Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mambo Makuu Katika Barua za Yohana na ya Yuda

Mambo Makuu Katika Barua za Yohana na ya Yuda

Neno la Yehova Liko Hai

Mambo Makuu Katika Barua za Yohana na ya Yuda

BARUA tatu za mtume Yohana ambazo inaelekea ziliandikwa mwaka wa 98 W.K. huko Efeso, ni kati ya vitabu vya mwisho vya Maandiko yaliyoongozwa na roho takatifu. Barua mbili za kwanza zinawatia moyo Wakristo waendelee kutembea katika nuru na kupinga uasi-imani. Katika barua ya tatu, Yohana anazungumza kuhusu kutembea katika kweli na pia anawatia moyo Wakristo washirikiane.

Katika barua aliyoandika karibu mwaka wa 65 W.K. huko Palestina, Yuda, ndugu wa kambo wa Yesu anawaonya Wakristo wenzake kuhusu watu waovu ambao walikuwa wameingia kisirisiri ndani ya kutaniko, naye anawapa mashauri kuhusu kupinga uvutano mbaya. Kukazia uangalifu ujumbe ulio katika barua tatu za Yohana na barua ya Yuda kunaweza kutusaidia kuendelea kuwa na nguvu katika imani hata tukipata vipingamizi.—Ebr. 4:12.

ENDELEA KUTEMBEA KATIKA NURU NA UPENDO NA KWA IMANI

(1 Yohana 1:1–5:21)

Barua ya kwanza ya Yohana iliandikwa kwa ajili ya wote walio katika ushirika na Kristo, na ina mashauri mazuri ya kuwasaidia Wakristo kupinga uasi-imani na kubaki imara kwa ajili ya kweli na uadilifu. Anakazia uhitaji wa kuendelea kutembea katika nuru na upendo na kwa imani.

Yohana anaandika hivi: “Ikiwa tunatembea katika nuru kama yeye [Mungu] mwenyewe alivyo katika nuru, tuna ushirika sisi kwa sisi.” Na kwa kuwa Mungu ndiye Chanzo cha upendo, mtume huyo anasema: “Acheni tuendelee kupendana.” Ingawa “kumpenda Mungu” kunatuchochea ‘kuzishika amri zake,’ tunaushinda ulimwengu kupitia “imani yetu” katika Yehova Mungu, Neno lake, na Mwana wake.—1 Yoh. 1:7; 4:7; 5:3, 4.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

2:2; 4:10—Yesu ni “dhabihu ya upatanisho” kwa njia gani? Kupatanisha kunamaanisha “kutuliza,” au “kuridhisha.” Yesu alitoa uhai wake kuwa dhabihu ya upatanisho kwa njia ya kwamba aliridhisha au kutosheleza matakwa ya haki kamilifu. Kwa msingi wa dhabihu hiyo, Mungu anaweza kuonyesha rehema na kusamehe dhambi za wale walio na imani katika Yesu.—Yoh. 3:16; Rom. 6:23.

2:7, 8—Ni amri gani ambayo Yohana anasema ni “ya zamani” na pia ni “mpya”? Yohana anazungumzia amri inayohusu upendo wa kindugu wa kujidhabihu. (Yoh. 13:34) Anasema kwamba ni “ya zamani” kwa sababu Yesu aliitoa miaka zaidi ya 60 kabla ya Yohana kuandika barua yake ya kwanza ambayo iliongozwa na roho. Kwa hiyo, waamini wamekuwa nayo “tangu mwanzo” wa maisha yao wakiwa Wakristo. Amri hiyo pia ni “mpya” kwa sababu inahusisha mengi zaidi ya ‘kumpenda mwenzako kama wewe mwenyewe’ na inatia ndani upendo wa kujidhabihu.—Law. 19:18; Yoh. 15:12, 13.

3:2—Ni nini ambacho ‘hakijafunuliwa’ kwa Wakristo watiwa-mafuta, na ni nani ambaye watamwona “kama vile yeye alivyo”? Kile ambacho hakijafunuliwa kwao ni jinsi watakavyokuwa watakapofufuliwa na kwenda mbinguni wakiwa na miili ya roho. (Flp. 3:20, 21) Hata hivyo, wanajua kwamba “wakati wowote [Mungu] atakapofunuliwa [watakuwa] kama yeye, kwa sababu [watamwona] kama vile yeye alivyo,” yaani, “Roho.”—2 Kor. 3:17, 18.

