Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Kesheni’

‘Kesheni’

‘Kesheni’

‘Mwisho wa mambo yote umekaribia. Kesheni kuhusiana na sala.’—1 PET. 4:7.

1. Ni nini kilichokuwa kichwa cha mafundisho ya Yesu?

YESU KRISTO alipokuwa duniani, kichwa cha mafundisho yake kilikuwa Ufalme wa Mungu. Kupitia Ufalme huo, Yehova atatetea enzi yake kuu ya ulimwengu wote na kutakasa jina lake. Hivyo, Yesu aliwafundisha wanafunzi wake kusali hivi kwa Mungu: “Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.” (Mt. 4:17; 6:9, 10) Hivi karibuni serikali hiyo ya Ufalme itakomesha ulimwengu wa Shetani na kuhakikisha kwamba mapenzi ya Mungu yanatendeka duniani pote. Kama Danieli alivyotabiri, Ufalme wa Mungu “utazivunja na kuzikomesha falme hizi zote [za leo], nao utasimama mpaka wakati usio na kipimo.”—Dan. 2:44.

2. (a) Wafuasi wa Yesu wangejua jinsi gani kwamba kuwapo kwake katika mamlaka ya Ufalme kumeanza? (b) Ishara hiyo ingeonyesha jambo gani lingine?

2 Kwa kuwa kuja kwa Ufalme wa Mungu kulikuwa muhimu sana kwa wafuasi wa Yesu, walimuuliza hivi: “Ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?” (Mt. 24:3) Ishara yenye kuonekana ingetolewa kwa sababu watu walio duniani hawangeona kuwapo kwa Kristo katika mamlaka ya Ufalme. Ishara hiyo ingehusisha mambo mbalimbali yaliyotabiriwa katika Maandiko. Hivyo, wafuasi wa Yesu wanaoishi wakati huo wangetambua kwamba tayari ameanza kutawala mbinguni. Pia, huo ungekuwa mwanzo wa kipindi cha wakati ambacho kinaitwa katika Biblia “siku za mwisho” za mfumo mwovu wa mambo uliopo duniani sasa.—2 Tim. 3:1-5, 13; Mt. 24:7-14.

Kesheni Katika Siku za Mwisho

3. Kwa nini Wakristo wanahitaji kukesha?

3 Mtume Petro aliandika hivi: “Mwisho wa mambo yote umekaribia. Kwa hiyo, iweni na utimamu wa akili, na kukesha kuhusiana na sala.” (1 Pet. 4:7) Wafuasi wa Yesu wanahitaji kukesha na kutazama matukio ya ulimwengu ambayo yanaonyesha kwamba kuwapo kwake katika mamlaka ya Ufalme kumeanza. Na wanahitaji kukesha hata zaidi kadiri mwisho wa mfumo huu mwovu wa mambo unavyokaribia. Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Endeleeni kukesha, kwa maana hamjui bwana wa nyumba anakuja wakati gani [kutekeleza hukumu juu ya ulimwengu wa Shetani].”—Marko 13:35, 36.

4. Eleza tofauti iliyopo kati ya mtazamo wa watu ambao ni sehemu ya ulimwengu wa Shetani na mtazamo wa watumishi wa Yehova. (Tia ndani sanduku.)

4 Watu kwa ujumla wako chini ya utawala wa Shetani, nao hawatambui maana ya matukio ya ulimwengu. Hawatambui kuwapo kwa Kristo katika mamlaka ya Ufalme. Lakini wafuasi wa kweli wa Kristo wamekesha na wametambua maana halisi ya mambo ambayo yalitukia katika karne iliyopita. Tangu mwaka wa 1925, Mashahidi wa Yehova wametambua kwamba Vita vya Kwanza vya Ulimwengu na matukio yaliyofuata ni uthibitisho hakika wa kwamba kuwapo kwa Kristo katika mamlaka ya Ufalme mbinguni kulianza mwaka wa 1914. Hivyo, siku za mwisho za mfumo huu mwovu wa mambo unaotawaliwa na Shetani zilikuwa zimeanza. Watu wengi ambao wanatambua mambo kwa wepesi wanaona kwamba kuna tofauti kubwa kati ya kipindi cha kabla ya Vita vya Kwanza vya Ulimwengu na kipindi kilichofuata.—Ona sanduku “Kipindi cha Msukosuko Kilianza.”

