Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Waadilifu Watamsifu Mungu Milele

Waadilifu Watamsifu Mungu Milele

Waadilifu Watamsifu Mungu Milele

“Mwadilifu atakuwa kumbukumbu . . . Uadilifu wake unasimama milele.”—ZAB. 112:6, 9.

1. (a) Ni wakati gani ujao wenye furaha unaowangojea wote ambao Mungu anawaona kuwa waadilifu? (b) Ni swali gani linalotokea?

NI WAKATI ujao mzuri kama nini unaowangojea wanadamu wote ambao Mungu anawaona kuwa waadilifu! Watafurahi kujifunza milele mengi zaidi kuhusu sifa nzuri za Yehova. Mioyo yao inabubujika kwa sifa wanapoendelea kujifunza kuhusu kazi za Mungu za uumbaji. Ili wafurahie wakati huo ujao wenye utukufu wanahitaji kudumisha sifa ya “uadilifu,” ambayo inakaziwa katika Zaburi ya 112. Lakini Yehova, Mungu mtakatifu na mwadilifu, anaweza kuwaona jinsi gani wanadamu watenda-dhambi kuwa waadilifu? Hata tujitahidi kadiri gani kufanya yaliyo sawa, tunafanya makosa, na nyakati nyingine tunafanya makosa mazito.—Rom. 3:23; Yak. 3:2.

2. Ni miujiza gani miwili ambayo Yehova alifanya kwa upendo?

2 Kwa upendo, Yehova alitoa suluhisho kamilifu. Jinsi gani? Kwanza, Yehova alihamisha kimuujiza uhai wa Mwana wake mpendwa na kuutia katika tumbo la uzazi la bikira ili azaliwe akiwa mwanadamu mkamilifu. (Luka 1:30-35) Kisha, baada ya maadui wa Yesu kumuua, Yehova alifanya muujiza mwingine mkubwa. Mungu alimfufua Yesu akiwa kiumbe wa roho mwenye utukufu.—1 Pet. 3:18.

3. Kwa nini Mungu alipendezwa kumpa Mwana wake thawabu ya uhai wa kimbingu?

3 Yehova alimthawabisha Mwana wake Yesu kwa kumpa kitu fulani ambacho hakuwa nacho kabla ya kuwa mwanadamu, yaani, uhai usioweza kuharibika mbinguni. (Ebr. 7:15-17, 28) Yehova alipendezwa kufanya hivyo kwa sababu Yesu alishika utimilifu mkamilifu chini ya majaribu makali. Hivyo, Yesu alimpa Baba yake kitu kilicho bora kabisa, ndiyo kikamilifu, yaani, jibu kwa uwongo wa Shetani wa kwamba wanadamu wanamtumikia Mungu wakiwa na nia ya ubinafsi au uchoyo na si kwa sababu ya upendo mkamilifu.—Met. 27:11.

4. (a) Baada ya kurudi mbinguni, Yesu alifanya nini kwa ajili yetu, na Yehova aliitikia jinsi gani? (b) Unahisi jinsi gani kuhusu yale ambayo Yehova na Yesu wamefanya kwa ajili yako?

4 Akiwa mbinguni, Yesu alifanya mengi zaidi. ‘Alionekana mbele za uso wa Mungu kwa ajili yetu’ akiwa na thamani ya “damu yake mwenyewe.” Baba yetu wa mbinguni alikubali kwa fadhili toleo lenye thamani la Yesu kuwa “dhabihu ya upatanisho kwa ajili ya dhambi zetu.” Kwa hiyo, tukiwa na ‘dhamiri zilizosafishwa,’ tunaweza kutoa “utumishi mtakatifu kwa Mungu aliye hai.” Hiyo ni sababu nzuri kama nini ya kukubaliana na maneno ya kwanza ya Zaburi ya 112, “Msifuni Yah!”Ebr. 9:12-14, 24; 1 Yoh. 2:2.

5. (a) Tunapaswa kufanya nini ili tudumishe msimamo wa uadilifu machoni pa Mungu? (b) Zaburi ya 111 na ile ya 112 zimepangwa kwa utaratibu gani?