5:5-8—Maji, damu, na roho ilitoa ushahidi jinsi gani na kuthibitisha kwamba “Yesu ndiye Mwana wa Mungu”? Maji yalitoa ushahidi kwa sababu Yesu alipobatizwa katika maji, Yehova mwenyewe alisema kwamba anamkubali akiwa Mwana Wake. (Mt. 3:17) Damu ya Yesu, au uhai wake, uliotolewa kuwa “fidia inayolingana kwa ajili ya wote,” ulionyesha pia kwamba Yesu ni Mwana wa Mungu. (1 Tim. 2:5, 6) Nayo roho takatifu ilitoa ushahidi wa kwamba Yesu ni Mwana wa Mungu iliposhuka juu yake wakati alipobatizwa, na kumwezesha ‘kupita katika nchi akitenda mema na kuwaponya wote waliokandamizwa na Ibilisi.’—Yoh. 1:29-34; Mdo. 10:38.

Mambo Tunayojifunza:

2:9-11; 3:15. Mkristo akiruhusu kitu chochote au mtu yeyote aharibu upendo wake wa kindugu, anatembea katika giza la kiroho, hajui anakoenda.

ENDELEA ‘KUTEMBEA KATIKA KWELI’

(2 Yohana 1-13)

Yohana anaanza barua yake ya pili kwa kusema hivi: “Mwanamume mzee, kwa bibi aliyechaguliwa, na kwa watoto wake.” Anashangilia kwa sababu amekuta “baadhi ya watoto [wake] wanatembea katika kweli.”—2 Yoh. 1, 4.

Baada ya kuwatia moyo wasitawishe upendo, Yohana anaandika hivi: “Upendo unamaanisha hivi, kwamba tuendelee kutembea kulingana na amri zake.” Pia, Yohana anaonya kuhusu “yule mdanganyifu na mpinga-Kristo.”—2 Yoh. 5-7.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

1, 13—Yule “bibi aliyechaguliwa” ni nani? Huenda Yohana anazungumza kuhusu mwanamke fulani ambaye anamwita Kyria, neno la Kigiriki linalomaanisha “bibi.” Au huenda anatumia usemi wa mfano kuhusu kutaniko fulani ili watesaji wasijue. Ikiwa anazungumza kuhusu kutaniko fulani, basi washiriki wa kutaniko hilo ni watoto wake, nao “watoto wa dada [yake]” ni washiriki wa kutaniko lingine.

7—Ni ‘kuja’ gani kwa Yesu ambako Yohana anazungumzia hapa, na ni jinsi gani wadanganyifu ‘hawakiri’ hilo? Si ‘kuja’ kwa baadaye kwa Yesu kusikoonekana. Badala yake ni kuja kwake katika mwili na kutiwa mafuta ili awe Kristo. (1 Yoh. 4:2) Wadanganyifu hawakiri kuja huko katika mwili. Labda wanapinga kwamba Yesu alikuwapo au wanakataa kwamba alitiwa mafuta na roho takatifu.

Mambo Tunayojifunza:

2, 4. Ili tupate wokovu ni lazima tujue “kweli,” yaani, mafundisho yote ya Kikristo ambayo ni sehemu ya Biblia, na kushikamana nayo.—3 Yoh. 3, 4.

8-11. Ikiwa hatutaki kupoteza ‘fadhili zisizostahiliwa, rehema na amani kutoka kwa Mungu Baba na kutoka kwa Yesu Kristo,’ na pia ushirika wetu wenye upendo pamoja na waamini wenzetu, tunapaswa ‘kujihadhari’ kiroho na kuwakataa kabisa wale ambao ‘hawakai katika fundisho la Kristo.’—2 Yoh. 3.

IWENI “WAFANYAKAZI WENZI KATIKA KWELI”

(3 Yohana 1-14)

Yohana anaandika barua yake ya tatu kwa rafiki yake Gayo. Anaandika hivi: “Sina sababu nyingine kubwa zaidi ya kuwa na shukrani kuliko mambo haya, kwamba niwe nikisikia watoto wangu wanaendelea kutembea katika kweli.”—3 Yoh. 4.

Yohana anampongeza Gayo kwa sababu ya ‘kufanya kazi ya uaminifu’ ya kuwasaidia ndugu wageni. Mtume huyo anasema hivi: “Sisi tuna wajibu wa kuwakaribisha watu wa namna hiyo, ili tuwe wafanyakazi wenzi katika kweli.”—3 Yoh. 5-8.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

11—Kwa nini watu fulani wanatenda mabaya? Hawathamini mambo ya kiroho, na hawamwoni Mungu kwa macho yao ya ufahamu. Kwa kuwa hawawezi kumwona Mungu kihalisi, wanatenda kana kwamba Mungu hawaoni.—Eze. 9:9.

