Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Sala Fulani Hazijibiwi?

Kwa Nini Sala Fulani Hazijibiwi?

Wasomaji Wetu Wanauliza

Kwa Nini Sala Fulani Hazijibiwi?

Mungu anaweza kufikiwa na kila mtu kwa uhuru. Kama tu baba mwenye upendo anavyofurahi watoto wake wanapozungumza naye waziwazi, Yehova Mungu anafurahi tunaposali kwake. Wakati huohuo, kama baba mwenye hekima, Mungu ana sababu nzuri za kukataa kujibu maombi fulani. Je, sababu zake za kufanya hivyo hazieleweki, au mambo fulani katika Biblia yanaweza kutusaidia kuelewa kwa nini hajibu sala hizo?

Mtume Yohana anaeleza hivi: “Huu ndio uhakika ambao tunao kwake, kwamba, hata tukiomba nini kulingana na mapenzi yake, yeye hutusikia.” (1 Yohana 5:14) Maombi yetu yanapaswa kupatana na mapenzi ya Mungu. Watu fulani wanaomba vitu ambayo havipatani kabisa na mapenzi ya Mungu, kama vile, kushinda bahati-nasibu au shindano la kamari. Wengine wanasali wakiwa na nia mbaya. Mwanafunzi Yakobo anaonya dhidi ya kusali kwa njia hiyo mbaya, akisema: “Mnaomba, na bado hampokei, kwa sababu mnaomba kwa kusudi baya, ili mvitumie kwa tamaa zenu za mwili.”—Yakobo 4:3.

Kwa mfano, wazia kwamba timu mbili za mpira zinasali ili zishinde. Mungu hawezi kutazamiwa kujibu sala kama hizo zinazopingana. Jambo hilo pia ni kweli kuhusu vita vya kisasa ambavyo pande zote zinasali ili zishinde.

Wale wanaoidharau sheria ya Mungu wanasali bure. Wakati mmoja Yehova alilazimika kuwaambia hivi waabudu wanafiki: “Nanyi mnaponyoosha mikono yenu, mimi huficha macho yangu kutoka kwenu. Hata mjapotoa sala nyingi, mimi sisikilizi; mikono yenu imejaa umwagaji wa damu.” (Isaya 1:15) Biblia inasema: “Anayegeuzia mbali sikio lake asiisikie sheria—hata sala yake ni chukizo.”—Methali 28:9.

Kwa upande mwingine, nyakati zote Yehova atasikiliza sala za unyoofu za waabudu wanaofanya yote wanayoweza ili wamtumikie kupatana na mapenzi yake. Hata hivyo, je, linamaanisha kwamba atajibu maombi yao yote? Hapana. Fikiria mifano kadhaa ya Kimaandiko.

Ingawa Musa alikuwa na uhusiano wa karibu sana pamoja na Mungu, yeye pia alipaswa kuomba “kulingana na mapenzi [ya Mungu].” Kinyume na kusudi la Mungu, Musa aliomba aruhusiwe kuingia katika nchi ya Kanaani: “Acha nivuke, tafadhali, niione hiyo nchi nzuri iliyo ng’ambo ya Yordani.” Lakini, hapo awali Musa alikuwa ameambiwa kwamba hangaliweza kuingia katika nchi hiyo kwa sababu ya dhambi aliyokuwa amefanya. Kwa hiyo, badala ya kukubali ombi la Musa, Yehova alimwambia: “Imetosha! Usiseme nami tena kamwe juu ya jambo hili.”—Kumbukumbu la Torati 3:25, 26; 32:51.

Mtume Paulo alisali ili apate kitulizo kutoka kwa kile alichokiita “mwiba katika mwili.” (2 Wakorintho 12:7) Huenda ikawa “mwiba” huo ulirejelea ugonjwa fulani wa macho wa kudumu au kuteswa kila wakati na wapinzani na “ndugu wa uwongo.” (2 Wakorintho 11:26; Wagalatia 4:14, 15) Paulo aliandika hivi: “Mara tatu nilimsihi Bwana kwamba huo uniondoke.” Hata hivyo, Mungu alijua kwamba ikiwa Paulo angeendelea kuhubiri licha ya kuwa na “mwiba katika mwili,” hilo lingeonyesha kwamba Mungu alimtia nguvu na kwamba Paulo alimtegemea kabisa. Hivyo, badala ya kujibu ombi la Paulo, Mungu alimwambia: “Nguvu zangu zinakamilishwa katika udhaifu.”—2 Wakorintho 12:8, 9.

Ndiyo, Mungu anajua vizuri kuliko sisi ikiwa inafaa kujibu maombi fulani tunayotoa. Sikuzote Yehova anajibu kwa njia inayotufaidi, kupatana na makusudi yake yenye upendo yaliyorekodiwa katika Biblia.