Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Wanaendelea Kumfuata Mwana-kondoo’

‘Wanaendelea Kumfuata Mwana-kondoo’

‘Wanaendelea Kumfuata Mwana-kondoo’

“Hao ndio wale wanaoendelea kumfuata Mwana-Kondoo popote anapoenda.”—UFU. 14:4.

1. Wanafunzi wa kweli wa Yesu walihisi namna gani kuhusu kumfuata?

BAADA ya miaka miwili na nusu hivi ya huduma yake, Yesu alikuwa “akifundisha katika kusanyiko la watu wote katika Kapernaumu.” “Wengi kati ya wanafunzi wake wakaenda zao kwenye mambo yaliyo nyuma wakawa hawatembei tena pamoja naye” kwa sababu waliona kwamba maneno yake yanashtua. Yesu alipowauliza mitume wake 12 ikiwa walitaka pia kwenda, Simoni Petro alimjibu hivi: “Bwana, tutaenda kwa nani? Wewe una maneno ya uzima wa milele; na sisi tumeamini na tumejua kwamba wewe ndiye Mtakatifu wa Mungu.” (Yoh. 6:48, 59, 60, 66-69) Wanafunzi wa kweli wa Yesu hawakuacha kumfuata. Baada ya kutiwa mafuta kwa roho takatifu, waliendelea kujitiisha kwa mwongozo wa Yesu.—Mdo. 16:7-10.

2. (a) “Mtumwa mwaminifu na mwenye busara” au ‘msimamizi mwaminifu’ ni nani? (b) Mtumwa huyo amejiwekea jinsi gani rekodi bora ya “kumfuata Mwana-Kondoo”?

2 Tunaweza kusema nini kuhusu Wakristo watiwa-mafuta katika nyakati zetu? Katika unabii wake kuhusu “ishara ya kuwapo [kwake] na ya umalizio wa mfumo wa mambo,” Yesu alikiita kikundi cha wafuasi wake waliotiwa mafuta kwa roho duniani kuwa “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” au “msimamizi-nyumba mwaminifu.” (Mt. 24:3, 45; Luka 12:42) Wakiwa kikundi, jamii hiyo ya mtumwa imeweka rekodi bora ya “kumfuata Mwana-Kondoo popote anapoenda.” (Soma Ufunuo 14:4, 5.) Washiriki wa jamii hiyo ni mabikira katika njia ya kiroho kwa kuwa hawajichafui na imani na mazoea ya “Babiloni Mkubwa,” milki ya ulimwenguni pote ya dini ya uwongo. (Ufu. 17:5) Mafundisho ya uwongo ‘hayakupatikana katika vinywa vyao,’ na ‘hawajatiwa dosari’ na ulimwengu wa Shetani. (Yoh. 15:19) Wakati ujao, watiwa-mafuta waliobaki duniani ‘watamfuata’ Mwana-Kondoo mpaka mbinguni.—Yoh. 13:36.

3. Kwa nini ni jambo la maana kwetu kuitumaini jamii ya mtumwa?

3 Yesu alimweka rasmi mtumwa mwaminifu na mwenye busara “juu ya watumishi wake wa nyumbani,” yaani, washiriki mmoja-mmoja wa jamii ya mtumwa, ili “awape chakula chao kwa wakati unaofaa.” Pia, amemweka rasmi mtumwa huyo “juu ya mali zake zote.” (Mt. 24:45-47) “Mali” hizo zinatia ndani hesabu inayoongezeka ya “umati mkubwa” wa “kondoo wengine.” (Ufu. 7:9; Yoh. 10:16) Je, washiriki mmoja-mmoja wa jamii ya watiwa-mafuta na “kondoo wengine” hawapaswi kumtumaini mtumwa aliyewekwa juu yao? Tuna sababu nyingi zinazoonyesha kwa nini jamii ya mtumwa inastahili kutumainiwa. Sababu mbili kuu ni: (1) Yehova anaitumaini jamii ya mtumwa. (2) Yesu pia anaitumaini jamii ya mtumwa. Acheni tuchunguze mambo yanayothibitisha kwamba Yehova Mungu na Yesu Kristo wanamtumaini kabisa mtumwa mwaminifu na mwenye busara.

