Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Siku Yangu Haikuwa Imefika”

“Siku Yangu Haikuwa Imefika”

“Siku Yangu Haikuwa Imefika”

Dereva wa lori kubwa la takataka alishindwa kulidhibiti. Lori hilo lilipanda kando ya barabara na kuwagonga wenzi wawili wa ndoa na mwanamume mwenye umri wa miaka 23. Kulingana na ripoti ya gazeti moja la jiji la New York, wenzi hao wa ndoa walikufa papo hapo na kijana huyo akapoteza fahamu. Alipopata fahamu na kuona kilichokuwa kimetukia, alijiambia hivi: ‘Siamini macho yangu. Mungu, tafadhali nisaidie nikabiliane na jambo hili.’ Kisha akasema, “Siku yangu haikuwa imefika.”

HUENDA umesikia kuhusu visa kama hivyo. Mtu anapoponea chupuchupu, watu wanasema, ‘Siku yake haikuwa imefika,’ lakini mtu anapokufa katika aksidenti isiyo ya kawaida, watu wanasema, ‘Siku yake ilikuwa imefika’ au ‘Ni mapenzi ya Mungu.’ Iwe watasema alikufa kwa sababu ya majaliwa, bahati, au yalikuwa mapenzi ya Mungu, wana maoni yaleyale. Watu wengi wanaamini kwamba mambo yanayowapata maishani na matokeo yake yameamuliwa mapema na hawawezi kubadili hali hiyo. Watu wamekuwa na maoni hayo tangu zamani na hayatokei tu mtu anapokufa au aksidenti inapotokea.

Kwa mfano, Wababiloni wa kale waliamini kwamba mambo ya wanadamu yanaongozwa na nyota na miendo yake. Kwa hiyo, walikuwa na kawaida ya kuchunguza anga ili kupata ishara za kuwaongoza. Wagiriki na Waroma waliabudu miungu ya kike ya majaliwa, ambayo nyakati nyingine ilionekana kuwa uwezo wao wa kuamua ikiwa watu wangekuwa na wakati ujao mzuri au mbaya ulizidi ule wa miungu yao mikuu, Zeu na Sumbula.

Katika nchi za Mashariki, Wahindu na Wabudha wanaamini kwamba mambo yanayompata mtu sasa ni matokeo ya mambo aliyofanya katika maisha yake ya zamani, na matendo yake ya sasa yataamua mambo yatakayompata katika maisha yake yanayofuata. Dini nyingine, kutia ndani dini nyingi zinazodai kuwa za Kikristo, zinakubaliana na fundisho hilo kuhusu maisha ya mtu yanapangiwa mapema.

Kwa hiyo, haishangazi kwamba hata katika kizazi hiki cha kisasa kinachoamini mambo hakika, watu wengi wanaamini kwamba hali zao maishani, shughuli zao za kila siku, na matokeo ya maisha yao yanaongozwa na majaliwa na hawawezi kufanya lolote kubadili hali. Je, wewe una maoni hayo? Je, kweli matukio katika maisha, kufanikiwa kwa mtu na kutofanikiwa, kuzaliwa na kufa, kumeamuliwa mapema? Je, maisha yako yanaongozwa na majaliwa? Acheni tuone jinsi Biblia inavyoweza kutusaidia kujibu maswali hayo.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 3]

Ken Murray/New York Daily News