Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sababu Tano za Kumwogopa Mungu na Si Mwanadamu

Sababu Tano za Kumwogopa Mungu na Si Mwanadamu

Sababu Tano za Kumwogopa Mungu na Si Mwanadamu

KIJANA huyo alifurahi na kushangaa. Hakutazamia jambo ambalo lilikuwa limetokea. Mazungumzo yake na Mashahidi wa Yehova wawili yalimfunza jambo jipya. Kwa miaka mingi alikuwa amejiuliza kwa nini Mungu anaruhusu watu wateseke, lakini sasa swali hilo lilikuwa limejibiwa kutoka kwa Biblia. Hakujua kwamba Biblia ina habari nyingi yenye thamani na yenye kugusa moyo.

Dakika chache baada ya wageni hao kuondoka, mwanamke aliyekuwa amemkodisha kijana huyo nyumba aliingia kwa fujo na kumwuliza hivi kwa hasira, “Hao ni akina nani?”

Akiwa ameshangaa, kijana huyo hakumjibu.

“Mimi ninajua watu hao ni akina nani,” mwanamke huyo akamfokea, “na ukiwakaribisha tena utahama na kutafuta nyumba kwingine!”

Alibamiza mlango na kuondoka.

Wafuasi wa Kweli wa Kristo Wanatazamia Upinzani

Jambo lililompata kijana huyo ni la kawaida. Neno la Mungu, Biblia, linaeleza hivi: “Wote wanaotamani kuishi kwa ujitoaji-kimungu katika ushirika na Kristo Yesu watateswa pia.” (2 Timotheo 3:12) Kwa kawaida Wakristo wa kweli hawapendwi na hawajawahi kupendwa. Kwa nini? Mtume Yohana aliwaambia hivi Wakristo wenzake: “Tunajua tunatokana na Mungu, lakini ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu.” Pia, Shetani Ibilisi anaelezwa kuwa “kama simba anayenguruma, akitafuta kummeza mtu.” (1 Yohana 5:19; 1 Petro 5:8) Kuogopa wanadamu ni moja kati ya silaha ambazo Shetani anatumia kwa mafanikio.

Hata Yesu Kristo, ambaye alifanya mambo mengi sana mema na hakufanya dhambi yoyote, alidhihakiwa na kuteswa. Alisema hivi: “Walinichukia bila sababu.” (Yohana 15:25) Usiku uliotangulia kifo chake, aliwatayarisha wafuasi wake kwa kuwaambia hivi: “Ikiwa ulimwengu unawachukia ninyi, mnajua kwamba umenichukia mimi kabla ya kuwachukia ninyi. Kumbukeni neno nililowaambia, Mtumwa si mkuu kuliko bwana wake. Ikiwa wamenitesa mimi, watawatesa ninyi pia.”—Yohana 15:18, 20.

Kwa sababu hiyo, watu wengi walisitasita kuchukua msimamo upande wa ibada ya kweli. Biblia inasema hivi kuhusu wale waliokuwa wakimtafuta Yesu pindi moja: “Bila shaka, hakuna aliyekuwa akisema juu yake hadharani kwa sababu ya kuwaogopa Wayahudi.” (Yohana 7:13; 12:42) Viongozi wa kidini wa siku yake walitisha kumfukuza kutoka kwenye sinagogi mtu yeyote aliyemwamini Kristo. Kwa sababu hiyo, watu wengi hawakuwa Wakristo kwa sababu ya kuwaogopa wanadamu.—Matendo 5:13.

Baadaye, kutaniko la Kikristo lilipoanzishwa, tunasoma kwamba kutaniko hilo lilipata “mateso makubwa” huko Yerusalemu. (Matendo 8:1) Kwa kweli, katika Milki yote ya Roma, Wakristo walikabiliana na mateso. Watu mashuhuri huko Roma walimwambia hivi mtume Paulo: “Kwa habari ya madhehebu hii tunajua kwamba kila mahali huwa inasemwa vibaya.” (Matendo 28:22) Naam, Wakristo wa kweli walipingwa sana.