Yehova Anamtumaini Mtumwa Huyo

4. Kwa nini tunaweza kutumaini chakula cha kiroho tunachopewa na mtumwa mwaminifu na mwenye busara?

4 Fikiria kile kinachomwezesha mtumwa mwaminifu na mwenye busara kuandaa chakula cha kiroho chenye kujenga na cha wakati unaofaa. Yehova anasema: “Nitakufanya uwe na ufahamu na kukufundisha katika njia unayopaswa kuiendea.” Anaongeza hivi: “Nitakupa shauri jicho langu likiwa linakutazama.” (Zab. 32:8) Ndiyo, Yehova anampa mwongozo mtumwa huyo. Kwa hiyo, tunaweza kutumaini kabisa ufahamu, uelewaji, na mwongozo wa Kimaandiko ambao tunapokea kutoka kwa mtumwa huyo.

5. Ni nini kinachoonyesha kwamba roho ya Mungu inaitia nguvu jamii ya mtumwa?

5 Yehova pia anabariki jamii ya mtumwa kwa roho yake takatifu. Ingawa roho ya Yehova haionekani, matokeo yake juu ya wale wanaoongozwa nayo yanaonekana wazi. Fikiria mambo ambayo mtumwa mwaminifu na mwenye busara ameweza kutimiza katika kutoa ushahidi ulimwenguni pote kuhusu Yehova Mungu, Mwana wake, na Ufalme. Waabudu wa Yehova wanatangaza kwa bidii ujumbe wa Ufalme katika visiwa na nchi zaidi ya 230. Je, huo si uthibitisho usioweza kupingwa unaoonyesha kwamba roho ya Mungu inamtia nguvu mtumwa huyo? (Soma Matendo 1:8.) Jamii ya mtumwa inalazimika kufanya maamuzi ya maana sana inapoandaa chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa kwa ajili ya watu wa Yehova ulimwenguni pote. Jamii hiyo inapofanya maamuzi hayo na kuyatekeleza, inaonyesha upendo, upole, na sifa nyingine za matunda ya roho.—Gal. 5:22, 23.

6, 7. Yehova anamtumaini mtumwa mwaminifu kwa kadiri gani?

6 Ili uelewe Yehova anamtumaini mtumwa mwaminifu kadiri gani, fikiria mambo ambayo amewaahidi washiriki wa jamii hiyo. Mtume Paulo aliandika hivi: “Tarumbeta italia, na wafu watafufuliwa wakiwa wasioweza kuharibika, nasi tutabadilishwa. Kwa maana huu ulio wa kuharibika lazima uvae kutoweza kuharibika, na huu unaoweza kufa lazima uvae kutoweza kufa.” (1 Kor. 15:52, 53) Wafuasi watiwa-mafuta wa Kristo, ambao wanamtumikia Mungu kwa uaminifu na kufa wakiwa na miili inayoharibika ya kibinadamu, wanafufuliwa katika hali bora zaidi kuliko viumbe wa roho huku wakiwa na uzima wa milele. Wanapewa hali ya kutoweza kufa, yaani, uzima usio na mwisho na hali ya kutoweza kuangamizwa. Kwa kuongezea, wanapokea hali ya kutoweza kuharibika, kwa kuwa wanapewa miili ambayo haiwezi kuoza na inaelekea kwamba miili hiyo ina uwezo wa kujiendeleza kuishi. Kitabu cha Ufunuo 4:4 kinasema kwamba wafufuliwa hao wameketi juu ya viti vya ufalme na wana mataji ya dhahabu juu ya vichwa vyao. Utukufu wa kifalme unawangojea Wakristo watiwa-mafuta. Lakini kuna mengi zaidi.

7 Andiko la Ufunuo 19:7, 8 linasema: “Ndoa ya Mwana-Kondoo imefika na mke wake amejitayarisha. Ndiyo, amepewa ruhusa ya kupambwa kitani bora, changavu, safi, kwa maana hicho kitani bora humaanisha matendo ya uadilifu ya watakatifu.” Yehova amewachagua Wakristo watiwa-mafuta kuwa bibi-arusi wa Mwana wake wakati ujao. Kutoweza kuharibika, kutoweza kufa, utukufu wa kifalme, na “ndoa ya Mwana-Kondoo” ni zawadi nzuri ajabu kama nini! Zawadi hizo zote zinathibitisha waziwazi kwamba Mungu anawatumaini watiwa-mafuta, “wanaoendelea kumfuata Mwana-Kondoo popote anapoenda.”