5. Kwa nini ni jambo la maana kuendelea kukesha?

5 Kwa karibu karne moja sasa, matukio yenye kuogopesha ambayo yametukia ulimwenguni pote yameonyesha kwamba tunaishi katika siku za mwisho. Kuna muda mfupi sana ambao umebaki kabla ya Yehova kumpa Kristo amri ya kuongoza majeshi yenye nguvu ya kimalaika kuharibu ulimwengu wa Shetani. (Ufu. 19:11-21) Wakristo wa kweli wanaambiwa waendelee kukesha. Kwa hiyo, ni jambo la maana sana kuendelea kufanya hivyo tunapotazamia mwisho wa mfumo huu. (Mt. 24:42) Ni lazima tuendelee kuwa macho na kutimiza kazi fulani hususa duniani pote, chini ya mwelekezo wa Kristo.

Kazi ya Duniani Pote

6, 7. Katika siku za mwisho kumekuwa na ongezeko gani katika kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme?

6 Kazi ambayo watumishi wa Yehova wanapaswa kufanya ilitabiriwa kuwa sehemu ya ishara yenye mambo mbalimbali inayoonyesha kwamba tunaishi katika siku za mwisho za mfumo huu mwovu wa mambo. Yesu alifafanua kazi hiyo ya ulimwenguni pote alipotaja mambo mbalimbali ambayo yangetukia wakati wa mwisho. Katika unabii wake, alitaja pia maneno haya ya maana: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.”—Mt. 24:14.

7 Fikiria mambo fulani ya hakika yanayohusiana na maneno hayo ya unabii wa Yesu. Hesabu ya watu wanaotangaza habari njema ilikuwa ndogo sana siku za mwisho zilipoanza mwaka wa 1914. Kufikia sasa, hesabu hiyo imeongezeka sana. Kuna Mashahidi wa Yehova zaidi ya 7,000,000 wanaohubiri katika dunia yote, nao wako katika makutaniko zaidi ya 100,000. Watu wengine 10,000,000 walikusanyika pamoja na Mashahidi wa Yehova mwaka wa 2008 wakati wa Ukumbusho wa kifo cha Kristo. Hilo lilikuwa ongezeko kubwa sana la hudhurio ikilinganishwa na mwaka uliotangulia.

8. Kwa nini upinzani haujazuia kazi yetu ya kuhubiri isifanikiwe?

8 Ni ushahidi mkubwa kama nini unaotolewa kuhusu Ufalme wa Mungu katika mataifa yote kabla ya mwisho wa mfumo huu kufika! Hilo linatukia hata ingawa Shetani ndiye “mungu wa mfumo huu wa mambo.” (2 Kor. 4:4) Sehemu zote za kisiasa, za kidini, na za kibiashara za ulimwengu huu na njia zake za kusambaza propaganda zinaongozwa na Shetani. Basi, mafanikio yenye kustaajabisha ya kazi ya kuhubiri yametokana na nini? Lazima yawe yametegemezwa na Yehova. Hivyo, kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme inaendelea vizuri sana hata ingawa Shetani anajaribu kuisimamisha.

9. Kwa nini tunaweza kusema kwamba ufanisi wetu wa kiroho ni muujiza?

9 Tunaweza kusema kwamba mafanikio ya kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme na pia ongezeko na ufanisi wa kiroho wa watu wa Yehova ni muujiza. Bila utegemezo wa Mungu, ambao unatia ndani mwongozo na ulinzi kwa watu wake, kazi ya kuhubiri haingewezekana. (Soma Mathayo 19:26.) Tunaweza kuwa na uhakika kwamba roho takatifu ya Mungu ikiichochea mioyo ya watu wanaokesha ambao wako tayari kutumika, kazi hii ya kuhubiri itafanikiwa na kufikia mwisho, “ndipo ule mwisho utakapokuja.” Wakati huo unakaribia haraka.

