Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Mungu Anachukua Watoto Wawe Malaika Mbinguni?

Je, Mungu Anachukua Watoto Wawe Malaika Mbinguni?

Wasomaji Wetu Wanauliza

Je, Mungu Anachukua Watoto Wawe Malaika Mbinguni?

Mtoto anapokufa, huenda marafiki wa familia iliyofiwa wakajaribu kuwafariji kwa kusema kwamba, “Mungu alihitaji malaika mwingine mbinguni.” Je, kwa maoni yako, hilo linapatana na akili?

Ikiwa ni kweli kwamba Mungu anasababisha watoto wafe kwa sababu anahitaji malaika zaidi mbinguni, hilo lingeonyesha kwamba yeye hana hisia, na ni mkatili. Hata hivyo, Biblia inasema jambo tofauti. (Ayubu 34:10) Baba mwenye huruma hawezi kumchukua mtoto kutoka kwa wazazi wake ili tu aongeze idadi ya washiriki wa familia yake. Hata hivyo, hakuna mzazi wa kibinadamu aliye na huruma zaidi ya Yehova ambaye sifa yake kuu ni upendo. (1 Yohana 4:8) Upendo wake mwingi hauwezi kumruhusu atende kwa ukatili hivyo.

Jiulize, ‘Je, Mungu anahitaji malaika zaidi mbinguni?’ Biblia inasema kwamba utendaji wote wa Mungu ni mwema na mkamilifu. (Kumbukumbu la Torati 32:4) Kazi yake ya kuumba mamilioni ya malaika ilikuwa kamilifu kabisa, na hakukuwa na upungufu wowote. (Danieli 7:10) Je, Mungu alifanya makosa alipokadiria idadi ya malaika aliohitaji? Haiwezekani! Kwa kweli, Mungu Mweza-Yote hawezi kufanya kosa kama hilo. Ni kweli kwamba Yehova amechagua wanadamu fulani wawe viumbe wa roho wakiwa sehemu ya Ufalme wake wa kimbingu, lakini wanadamu hao hawawezi kuwa watoto wachanga wanapokufa.—Ufunuo 5:9, 10.

Sababu nyingine kwa nini Mungu hawezi kuwachukua watoto kutoka duniani wawe malaika mbinguni ni kwamba hilo halingepatana na kusudi lake la awali kuelekea watoto. Katika bustani ya Edeni, Mungu aliwaambia Adamu na Hawa: “Zaeni, muwe wengi, mjaze dunia na kuitiisha.” (Mwanzo 1:28) Watoto ni zawadi kutoka kwa Mungu, na alifanya wanadamu wawe na uwezo wa kupata watoto ili kutimiza kusudi lake la awali la kuijaza dunia familia ya watu waadilifu. Hakukusudia kamwe watoto wafe kisha wageuzwe kuwa viumbe vya roho. Biblia inasema wazi kwamba watoto ni “urithi kutoka kwa Yehova.” (Zaburi 127:3) Je, Yehova, Mungu mwenye upendo, anaweza kuwanyang’anya wazazi zawadi ambazo amewapa? La hasha!

Kifo cha mtoto kinaleta huzuni, uchungu, na maumivu. Basi wazazi waliofiwa wanaweza kuwa na tumaini gani? Biblia inaahidi kwamba Mungu atafufua mamilioni ya watu katika paradiso papa hapa duniani. Wazia watoto wenye afya wakiwa wamefufuliwa na kukutanishwa tena na wapendwa wao. (Yohana 5:28, 29) Ni mapenzi ya Mungu kwamba vijana wakue, wafurahie maisha, na kujifunza kumhusu Mungu na kusudi lake kwa dunia. Hivyo, watoto ambao wamekufa si malaika mbinguni bali wanangojea kufufuliwa katika paradiso duniani. Wakati huo, chini ya utunzaji wenye upendo wa Muumba wetu, vijana kwa wazee watafurahia kumwabudu Yehova Mungu kwa umilele wote.