tukafanya nini tukihangaikia afya yetu kupita kiasi?

8 Hatari ni kwamba Mkristo anaweza kuruhusu mahangaiko kuhusu afya yamzuie asitangulize mambo ya Ufalme. Tukihangaikia afya yetu kupita kiasi huenda tukajaribu kuwalazimisha wengine wafuate maoni yetu binafsi kuhusu faida za vyakula fulani, matibabu fulani, au dawa fulani. Kuhusiana na hilo, fikiria kanuni inayokaziwa na maneno haya ya Paulo: “Mhakikishe mambo yaliyo ya maana zaidi, ili muwe bila kasoro na msiwe mkiwakwaza wengine mpaka siku ya Kristo.”—Flp. 1:10.

Ni Mambo Gani Yaliyo ya Maana Zaidi?

9. Taja jambo moja la maana zaidi ambalo hatupaswi kupuuza, na kwa nini hatupaswi kulipuuza.

9 Tukishiriki kwa bidii katika kazi ya kuwaponya watu kiroho, tutakuwa tukihakikisha mambo yaliyo ya maana zaidi. Tunatimiza kazi hiyo kwa kuhubiri na kufundisha Neno la Mungu. Kazi hiyo ya shangwe inatunufaisha na kuwanufaisha wale tunaowafundisha. (Met. 17:22; 1 Tim. 4:15, 16) Mara kwa mara, magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! yanasimulia kuhusu ndugu na dada zetu wa kiroho ambao wana magonjwa hatari. Nyakati nyingine, masimulizi hayo yanaonyesha jinsi wanavyokabiliana na magonjwa yao au jinsi wanavyoepuka kuhangaikia hali yao kupita kiasi kwa kujitahidi kuwasaidia wengine wamjue Yehova na ahadi zake nzuri ajabu. *

10. Kwa nini matibabu tunayochagua ni ya maana?

10 Kila Mkristo ambaye ni mtu mzima anapokuwa mgonjwa, anapaswa ‘kuubeba mzigo wake mwenyewe’ wa daraka wa kuchagua matibabu. (Gal. 6:5) Lakini tunapaswa kukumbuka kwamba Yehova anatilia maanani matibabu tunayochagua. Kuheshimu kanuni za Biblia kunatuchochea ‘tujiepushe na damu,’ vivyo hivyo, kuheshimu sana Neno la Mungu kunapaswa kutuchochea tuepuke matibabu ambayo yanaweza kutudhuru kiroho au kuharibu uhusiano wetu pamoja na Yehova. (Mdo. 15:20) Mbinu fulani za kupima magonjwa na za matibabu zinatia ndani uchawi. Yehova aliwashutumu Waisraeli waasi-imani ambao walitumia “nguvu za uchawi,” au mazoea ya kuwasiliana na pepo. Alitangaza hivi: “Acheni kuleta ndani matoleo zaidi ya nafaka yasiyo na thamani. Uvumba—ni chukizo kwangu. Mwezi mpya na sabato, kuita mkusanyiko—siwezi kuvumilia matumizi ya nguvu za uchawi pamoja na kusanyiko kuu.” (Isa. 1:13) Bila shaka, ugonjwa si sababu ya kufanya jambo ambalo linaweza kuzuia sala zetu na kuharibu uhusiano wetu pamoja na Mungu.—Omb. 3:44.

Ni Muhimu Kuwa na “Utimamu wa Akili”

11, 12. “Utimamu wa akili” unatusaidia jinsi gani tunapochagua matibabu?

11 Tunapokuwa wagonjwa, hatupaswi kutazamia Yehova atuponye kimuujiza, lakini tunaweza kusali ili atupe hekima ya kuchagua matibabu. Tunapochagua matibabu tunapaswa kutumia kanuni za Kimaandiko na busara. Ikiwa tuna ugonjwa hatari, ni jambo la hekima kutafuta maoni ya madaktari mbalimbali ikiwezekana, kama andiko la Methali 15:22 linavyosema: “Mipango huvunjika mahali ambapo hapana mazungumzo ya siri, lakini katika wingi wa washauri mambo hutimizwa.” Mtume Paulo aliwahimiza waamini wenzake ‘waishi kwa utimamu wa akili na uadilifu na ujitoaji-kimungu katikati ya mfumo wa mambo wa sasa.’—Tito 2:12.