14—“Rafiki” wanaotajwa hapo ni nani? Neno “rafiki” katika andiko hilo linatia ndani wengine zaidi ya watu walio na uhusiano wa karibu kati yao. Yohana anatumia neno hilo kuwahusu waamini wenzake kwa ujumla.

Mambo Tunayojifunza:

4. Watu wakomavu kiroho katika kutaniko wanapata shangwe kubwa wanapoona washiriki wachanga wa kutaniko ‘wakiendelea kutembea katika kweli.’ Na wazazi wanapata shangwe kubwa kama nini wanapofaulu kuwasaidia watoto wao kuwa watumishi wa Yehova!

5-8. Waangalizi wanaosafiri, wamishonari, wale wanaotumika katika Betheli au ofisi za tawi na wale walio katika utumishi wa upainia ni kati ya wale ambao wanafanya kazi kwa bidii kwa ajili ya ndugu zao kwa sababu wanawapenda na wanampenda Yehova. Imani yao inastahili kuigwa, na tunapaswa kuwategemeza kwa upendo.

9-12. Tunapaswa kuiga mfano wa Demetrio ambaye alikuwa mwaminifu, bali si yule mpiga-porojo Diotrefe, aliyekuwa mchongezi.

“JITUNZENI KATIKA UPENDO WA MUNGU”

(Yuda 1-25)

Yuda anasema kwamba wale wanaoingia kisirisiri katika kutaniko ni ‘wanung’unikaji, na walalamikaji juu ya fungu lao maishani, wanaoendelea kulingana na tamaa zao wenyewe.’ Nao “husema mambo ya kujigamba, huku wakisifu kwa kustaajabia watu mashuhuri.”—Yuda 4, 16.

Wakristo wanaweza kushinda namna gani uvutano mbaya? Yuda anaandika hivi: “Wapendwa, kumbukeni maneno ambayo mitume wa Bwana wetu Yesu Kristo waliyasema hapo mwanzoni.” Anaongezea hivi: “Jitunzeni katika upendo wa Mungu.”—Yuda 17-21.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

3, 4—Kwa nini Yuda aliwahimiza Wakristo ‘wafanye pigano kali kwa ajili ya imani’? Kwa sababu ‘watu wasiomwogopa Mungu walikuwa wameingia kisirisiri ndani ya kutaniko.’ Watu hao walikuwa ‘wakigeuza fadhili zisizostahiliwa za Mungu kuwa kisingizio cha mwenendo mpotovu.’

20, 21—Tunaweza ‘kujitunza wenyewe katika upendo wa Mungu’ kwa njia gani? Tunaweza kufanya hivyo kwa njia tatu: (1) kwa kujijenga wenyewe juu ya ‘imani yetu iliyo takatifu zaidi’ tunapojifunza Neno la Mungu kwa bidii na kushiriki kwa bidii katika kazi ya kuhubiri; (2) kwa kusali ‘tukiwa na roho takatifu,’ au kupatana na mwongozo wake; na (3) kwa kuwa na imani katika dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo ambayo inatuwezesha kupata uzima wa milele.—Yoh. 3:16, 36.

Mambo Tunayojifunza:

5-7. Je, waovu wanaweza kuepuka hukumu ya Yehova? Kulingana na mifano mitatu ya kuonya iliyotajwa na Yuda, haiwezekani.

8-10. Tunapaswa kufuata mfano wa Mikaeli yule malaika mkuu na kuwaheshimu wale waliopewa mamlaka na Mungu.

12. Waasi-imani wanaojifanya kuwa wana upendo ni hatari kwa imani yetu kama miamba iliyofichwa chini ya maji ilivyo hatari kwa meli au waogeleaji. Huenda walimu wa uwongo wakaonekana kuwa wakarimu, lakini wao ni kama mawingu yasiyo na maji kwa kuwa hawana chochote kiroho. Watu hao ni kama miti iliyokufa isiyozaa matunda katika majira ya mpukutiko. Wanakabili uharibifu kama miti iliyong’olewa pamoja na mizizi. Ni hekima kwetu kuepuka waasi-imani.

22, 23. Wakristo wa kweli wanachukia mabaya. Washiriki wakomavu katika kutaniko, hasa waangalizi waliowekwa rasmi, wanajaribu kuwaokoa “watu fulani walio na shaka” kwa kuwanyakua kutoka katika moto wa uharibifu wa milele, wanapowasaidia kiroho.

[Picha katika ukurasa wa 28]

Maji, roho, na damu zilitoa ushahidi kwamba “Yesu ndiye Mwana wa Mungu”