5 Ili tudumishe msimamo wa uadilifu machoni pa Mungu, tunapaswa kuendelea kuwa na imani katika damu ya Yesu iliyomwagwa. Tunapaswa kumshukuru Yehova kila siku kwa sababu anatupenda sana. (Yoh. 3:16) Pia, tunahitaji kuendelea kujifunza Neno la Mungu na kufanya yote tunayoweza kuishi kupatana na ujumbe wake. Zaburi ya 112 ina mashauri mazuri kwa wote wanaotaka kudumisha dhamiri safi mbele za Mungu. Zaburi hiyo inakamilisha Zaburi ya 111. Zaburi hizo mbili zinaanza kwa maneno “Msifuni Yah!” au “Haleluya!” na zinafuatwa na mistari 22, kila mstari unaanza na moja ya herufi 22 za alfabeti ya Kiebrania. *

Chanzo cha Furaha

6. “Mtu” anayemwogopa Mungu ambaye anazungumziwa kwenye Zaburi ya 112 anabarikiwa jinsi gani?

6 “Mwenye furaha ni mtu anayemwogopa Yehova, ambaye amependezwa sana na amri zake. Uzao wake utakuwa wenye nguvu duniani. Nacho kizazi cha wanyoofu, kitabarikiwa.” (Zab. 112:1, 2) Ona kwamba mtunga-zaburi anataja kwanza “mtu” mmoja kisha anatumia neno la wingi “wanyoofu” katika sehemu ya mwisho ya mstari wa 2. Hilo linaonyesha kwamba huenda Zaburi ya 112 inazungumzia kikundi cha watu wengi. Inapendeza kujua kwamba mtume Paulo aliongozwa na roho ya Mungu kutumia maneno ya Zaburi 112:9 kuwahusu Wakristo katika karne ya kwanza. (Soma 2 Wakorintho 9:8, 9.) Zaburi hiyo inaonyesha vizuri kama nini jinsi wafuasi wa Kristo walio duniani leo wanavyoweza kuwa wenye furaha!

7. Kwa nini watumishi wa Mungu wanahitaji kuwa na woga unaofaa wa kutompendeza, na unapaswa kuhisi jinsi gani kuhusu amri za Mungu?

7 Kama inavyoonyeshwa kwenye Zaburi 112:1, Wakristo hao wa kweli wanapata furaha kubwa wanapoendelea kutembea katika ‘kumwogopa Yehova.’ Woga huo unaofaa wa kutompendeza Mungu unawasaidia kushinda roho ya ulimwengu wa Shetani. ‘Wanapendezwa sana’ kujifunza Neno la Mungu na kutii amri zake. Hilo linatia ndani amri ya kuhubiri habari njema ya Ufalme duniani pote. Wanajitahidi kuwafanya watu kutoka katika mataifa yote kuwa wanafunzi huku wakiwaonya waovu kuhusu kuja kwa siku ya hukumu ya Mungu.—Eze. 3:17, 18; Mt. 28:19, 20.

8. (a) Watu wa Mungu waliojitoa wamethawabishwa jinsi gani leo kwa sababu ya bidii yao? (b) Ni baraka gani za wakati ujao zinazowangojea wale walio na tumaini la kidunia?

8 Kwa sababu ya kutii amri hizo, hesabu ya watumishi wa Mungu duniani leo imefikia milioni saba hivi. Ni nani anayeweza kukataa kwamba watu wake wamekuwa “wenye nguvu duniani”? (Yoh. 10:16; Ufu. 7:9, 14) Na ‘watabarikiwa’ kama nini Mungu atakapotimiza kusudi lake! Wakiwa kikundi, wale walio na tumaini la kidunia watalindwa hai kwenye “dhiki kuu” inayokuja, nao watafanyiza “dunia mpya” ambamo “uadilifu utakaa.” Baada ya muda, wale watakaookoka Har–Magedoni ‘watabarikiwa’ hata zaidi. Watakuwa tayari kuwakaribisha mamilioni ya watu watakaofufuliwa. Ni tarajio lenye kusisimua kama nini! Mwishowe, wale ‘wanaopendezwa sana’ na amri za Mungu watafikia ukamilifu wa kibinadamu na watafurahia milele kuwa na “uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.”—2 Pet. 3:13; Rom. 8:21.

