Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuzaliwa Upya—Kunatimiza Nini?

Kuzaliwa Upya—Kunatimiza Nini?

Kuzaliwa Upya—Kunatimiza Nini?

KWA nini Yesu alitumia maneno ‘kuzaliwa kwa roho’ alipozungumzia kubatizwa kwa roho takatifu? (Yohana 3:5) Neno “kuzaliwa” linapotumiwa kwa njia ya mfano linamaanisha “mwanzo.” Hivyo, maneno “kuzaliwa upya” yanamaanisha “mwanzo mpya.” Kwa hiyo, maneno ya mfano “kuzaliwa” na “kuzaliwa upya” yanakazia kwamba uhusiano kati ya Mungu na wale wanaobatizwa kwa roho takatifu utakuwa na mwanzo mpya. Badiliko hilo katika uhusiano linatokea jinsi gani?

Alipoeleza jinsi Mungu anavyowatayarisha wanadamu ili watawale mbinguni, mtume Paulo alitumia mfano wa familia. Aliwaandikia Wakristo wa siku zake kwamba ‘wangefanywa kuwa wana’ na kwa hiyo Mungu angewatendea “kama wana.” (Wagalatia 4:5; Waebrania 12:7) Ili kuona jinsi mfano wa kufanywa kuwa mwana unavyomsaidia mtu kuelewa badiliko linalotokea mtu anapobatizwa kwa roho takatifu, fikiria tena ule mfano wa mwanamume kijana anayetaka kujiunga na shule ya wanafunzi ambao ni watoto wa wenyeji.

Badiliko Linalotokana na Kufanywa Kuwa Mwana

Katika mfano huo, kijana huyo hawezi kujiunga na shule hiyo kwa sababu yeye si mwenyeji. Sasa, wazia kwamba siku moja, badiliko kubwa linatokea. Kijana huyo anafanywa kuwa mwana kisheria na baba katika familia ya wenyeji. Jambo hilo linaleta mabadiliko gani kwa yule kijana? Kwa sababu amefanywa kuwa mwana, sasa anaweza kuwa na haki sawa na vijana wenyeji—kutia ndani haki ya kujiunga na ile shule. Kufanywa kuwa mwana kisheria kumebadili kabisa maisha yake.

Jambo hilo linafanana na yale yanayowapata wale wanaozaliwa upya, ingawa kwa njia kubwa zaidi. Fikiria mambo kadhaa yanayofanana. Yule kijana katika mfano atakubaliwa katika ile shule mradi tu atimize takwa la kujiunga na shule hiyo, yaani, kuwa mwenyeji kisheria. Lakini hawezi kutimiza takwa hilo bila msaada. Vivyo hivyo, wanadamu fulani watakuwa watawala katika Ufalme wa Mungu, au serikali ya mbinguni, mradi tu watimize takwa la kuingia humo, yaani, “kuzaliwa tena.” Hata hivyo, hawawezi kutimiza takwa hilo bila msaada kwa sababu Mungu ndiye anayefanya mtu azaliwe upya.

Ni nini kilichobadili hali ya yule kijana? Kufanywa kuwa mwana kisheria. Bila shaka, asili ya kijana yule haikubadilika alipofanywa kuwa mwana, bado alikuwa mtu yuleyule. Hata hivyo, baada ya kufanywa kuwa mwana kisheria, hali ya kijana huyo ilibadilika. Alikuwa na mwanzo mpya, kana kwamba amezaliwa upya. Alikubaliwa kuwa mwana kisheria, jambo lililompa haki ya kujiunga na ile shule na pia kuwa mtoto wa familia ya yule baba aliyemfanya kuwa mwana.

Vivyo hivyo, Yehova alibadili hali ya wanadamu wasio wakamilifu kwa kuanzisha mpango wa kisheria wa kuwafanya kuwa watoto wake. Mtume Paulo aliyekuwa mmoja wa watoto hao aliwaandikia Wakristo wenzake hivi: “Mlipokea roho ya kufanywa kuwa wana, roho ambayo kupitia hiyo tunapaaza sauti: ‘Abba, Baba!’ Roho yenyewe hutoa ushahidi pamoja na roho yetu kwamba sisi ni watoto wa Mungu.” (Waroma 8:15, 16) Ndiyo, kwa kufanywa kuwa wana, Wakristo hao walifanywa kuwa sehemu ya familia ya Mungu, au “watoto wa Mungu.”—1 Yohana 3:1; 2 Wakorintho 6:18.

Kusema kweli, asili ya wale ambao Mungu aliwafanya kuwa wana haikubadilika, kwa kuwa bado walikuwa watu wasio wakamilifu. (1 Yohana 1:8) Hata hivyo, kama Paulo alivyoendelea kueleza, baada ya matakwa ya kisheria ya kufanywa kuwa wana kutimizwa, hali yao ilibadilika. Wakati huohuo, roho ya Mungu iliwapa usadikisho wenye nguvu sana kwamba wangeishi mbinguni pamoja na Kristo. (1 Yohana 3:2) Usadikisho huo waliopewa na roho takatifu uliwafanya wawe na maoni tofauti kabisa kuhusu maisha. (2 Wakorintho 1:21, 22) Ndiyo, walikuwa na mwanzo mpya—walizaliwa upya kwa njia ya mfano.

Biblia inasema hivi kuwahusu wanadamu waliofanywa kuwa wana na Mungu: “Watakuwa makuhani wa Mungu na wa Kristo, nao watatawala wakiwa wafalme pamoja naye ile miaka elfu.” (Ufunuo 20:6) Wanadamu waliofanywa kuwa wana na Mungu watakuwa wafalme katika Ufalme wa Mungu, au serikali ya mbinguni, pamoja na Kristo. Mtume Petro aliwaambia Wakristo wenzake kwamba wangepokea “urithi usioharibika na usiotiwa unajisi na usiofifia” ambao “umewekwa akiba mbinguni” kwa ajili yao. (1 Petro 1:3, 4) Huo ni urithi wenye thamani kama nini!

Hata hivyo, habari hiyo kuhusu utawala pia inazusha swali hili: Ikiwa wale waliozaliwa tena watatawala wakiwa wafalme mbinguni, watatawala akina nani? Swali hilo litajibiwa katika habari inayofuata.

[Picha katika ukurasa wa 10]

Paulo alisema nini kuhusu kufanywa kuwa wana?