“Ile Dhiki Kuu”

10. Yesu alisema nini kuhusu ile dhiki kuu inayokuja?

10 Mwisho wa mfumo huu mwovu utakuja wakati wa “ile dhiki kuu.” (Ufu. 7:14) Biblia haituambii dhiki hiyo itadumu kwa muda gani, lakini Yesu alisema hivi: “Ndipo kutakapokuwa na dhiki kuu ya namna ambayo haijapata kutukia tangu mwanzo wa ulimwengu mpaka sasa, hapana, wala haitatukia tena.” (Mt. 24:21) Tunapofikiria dhiki ambayo tayari ulimwengu huu umepata, kama vile Vita vya Pili vya Ulimwengu wakati ambapo inakadiriwa watu milioni 50 mpaka 60 walikufa, dhiki kuu inayokuja itakuwa kali kwelikweli. Itafikia upeo katika vita vya Har–Magedoni. Wakati huo, Yehova atatumia majeshi yake ya kutekeleza hukumu ili kuharibu sehemu zote zinazobaki za mfumo wa kidunia wa Shetani.—Ufu. 16:14, 16.

11, 12. Ni tukio gani litakaloonyesha kwamba ile dhiki kuu imeanza?

11 Unabii wa Biblia hautaji tarehe ambayo kipindi cha kwanza cha ile dhiki kuu kitaanza, lakini unatuambia ni tukio gani lisilo la kawaida litakaloonyesha kwamba kimeanza. Tukio hilo ni lile la mamlaka za kisiasa kuharibu dini yote ya uwongo. Katika unabii wa Biblia ulio katika Ufunuo sura ya 17 na 18, dini ya uwongo inalinganishwa na kahaba ambaye amefanya ngono haramu na mifumo ya kisiasa duniani. Andiko la Ufunuo 17:16 linaonyesha kwamba hivi karibuni wakati utafika ambapo mifumo hiyo ya kisiasa ‘itamchukia yule kahaba na kumfanya kuwa ukiwa na uchi, nayo itakula sehemu zake zenye nyama na kumteketeza kabisa kwa moto.’

12 Wakati utakapofika wa jambo hilo kutukia, Mungu ‘atalitia hilo ndani ya mioyo ya [watawala wa kisiasa] ili kutekeleza wazo lake’ la kuharibu dini yote ya uwongo. (Ufu. 17:17) Kwa hiyo, tunaweza kusema kwamba uharibifu huo umetoka kwa Mungu. Ni hukumu yake juu ya dini ya kinafiki ambayo kwa muda mrefu sana imefundisha mafundisho yasiyopatana na mapenzi ya Mungu na imewatesa watumishi wake. Ulimwengu kwa ujumla hautazamii uharibifu huo unaokuja wa dini ya uwongo. Lakini watumishi waaminifu wa Yehova wanautazamia. Na katika kipindi hiki chote cha siku za mwisho, wamekuwa wakiwaambia watu kuhusu uharibifu huo.

13. Ni jambo gani linaloonyesha kwamba mwisho wa dini ya uwongo utatukia haraka sana?

13 Watu watashtuka sana kuona dini ya uwongo ikiharibiwa. Unabii wa Biblia unaonyesha kwamba hata “wafalme wa dunia” watatangaza hivi kuhusu uharibifu huo: “Ole, ole, . . . kwa sababu katika saa moja hukumu yako imefika!” (Ufu. 18:9, 10, 16, 19) Biblia inatumia maneno katika “saa moja” kuonyesha kwamba kwa njia fulani tukio hilo litatukia haraka sana.

14. Maadui wa Yehova watakapowashambulia watumishi wake mwishowe, Mungu atafanya nini?

14 Tunaelewa kwamba muda fulani baada ya dini ya uwongo kuharibiwa, watumishi wa Yehova ambao wamekuwa wakitangaza ujumbe wake wa hukumu watashambuliwa. (Eze. 38:14-16) Shambulizi hilo linapoanza, washambuliaji hao watalazimika kumkabili Yehova, ambaye anaahidi kuwalinda watu wake waaminifu. Yehova anatangaza hivi: “Katika ukali wangu, katika moto wa ghadhabu yangu, nitalazimika kusema. . . . Nao watalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova.” (Soma Ezekieli 38:18-23.) Mungu anasema hivi katika Neno lake: “Yeye anayewagusa ninyi [watumishi wake waaminifu] anaigusa mboni ya jicho langu.” (Zek. 2:8) Kwa hiyo, maadui wake wanapoanza kuwashambulia watumishi wake ulimwenguni pote, Yehova atachukua hatua. Atachukua hatua ambayo itaongoza kwenye upeo au sehemu ya mwisho ya ile dhiki kuu, yaani, Har–Magedoni. Chini ya amri ya Kristo, majeshi yenye nguvu ya malaika yatatekeleza hukumu za Yehova juu ya ulimwengu wa Shetani.