Kutumia Utajiri kwa Hekima

9, 10. Wakristo wa kweli wametumia jinsi gani utajiri wao wa kiroho, na uadilifu wao utasimama milele jinsi gani?

9 “Vitu vyenye thamani na utajiri vimo nyumbani mwake; nao uadilifu wake unasimama milele. Ameangaza katika giza kama nuru kwa walio wanyoofu. Yeye ni mwenye neema na mwenye rehema na mwadilifu.” (Zab. 112:3, 4) Katika nyakati za Biblia, watumishi fulani wa Mungu walijulikana kwa sababu ya utajiri wao. Na katika maana nyingine, wale ambao wana kibali cha Mungu wanakuwa matajiri kikweli, hata ikiwa si kimwili. Ukweli ni kwamba, wale ambao wanaamua kujinyenyekeza machoni pa Mungu huenda wakawa maskini na wenye kudharauliwa, kama ilivyokuwa katika siku za Yesu. (Luka 4:18; 7:22; Yoh. 7:49) Lakini iwe mtu ana vitu vingi au vichache vya kimwili, anaweza kuwa tajiri kiroho.—Mt. 6:20; 1 Tim. 6:18, 19; soma Yakobo 2:5.

10 Wakristo watiwa-mafuta, pamoja na waandamani wao, hawawanyimi wengine utajiri wao wa kiroho. Badala yake, ‘wameangaza kama nuru kwa walio wanyoofu’ katika ulimwengu wa Shetani wenye giza. Wanafanya hivyo kwa kuwasaidia wengine wafaidike na hazina za kiroho za hekima na ujuzi wa Mungu. Wapinzani wamejaribu kusimamisha kazi ya kuhubiri Ufalme lakini wameshindwa. Badala yake, matunda ya kazi hiyo ya uadilifu ‘yatasimama milele.’ Kwa kubaki waadilifu chini ya majaribu, watumishi wa Mungu wanaweza kuwa na uhakika wa kuishi daima, ‘kusimama milele.’

11, 12. Watu wa Mungu wanatumia vitu vyao vya kimwili katika njia gani?

11 Watu wa Mungu, wale wa jamii ya mtumwa ambaye ni mtiwa-mafuta na wale wa “umati mkubwa,” wamejithibitisha kuwa wakarimu kuhusiana na vitu vya kimwili. Zaburi 112:9 inasema hivi: “Amegawa kwa wingi; amewapa maskini.” Mara nyingi, Wakristo wa kweli leo wanatoa michango kwa ajili ya Wakristo wenzao na hata kwa ajili ya majirani wao wenye uhitaji. Pia, wanatumia mali za kimwili ili kutegemeza kampeni za kutoa misaada wakati wa misiba. Kama Yesu alivyoonyesha, furaha ya kweli inatokana pia na kutoa.—Soma Matendo 20:35; 2 Wakorintho 9:7.

12 Zaidi ya hayo, fikiria gharama za kuchapisha gazeti hili katika lugha 172, na nyingi ya lugha hizo zinazungumzwa na watu ambao ni maskini. Fikiria pia ukweli wa kwamba gazeti hili linapatikana katika lugha mbalimbali za ishara zinazotumiwa na viziwi, na pia katika maandishi ya vipofu.