12 Watu wengi wanakabili hali kama ya mwanamke fulani mgonjwa katika siku za Yesu. Tunasoma hivi katika Marko 5:25, 26: “Kulikuwa na mwanamke aliyekuwa na mtiririko wa damu kwa miaka kumi na miwili, naye alikuwa ameumizwa sana na matabibu wengi na alikuwa ametumia mali zake zote naye hakuwa amefaidika bali, badala yake, hali yake ikawa mbaya zaidi.” Yesu alimponya mwanamke huyo na kumtendea kwa huruma. (Marko 5:27-34) Kwa sababu ya kukata tamaa, Wakristo fulani wamechagua matibabu au njia za kupima magonjwa ambazo zinapingana na kanuni za ibada safi.

13, 14. (a) Shetani anaweza kuvunja utimilifu wetu jinsi gani kupitia matibabu tunayochagua? (b) Kwa nini tunapaswa kuepuka kitu chochote ambacho kinahusiana hata kwa kadiri ndogo na zoea la kuwasiliana na pepo?

13 Shetani atatumia njia yoyote ili kutufanya tuiache ibada ya kweli. Kama vile anavyotumia upotovu wa maadili katika ngono na tamaa ya vitu vya kimwili ili kuwaangusha watu fulani, ndivyo anavyojaribu kuvunja utimilifu wa wengine kupitia matibabu yasiyofaa ambayo yanatia ndani nguvu za uchawi na kuwasiliana na pepo. Tunasali ili Yehova atukomboe kutoka kwa “yule mwovu” na kutoka katika “kila namna ya uasi-sheria.” Kwa hivyo, hatupaswi kumpa Shetani nafasi ya kutunasa kwa kujihusisha na jambo lolote ambalo linatia ndani kuwasiliana na pepo na uchawi.—Mt. 6:13; Tito 2:14.

14 Yehova aliwakataza Waisraeli wasifanye uaguzi na uchawi. (Kum. 18:10-12) Paulo anasema kwamba “mazoea ya kuwasiliana na pepo” ni kati ya “matendo ya mwili.” (Gal. 5:19, 20) Kwa kuongezea, “wale wanaozoea kuwasiliana na pepo” hawataingia katika mfumo mpya wa mambo wa Yehova. (Ufu. 21:8) Basi, ni wazi kwamba kitu chochote ambacho kinahusiana hata kwa kadiri ndogo na zoea la kuwasiliana na pepo kinamchukiza Yehova.

“Usawaziko Wenu na Ujulikane”

15, 16. Kwa nini tunahitaji kuchagua matibabu kwa hekima, na baraza linaloongoza la karne ya kwanza lilitoa mashauri gani yenye hekima?

15 Kwa hivyo, ikiwa tuna shaka kuhusu matibabu fulani au njia yoyote ya kupima magonjwa, ni jambo la hekima kuikataa. Hata hivyo, hilo halimaanishi kwamba ikiwa hatuelewi matibabu fulani basi yanatia ndani zoea la kuwasiliana na pepo. Ili tuwe na maoni yanayopatana na Maandiko kuhusu matibabu, tunahitaji utambuzi na vilevile hekima inayotegemea Neno la Mungu. Tunahimizwa hivi katika Methali sura ya 3: “Mtegemee Yehova kwa moyo wako wote wala usitegemee uelewaji wako mwenyewe. Mtambue yeye katika njia zako zote, naye atanyoosha mapito yako. . . . Linda hekima inayotumika na uwezo wa kufikiri, nazo zitakuwa uzima kwa nafsi yako.”—Met. 3:5, 6, 21, 22.

16 Kwa hiyo, tunapojitahidi kuwa na afya nzuri iwezekanavyo tunapaswa kuwa waangalifu ili tusipoteze kibali cha Mungu tunapokabiliana na magonjwa au uzee. Katika matibabu, kama ilivyo katika mambo mengine, acheni tuishi kupatana na kanuni za Biblia ili ‘usawaziko wetu ujulikane kwa watu wote.’ (Flp. 4:5) Katika barua moja ya maana sana, baraza linaloongoza la karne ya kwanza liliwaagiza Wakristo wajiepushe na ibada ya sanamu, damu, na uasherati. Barua hiyo iliwahakikishia hivi: “Mkijiepusha kwa uangalifu na mambo haya, mtafanikiwa.” (Mdo. 15:28, 29) Kwa njia gani?