Hata leo, Shetani bado anawazuia watu wengi wasiwe wafuasi wa kweli wa Kristo kwa kuwafanya wawaogope wanadamu. Watu wanyoofu wanaojifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova wanakabili upinzani au dhihaka shuleni, kazini, kutoka kwa majirani, au marafiki. Huenda wakaogopa kupoteza heshima, marafiki, au msaada wa kimwili. Katika maeneo fulani ya mashambani, wakulima wanaogopa kwamba huenda majirani wakakataa kuwasaidia kuvuna au kuwalinda wanyama wao. Hata hivyo, licha ya hayo, mamilioni wameazimia kumwiga Yesu Kristo kwa kumtegemea Mungu na kuishi kupatana na Neno la Mungu. Yehova amewabariki kwa kufanya hivyo.

Kwa Nini Umwogope Mungu, Si Mwanadamu

Biblia inatusihi tumwogope Mungu, si mwanadamu. Inasema: “Kumwogopa Yehova ni mwanzo wa hekima.” (Zaburi 111:10) Woga huo si hofu isiyofaa, bali ni woga wa kutompendeza Mpaji-Uhai wetu. Kumwogopa Mungu kunahusiana sana na kumpenda. Lakini kwa nini tunapaswa kumwogopa Mungu na si mwanadamu? Acheni tuchunguze sababu tano.

1 Yehova Ndiye Aliye Mkuu Zaidi. Yehova ana nguvu nyingi sana kuliko mwanadamu yeyote. Kwa kumwogopa Mungu, tunajitambulisha kuwa sisi tuko upande wa Mweza-Yote, ambaye kwake “mataifa ni kama tone kutoka katika ndoo.” (Isaya 40:15) Kwa kuwa Mungu ni mweza-yote, ana uwezo wa kushinda “silaha yoyote itakayofanywa juu” ya wale walio washikamanifu kwake. (Isaya 54:17) Na kwa kuwa yeye ndiye atakayeamua ni nani watakaopata uzima wa milele, ni jambo la hekima kutoruhusu chochote kituzuie kujifunza kumhusu yeye na kufanya mapenzi yake.—Ufunuo 14:6, 7.

2 Mungu atatusaidia na kutulinda. Biblia inasema hivi katika Methali 29:25: “Kutetemeshwa na wanadamu ndiko huleta mtego, lakini yeye anayemtegemea Yehova atalindwa.” Kumwogopa mwanadamu ni mtego kwa sababu kunaweza kutufanya tusijitambulishe waziwazi kwamba tunamwamini Mungu. Mungu anatuhakikishia hivi kuhusu nguvu zake za kuokoa: “Usiogope, kwa maana mimi nipo pamoja nawe. Usitazame huku na huku, kwa maana mimi ni Mungu wako. Nitakutia nguvu. Nitakusaidia kwelikweli. Nitakushika kwelikweli kwa mkono wangu wa kuume wa uadilifu.”—Isaya 41:10.

3 Mungu anawapenda wale wanaomkaribia. Mtume Paulo aliandika maneno haya yenye kugusa moyo: “Nimesadiki kwamba wala kifo wala uzima wala malaika wala serikali wala mambo yaliyopo sasa wala mambo yatakayokuja wala nguvu wala kimo wala kina wala uumbaji mwingine wowote havitaweza kututenga na upendo wa Mungu ulio katika Kristo Yesu Bwana wetu.” (Waroma 8:37-39) Tukijifunza kumtegemea na kumtii Mungu, tunaweza kufurahia kifungo kisichovunjika cha upendo pamoja na Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote. Hilo ni pendeleo kubwa kama nini!

4 Tunathamini sana mambo yote ambayo Mungu ametufanyia. Yehova ni Muumba wetu ambaye ametupa uhai. Zaidi ya hilo, mbali na kutuandalia mambo muhimu maishani, ametupa vitu ambavyo vinafanya maisha yawe yenye kupendeza. Kwa kweli, yeye ndiye Chanzo cha kila zawadi njema. (Yakobo 1:17) Daudi, mwanamume mwaminifu aliyethamini fadhili zenye upendo za Mungu aliandika hivi: “Wewe mwenyewe umefanya mambo mengi, Ee Yehova Mungu wangu, naam, kazi zako za ajabu na mawazo yako kutuelekea . . . Zimekuwa nyingi sana kuliko vile ninavyoweza kusimulia.”—Zaburi 40:5.

