Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Anastahili Kusifiwa kwa Umoja

Yehova Anastahili Kusifiwa kwa Umoja

 Yehova Anastahili Kusifiwa kwa Umoja

“Msifuni Yah!”—ZAB. 111:1.

1, 2. Neno “Haleluya” linamaanisha nini, na linatumiwa jinsi gani katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo?

“HALELUYA!” Ni jambo la kawaida sana kusikia neno hilo katika makanisa ya dini zinazodai kuwa za Kikristo. Watu fulani hata wanalitumia neno hilo mara nyingi katika mazungumzo yao ya kila siku. Hata hivyo, ni wachache sana wanaojua kwamba neno hilo lina maana takatifu, na watu wengi ambao wanatumia neno hilo wanaishi maisha yanayomvunjia Mungu heshima. (Tito 1:16) Kamusi moja ya Biblia inaeleza kwamba “Haleluya,” ni “neno linalotumiwa na waandikaji wa zaburi mbalimbali ili kutuomba sote tujiunge nao kumsifu Yehova.” Kwa kweli, wasomi wengi wa Biblia wanasema kwamba neno “Haleluya” linamaanisha “‘Msifuni Yah,’ [yaani] Yehova.”

2 Inaeleweka kwa nini katika Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya neno hilo katika Zaburi 111:1 limetafsiriwa kuwa “Msifuni Yah!” Tafsiri ya Kigiriki ya neno hilo inaonekana mara nne kwenye Ufunuo 19:1-6 katika kusherehekea mwisho wa dini ya uwongo. Hilo litakapotukia, waabudu wa kweli watakuwa na sababu ya pekee ya kutumia neno “Haleluya” kwa njia ya heshima.

Kazi Zake Kuu

3. Ni nini kusudi letu kuu la kukusanyika kwa ukawaida?

3 Mtungaji wa Zaburi ya 111 anatoa sababu nyingi kwa nini Yehova anastahili kusifiwa na wanadamu wote kwa umoja. Mstari wa kwanza unasema hivi: “Nitamsifu Yehova kwa moyo wangu wote katika kikundi cha rafiki za karibu walio wanyoofu na katika kusanyiko.” Leo, Mashahidi wa Yehova wanahisi vivyo hivyo. Kusudi letu kuu la kukusanyika kwa ukawaida, iwe katika makutaniko yetu au katika makusanyiko makubwa, ni kumsifu Yehova.

4. Wanadamu wanaweza kuzitafuta kazi za Yehova jinsi gani?

4 “Kazi za Yehova ni kuu, zinazotafutwa na wale wote wanaopendezwa nazo.” (Zab. 111:2) Ona neno “zinazotafutwa.” Kulingana na kitabu kimoja, mstari huo unaweza kuwahusu wanadamu ambao “wanatafakari na kujifunza kwa bidii sana” kuhusu kazi za Mungu. Yehova aliumba vitu vyote akiwa na kusudi zuri ajabu. Aliliweka jua, dunia, na mwezi mahali ambapo panafaa kabisa ili dunia yetu ipate joto na nuru, usiku na mchana, majira na mawimbi.

5. Maendeleo ya wanadamu katika kuuelewa ulimwengu yamefunua nini?

5 Wanasayansi wamegundua mambo mengi sana kuhusu mahali ambapo dunia ipo katika mfumo wetu wa jua, na pia kuhusu mzunguko kamili, ukubwa, na uzito wa mwezi wetu ambao ni mkubwa. Mpangilio na mahusiano kati ya vitu hivyo vya angani, unawezesha kuwe na mabadiliko yenye kuvutia na ya kawaida ya majira. Pia, wanadamu wamejifunza mambo mengi kuhusu vipimo sahihi vya nguvu za asili zilizo katika ulimwengu wote. Hivyo, katika makala moja yenye kichwa “Ulimwengu Uliobuniwa ‘kwa Ustadi Kabisa’,” profesa mmoja wa uinjinia alisema: “Ni rahisi kuelewa kwa nini wanasayansi wengi wamebadili maoni yao katika miaka 30 iliyopita, wakikubali kwamba mtu anahitaji kuwa na imani kubwa ili kuamini kwamba ulimwengu ulijitokeza wenyewe tu. Kadiri tunavyoelewa zaidi kuhusu dunia yetu iliyobuniwa kwa ustadi mwingi ndivyo tunavyokuwa na uthibitisho zaidi wa kuwapo kwa mbuni mwenye akili.”