Kuhangaikia Matibabu kwa Usawaziko Tukitazamia Afya Kamilifu Wakati Ujao

17. Tumepata faida gani za kimwili kwa sababu ya kufuata kanuni za Biblia?

17 Kila mmoja wetu anapaswa kujiuliza hivi: ‘Je, ninaona jinsi ambavyo nimefaidika kibinafsi kwa sababu ya kutii kabisa kanuni za Biblia kuhusu damu na uasherati?’ Fikiria pia faida ambazo tumepata kwa sababu ya kujitahidi ‘kujisafisha wenyewe kila unajisi wa mwili na roho.’ (2 Kor. 7:1) Tukifuata viwango vya Biblia kuhusu usafi wa kimwili, tunaepuka magonjwa mengi. Tunafanikiwa kwa sababu tunajiepusha na uchafu wa kiroho na wa kimwili unaosababishwa na kuvuta sigara na kutumia dawa za kulevya. Fikiria pia faida za kiafya ambazo tunapata kwa sababu ya kula na kunywa kwa kiasi. (Soma Methali 23:20; Tito 2:2, 3.) Ingawa mambo kama vile kupumzika na kufanya mazoezi ya kimwili yanaweza kuchangia afya nzuri, tumefanikiwa kimwili na kiroho hasa kwa sababu tunafuata mwongozo wa Kimaandiko.

18. Tunapaswa kuhangaikia nini hasa, na tunatazamia unabii gani kuhusu afya utimie?

18 Zaidi ya yote, tunapaswa kutunza afya yetu ya kiroho na kutia nguvu uhusiano wetu wa pekee sana pamoja na Baba yetu wa mbinguni, ambaye ndiye Chanzo cha “uzima [wetu] wa sasa na ule utakaokuja” katika ulimwengu mpya ambao ameahidi. (1 Tim. 4:8; Zab. 36:9) Katika ulimwengu mpya wa Mungu, tutaponywa kabisa kiroho na kimwili tutakaposamehewa dhambi kwa msingi wa dhabihu ya Yesu ya fidia. Yesu Kristo, Mwana-Kondoo wa Mungu, atatuongoza “kwenye chemchemi za maji ya uzima,” na Mungu atafuta kila chozi katika macho yetu. (Ufu. 7:14-17; 22:1, 2) Pia, tutaona unabii huu wenye kusisimua ukitimia: “Hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’”—Isa. 33:24.

19. Tunaweza kuwa na uhakika gani tunapotunza afya yetu kwa usawaziko?

19 Tunasadiki kwamba ukombozi wetu unakaribia, na tunangojea kwa hamu siku ambayo Yehova ataondoa kifo na magonjwa yanayowakumba wanadamu. Kwa sasa, tuna uhakika kwamba Baba yetu mwenye upendo atatusaidia kuvumilia uchungu na magonjwa yanayotulemea kwa sababu ‘anatujali.’ (1 Pet. 5:7) Basi, acheni tutunze afya yetu lakini tufanye hivyo sikuzote kupatana na maagizo ya wazi yaliyo katika Neno la Mungu lililoongozwa na roho yake!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Orodha ya habari kama hizo iko katika sanduku kwenye ukurasa wa 17 wa gazeti la Mnara wa Mlinzi la Septemba 1, 2003 (1/9/2003).

Kwa Kupitia

• Ni nani anayesababisha magonjwa, na ni nani atakayetuondolea madhara ya dhambi?

• Ingawa kuhangaikia afya yetu ni jambo la kawaida, tunapaswa kuepuka nini?

• Kwa nini Yehova anatilia maanani matibabu tunayochagua?

• Tunapata faida gani tunapofuata kanuni za Biblia kuhusu afya?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 23]

Wanadamu hawakuumbwa ili wazeeke na kuwa wagonjwa

[Picha katika ukurasa wa 25]

Watu wa Yehova wanapata shangwe katika huduma hata wakiwa na matatizo ya kiafya