Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ni Mungu Tu Anayeweza Kuiokoa Dunia

Ni Mungu Tu Anayeweza Kuiokoa Dunia

Ni Mungu Tu Anayeweza Kuiokoa Dunia

“KITO CHA BLUU KINACHONG’AA.” Hivyo ndivyo mwanaanga Edgar Mitchell alivyofafanua dunia alipoiona angani.

Mungu alifanya mambo mengi ili kutayarisha dunia iwe makao ya mwanadamu. Uumbaji wake uliwachochea malaika kupaaza sauti “kwa kushangilia.” (Ayubu 38:7) Baada ya kuchunguza maajabu ya sayari yetu, hata sisi tuna sababu za kushangilia. Kuna mifumo mingi tata inayowezesha uhai usitawi duniani. Katika mfumo mmoja unaojulikana sana, mimea inatumia mwangaza wa jua, kaboni dioksidi kutoka kwa hewa, na maji ili kutokeza chakula. Mfumo huo unatokeza oksijeni ambayo ni muhimu kwa uhai wetu.

Biblia inaonyesha kwamba Mungu alimkabidhi mwanadamu jukumu la kuitunza dunia. (Mwanzo 1:28; 2:15) Hata hivyo, ili mifumo ya dunia itende kwa njia inayofaa, mwanadamu alihitaji kuwa na mtazamo unaofaa. Kwa kweli, alipaswa kuyapenda makao yake ya kidunia. Alipaswa kuwa na tamaa ya kuyadumisha katika hali nzuri. Lakini kwa kuwa mwanadamu alipewa uhuru wa kuchagua, kulikuwa na uwezekano wa kwamba atachagua kuitumia vibaya na kuiharibu dunia. Na hivyo ndivyo amefanya. Kutojali na pupa ya mwanadamu kumeleta matokeo mabaya sana.

Baadhi ya matatizo ni: (1) Ukataji wa miti ambao unaathiri uwezo wa dunia wa kufyonza kaboni dioksidi, jambo ambalo linaweza kufanya hali ya hewa ibadilike sana. (2) Kutumia dawa za kuua wadudu kupita kiasi kunaangamiza wadudu wanaofaidi mazingira kwa njia mbalimbali, kutia ndani kuchavusha mimea. (3) Kuvua kupita kiasi na kuchafua bahari na mito kumepunguza sana idadi ya samaki. (4) Kutumia kwa pupa mali za asili za dunia kumepunguza akiba ya vitu hivyo kwa ajili ya vizazi vya wakati ujao na inadhaniwa kunachochea kuongezeka kwa joto duniani. Wanamazingira fulani wanasema kwamba kuyeyuka na kuvunjika kwa miamba ya barafu katika maeneo ya Aktiki na Antaktiki ni uthibitisho wa kuongezeka kwa joto duniani.

Kwa sababu ya kuongezeka kwa misiba ya asili, huenda watu fulani wakasema kwamba dunia inalalamika, na kuwasababishia wanadamu matatizo. Mungu alitupa dunia bila malipo. Kwa kweli, wanadamu hawalipi kodi ili waishi duniani. (Mwanzo 1:26-29) Hata hivyo, matukio ya sasa ya dunia yanaonyesha kwamba watu wengi hawataki kutunza makao yao maridadi. Badala yake, wanadamu wanafuatilia tamaa na utendaji wao wa kibinafsi. Kwa kweli, wamekuwa wakaaji wabaya wa dunia, ‘wanaiharibu dunia,’ kama ilivyotabiriwa katika Ufunuo 11:18.

Unabii wa Biblia unaonyesha kwamba Mungu Mweza-Yote, Yehova, Muumba wa mifumo ya dunia inayoendeleza uhai, amesema kwamba wakati umefika wa “kuwafukuza” wakaaji hao wabaya. (Sefania 1:14; Ufunuo 19:11-15) Kabla ya wanadamu kuharibu kabisa dunia, Mungu atatenda mapema kuliko tunavyotarajia. * (Mathayo 24:44) Kwa kweli, ni Mungu tu anayeweza kuiokoa dunia.

[Maelezo ya chini]

^ fu. 7 Kwa habari zaidi kuhusu uharaka wa nyakati hizi, ona broshua Endeleeni Kukesha! iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.