Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wachache Watawala, Wengi Wanufaika

Wachache Watawala, Wengi Wanufaika

Wachache Watawala, Wengi Wanufaika

TANGU siku za mitume, Mungu amekuwa akichagua Wakristo wachache waaminifu kutoka kati ya wanadamu na kuwafanya kuwa wana. Badiliko la hawa waliofanywa kuwa wana ni kamili sana hivi kwamba Neno la Mungu linalifafanua kuwa kuzaliwa upya. Kusudi la kuzaliwa upya ni kuwatayarisha watumishi hao wa Mungu kuwa watawala mbinguni. (2 Timotheo 2:12) Ili wawe watawala, wanafufuliwa kuishi mbinguni. (Waroma 6:3-5) Huko mbinguni, “watatawala wakiwa wafalme juu ya dunia” pamoja na Kristo.—Ufunuo 5:10; 11:15.

Hata hivyo, Neno la Mungu pia linasema kwamba watu wengine mbali na hao waliozaliwa upya watapokea wokovu wa milele. Biblia (katika Maandiko ya Kiebrania na pia Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo), inataja kwamba Mungu ataokoa makundi mawili ya watu—kundi dogo la watawala watakaoishi mbinguni na kundi kubwa la raia watakaoishi duniani. Kwa mfano, ona yale ambayo mtume Yohana aliwaandikia Wakristo wenzake waliokuwa wamezaliwa upya. Alisema hivi kumhusu Yesu: “Yeye ni dhabihu ya upatanisho kwa ajili ya dhambi zetu [lile kundi dogo], lakini si kwa ajili ya zetu tu bali pia kwa ajili ya zile za ulimwengu wote [lile kundi kubwa].”—1 Yohana 2:2.

Vivyo hivyo, mtume Paulo aliandika: “Uumbaji [lile kundi kubwa] unangojea na kutazamia kwa hamu kufunuliwa kwa wana wa Mungu [lile kundi dogo].” (Waroma 8:19-21) Maneno hayo ya mtume Yohana na Paulo yaeleweke jinsi gani? Kwa njia hii: Wale wanaozaliwa upya watakuwa watawala katika serikali ya mbinguni. Kwa kusudi gani? Ili wawaletee manufaa ya milele mamilioni ya watu watakaoishi duniani wakiwa raia wa serikali ya Mungu. Kwa hiyo, Yesu aliwafundisha wanafunzi wake wasali hivi: “Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.Mathayo 6:10.

Maandiko ya Kiebrania pia yanataja makundi mawili ya watu watakaookolewa. Kwa mfano, ona yale Yehova aliyomwambia Abrahamu, babu ya Yesu: “Kupitia kwa uzao wako [lile kundi dogo] mataifa yote ya dunia [lile kundi kubwa] hakika yatajibariki kwa sababu wewe umeisikiliza sauti yangu.” (Mwanzo 22:18) Ndiyo, mataifa yote yangepata baraka kupitia “uzao” wa Abrahamu.

“Uzao” huo ni nani? Ni Yesu Kristo pamoja na wale waliozaliwa upya na kufanywa kuwa wana wa Mungu. Mtume Paulo anaeleza: “Ikiwa ninyi ni wa Kristo, ninyi kwa kweli ni uzao wa Abrahamu.” (Wagalatia 3:16, 29) Watu wa mataifa yote watapata baraka gani kupitia “uzao” huo? Watapata pendeleo la kukubalika machoni pa Mungu na kufurahia uzima wa milele katika dunia paradiso. Mtunga-zaburi Daudi alitabiri hivi: “Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.”—Zaburi 37:29; Isaya 45:18; Ufunuo 21:1-5.

Ni kweli kwamba watu wachache tu ndio wanaochaguliwa kutawala mbinguni, lakini manufaa ya ufalme huo wa mbinguni—uzima wa milele duniani na baraka nyinginezo—ni kwa ajili ya wengi. Tunatumaini kwamba wewe na familia yako mtakuwa kati ya wale watakaopata manufaa ya milele ambayo Ufalme wa Mungu utaleta.

[Picha katika ukurasa wa 12]

Mamilioni ya watu watabarikiwa kwa uzima wa milele duniani. Je, utakuwa mmoja wao?