Jinsi Tunavyopaswa Kutenda

15. Tunapaswa kufanya nini kwa kuwa tunajua kwamba mwisho wa mfumo huu uko karibu?

15 Tunapaswa kufanya nini tunapojua kwamba mwisho wa mfumo huu mwovu unakaribia haraka? Mtume Petro aliandika hivi: “Kwa kuwa hivyo vitu vyote vitayeyushwa jinsi hiyo, ninyi mnapaswa kuwa watu wa namna gani katika matendo matakatifu ya mwenendo na vitendo vya ujitoaji-kimungu!” (2 Pet. 3:11) Maneno hayo yanakazia kwamba tunahitaji kuwa waangalifu sana na kuhakikisha kwamba mwenendo wetu unapatana na matakwa ya Mungu na maisha yetu yanatia ndani matendo ya ujitoaji-kimungu, na hivyo kuonyesha kwamba tunampenda Yehova. Matendo hayo yanatia ndani kufanya yote tunayoweza katika kuhubiri habari njema ya Ufalme kabla ya mwisho kuja. Pia, Petro aliandika hivi: ‘Mwisho wa mambo yote umekaribia. . . . Kesheni kuhusiana na sala.’ (1 Pet. 4:7) Tunamkaribia Yehova na kuonyesha kwamba tunampenda kwa kusali kwake kwa ukawaida, na kumwomba atuongoze kupitia roho yake takatifu na kutaniko lake la ulimwenguni pote.

16. Kwa nini tunapaswa kufuata kwa ukaribu mashauri ya Mungu?

16 Katika nyakati hizi za hatari, tunahitaji kufuata kwa ukaribu shauri hili la Neno la Mungu: “Endeleeni kuangalia sana kwamba jinsi mnavyotembea si kama watu wasio na hekima bali kama watu wenye hekima, mkijinunulia wakati unaofaa, kwa sababu siku hizi ni zenye uovu.” (Efe. 5:15, 16) Uovu ni mwingi sana sasa kuliko wakati mwingine wowote katika historia. Shetani amebuni mambo mengi ili kuwazuia watu wasifanye mapenzi ya Yehova au ili kuwakengeusha. Tukiwa watumishi wa Mungu, tunajua jambo hilo, na hatutaki kuruhusu jambo lolote livunje ushikamanifu wetu kwa Mungu. Pia, tunajua mambo ambayo yatatukia hivi karibuni, na tunaweza kuwa na uhakika katika Yehova na makusudi yake.—Soma 1 Yohana 2:15-17.

17. Eleza jinsi waokokaji wa Har–Magedoni watakavyotenda ufufuo utakapotukia.

17 Ahadi nzuri ajabu ya Mungu ya kuwafufua wafu itatimia, kwa maana “kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.” (Mdo. 24:15) Ona jinsi ahadi hiyo inavyokaziwa: “Kutakuwa na ufufuo”! Hakuna shaka kuhusu jambo hilo, kwa sababu Yehova ametupa ahadi hiyo! Andiko la Isaya 26:19 linaahidi hivi: “Wafu wako wataishi. . . . Amkeni, pigeni vigelegele kwa shangwe, enyi mnaokaa mavumbini! . . . Dunia itawaacha hata wale wasiojiweza katika kifo waanguke katika kuzaliwa.” Maneno hayo yalitimia kwa mara ya kwanza watu wa kale wa Mungu waliporudishwa katika nchi yao, nayo yanatupa uhakika kwamba yatatimia kihalisi katika ulimwengu mpya unaokuja. Kutakuwa na shangwe kubwa kama nini wale watakaofufuliwa watakapoungana tena na wapendwa wao! Ndiyo, mwisho wa ulimwengu wa Shetani uko karibu, na ulimwengu mpya wa Mungu u karibu sana. Ni jambo la maana kama nini tuendelee kukesha!