6. Unahisi jinsi gani kuhusu namna Mungu alivyomuumba mwanadamu?

6 Kazi nyingine kubwa ya uumbaji ni jinsi Mungu alivyotuumba. (Zab. 139:14) Alipowaumba wanadamu, Mungu aliwapa akili, mwili wenye viungo vingi, uwezo na nguvu za kufanya kazi. Kwa mfano, kuna muujiza pia unaohusu uwezo tuliopewa na Mungu wa kuzungumza na kusikiliza, na pia uwezo wa kuandika na kusoma. Watu wengi wana uwezo huo mbalimbali. Pia, mwili wako una uwezo wa ajabu wa kusimama wima. Inastaajabisha sana kuona jinsi mwili wetu ulivyoumbwa, uwezo wetu wa kutembea na kufanya kazi, na jinsi kemikali zinavyofanya kazi katika mwili wetu, kama vile kutumia chakula ili kutokeza nishati au nguvu mwilini. Zaidi ya hayo, jinsi neva au mishipa ya fahamu inavyoshirikiana kwa njia ya ajabu ili kuwezesha akili na hisi zako kufanya kazi, hakuwezi kulinganishwa na chochote kile ambacho wanasayansi wametengeneza. Kwa kweli, mambo yote ambayo wanadamu wanatimiza yanawezekana tu kwa sababu ya akili na hisi ambazo wamepewa. Hata injinia aliyezoezwa vizuri zaidi na mwenye uwezo zaidi hangeweza kutengeneza kitu chochote kilicho maridadi na chenye faida sana kama vidole vyako kumi vya mikono na miguu. Jiulize hivi: ‘Je, kazi za ufundi na ujenzi wenye kustaajabisha zingetimizwa bila kutumia kwa ustadi vidole tulivyopewa na Mungu?’

Kazi Kuu za Mungu na Sifa Zake

7. Kwa nini tunapaswa kuiona Biblia kuwa moja ya kazi kuu za Mungu?

7 Kazi kuu za Yehova zinatia ndani mambo mengine yenye kustaajabisha ambayo amefanya kwa ajili ya wanadamu, kama yanavyoelezwa katika Biblia. Kitabu hicho chenyewe chenye kupatana ni kazi kuu ya Mungu. Tofauti na kitabu kingine, kitabu hicho kwa kweli ‘kimeongozwa na roho ya Mungu nacho ni chenye faida kwa kufundisha.’ (2 Tim. 3:16) Kwa mfano, kitabu cha kwanza cha Biblia, Mwanzo, kinaeleza jinsi Mungu alivyoondoa uovu duniani katika siku za Noa. Kitabu cha pili, Kutoka, kinaonyesha jinsi Yehova alivyoutetea Uungu wake kwa kuwakomboa Waisraeli kutoka katika utumwa wa Wamisri. Inaelekea mtunga-zaburi alikuwa akifikiria matukio hayo alipochochewa kusema hivi: “Utendaji [wa Yehova] ni utukufu na fahari, na uadilifu wake unasimama milele. Amefanya ukumbusho kwa ajili ya kazi zake za ajabu. Yehova ni mwenye neema na mwenye rehema.” (Zab. 111:3, 4) Je, hukubali kwamba utendaji wa Yehova katika historia yote, kutia ndani mambo ambayo amefanya wakati wa maisha yako, ni ukumbusho wa “utukufu na fahari” yake?

8, 9. (a) Kazi za Mungu zinatofautiana namna gani na kazi nyingi za wanadamu? (b) Taja sifa fulani za Mungu ambazo unathamini.

