Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Biblia Inabadili Maisha

Biblia Inabadili Maisha

Biblia Inabadili Maisha

Ni nini kilichomchochea mwanamke fulani aliyekuwa na biashara ya magendo ya almasi na aliyekuwa akimwibia mwajiri wake abadilike na kuwa mfanyakazi mnyoofu? Ni nini kilichomsaidia mwanamke aliyejaribu mara mbili kujiua awe na kusudi maishani? Mtu aliyekuwa mraibu wa kileo na dawa za kulevya alipata nguvu jinsi gani za kuacha uraibu wake? Ona mambo ambayo walisema.

MAELEZO MAFUPI KUMHUSU

JINA: MARGARET DEBRUYN

UMRI: 45

NCHI: BOTSWANA

HISTORIA: MFANYABIASHARA YA MAGENDO NA MWIZI

MAISHA YANGU YA ZAMANI: Baba yangu alikuwa Mjerumani lakini akawa raia wa Afrika-Kusini-Magharibi (ambayo sasa ni Namibia). Mama yangu alikuwa wa kabila la Mangologa huko Botswana. Nilizaliwa huko Gobabis, Namibia.

Katika miaka ya 1970, serikali ya Afrika Kusini ilikuwa na uvutano mkubwa juu ya Namibia na iliweka sheria za ubaguzi wa rangi katika miji na vijiji vyote. Kwa kuwa wazazi wangu walikuwa wa rangi tofauti, walishinikizwa waachane. Kwa hiyo, mama yangu aliondoka na mimi pamoja na ndugu na dada zangu na kurudi Ghansi, Botswana.

Mnamo 1979, nilihamia Lobatse, Botswana, na kuishi na wazazi wa kambo ambako nilimalizia shule. Baadaye niliajiriwa katika gereji moja ambako nilifanya kazi ya ukarani. Tangu utotoni niliamini kwamba Mungu hawaandalii watu chochote, na kwamba unahitaji kufanya lolote unaloweza, iwe ni sawa au si sawa, ili kujiandalia na kuandalia familia yako mahitaji.

Kwa kuwa nilikuwa na cheo fulani kazini, nilitumia nafasi hiyo kumwibia mwajiri wangu sehemu za gari. Kila mara gari-moshi lilipopitia mjini usiku, mimi na wenzangu tulilidandia na kuiba chochote ambacho tungepata. Pia nilijihusisha katika biashara ya magendo ya almasi, dhahabu, na shaba. Nilianza kutumia dawa za kulevya, nikawa mjeuri sana, na nilikuwa na wapenzi wengi sana.

Kisha, mnamo 1993, nilishikwa nikiiba na nikafutwa kazi. Waliodai kuwa rafiki zangu walitoroka wakiogopa kwamba wao pia watashikwa. Jambo hilo liliniumiza sana na nikaamua sitamwamini tena mtu yeyote.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU: Mnamo 1994, nilikutana na Tim na Virginia, Mashahidi wa Yehova ambao walikuwa wamishonari. Walizungumza pamoja nami mahali nilipokuwa nikifanya kazi na wakanisaidia kujifunza kuhusu Biblia wakati wa chakula cha mchana. Baadaye, nilipohisi ninaweza kuwaamini, niliwaruhusu waje nyumbani kwangu tujifunze Biblia.

Punde si punde nilitambua kwamba ili nimpendeze Mungu nilihitaji kufanya mabadiliko fulani maishani. Kwa mfano, nilijifunza katika 1 Wakorintho 6:9, 10 kwamba “wala waasherati, . . . wala wezi, wala watu wenye pupa, wala walevi, wala watukanaji, wala wanyang’anyi hawataurithi ufalme wa Mungu.” Nilianza kuacha mazoea yangu mabaya moja baada ya lingine. Niliacha kuiba. Niliacha kushirikiana na majambazi tuliofahamiana tangu utotoni. Kisha, kwa nguvu za Yehova, niliwafukuza wapenzi wangu wote.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA: Nimejitahidi sana kudhibiti hasira yangu na kujizuia nisiwafokee watoto wangu walipofanya makosa. (Waefeso 4:31) Mimi ninajaribu kusuluhisha mambo katika njia ya amani. Njia hiyo ya kuwasiliana imeleta matokeo mazuri na kutufanya tuwe na uhusiano wa karibu tukiwa familia.

Rafiki zangu wa zamani na pia majirani, wameona kwamba wanaweza kunitumaini. Nimekuwa mfanyakazi anayetumainiwa anayeweza kushughulikia bidhaa na pesa kwa unyoofu. Hivyo, ninaweza kujiruzuku ninapotumia wakati wangu mwingi kuwasaidia wengine wajifunze kuhusu Biblia. Ninakubaliana kabisa na maneno ya Methali 10:22: “Baraka ya Yehova—hiyo ndiyo hutajirisha, naye haongezi maumivu pamoja nayo.”

