Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kaza Macho Yako Kwenye Tuzo

Kaza Macho Yako Kwenye Tuzo

Kaza Macho Yako Kwenye Tuzo

“Ninafuatilia kuelekea ule mradi kwa ajili ya tuzo.”—FLP. 3:14.

1. Mtume Paulo aliahidiwa tuzo gani?

MTUME Paulo, ambaye aliitwa pia Sauli wa Tarso, alizaliwa katika familia maarufu. Gamalieli, yule mwalimu mashuhuri wa Sheria ndiye aliyemwelimisha katika dini ya mababu zake. (Mdo. 22:3) Paulo angekuwa na kazi nzuri sana; lakini aliacha dini yake na kuwa Mkristo. Alitazamia kwa hamu tuzo au zawadi ambayo aliahidiwa ya uzima wa milele, yaani, kuwa mfalme asiyeweza kufa na kuhani katika Ufalme wa mbinguni wa Mungu. Ufalme huo utatawala juu ya dunia ambayo itakuwa paradiso.—Mt. 6:10; Ufu. 7:4; 20:6.

2, 3. Paulo alithamini kadiri gani tuzo ya kuishi mbinguni?

2 Paulo alionyesha jinsi alivyothamini sana tuzo hiyo, aliposema hivi: “Vitu vilivyokuwa faida kwangu, hivyo nimeviona kuwa hasara kwa sababu ya Kristo. Kwa hiyo, kwa kweli naviona vitu vyote kuwa hasara kwa sababu ya thamani bora zaidi ya kumjua Kristo Yesu Bwana wangu. Kwa sababu yake nimekubali hasara ya vitu vyote nami naviona kuwa takataka nyingi.” (Flp. 3:7, 8) Baada ya kujifunza kweli kuhusu kusudi la Yehova kwa ajili ya wanadamu, Paulo aliona mambo ambayo watu wengi wanayaona kuwa ya maana, yaani, cheo, utajiri, kazi nzuri, na umaarufu, kuwa takataka.

3 Kuanzia wakati huo, Paulo alihangaikia hasa ujuzi wenye thamani kuhusu Yehova na Kristo. Yesu alisema hivi kuhusu ujuzi huo aliposali kwa Mungu: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.” (Yoh. 17:3) Tamaa ya Paulo ya kupata uzima wa milele inaonekana katika maneno yake yaliyo kwenye Wafilipi 3:14: “Ninafuatilia kuelekea ule mradi kwa ajili ya tuzo la mwito wa Mungu wa kwenda juu kwa njia ya Kristo Yesu.” Naam, alikaza macho yake kwenye tuzo ya uzima wa milele mbinguni akiwa sehemu ya serikali ya Ufalme wa Mungu.

Kuishi Milele Duniani

4, 5. Mamilioni ya watu wanaofanya mapenzi ya Mungu leo watapata tuzo gani?

4 Wengi wa wale wanaochagua kufanya mapenzi ya Mungu, wanapaswa kujitahidi kupata tuzo ya uzima wa milele katika ulimwengu mpya wa Mungu. (Zab. 37:11, 29) Yesu alithibitisha kwamba hilo ni tumaini hakika. Alisema hivi: “Wenye furaha ni wale walio na tabia-pole, kwa kuwa watairithi dunia.” (Mt. 5:5) Kama Zaburi 2:8 inavyoonyesha, Yesu hasa ndiye atakayeirithi dunia, naye atatawala pamoja na wengine 144,000 mbinguni. (Dan. 7:13, 14, 22, 27) Wale kondoo wengine watakaoishi duniani ‘watarithi’ makao ya kidunia ya Ufalme ‘uliotayarishwa kwa ajili yao tangu kuwekwa msingi wa ulimwengu.’ (Mt. 25:34, 46) Na tunahakikishiwa kwamba mambo yote hayo yatatukia kwa sababu Mungu, ambaye ameyaahidi, ‘hawezi kusema uwongo.’ (Tito 1:2) Tunaweza kuwa na uhakika kwamba ahadi za Mungu zitatimia kama Yoshua alivyokuwa na uhakika alipowaambia Waisraeli hivi: “Halikukosa kutimia hata neno moja kati ya maneno yote mema ambayo Yehova Mungu wenu amewaambia ninyi. Yote yametimia kwenu. Halikukosa kutimia hata neno moja kati ya hayo.”—Yos. 23:14.

5 Maisha katika ulimwengu mpya wa Mungu hayatakuwa kama maisha ya sasa yenye kuvunja moyo. Yatakuwa tofauti sana: hakutakuwa na vita, uhalifu, umaskini, ukosefu wa haki, ugonjwa, na kifo. Wakati huo, watu watakuwa na afya kamilifu na wataishi katika dunia iliyogeuzwa kuwa paradiso. Maisha hayo yatakuwa yenye kuridhisha sana hata kupita matarajio yetu. Ndiyo, kila siku watu watakuwa na furaha tele. Hiyo ni tuzo bora kama nini!