8 Ona kwamba mtunga-zaburi anakazia pia sifa bora za Yehova, kama vile uadilifu, neema, na rehema. Unajua kwamba mara nyingi kazi za wanadamu wenye dhambi hazitegemei uadilifu. Mara nyingi zinafanywa kwa pupa, tamaa, na majivuno. Hilo linathibitishwa na silaha za ukatili ambazo wanadamu wametengeneza kwa ajili ya vita wanavyosababisha na kwa sababu ya faida za kiuchumi. Silaha hizo zinasababisha taabu na mateso makubwa kwa mamilioni ya watu wasio na hatia. Pia, kazi nyingi za wanadamu zimesababisha mateso kwa watu maskini wanaokandamizwa. Mfano mmoja ambao wengi wanaweza kutaja ni ule wa jinsi watumwa walivyotumiwa kujenga mapiramidi. Mapiramidi hayo yalitumiwa hasa kama makaburi ya Mafarao wenye kiburi. Zaidi ya hayo, kazi nyingi za wanadamu leo ni zenye kukandamiza na pia ‘zinaiharibu dunia.’—Soma Ufunuo 11:18.

9 Ni tofauti kama nini na kazi za Yehova, ambazo sikuzote zinategemea mambo yaliyo sawa! Kazi zake zinatia ndani maandalizi yake yenye rehema ya kuwaokoa wanadamu wenye dhambi. Kwa kuandaa fidia au dhabihu ya ukombozi, Mungu alikuwa ‘akionyesha wazi uadilifu wake mwenyewe.’ (Rom. 3:25, 26) Kwa kweli, “uadilifu wake unasimama milele”! Mungu ameonyesha neema kwa kushughulika na wanadamu wenye dhambi kwa subira. Nyakati nyingine, hata alitumia neno “tafadhali” alipowasihi waache njia zao mbaya na kufanya yaliyo sawa.—Soma Ezekieli 18:25.

Ni Mwaminifu kwa Ahadi Zake

10. Ni mfano gani wa uaminifu ambao Yehova aliweka kuhusiana na agano lake pamoja na Abrahamu?

10 “Amewapa chakula wale wanaomwogopa. Mpaka wakati usio na kipimo, atalikumbuka agano lake.” (Zab. 111:5) Inaonekana hapa mtunga-zaburi anazungumza kuhusu agano la Kiabrahamu. Yehova aliahidi kuubariki uzao wa Abrahamu na akasema kwamba wangeyamiliki malango ya maadui wao. (Mwa. 22:17, 18; Zab. 105:8, 9) Katika utimizo wa kwanza wa ahadi hizo, uzao wa Abrahamu ulikuwa taifa la Israeli. Kwa muda mrefu taifa hilo lilikuwa utumwani huko Misri, lakini “Mungu akalikumbuka agano lake pamoja na Abrahamu” naye akawakomboa. (Kut. 2:24) Jinsi Yehova alivyoshughulika nao kunaonyesha kwamba yeye ni mkarimu. Aliwapa chakula cha kimwili cha kuitegemeza miili yao na chakula cha kiroho kwa ajili ya akili na mioyo yao. (Kum. 6:1-3; 8:4; Neh. 9:21) Katika karne zilizofuata, taifa hilo mara nyingi lilimwacha Mungu, hata hivyo alituma manabii ili kuwahimiza wamrudie. Zaidi ya miaka 1,500 baada ya kuwakomboa Waisraeli kutoka Misri, Mungu alimtuma Mwana wake mzaliwa-pekee duniani. Wayahudi wengi walimkataa Yesu na hata walimtoa ili auawe. Kisha, Yehova akaanzisha taifa jipya, taifa la kiroho, “Israeli wa Mungu.” Pamoja na Kristo, taifa hilo ni uzao wa kiroho wa Abrahamu, uzao ambao Yehova alitabiri kuwa angeutumia kuwabariki wanadamu.—Gal. 3:16, 29; 6:16.

11. Yehova anaendelea jinsi gani ‘kukumbuka agano lake’ pamoja na Abrahamu?

11 Yehova anaendelea ‘kukumbuka agano lake’ na baraka alizoahidi kupitia agano hilo. Leo, anaandaa chakula kingi cha kiroho katika lugha zaidi ya 400. Pia, anaendelea kujibu sala kuhusu mahitaji yetu ya kimwili, kulingana na maneno haya: “Utupe mkate wetu kwa ajili ya siku kulingana na mahitaji ya siku hiyo.”—Luka 11:3; Zab. 72:16, 17; Isa. 25:6-8.