Yesu Anamtumaini Mtumwa Huyo

8. Yesu anaonyesha jinsi gani kwamba anawatumaini wafuasi wake waliotiwa mafuta kwa roho?

8 Ni mambo gani yanayothibitisha kwamba Yesu anawatumaini kabisa wafuasi wake waliotiwa mafuta kwa roho? Usiku wa mwisho wa maisha yake duniani, Yesu aliwapa ahadi mitume wake 11 waaminifu, alipowaambia hivi: “Ninyi ndio mmeshikamana nami katika majaribu yangu; nami ninafanya agano pamoja nanyi, sawa na vile Baba yangu alivyofanya agano pamoja nami, kwa ajili ya ufalme, ili mpate kula na kunywa mezani pangu katika ufalme wangu, na kuketi juu ya viti vya ufalme kuyahukumu makabila kumi na mawili ya Israeli.” (Luka 22:28-30) Agano ambalo Yesu alifanya wakati huo na wale 11 litawahusisha Wakristo wote watiwa-mafuta 144,000. (Luka 12:32; Ufu. 5:9, 10; 14:1) Je, Yesu angefanya agano la kushiriki mamlaka ya Ufalme pamoja nao ikiwa hangekuwa akiwatumaini?

9. ‘Mali zote za Kristo’ zinatia ndani nini?

9 Kwa kuongezea, Yesu Kristo amemweka rasmi mtumwa mwaminifu na mwenye busara “juu ya mali zake zote,” yaani, mali zote za Ufalme duniani. (Mt. 24:47) Mali hizo zinatia ndani vifaa vilivyo katika makao makuu ya ulimwenguni pote ya Mashahidi wa Yehova, ofisi za tawi katika nchi mbalimbali, na Majumba ya Kusanyiko na Majumba ya Ufalme ulimwenguni pote. Pia zinatia ndani kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme na kufanya wanafunzi. Je, kuna mtu yeyote anayeweza kumkabidhi mtu asiyemtumaini vitu vyake vyenye thamani ili avitunze na kuvitumia?

10. Ni nini kinachoonyesha kwamba Yesu Kristo yupo pamoja na wafuasi wake watiwa-mafuta?

10 Muda mfupi kabla ya kupanda mbinguni, Yesu aliyefufuliwa aliwatokea wanafunzi wake waaminifu na kuwaahidi hivi: “Tazama! mimi nipo pamoja nanyi siku zote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mt. 28:20) Je, Yesu ametimiza ahadi hiyo? Katika miaka 15 ambayo imepita, hesabu ya makutaniko ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote imeongezeka kutoka 70,000 mpaka zaidi ya 100,000, yaani, ongezeko la zaidi ya asilimia 40. Ni wanafunzi wangapi wapya ambao wameongezeka? Wanafunzi karibu milioni 4.5 wamebatizwa katika miaka 15 ambayo imepita, kwa wastani, hao ni wanafunzi zaidi ya 800 kila siku. Ongezeko hilo kubwa sana linaonyesha wazi kwamba Kristo anawaongoza wafuasi wake watiwa-mafuta katika mikutano yao ya kutaniko naye anawategemeza katika kazi yao ya kufanya wanafunzi.

Mtumwa Huyo Ni Mwaminifu na Mwenye Busara

11, 12. Mtumwa ameonyesha jinsi gani kwamba ni mwaminifu na mwenye busara?

11 Kwa kuwa Yehova Mungu na Yesu Kristo wanamtumaini kabisa mtumwa mwaminifu na mwenye busara, je, hatupaswi pia kumtumaini? Kwa kweli, mtumwa huyo ameonyesha kwamba yeye ni mwaminifu katika kutimiza kazi aliyopewa. Kwa mfano, gazeti la Mnara wa Mlinzi limekuwa likichapishwa kwa muda wa miaka 130. Mikutano na makusanyiko ya Mashahidi wa Yehova yanaendelea kutujenga kiroho.