6, 7. (a) Yesu alionyesha jinsi gani mambo tunayoweza kutarajia yatukie katika ulimwengu mpya wa Mungu? (b) Ni kwa njia gani wafu pia watapewa nafasi ya kuanza maisha mapya?

6 Yesu alipokuwa duniani, alitiwa nguvu na roho takatifu ya Mungu ili kuonyesha mambo mazuri ajabu yatakayotukia duniani pote katika ulimwengu mpya. Kwa mfano, Yesu alimwambia mwanamume aliyekuwa amepooza kwa miaka 38 atembee. Biblia inasema mwanamume huyo alianza kutembea. (Soma Yohana 5:5-9.) Pindi nyingine, Yesu alikutana na “mtu aliyekuwa kipofu tangu kuzaliwa” naye akamponya. Baadaye, mtu huyo ambaye hapo mwanzoni alikuwa kipofu aliulizwa ni nani Aliyemponya, naye akajibu hivi: “Kutoka zamani za kale haijasikiwa kamwe kwamba mtu yeyote alifungua macho ya mtu aliyezaliwa akiwa kipofu. Kama mtu huyu hangekuwa ametoka kwa Mungu, hangeweza kufanya lolote.” (Yoh. 9:1, 6, 7, 32, 33) Yesu alifanya yote hayo kwa sababu alipewa nguvu na Mungu. Kila mahali alipoenda, Yesu ‘aliwaponya wale waliohitaji kuponywa.’—Luka 9:11.

7 Zaidi ya kuwaponya wagonjwa na walemavu, Yesu aliwafufua wafu pia. Kwa mfano, msichana mmoja mwenye umri wa miaka 12 alikufa na wazazi wake wakahuzunika sana. Lakini Yesu alisema hivi: “Mwanamwali, ninakuambia, Simama!” Naye akasimama! Je, unaweza kuwazia jinsi wazazi wake na wengine waliokuwa hapo walivyohisi? (Soma Marko 5:38-42.) Katika ulimwengu mpya wa Mungu, kutakuwa na “shangwe kubwa” mabilioni ya watu watakapofufuliwa, kwa maana “kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.” (Mdo. 24:15; Yoh. 5:28, 29) Watapewa nafasi ya kuanza maisha mapya na tazamio la kuishi kuanzia wakati huo na kuendelea, ndiyo, hata milele.

8, 9. (a) Wakati wa Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo, ni nini kitakachotukia kuelekea dhambi tuliyorithi kutoka kwa Adamu? (b) Wafu watahukumiwa kwa msingi gani?

8 Wale watakaofufuliwa watapewa nafasi ya kupata uzima. Hawatahukumiwa kwa sababu ya dhambi walizofanya kabla ya kufa. (Rom. 6:7) Wakati wa Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo, faida za dhabihu ya fidia zitakapotumiwa, raia watiifu wa Ufalme watafikia ukamilifu, na mwishowe watawekwa huru kabisa kutoka katika matokeo mabaya yote ya dhambi ya Adamu. (Rom. 8:21) Yehova “atameza kifo milele, na Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova hakika atafuta machozi katika nyuso zote.” (Isa. 25:8) Pia, Neno la Mungu linasema kwamba ‘vitabu vya kukunjwa vitafunguliwa,’ kuonyesha kwamba wale wanaoishi wakati huo watapewa habari mpya. (Ufu. 20:12) Dunia itakapokuwa ikigeuzwa kuwa paradiso, “wakaaji wa nchi yenye kuzaa hakika watajifunza uadilifu.”—Isa. 26:9.

9 Wale watakaofufuliwa watahukumiwa, si kwa msingi wa dhambi waliyorithi kutoka kwa Adamu, bali kwa msingi wa mambo ambayo wao wenyewe wataamua kutenda. Andiko la Ufunuo 20:12 linasema: “Wafu wakahukumiwa kutokana na mambo yale yaliyoandikwa katika vile vitabu kulingana na matendo yao,” yaani, mambo watakayotenda baada ya kufufuliwa. Hilo linaonyesha vizuri kama nini haki, rehema, na upendo wa Yehova! Zaidi ya hayo, mambo yenye kuumiza yaliyowapata maishani katika ulimwengu huu wa kale “hayatakumbukwa akilini, wala hayataingia moyoni.” (Isa. 65:17) Wakiwa na habari mpya zenye kujenga na maisha yaliyojaa mambo mazuri, hawatataabishwa tena na mambo mabaya ya zamani. Mambo hayo ya zamani yatasahauliwa. (Ufu. 21:4) Itakuwa hivyo pia kwa “umati mkubwa,” ambao utaokoka Har–Magedoni.—Ufu. 7:9, 10, 14.