Mwenye Neema na Haki

13. Ni nani wanaoweka vielelezo bora katika kutoa kwa fadhili, na tunaweza kuiga kielelezo chao jinsi gani?

13 “Mtu mwenye neema na anayekopesha ni mwema.” (Zab. 112:5) Bila shaka, umeona kwamba watu ambao wanawasaidia wengine si wenye neema au fadhili sikuzote. Watu fulani wanasaidia ili kuonyesha kwamba wana mali nyingi au wanashurutishwa kusaidia. Haifurahishi kusaidiwa na mtu ambaye anakufanya uhisi kwamba wewe ni mtu wa hali ya chini au wewe ni msumbufu au mzigo. Kinyume na hilo, ni jambo lenye kuburudisha kama nini kusaidiwa na mtu ambaye ni mwenye fadhili. Yehova ni kielelezo bora kabisa katika kuonyesha fadhili, ni Mtoaji mwenye furaha. (1 Tim. 1:11; Yak. 1:5, 17) Yesu Kristo alimwiga kikamilifu Baba yake mwenye fadhili. (Marko 1:40-42) Kwa hiyo, ili tuonwe na Mungu kuwa waadilifu, tunatoa kwa furaha na kwa fadhili, hasa katika utumishi wa shambani tunapowatolea majirani wetu msaada wa kiroho.

14. Tunaweza ‘kutegemeza mambo yetu kwa haki’ katika njia gani?

14 “Yeye hutegemeza mambo yake kwa haki.” (Zab. 112:5) Kama ilivyotabiriwa, jamii ya msimamizi-nyumba mwaminifu inatunza mali za Bwana wake kulingana na haki ya Yehova. (Soma Luka 12:42-44.) Hilo linaonekana katika mwongozo wa Kimaandiko unaotolewa kwa wazee, ambao nyakati nyingine wanashughulikia visa vya dhambi nzito kutanikoni. Njia ya haki ya kushughulikia mambo inaonekana wazi pia katika mwongozo unaotegemea Biblia ambao jamii ya mtumwa inatoa kuhusu jinsi makutaniko yote, makao ya wamishonari, na Betheli zinavyopaswa kuendeshwa. Si wazee tu wanaopaswa kutenda kwa haki bali pia Wakristo wengine wanapaswa kuonyesha haki wanaposhughulika na Wakristo wenzao na watu wasio waamini, na pia wanaposhughulikia mambo ya kibiashara.—Soma Mika 6:8, 11.

Baraka kwa Mwadilifu

15, 16. (a) Habari mbaya za ulimwengu zina matokeo gani juu ya waadilifu? (b) Watumishi wa Mungu wameazimia kuendelea kufanya nini?

15 “Kwa kuwa hatatikiswa kamwe. Mwadilifu atakuwa kumbukumbu mpaka wakati usio na kipimo. Hataogopa hata habari mbaya. Moyo wake ni imara, umefanywa umtegemee Yehova. Moyo wake hauwezi kutikiswa; hataogopa, mpaka awatazame wapinzani wake.” (Zab. 112:6-8) Katika historia yote, hakujawahi kamwe kuwa na habari nyingi mbaya kama leo, kutia ndani habari za vita, ugaidi, magonjwa mapya na magonjwa ya zamani ambayo yameanza tena kutokea, uhalifu, umaskini, na uharibifu wa mazingira. Wale ambao Mungu anawaona kuwa waadilifu hawawezi kuepuka matokeo mabaya ya habari hizo mbaya, lakini hawafi moyo kwa sababu ya woga. Badala yake, mioyo yao iko “imara” na ‘haitikiswi’ kwa kuwa wanatazamia wakati ujao wakiwa na uhakika, huku wakijua kwamba ulimwengu mpya wa Mungu wenye uadilifu unakaribia. Wanaweza kuvumilia misiba inayotokea kwa sababu wanategemea msaada wa Yehova. Haruhusu kamwe waadilifu wake ‘watikisike,’ anawapa nguvu ili wavumilie.—Flp. 4:13.