12 Mtumwa mwaminifu ni mwenye busara pia kwa sababu hatendi kwa kimbelembele, hamtangulii Yehova, wala habaki nyuma wakati mwongozo wa Mungu kuhusiana na suala fulani unapokuwa wazi. Kwa mfano, viongozi wa dini za uwongo wanapounga mkono waziwazi au kimya-kimya uchoyo na mwenendo usio wa Kikristo wa watu wa ulimwengu na kuuona kuwa wa kawaida, yule mtumwa anatoa maonyo kuhusu mitego ya mfumo mwovu wa Shetani. Mtumwa huyo anaweza kutoa maonyo yenye hekima ya wakati unaofaa kwa sababu Yehova Mungu na Yesu Kristo wanambariki. Hivyo, tunapaswa kumtumaini kabisa mtumwa huyo. Hata hivyo, tunaweza kuonyesha jinsi gani kwamba tunamtumaini mtumwa mwaminifu na mwenye busara?

‘Nenda Pamoja’ na Watiwa-Mafuta Wanapomfuata Mwana-Kondoo

13. Kulingana na unabii wa Zekaria, tunaweza kuonyesha jinsi gani kwamba tunamtumaini mtumwa mwaminifu na mwenye busara?

13 Kitabu cha Biblia cha Zekaria kinasema kwamba “watu kumi” wanamkaribia “mtu aliye Myahudi” na kusema: “Tutakwenda pamoja nanyi.” (Soma Zekaria 8:23.) Kwa kuwa neno “nanyi” linatumiwa kumhusu “mtu aliye Myahudi,” hilo linamaanisha kwamba anawakilisha kikundi cha watu. Katika nyakati zetu, anawakilisha mabaki ya Wakristo waliotiwa mafuta kwa roho, sehemu ya “Israeli wa Mungu.” (Gal. 6:16) Wale “watu kumi kutoka katika lugha zote za mataifa” wanawakilisha umati mkubwa wa kondoo wengine. Wakristo watiwa-mafuta wanapomfuata Yesu popote anapoenda, umati mkubwa ‘unaenda pamoja’ na, au unafuatana na, mtumwa mwaminifu na mwenye busara. Washiriki wa umati mkubwa hawapaswi kamwe kuona haya au aibu kujitambulisha kuwa waandamani wa “washiriki wa mwito wa mbinguni.” (Ebr. 3:1) Yesu haoni aibu kuwaita watiwa-mafuta “ndugu” zake.—Ebr. 2:11.

14. Tunaweza kufanya nini ili kuwaunga mkono kwa ushikamanifu ndugu za Kristo?

14 Kwa maoni ya Yesu Kristo, wale wanaowaunga mkono kwa ushikamanifu ndugu zake wanamuunga yeye mkono. (Soma Mathayo 25:40.) Basi, wale walio na tumaini la kuishi duniani wanaweza kuwaunga mkono jinsi gani ndugu watiwa-mafuta wa Kristo? Hasa ni kwa kuwasaidia katika kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme. (Mt. 24:14; Yoh. 14:12) Hesabu ya watiwa-mafuta duniani imepungua kadiri ambavyo miaka imepita, lakini hesabu ya kondoo wengine imeongezeka. Wale walio na tumaini la kuishi duniani wanaposhiriki katika kazi ya kutoa ushahidi, ikiwezekana wakiwa wahubiri wa wakati wote, wanawasaidia wale waliotiwa mafuta kwa roho kutimiza kazi waliyopewa ya kufanya wanafunzi. (Mt. 28:19, 20) Hatupaswi kupuuza nafasi tulizo nazo za kuitegemeza kazi hiyo kwa kutoa michango ya kifedha kwa njia mbalimbali.

15. Wakristo mmoja-mmoja wanapaswa kuwa na maoni gani kuhusu maamuzi ya kitengenezo yanayofanywa na yule mtumwa na chakula cha kiroho cha wakati unaofaa ambacho anatoa?