Nguvu za Ajabu za Yehova

12. Ni katika njia gani Waisraeli wa kale walipewa “urithi wa mataifa”?

12 “Nguvu za kazi zake amewatangazia watu wake, kwa kuwapa urithi wa mataifa.” (Zab. 111:6) Tukio moja kuu katika historia ya Israeli ambalo huenda mtunga-zaburi alikuwa akifikiria lilikuwa kukombolewa kimuujiza kutoka Misri. Yehova alipowaruhusu mwishowe Waisraeli waingie katika Nchi ya Ahadi, waliweza kuzishinda falme zilizokuwa upande wa mashariki na magharibi wa Mto Yordani. (Soma Nehemia 9:22-25.) Ndiyo, Yehova aliwapa Waisraeli “urithi wa mataifa.” Ulikuwa wonyesho mkubwa kama nini wa nguvu za Mungu!

13, 14. (a) Huenda mtunga-zaburi alikuwa akifikiria wonyesho gani wa nguvu za Mungu kuhusiana na Babiloni? (b) Yehova ametimiza matendo gani mengine makubwa ya ukombozi?

13 Hata hivyo, sote tunajua vizuri kwamba ingawa Yehova aliwafanyia Waisraeli mambo mengi, hawakumheshimu wala hawakuwaheshimu mababu zao Abrahamu, Isaka, na Yakobo. Waliendelea kuasi mpaka Mungu alipolitumia taifa la Babiloni kuwaondoa katika nchi yao na kuwapeleka uhamishoni. (2 Nya. 36:15-17; Neh. 9:28-30) Ikiwa mtungaji wa Zaburi ya 111 aliishi baada ya Waisraeli kurudi kutoka uhamishoni Babiloni, kama wasomi fulani wa Biblia wanavyosema, basi alikuwa na sababu nzuri zaidi ya kumsifu Yehova kwa sababu ya ushikamanifu na nguvu Zake. Mungu alionyesha ushikamanifu na nguvu zake kwa kuwakomboa Wayahudi kutoka Babiloni, serikali yenye nguvu ambayo ilikuwa na sheria ya kutowaacha huru mateka wake.—Isa. 14:4, 17.

14 Karne tano hivi baadaye, Yehova alitumia nguvu zake kwa njia kubwa zaidi kuwakomboa wanadamu wenye kutubu kutoka katika utumwa wa dhambi na kifo. (Rom. 5:12) Faida moja ni kwamba njia ilifunguliwa kwa ajili ya wanadamu 144,000 kuwa wafuasi watiwa-mafuta wa Kristo. Katika mwaka wa 1919, Yehova alitumia nguvu zake kukomboa mabaki wachache wa watiwa-mafuta hao kutoka katika utekwa wa dini ya uwongo. Ni nguvu za Mungu tu ambazo zimewawezesha kutimiza mambo ambayo wanafanya wakati huu wa mwisho. Baada ya kujithibitisha kuwa waaminifu mpaka kifo, watatawala dunia pamoja na Yesu Kristo wakiwa mbinguni kwa faida ya wanadamu wenye kutubu. (Ufu. 2:26, 27; 5:9, 10) Watairithi dunia katika njia kubwa zaidi kuliko Waisraeli wa kale.—Mt. 5:5.

Kanuni za Milele Zenye Kutegemeka

15, 16. (a) Kazi za mikono ya Mungu zinatia ndani nini? (b) Mungu aliwapa Waisraeli wa kale amri gani?

