Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Uthibitisho Mkubwa Zaidi wa Upendo wa Mungu

Uthibitisho Mkubwa Zaidi wa Upendo wa Mungu

Mkaribie Mungu

Uthibitisho Mkubwa Zaidi wa Upendo wa Mungu

Mwanzo 22:1-18

ABRAHAMU alimpenda Mungu. Mzee huyo mwaminifu wa ukoo alimpenda pia Isaka, mwana wake wa uzeeni. Lakini Isaka alipokuwa na umri wa miaka 25 hivi, Abrahamu alikabili jaribu lililopingana na hisia za kawaida za baba. Mungu alimwambia amdhabihu mwana wake. Hata hivyo, Isaka hakuuawa. Wakati Abrahamu alikuwa karibu kumwua, Mungu aliingilia kati kupitia malaika. Simulizi hilo la Biblia, lililoandikwa katika Mwanzo 22:1-18, lilionyesha kwa njia ya kinabii upendo mkubwa sana wa Mungu kutuelekea.

Mstari wa 1 unasema hivi: “Mungu . . . akamjaribu Abrahamu.” Abrahamu alikuwa na imani, lakini sasa imani yake ilijaribiwa kwa njia ambayo haikuwa imewahi kujaribiwa tena. Mungu alisema: “Tafadhali, mchukue mwana wako, mwana wako wa pekee unayempenda sana, Isaka, . . . umtoe kama toleo la kuteketezwa juu ya mmoja kati ya milima ambao nitakuonyesha.” (Mstari wa 2) Kumbuka kwamba Mungu hawaachi watumishi wake wajaribiwe kupita wanavyoweza kuhimili. Kwa hiyo, jaribu hilo lilionyesha kwamba Mungu hakuwa na shaka kumhusu Abrahamu.—1 Wakorintho 10:13.

Abrahamu alitii bila kusitasita. Tunasoma hivi: “Abrahamu akaamka asubuhi na mapema na kumtandika punda wake, akachukua wawili kati ya watumishi wake na Isaka mwana wake; naye akapasua kuni kwa ajili ya toleo la kuteketezwa. Kisha akaondoka, akafunga safari.” (Mstari wa 3) Ni wazi kwamba Abrahamu hakumwambia mtu yeyote kuhusu mambo hususa ya jaribu hilo.

Alisafiri kwa siku tatu na hilo lilimpa wakati wa kutafakari kwa uzito. Lakini imani ya Abrahamu haikufifia. Maneno aliyosema yalionyesha hilo. Alipoona mlima uliokuwa umechaguliwa, aliwaambia hivi watumishi wake: “Ninyi kaeni hapa . . . , lakini mimi na huyu mvulana tunataka kwenda mbele huko tukaabudu, halafu tutarudi hapa mlipo.” Isaka alipomwuliza baba yake kuhusu kondoo wa kutolewa kama dhabihu, Abrahamu alisema: “Mungu mwenyewe ataandaa kondoo.” (Mstari wa 5, 8) Abrahamu alitarajia kwamba atarudi na mwanaye. Kwa nini? Kwa sababu “alifikia uamuzi kwamba Mungu alikuwa na uwezo wa kumfufua [Isaka] hata kutoka kwa wafu.”—Waebrania 11:19.

Wakiwa juu mlimani, Abrahamu alichukua “kisu cha kuchinjia ili amuue mwana wake,” lakini malaika akamzuia. Kisha Mungu akaandaa kondoo-dume aliyenaswa kichakani ili Abrahamu amtoe kuwa dhabihu “badala ya mwana wake.” (Mstari wa 10-13) Kwa maoni ya Mungu, ni kana kwamba Isaka alikuwa ametolewa kuwa dhabihu. (Waebrania 11:17) “Mbele za Mungu,” anaeleza msomi mmoja, “nia ya kufanya hivyo ilikuwa sawa na tendo lenyewe.”

Uhakika ambao Yehova alikuwa nao katika Abrahamu ulithibitika kuwa wa kweli. Na imani ya Abrahamu katika Yehova ilithawabishwa, kwa kuwa Mungu alirudia agano alilokuwa amefanya na Abrahamu na akahusisha watu wengi zaidi. Katika agano hilo aliahidi kuwabariki watu wa mataifa yote.—Mstari wa 15-18.

Mungu alimzuia Abrahamu kutoa dhabihu ambayo Yeye mwenyewe hakujizuia kutoa. Utayari wa Abrahamu wa kumtoa Isaka ulionyesha jinsi Mungu angemtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, Yesu, kwa ajili ya dhambi zetu. (Yohana 3:16) Dhabihu ya Kristo ndio uthibitisho mkubwa zaidi wa kwamba Yehova anatupenda. Kwa kuwa Mungu amejidhabihu sana hivyo kwa ajili yetu, tunapaswa kujiuliza hivi, ‘Niko tayari kujidhabihu kadiri gani ili kumpendeza Mungu?’