15 Tukiwa Mkristo mmoja-mmoja, tuna maoni gani kuhusu chakula cha kiroho cha wakati unaofaa kinachotolewa na mtumwa mwaminifu kupitia vichapo vinavyotegemea Biblia na mikutano na makusanyiko ya Kikristo? Je, tunakula chakula hicho kwa uthamini na kutumia bila kukawia mambo tunayojifunza? Tunaitikia jinsi gani maamuzi ya kitengenezo yanayofanywa na yule mtumwa? Tunapotii kwa kupenda mwongozo unaotolewa tunaonyesha kwamba tuna imani katika mpango wa Yehova.—Yak. 3:17.

16. Kwa nini Wakristo wote wanapaswa kuwasikiliza ndugu za Kristo?

16 Yesu alisema: “Kondoo wangu huisikiliza sauti yangu, nami ninawajua, nao wananifuata.” (Yoh. 10:27) Ndivyo ilivyo na Wakristo watiwa-mafuta. Namna gani wale ‘wanaoenda pamoja’ nao? Ni lazima wao pia wamsikilize Yesu. Ni lazima wawasikilize pia ndugu zake kwa sababu wamekabidhiwa daraka kubwa la kushughulikia hali ya kiroho ya watu wa Mungu. Kuisikiliza sauti ya ndugu za Kristo kunatia ndani nini?

17. Kuisikiliza jamii ya mtumwa kunatia ndani nini?

17 Leo, mtumwa mwaminifu na mwenye busara anawakilishwa na Baraza Linaloongoza, ambalo linaongoza na kupanga kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme duniani pote. Washiriki wa Baraza Linaloongoza ni wazee wenye uzoefu, ambao wametiwa mafuta kwa roho. Tunaweza kusema kwamba wazee hao hasa ndio “wale ambao wanaongoza” katikati yetu. (Ebr. 13:7) Waangalizi hao watiwa-mafuta wana “mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana” kwa sababu wanawatunza watangazaji wa Ufalme karibu 7,000,000 ulimwenguni pote katika makutaniko zaidi ya 100,000. (1 Kor. 15:58) Kuisikiliza jamii ya mtumwa kunamaanisha kushirikiana kikamili na Baraza lake Linaloongoza.

Wale Wanaomsikiliza Yule Mtumwa Wanabarikiwa

18, 19. (a) Wale wanaomsikiliza mtumwa mwaminifu na mwenye busara wanabarikiwa jinsi gani? (b) Tunapaswa kuazimia kufanya nini?

18 Tangu alipowekwa rasmi, mtumwa mwaminifu na mwenye busara amekuwa ‘akileta wengi kwenye uadilifu.’ (Dan. 12:3) Watu hao walioletwa wanatia ndani wale walio na tumaini la kuokoka uharibifu wa mfumo huu mwovu wa mambo. Ni baraka kama nini kuwa na msimamo huo wa uadilifu mbele za Mungu!

19 Wakati ujao, wakati ‘lile jiji takatifu, Yerusalemu Jipya [lenye washiriki 144,000], litakaposhuka kutoka mbinguni kwa Mungu likiwa limetayarishwa kama bibi-arusi aliyepambwa kwa ajili ya mume wake,’ wale watakaokuwa wameisikiliza sauti ya mtumwa wake watapata baraka gani? Biblia inasema: “Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.” (Ufu. 21:2-4) Acheni tujitahidi kadiri tuwezavyo kumsikiliza Kristo na ndugu zake wenye kutumainika waliotiwa mafuta kwa roho.

Umejifunza Nini?

• Ni nini kinachoonyesha kwamba Yehova anamtumaini mtumwa mwaminifu na mwenye busara?

• Ni nini kinachoonyesha kwamba Yesu Kristo anaitumaini kabisa jamii ya mtumwa?

• Kwa nini tunapaswa kumtumaini yule msimamizi-nyumba mwaminifu?

• Tunaonyesha jinsi gani kwamba tunamtumaini mtumwa mwaminifu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 25]

Unajua Yehova amemchagua nani kuwa bibi-arusi wa Mwana wake wakati ujao?

[Picha katika ukurasa wa 26]

Yesu Kristo amemkabidhi mtumwa mwaminifu na mwenye busara “mali” zake

[Picha katika ukurasa wa 27]

Tunaposhiriki katika kazi ya kutoa ushahidi, tunawaunga mkono wale waliotiwa mafuta kwa roho