10. (a) Eleza jinsi ambavyo maisha yatakuwa katika ulimwengu mpya wa Mungu. (b) Ni jambo gani linaloweza kukusaidia kukaza macho yako kwenye tuzo?

10 Katika ulimwengu mpya wa Mungu, watu wataishi bila kuwa wagonjwa tena au kufa. “Hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’” (Isa. 33:24) Mwishowe, wakaaji wa dunia mpya wataamka kila asubuhi wakiwa na afya kamilifu, wakisisimuka huku wakitazamia siku nyingine yenye kufurahisha. Watatazamia kazi yenye kuridhisha na kushirikiana na wengine wanaowajali. Kwa kweli, maisha hayo ni tuzo bora kama nini! Tunakuomba ufungue Biblia yako ili usome unabii wa Isaya 33:24 na 35:5-7. Jaribu kuwazia ukiwa katika hali hizo. Hilo litakusaidia kukaza macho yako kwenye tuzo.

Watu Walioacha Kukaza Macho Kwenye Tuzo

11. Eleza mwanzo mzuri wa utawala wa Sulemani.

11 Baada ya kujifunza kuhusu tuzo hiyo, tunapaswa kufanya bidii sana kuendelea kukaza macho yetu kwenye tuzo hiyo kwa sababu tunaweza kuacha kuikazia macho. Kwa mfano, Sulemani alipoanza kutawala akiwa mfalme katika Israeli la kale, alimwomba Mungu kwa unyenyekevu ampe uelewaji na utambuzi ili awahukumu watu Wake kwa njia inayofaa. (Soma 1 Wafalme 3:6-12.) Biblia inasema, “Mungu akaendelea kumpa Sulemani hekima na uelewaji kwa wingi sana.” Kwa kweli, “hekima ya Sulemani ilikuwa pana zaidi kuliko hekima ya watu wengine wote wa Mashariki na kuliko hekima yote ya Misri.”—1 Fal. 4:29-32.

12. Yehova aliwapa onyo gani wale ambao wangekuwa wafalme katika Israeli?

12 Hata hivyo, mapema Yehova alikuwa ameonya kwamba mtu yeyote aliyekuwa mfalme hakupaswa ‘kuongeza farasi kwa ajili yake’ na hakupaswa ‘kuzidisha wake kwa ajili yake, ili moyo wake usigeuke kando.’ (Kum. 17:14-17) Ikiwa mfalme angejiongezea farasi, angeonyesha kwamba anategemea nguvu za kijeshi ili kulinda taifa badala ya kumtegemea Yehova, ambaye ndiye Mlinzi. Na kujiongezea wake kungekuwa hatari kwa sababu wengine wao wangetoka katika mataifa jirani ya kipagani yaliyojihusisha na ibada ya uwongo, na wake hao wangemgeuza mfalme huyo kutoka kwenye ibada ya kweli ya Yehova.

13. Kwa nini Sulemani aliacha kukazia macho baraka alizokuwa amepewa?

13 Sulemani hakutii maonyo hayo. Badala yake, alifanya mambo yaleyale ambayo Yehova aliwakataza wafalme wasifanye. Alijikusanyia maelfu ya farasi na wapanda-farasi. (1 Fal. 4:26) Pia, akawa na wake 700 na masuria 300, wengi wao kutoka mataifa jirani ya kipagani. Wanawake hao ‘waliugeuza moyo wake ukaifuata miungu mingine; na moyo wake haukuwa mkamilifu kwa Yehova.’ Sulemani alijihusisha na ibada ya uwongo yenye kuchukiza ya mataifa ya kipagani ambayo wake zake wa kigeni walimshawishi kufuata. Hivyo, Yehova alisema kwamba ‘angeurarua ufalme’ kutoka kwa Sulemani.—1 Fal. 11:1-6, 11.

14. Kutotii kwa Sulemani na kwa taifa la Israeli kulikuwa na matokeo gani?

14 Sulemani hakukazia tena fikira pendeleo lake lenye thamani la kumwakilisha Mungu wa kweli. Mfalme huyo alijihusisha sana na ibada ya uwongo. Baada ya muda, taifa lote likaasi imani, nalo likaharibiwa mwaka wa 607 K.W.K. Hata ingawa baadaye Wayahudi walirudisha ibada ya kweli, karne nyingi baadaye Yesu alilazimika kutangaza hivi: “Ufalme wa Mungu utachukuliwa kutoka kwenu na kupewa taifa lenye kuzaa matunda yake.” Hilo ndilo lililotukia. Yesu alitangaza: “Tazama! Nyumba yenu mmeachiwa hali ya ukiwa.” (Mt. 21:43; 23:37, 38) Kwa sababu ya kukosa uaminifu, taifa hilo lilipoteza pendeleo kubwa la kumwakilisha Mungu wa kweli. Mwaka wa 70 W.K., majeshi ya Roma yaliharibu Yerusalemu na hekalu, na wengi kati ya Wayahudi waliobaki wakawa watumwa.

