Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuzaliwa Upya—Je, Ni Uamuzi wa Mtu Binafsi?

Kuzaliwa Upya—Je, Ni Uamuzi wa Mtu Binafsi?

Kuzaliwa Upya—Je, Ni Uamuzi wa Mtu Binafsi?

NI NANI anayefanya mtu azaliwe upya? Wahubiri fulani wananukuu maneno haya ya Yesu wanapowahimiza wasikilizaji wao wazaliwe tena: “Ninyi lazima mzaliwe tena.” (Yohana 3:7) Wahubiri hao wanatumia maneno hayo kana kwamba ni amri, wakiwaambia watu wazaliwe tena. Hivyo wanahubiri kwamba kila mwamini anapaswa kumtii Yesu na kuchukua hatua zinazohitajiwa ili azaliwe upya. Kulingana na maoni yao, mtu binafsi anaweza kuchagua kuzaliwa upya. Lakini je, maoni hayo yanapatana na mambo ambayo Yesu alimwambia Nikodemo?

Unaposoma kwa makini maneno ya Yesu, utaona kuwa yeye hakufundisha kwamba mtu binafsi ndiye anayechagua kuzaliwa upya. Kwa nini tunasema hivyo? Neno la Kigiriki linalotafsiriwa ‘kuzaliwa tena’ linaweza pia kutafsiriwa “kuzaliwa kutoka juu.” * Hivyo, mtu anazaliwa upya “kutoka juu,” yaani, “kutoka mbinguni,” au “kutoka kwa Baba.” (Yohana 19:11; Yakobo 1:17) Ndiyo, Mungu ndiye anayefanya mtu azaliwe upya.—1 Yohana 3:9.

Tukikumbuka kwamba neno la awali la Kigiriki linaweza kumaanisha kuzaliwa “kutoka juu,” si vigumu kuelewa kwa nini mtu binafsi hawezi kuchagua kuzaliwa upya. Fikiria kuzaliwa kwako mwenyewe. Je, uliweza kuchagua kuzaliwa? Hapana. Vivyo hivyo, si juu ya mwamini kuchagua kuzaliwa upya. Tunaweza kuzaliwa upya tu kwa sababu Mungu, Baba yetu wa mbinguni, anafanya tuzaliwe upya. (Yohana 1:13) Hivyo, kwa kufaa mtume Petro anasema hivi: “Abarikiwe Mungu na Baba ya Bwana wetu Yesu Kristo, kwa maana kulingana na rehema yake kubwa alituzaa sisi upya.”—1 Petro 1:3.

Je, Yesu Alituamuru Tuzaliwe Tena?

Huenda wengine wakauliza, ‘Ikiwa ni kweli kwamba mtu binafsi hawezi kuchagua kuzaliwa tena, kwa nini Yesu alitoa amri hii: “Ninyi lazima mzaliwe tena”?’ Hilo ni swali zuri. Kwa sababu, kama maneno ya Yesu ni amri, basi angekuwa akituagiza tufanye jambo tusiloweza, na Yesu hangetoa amri kama hiyo. Hivyo basi, maneno lazima “mzaliwe tena” yaeleweke jinsi gani?

Unapotazama kwa makini lugha ya awali utaona kwamba maneno hayo hayaonyeshi kwamba Yesu alitoa amri. Alikuwa akitoa maelezo tu. Kwa maneno mengine, Yesu aliposema lazima “mzaliwe tena,” alikuwa akieleza ukweli wa mambo, hakutoa amri. Alisema: “Hamna budi kuzaliwa kutoka juu.”—Yohana 3:7, Modern Young’s Literal Translation.

Ili kuelewa tofauti kati ya kutoa amri na kueleza jambo, fikiria mfano huu. Wazia jiji ambalo lina shule kadhaa. Mojawapo ya shule hizo imetengwa kwa ajili ya wanafunzi ambao ni watoto wa wenyeji wanaoishi mbali na jiji. Siku moja, mwanamume kijana ambaye si mwenyeji anamwambia mkuu wa shule hivi: “Ninataka kujiunga na shule yenu.” Mkuu huyo anamwambia, “Ili ujiunge na shule hii, lazima uwe mwenyeji.” Kwa kweli, maneno ya mkuu wa shule si amri. Hamwagizi mwanafunzi huyo, “Uwe mwenyeji!” Mkuu wa shule anaeleza tu ukweli wa mambo, yaani, takwa la kujiunga na shule hiyo. Vivyo hivyo, Yesu aliposema: “Ninyi lazima mzaliwe tena,” alikuwa tu anaeleza ukweli wa mambo, yaani, takwa la “kuingia katika Ufalme wa Mungu.”

Wazo hilo la mwisho, yaani, Ufalme wa Mungu, linahusiana na swali lingine kuhusu kuzaliwa upya. Swali hilo ni: Kusudi la kuzaliwa upya ni nini? Kujua jibu la swali hilo ni muhimu ili kuelewa kwa usahihi maana ya kuzaliwa tena.

[Maelezo ya chini]

^ fu. 3 Katika Biblia kadhaa, Yohana 3:3 limetafsiriwa kwa njia hiyo. Kwa mfano, A Literal Translation of the Bible inasema: “Mtu asipozaliwa kutoka juu, hawezi kuuona Ufalme wa Mungu.”

[Picha katika ukurasa wa 6]

Kuzaliwa upya na kuzaliwa kihalisi kunafanana jinsi gani?