Je, Unakumbuka?

• Ni nini kilichokuwa kichwa cha mafundisho ya Yesu?

• Kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme imeenea kadiri gani leo?

• Kwa nini ni jambo la maana sana kukesha?

• Kwa nini ahadi iliyo katika Matendo 24:15 inakutia moyo?

[Maswali ya Funzo]

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 16, 17]

KIPINDI CHA MSUKUSUKO KILIANZA

Katika mwaka wa 2007, Alan Greenspan aliandika kitabu fulani (The Age of Turbulence: Adventures in a New World, yaani, Kipindi cha Msukosuko: Matukio Yasiyo ya Kawaida Katika Ulimwengu Mpya). Kwa karibu miaka 20, alikuwa mwenyekiti wa kamati inayosimamia mfumo wa benki wa Marekani (United States Federal Reserve Board). Greenspan anakazia tofauti kubwa kati ya hali ya ulimwengu kabla ya 1914 na mambo yaliyotukia baadaye:

“Ripoti zote za kihistoria zinaonyesha kwamba kabla ya 1914, ulimwengu ulionekana kuwa unaelekea kwenye ustaarabu wa hali ya juu; ilionekana kwamba wanadamu wangefikia ukamilifu. Katika karne ya 19, biashara ya utumwa yenye ukatili ilikomeshwa. Ni kana kwamba jeuri ya kinyama ilikuwa ikipungua. . . . Maendeleo ya kitekinolojia ulimwenguni pote yalikuwa yamesonga sana katika karne yote ya 19, na kutokeza reli, simu, umeme, sinema, gari, na vifaa chungu nzima vya kutumiwa nyumbani. Sayansi ya kitiba, lishe bora zaidi, na maji safi ya kunywa yalikuwa yameongeza muda wa kuishi . . . Kila mtu ulimwenguni alihisi kwamba maendeleo hayo yatadumu.”

Lakini . . . “Vita vya Kwanza vya Ulimwengu viliharibu ustaarabu hata kuliko Vita vya Pili vya Ulimwengu vilivyosababisha uharibifu mkubwa: vita hivyo vya kwanza viliharibu mambo ya maana sana. Siwezi kusahau miaka hiyo ya kabla ya Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, wakati ambapo wanadamu walikuwa na matumaini makubwa na ya kudumu ya wakati ujao. Leo maoni yetu ni tofauti sana na yalivyokuwa karne moja iliyopita lakini huenda yanapatana zaidi na uhalisi wa mambo. Je, ugaidi, ongezeko la joto duniani, au kuibuka tena kwa utetezi wa haki za kibinadamu utaharibu maendeleo yanayotokana na utandawazi kama Vita vya Kwanza vya Ulimwengu vilivyoharibu maendeleo yaliyokuwapo kabla ya vita hivyo? Hakuna aliye na uhakika kuhusu jambo hilo.”

Greenspan anakumbuka maneno yaliyosemwa na mwalimu wake aliyekuwa Profesa wa Uchumi, Benjamin M. Anderson (1886-1949): “Wale ambao wangeweza kuelewa mambo na kukumbuka jinsi ulimwengu ulivyokuwa kabla ya Vita vya Kwanza vya Ulimwengu wanatamani sana wakati huo. Wakati huo, watu walihisi usalama fulani ambao umetoweka tangu hapo.”—Economics and the Public Welfare.

Mkataa kama huo umefikiwa katika kitabu kimoja (A World Undone), cha G. J. Meyer, kilichochapishwa mwaka wa 2006. Tunasoma hivi: “Mara nyingi inasemekana kwamba matukio ya kihistoria ‘yalibadili kila kitu.’ Hilo ni kweli hasa kuhusiana na vile Vita Vikuu [1914-1918]. Kwa hakika, vita hivyo vilibadili kila kitu: si mipaka tu, si serikali na wakati ujao wa mataifa tu, bali pia maoni ya watu kuhusu ulimwengu na kujihusu tangu wakati huo. Vita hivyo vilitokeza ulimwengu tofauti kabisa ambao haukuwa salama kama ilivyokuwa zamani.”

[Picha katika ukurasa wa 18]

Katika Har–Magedoni, Yehova atatumia majeshi yenye nguvu ya malaika