16 Waadilifu wa Mungu wanapaswa pia kuvumilia chuki na uwongo unaoenezwa na wapinzani, lakini mbinu hizo zimeshindwa na zitaendelea kushindwa kuwanyamazisha Wakristo wa kweli. Badala yake, watumishi wa Mungu wanaendelea kubaki imara na wasiotikiswa katika kazi ambayo wamepewa na Yehova ya kuhubiri habari njema ya Ufalme na kujifunza na wote wanaokubali. Bila shaka, waadilifu wataendelea kupata upinzani kadiri mwisho unavyokaribia. Chuki hiyo itafikia upeo wakati Shetani Ibilisi atakapowashambulia ulimwenguni pote akiwa Gogu wa Magogu. Mwishowe, ‘tutawatazama wapinzani wetu’ wakiangamizwa kabisa. Litakuwa jambo lenye kusisimua kama nini kuona jina la Yehova likitakaswa kabisa!—Eze. 38:18, 22, 23.

‘Kuinuliwa kwa Utukufu’

17. Mwadilifu ‘atainuliwa kwa utukufu’ jinsi gani?

17 Itakuwa shangwe kama nini kumsifu Yehova kwa umoja, bila upinzani kutoka kwa Ibilisi na ulimwengu wake! Wote ambao wanadumisha msimamo wa uadilifu machoni pa Mungu watamsifu kwa furaha milele. Hawatashindwa, kwa kuwa Yehova anaahidi pia kwamba “pembe” ya mwadilifu “itainuliwa kwa utukufu.” (Zab. 112:9) Mwadilifu wa Yehova atashangilia kwa ushindi atakapoona maadui wote wa enzi kuu ya Yehova wakishindwa.

18. Maneno ya kumalizia ya Zaburi ya 112 yatatimia jinsi gani?

18 “Mwovu ataona na hakika atakasirika. Atasaga meno yake na kuyeyuka. Tamaa ya waovu itaangamia.” (Zab. 112:10) Wote ambao wanaendelea kuwapinga watu wa Mungu ‘watayeyuka’ katika tamaa na chuki yao hivi karibuni. Tamaa yao ya kutaka kuona kazi yetu ikikomeshwa itaangamia pamoja nao wakati wa “dhiki kuu” inayokuja.—Mt. 24:21.

19. Tunaweza kuwa na hakika kuhusu jambo gani?

19 Je, utakuwa kati ya waokokaji wenye furaha wa ushindi huo mkubwa? Au ikitukia kwamba kwa sababu ya ugonjwa au uzee unakufa kabla ya mwisho wa ulimwengu wa Shetani, je, utakuwa kati ya “waadilifu” ambao watafufuliwa? (Mdo. 24:15) Jibu linaweza kuwa ndiyo ikiwa unaendelea kuwa na imani katika dhabihu ya ukombozi ya Yesu na ikiwa unamwiga Yehova, kama wanavyofanya wale wanaowakilishwa na yule “mtu” mwadilifu anayezungumziwa katika Zaburi ya 112. (Soma Waefeso 5:1, 2.) Yehova atahakikisha kwamba “kumbukumbu” na matendo ya uadilifu ya watu kama hao hayatasahauliwa kamwe. Watakumbukwa na kupendwa na Yehova milele na milele.—Zab. 112:3, 6, 9.

[Maelezo ya chini]

^ fu. 5 Uhakika wa kwamba zaburi hizo mbili zinakamilishana unaonekana katika mpangilio wake na pia katika mambo yaliyomo. Sifa za Mungu ambazo zinatukuzwa katika Zaburi ya 111 zinaigwa na “mtu” anayezungumziwa katika Zaburi ya 112 ambaye anamwogopa Mungu, kama tunavyoweza kuona tunapolinganisha Zaburi 111:3, 4 na Zaburi 112:3, 4.

Maswali ya Kutafakari

• Tuna sababu gani mbalimbali za kusema “Haleluya” kwa sauti?

• Ni matukio gani leo yanayowafanya Wakristo wa kweli wawe na furaha sana?

• Yehova anapenda mtoaji wa aina gani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 25]

Ili kuendelea kuwa na msimamo wa uadilifu machoni pa Mungu, ni lazima tuwe na imani katika damu ya Yesu iliyomwagwa

[Picha katika ukurasa wa 26]

Michango inayotolewa kwa moyo wa kupenda inasaidia katika kazi ya kutoa misaada na kusambaza vichapo vya Biblia