MAELEZO MAFUPI KUMHUSU

JINA: GLORIA ELIZARRARÁS DE CHOPERENA

UMRI: 37

NCHI: MEXICO

HISTORIA: ALIJARIBU KUJIUA

MAISHA YANGU YA ZAMANI: Nililelewa katika eneo la matajiri la Naucalpan, huko Mexico. Tangu nilipokuwa kijana nilikuwa mwasi na nilipenda kwenda kwenye karamu. Nilianza kuvuta sigara nilipokuwa na umri wa miaka 12, kutumia kileo nilipokuwa na umri wa miaka 14, na kutumia dawa za kulevya nilipokuwa na umri wa miaka 16. Miaka michache baadaye, niliondoka nyumbani. Wengi wa rafiki zangu walitoka katika familia zilizokuwa na matatizo, ambako walipigwa au kutukanwa. Ilionekana kwangu kwamba maisha hayakuwa na kusudi na nilijaribu mara mbili kujiua.

Nilipokuwa na umri wa miaka 19 nilianza kuwa mwanamitindo. Kwa sababu hiyo, nilishirikiana na wanasiasa na watu wengine mashuhuri. Mwishowe niliolewa na kupata watoto, lakini mimi ndiye nilifanya maamuzi yote ya familia. Pia niliendelea kuvuta sigara, kutumia kileo, na kushirikiana na watu mashuhuri. Nilitumia matusi na nilipenda kusema mizaha michafu. Nilikuwa na hasira kali.

Watu wengi niliochagua kushirikiana nao waliishi maisha kama hayo. Kwa maoni yao, ni kama nilikuwa na kila kitu. Lakini maisha yangu yaliendelea kuwa matupu, bila kusudi.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU: Nilianza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova mnamo 1998. Biblia ilinifundisha kwamba maisha yana kusudi. Nilijifunza kwamba Yehova Mungu anakusudia kuifanya dunia iwe Paradiso tena, kwamba atawafufua wafu, na kwamba ninaweza kuishi katika Paradiso hiyo.

Pia nilijifunza kwamba njia ya kuonyesha ninampenda Mungu ni kumtii. (1 Yohana 5:3) Mwanzoni haikuwa rahisi kufanya hivyo kwa sababu sikuwa nimewahi kukubali kuongozwa na mtu yeyote. Hata hivyo, mwishowe nilikubali kwamba siwezi kuendelea kuongoza maisha yangu mwenyewe. (Yeremia 10:23) Nilisali Yehova aniongoze. Nilimwomba anisaidie nipatanishe maisha yangu na viwango vyake na kuwafundisha watoto wangu kuishi kwa njia tofauti na jinsi nilivyoishi.

Ilikuwa vigumu sana kwangu kufanya mabadiliko yaliyohitajika, lakini nilianza kufuata shauri linalopatikana kwenye Waefeso 4:22-24: “Mnapaswa kuuondolea mbali utu wa zamani unaolingana na mwenendo wenu wa kwanza . . . na mnapaswa kuvaa utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli na ushikamanifu.” Ili nivae utu mpya nilipaswa kuacha mazoea mabaya kama vile kuvuta sigara, na nilipaswa kujifunza lugha mpya isiyo na matusi. Ilinichukua miaka mitatu hivi kufanya mabadiliko yaliyohitajiwa ili nibatizwe na kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova.

Kwa kuongezea, nilianza kuchukua kwa uzito jukumu langu nikiwa mke na mama. Nilianza kufuata shauri lililo kwenye 1 Petro 3:1, 2: “Ninyi wake, jitiisheni kwa waume zenu wenyewe, ili, ikiwa wowote si watiifu kwa lile neno, wavutwe bila neno kupitia mwenendo wa wake zao, kwa sababu wamekwisha kushuhudia kwa macho mwenendo wenu ulio safi kiadili pamoja na heshima kubwa.”

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA: Ninamshukuru sana Yehova kwa kuwa sasa ninajua kwamba maisha yana kusudi. Ninahisi kwamba sasa mimi ni mtu mzuri zaidi na ninaweza kuwalea watoto wangu kwa njia nzuri zaidi. Mara kwa mara, moyo wangu unanihukumu kwa sababu ya mambo niliyofanya zamani, lakini Yehova anaujua moyo wangu. (1 Yohana 3:19, 20) Bila shaka, kuishi kupatana na viwango vya Biblia kumenilinda nisipatwe na madhara na kumeniletea amani ya moyoni.

MAELEZO MAFUPI KUMHUSU

JINA: JAILSON CORREA DE OLIVEIRA

UMRI: 33

NCHI: BRAZILI

HISTORIA: MRAIBU WA KILEO NA DAWA ZA KULEVYA

MAISHA YANGU YA ZAMANI: Nilizaliwa huko Brazili, katika jiji la Baģe, lililo na watu 100,000 hivi, karibu na mpaka wa Brazili na Uruguai. Kazi kuu ya eneo hilo ilikuwa kulima na kufuga ng’ombe. Nililelewa katika wilaya maskini ambako magenge yaliendeleza jeuri, na vijana wengi walitumia kileo na dawa za kulevya.