15 “Kazi za mikono yake ni kweli na hukumu; maagizo yake yote anayotoa ni yenye kutegemeka, yanategemezwa vema milele, mpaka wakati usio na kipimo, yanafanywa katika kweli na unyoofu.” (Zab. 111:7, 8) “Kazi za mikono [ya Yehova]” zilitia ndani mabamba mawili ya mawe ambayo juu yake Mungu aliandika sheria kumi za maana sana kwa ajili ya Israeli. (Kut. 31:18) Sheria hizo, pamoja na masharti yote mengine ambayo yalikuja kuwa sehemu ya agano la Sheria ya Musa, zinategemea kanuni za milele zenye kutegemeka.

16 Kwa mfano, moja ya amri, au sheria, kwenye mabamba hayo ilisema hivi: “Mimi Yehova Mungu wako ni Mungu anayetaka watu wajitoe kikamili.” Sheria hiyo inasema pia kwamba Yehova anaonyesha “fadhili zenye upendo kuelekea kizazi cha elfu kwa wale [wanaompenda] na kuzishika amri [zake].” Pia, mabamba hayo ya mawe yalikuwa na kanuni zinazodumu kama vile “mheshimu baba yako na mama yako” na “usiibe,” na pia sheria iliyoonyesha uelewaji wa ndani sana ambayo ilikataza kutamani vitu vya watu wengine.—Kut. 20:5, 6, 12, 15, 17.

Mkombozi Wetu Mtakatifu na Mwenye Kuogopesha

17. Waisraeli walikuwa na sababu gani nzuri za kuliona jina la Mungu kuwa takatifu?

17 “Ameutuma ukombozi kwa watu wake. Mpaka wakati usio na kipimo ameamuru agano lake. Jina lake ni takatifu na lenye kuogopesha.” (Zab. 111:9) Tena, huenda mtunga-zaburi alikuwa akifikiria ushikamanifu wa Yehova kuhusu ahadi ya agano lake kwa Abrahamu. Kwa hiyo, Yehova hakuwaacha watu wake kwanza wakiwa watumwa katika Misri ya kale na baadaye wakiwa mateka huko Babiloni. Katika hali hizo mbili, Mungu aliwakomboa watu wake. Hata ikiwa Mungu aliwakomboa katika mambo hayo mawili tu, Waisraeli walikuwa na sababu nzuri za kuliona jina la Mungu kuwa takatifu.—Soma Kutoka 20:7; Waroma 2:23, 24.

18. Kwa nini unahisi kwamba kuitwa kwa jina la Mungu ni pendeleo?

18 Hilo ni kweli pia kuhusu Wakristo leo ambao wamekombolewa kutoka katika utumwa mbaya sana wa dhambi na kifo. Tunapaswa kujitahidi sana kuishi kulingana na ombi la kwanza katika sala ya kielelezo: “Jina lako na litakaswe.” (Mt. 6:9) Kutafakari juu ya jina hilo tukufu kunapaswa kutuchochea kumwogopa Mungu. Mwandikaji wa Zaburi ya 111 alikuwa na maoni mazuri kuhusu kumwogopa Mungu, alisema hivi: “Kumwogopa Yehova ni mwanzo wa hekima. Wale wote wanaoyatenda maagizo yake wana ufahamu mwema.”Zab. 111:10.

19. Tutachunguza nini katika habari inayofuata?

19 Kumwogopa Mungu kwa njia inayofaa kutatusaidia kuchukia mambo mabaya. Kutatusaidia pia kuiga sifa nzuri za Mungu kama zinavyoonyeshwa katika Zaburi ya 112, ambayo tutachunguza katika  habari inayofuata. Zaburi hiyo inaonyesha jinsi tunavyoweza kustahili kuwa kati ya mamilioni ya watu ambao watafurahia kumsifu Mungu milele. Anastahili kabisa kusifiwa. “Sifa yake inasimama milele.”Zab. 111:10.

Maswali ya Kutafakari

• Kwa nini Yehova anastahili kusifiwa kwa umoja na wote?

• Ni sifa gani za Yehova zinazofunuliwa kupitia kazi zake?

• Una maoni gani kuhusu pendeleo la kuitwa kwa jina la Mungu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 20]

Kusudi letu kuu la kukusanyika kwa ukawaida ni kumsifu Yehova

[Picha katika ukurasa wa 23]

Sheria zote za Yehova zinategemea kanuni za milele zenye kutegemeka