Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mwamuzi Anayefanya Lililo Sawa Sikuzote

Mwamuzi Anayefanya Lililo Sawa Sikuzote

Mkaribie Mungu

Mwamuzi Anayefanya Lililo Sawa Sikuzote

Mwanzo 18:22-32

HAKI. Kutopendelea. Kutobagua. Je, sifa hizo nzuri hazikuvutii? Sote tumezaliwa na tamaa ya kutendewa kwa haki. Hata hivyo, inasikitisha kwamba kuna ukosefu wa haki leo. Lakini kuna Mwamuzi ambaye tunaweza kumtumaini—Yehova Mungu. Sikuzote yeye anafanya yaliyo sawa. Hilo lilionekana wazi katika mazungumzo kati ya Yehova na Abrahamu yaliyorekodiwa katika Mwanzo 18:22-32. *

Yehova alipomwambia Abrahamu kuhusu uamuzi Wake wa kuchunguza jinsi hali zilivyokuwa huko Sodoma na Gomora, Abrahamu alihofia usalama wa mtu yeyote mwadilifu aliyeishi huko kutia ndani, Loti, mpwa wake. Abrahamu alimsihi Yehova hivi: ‘Je, kweli utafagilia mbali mwadilifu pamoja na mwovu? Tuseme kuna watu waadilifu 50 katika jiji hilo. Je, wewe, hutasamehe mahali hapo kwa ajili ya wale waadilifu 50 ambao wamo ndani yake?’ (Mstari wa 23, 24) Mungu alisema kwamba hangeharibu majiji hayo ikiwa kungekuwa na watu waadilifu 50 tu. Abrahamu alimsihi Yehova mara tano zaidi, akipunguza idadi ya waadilifu hadi kufikia kumi. Kila mara, Mungu alisema kwamba hangeharibu majiji hayo kama kungekuwa na idadi ya watu waadilifu ambayo Abrahamu alitaja.

Je, Abrahamu alikuwa akibishana na Mungu? La hasha! Huo ungekuwa ukaidi kama nini! Sauti ya Abrahamu ilionyesha heshima na unyenyekevu. Alisema kwamba yeye ni “mavumbi na majivu” tu. Mara nne alionyesha heshima kwa kusema “tafadhali.” (Mstari wa 27, 30-32) Isitoshe, maneno ya Abrahamu yalionyesha kwamba alikuwa na uhakika Yehova angetenda kwa haki. Abrahamu alisema mara mbili kwamba lingekuwa jambo “lisilowaziwa” kwa Mungu kuwaharibu waadilifu pamoja na waovu. Mzee huyo wa ukoo alikuwa na hakika kwamba “Mwamuzi wa dunia yote” ‘angefanya lililo sawa.’—Mstari wa 25.

Je, Abrahamu alikuwa amekosea kwa yale aliyosema? Hapana na ndiyo. Alikuwa amekosea alipodokeza kwamba kulikuwa na watu waadilifu angalau kumi huko Sodoma na Gomora. Lakini hakuwa amekosea aliposema kwamba Mungu hatawahi ‘kumfagilia mbali mwadilifu pamoja na mwovu.’ Baadaye, Mungu alipoharibu majiji hayo maovu, Loti mwadilifu na binti zake wawili waliokoka wakisaidiwa na malaika.—2 Petro 2:7-9.

Simulizi hilo linatufundisha nini kumhusu Yehova? Kwa kumwambia Abrahamu kuhusu kusudi Lake la kuchunguza majiji hayo, ni kama Yehova alikuwa akimwalika aeleze hisia zake. Kisha akasikiliza kwa subira huku rafiki yake Abrahamu akieleza mahangaiko yaliyokuwa moyoni mwake. (Isaya 41:8) Hilo linatufundisha kwamba Yehova ni Mungu mnyenyekevu anayewaheshimu watumishi wake wa kidunia! Ni wazi kwamba tuna kila sababu ya kumtegemea kabisa Yehova, Mwamuzi anayefanya lililo sawa sikuzote.

[Maelezo ya chini]

^ fu. 1 Wakati huo, Yehova aliwakilishwa na malaika aliyezungumza kwa niaba Yake. Unaweza kupata mfano mwingine kwenye Mwanzo 16:7-11, 13.

[Picha katika ukurasa wa 24]

Abrahamu alimsihi Yehova kuhusu Sodoma na Gomora