15. Taja mifano ya watu walioacha kukazia fikira jambo ambalo lilikuwa la maana zaidi.

15 Yuda Iskariote alikuwa mmoja wa mitume 12 wa Yesu. Yuda alisikia mafundisho mazuri ya Yesu na kuona miujiza aliyofanya kwa msaada wa roho takatifu ya Mungu. Hata hivyo, Yuda hakuulinda moyo wake. Alikuwa amekabidhiwa sanduku ambalo lilikuwa na pesa za Yesu na za wale mitume 12. Lakini “alikuwa mwizi na alikuwa na sanduku la pesa na alikuwa akichukua pesa zilizowekwa ndani yake.” (Yoh. 12:6) Pupa yake ilionekana wazi kabisa alipopanga njama na wakuu wa makuhani wanafiki ili kumsaliti Yesu kwa vipande 30 vya fedha. (Mt. 26:14-16) Mtu mwingine aliyekosa kukazia fikira mambo ya maana zaidi ni Dema, mwandamani wa mtume Paulo. Dema hakuulinda moyo wake. Paulo alisema hivi: “Dema ameniacha kwa sababu aliupenda mfumo wa mambo wa sasa.”—2 Tim. 4:10; soma Methali 4:23.

Somo Tunalojifunza

16, 17. (a) Tunakabili upinzani wenye nguvu kadiri gani? (b) Ni nini kinachoweza kutusaidia kushinda kizuizi chochote ambacho Shetani anatuwekea?

16 Watumishi wote wa Mungu wanapaswa kufikiria kwa uzito mifano inayotajwa katika Biblia, kwa kuwa tunaambiwa hivi: “Basi mambo hayo yaliendelea kuwapata kuwa vielelezo, nayo yaliandikwa ili kuwa onyo kwetu sisi ambao tumefikiwa na miisho ya mifumo ya mambo.” (1 Kor. 10:11) Leo, tunaishi katika siku za mwisho za mfumo huu mwovu wa mambo.—2 Tim. 3:1, 13.

17 Shetani Ibilisi, “mungu wa mfumo huu wa mambo,” anajua kwamba “ana kipindi kifupi cha wakati.” (2 Kor. 4:4; Ufu. 12:12) Atafanya yote anayoweza kuwashawishi watumishi wa Yehova kuvunja utimilifu wao wa Kikristo. Shetani anaongoza ulimwengu huu, kutia ndani njia za ulimwengu za kusambaza propaganda. Hata hivyo, watu wa Yehova wana kitu fulani chenye nguvu hata zaidi, yaani, “nguvu zinazopita zile za kawaida.” (2 Kor. 4:7) Tunaweza kutegemea nguvu hizo kutoka kwa Mungu zitusaidie kushinda kizuizi chochote ambacho Shetani anatuwekea. Hivyo, tunahimizwa tusali kwa ukawaida, tukiwa na uhakika kwamba Yehova ‘atawapa roho takatifu wale wanaomwomba.’—Luka 11:13.

18. Tunapaswa kuwa na mtazamo gani kuelekea ulimwengu huu?

18 Tunaimarishwa pia tunapojua kwamba mfumo wote wa Shetani utaharibiwa hivi karibuni, lakini Wakristo wa kweli wataokoka. “Ulimwengu unapitilia mbali na pia tamaa yake, lakini yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.” (1 Yoh. 2:17) Kwa hiyo, si jambo la hekima hata kidogo kwa mtumishi yeyote wa Mungu kufikiri mfumo huu wa mambo una kitu chenye thamani ya kudumu kuliko uhusiano wake pamoja na Yehova. Ulimwengu huu unaotawaliwa na Shetani ni kama meli inayozama. Yehova amefanyiza kutaniko la Kikristo ambalo ni kama mashua ya kuwaokolea watumishi wake waaminifu. Watumishi hao wanaposonga kuingia katika ulimwengu mpya, wanaweza kuwa na uhakika kabisa katika ahadi hii: “Watenda-maovu watakatiliwa mbali, bali wale wanaomtumaini Yehova ndio watakaoimiliki dunia.” (Zab. 37:9) Hivyo basi, kaza macho yako kwenye tuzo hiyo bora!

Je, Unakumbuka?

• Paulo alikuwa na maoni gani kuhusu tuzo ambayo aliahidiwa?

• Wale watakaoishi milele duniani watahukumiwa kwa msingi gani?

• Ni hatua gani ya hekima unayopaswa kuchukua sasa?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 12, 13]

Unaposoma masimulizi ya Biblia, je, unajiwazia ukipata ile tuzo?