5 Huenda baadhi ya watu wanaotupinga wakabadilika. Unaweza kuwasaidia wale wanaokupinga kwa kushikilia msimamo wako na kuendelea kumwogopa na kumpenda Mungu. Fikiria watu wa jamaa ya Yesu. Mwanzoni hawakumwamini, bali walisema: “Amerukwa na akili.” (Marko 3:21; Yohana 7:5) Baadaye, baada ya Yesu kufa na kufufuliwa, wengi wao wakawa waamini. Yakobo na Yuda, ambao walikuwa ndugu wa kambo wa Yesu, hata waliandika sehemu fulani ya Biblia. Pia, Sauli aliyekuwa mpinzani mkali, baadaye alibadilika akawa mtume Paulo. Wengine ambao sasa wanatupinga wanaweza kuona kwamba tuna ukweli wa Biblia kwa sababu ya azimio letu imara la kudumu tukiwa waaminifu.—1 Timotheo 1:13.

Kwa mfano, Aberash, mwanamke mmoja anayeishi Afrika, alikuwa akisali apate kweli. Baada ya kuanza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova, alikabili upinzani mkali kutoka kwa washiriki wa familia yake na viongozi wa kidini. Baadhi ya watu wake wa ukoo, ambao walikuwa wameanza kujifunza, waliacha kwa sababu ya kuogopa wanadamu. Lakini Aberash alimwomba Mungu ampe nguvu na ujasiri na akabatizwa na kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Kulikuwa na matokeo gani? Wanane kati ya watu wake wa ukoo walipata ujasiri nao wakaanza tena kujifunza Biblia na wanafanya maendeleo makubwa ya kiroho.

Unaweza Kushinda Woga wa Mwanadamu

Ili uepuke kushindwa na woga wa mwanadamu, fanya yote unayoweza ili kuimarisha upendo wako kwa Mungu. Unaweza kufanya hivyo kwa kujifunza Biblia na kutafakari maandiko kama vile Waebrania 13:6, linalosema: “Yehova ni msaidizi wangu; sitaogopa. Mwanadamu anaweza kunitenda nini?” Usisahau sababu zinazoonyesha kwa nini kumwogopa Mungu ndilo jambo linalofaa na la hekima kuliko kumwogopa mwanadamu.

Pia, fikiria baraka nyingi unazopata kwa kufuata mambo unayojifunza katika Biblia. Unaweza kupata majibu yenye kuridhisha ya maswali muhimu maishani. Unaweza kupata hekima inayotumika ya kushughulikia hali ngumu maishani. Unaweza kuwa na tumaini zuri hata ingawa leo kuna hali zenye kutatanisha. Unaweza kumkaribia Mungu mweza-yote katika sala wakati wowote.

Mtume Yohana aliandika: “Ulimwengu unapitilia mbali na pia tamaa yake, lakini yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.” (1 Yohana 2:17) Sasa ndio wakati wa kusimama imara na kutembea kwa kumwogopa Mungu. Badala ya kushindwa na woga wa mwanadamu, unaweza kuchagua kutii himizo hili la Mungu: “Uwe na hekima, mwanangu, na kuufanya moyo wangu ushangilie, ili nipate kumjibu anayenidhihaki.” (Methali 27:11) Hilo ni pendeleo kubwa kama nini!

Kumbuka kwamba hakuna mwanadamu anayeweza kukupa kile ambacho Mungu atawapa wale wanaomwogopa: “Matokeo ya unyenyekevu na kumwogopa Yehova ni utajiri na utukufu na uzima.”—Methali 22:4.

[Picha katika ukurasa wa 14]

Kwa sababu ya ujasiri wake, wanane kati ya watu wa ukoo wa Aberash wanafurahia kujifunza Biblia