Nilipomaliza shule, nilianza kutumia kileo, kuvuta bangi, na kusikiliza muziki wa heavy-metal. Sikuamini kwamba kuna Mungu. Nilihisi kwamba kuteseka na mvurugo uliopo ulimwenguni unathibitisha hakuna Mungu.

Nilikuwa mpiga-gitaa na mwandishi wa nyimbo na mara nyingi nyimbo zangu zilichochewa na kitabu cha Biblia cha Ufunuo. Bendi yangu haikufanikiwa kama nilivyotazamia, kwa hiyo nikaanza kutumia dawa kali za kulevya. Sikujali kama nitakufa kwa sababu ya dawa hizo. Wanamuziki wengi niliowahusudu walikufa kwa njia hiyo.

Nilimwomba nyanya yangu aliyenilea pesa za kununua dawa hizo za kulevya. Nilimdanganya kila aliponiuliza ningefanya nini na pesa hizo. Jambo baya hata zaidi ni kwamba niliwasiliana na pepo. Nilipendezwa sana na uchawi kwani nilifikiri utanisaidia kuandika nyimbo nzuri zaidi.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU: Nilipoanza kujifunza Biblia na kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova, mtazamo na mwelekeo wangu ulianza kubadilika. Pole kwa pole nilianza kuwa na tamaa ya kuishi na kuwa na furaha. Kwa sababu ya mtazamo huo mpya, niliamua kunyoa nywele zangu ndefu. Nilikuwa nimezifuga kama ishara ya uasi na kutoridhika. Kisha nilitambua kwamba ili nipate kibali cha Mungu, nilihitaji kuacha kutumia kileo vibaya, dawa za kulevya, na kuvuta sigara. Pia niliona uhitaji wa kubadili muziki nilioupenda.

Mara ya kwanza nilipohudhuria mkutano wa Mashahidi wa Yehova, niliona Andiko fulani ukutani. Lilikuwa andiko la Methali 3:5, 6 linalosema: “Mtegemee Yehova kwa moyo wako wote wala usitegemee uelewaji wako mwenyewe. Mtambue yeye katika njia zako zote, naye atanyoosha mapito yako.” Kufikiria kuhusu andiko hilo kulinihakikishia kwamba Yehova atanisaidia nibadili maisha yangu iwapo ningemruhusu.

Lakini, kubadili maisha ambayo nimekuwa nayo kwa muda mrefu na kuacha uraibu wa kileo na dawa za kulevya kulikuwa jambo gumu sana kama kukata mkono wangu. (Mathayo 18:8, 9) Hayo si mabadiliko ambayo ningefanya pole kwa pole. Nilijua kwamba njia hiyo haingefaa katika kisa changu. Hivyo nilihitaji kuacha mara moja. Pia niliepuka maeneo na watu ambao wangenivuta nifuatie maisha yangu za zamani yenye madhara.

Nilijifunza kujivunia mambo niliyotimiza kila siku, na kutokazia fikiria mambo yaliyonivunja moyo. Nilihisi kwamba lingekuwa pendeleo kwangu kuwa safi kimwili, kiadili, na kiroho machoni pa Yehova. Nilisali na Yehova akanisaidia nisirudie njia zangu za zamani bali nisonge mbele. Nyakati nyingine niliteleza. Lakini bado nilisisitiza nijifunze Biblia na mwalimu wangu, hata ingawa nyakati nyingine bado nilikuwa mchovu kutokana na kulewa sana.

Nilikubaliana na ukweli niliojifunza kumhusu Mungu katika Biblia, kama vile, yeye anatujali tukiwa watu mmoja-mmoja, kwamba ataharibu dini ya uwongo, na kwamba anaunga mkono kazi ya kuhubiri inayofanywa ulimwengu pote. (Mathayo 7:21-23; 24:14; 1 Petro 5:6, 7) Kweli hizo zote zilipatana na akili. Mwishowe, niliamua kujiweka wakfu kwa Mungu. Nilitaka kumshukuru kwa mambo yote aliyokuwa amenifanyia.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA: Sasa ninaona kwamba maisha yangu yana kusudi. (Mhubiri 12:13) Na badala ya kuwaomba tu washiriki wa familia pesa, sasa nimeweza kuwasaidia. Nilimweleza nyanya yangu mambo niliyokuwa nikijifunza katika Biblia, naye sasa amejiweka wakfu kwa Yehova. Washiriki kadhaa wa familia yetu na pia mtu mmoja aliyekuwa katika bendi yangu wamejiweka wakfu kwa Yehova.

Sasa nimeoa na mimi na mke wangu tunatumia wakati wetu mwingi kuwafundisha wengine Biblia. Ninaona kwamba nimethawabishwa sana kwa kuwa nimejifunza ‘kumtegemea Yehova kwa moyo wangu wote.’

[Blabu katika ukurasa wa 29]

“Pole kwa pole nilianza kuwa na tamaa ya kuishi na kuwa na furaha”