Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Kwa nini Yesu alimwita Yehova “Abba, Baba,” aliposali?

Neno la Kiaramu ʼab·baʼʹ linaweza kumaanisha “baba” au “Ee Baba.” Linapatikana mara tatu katika Maandiko katika sala mbalimbali na linarejelea Baba wa mbinguni, Yehova. Neno hilo lilimaanisha nini Yesu alipokuwa duniani?

Kitabu kimoja (The International Standard Bible Encyclopedia) kinasema hivi: “Katika mazungumzo ya kawaida katika siku za Yesu, neno ʼabbāʼ lilitumiwa hasa na watoto wenye heshima waliokuwa na uhusiano wa karibu na baba zao.” Neno ʼabbāʼ lilitumiwa na mtoto alipozungumza na baba aliyempenda na lilikuwa kati ya maneno ya kwanza ambayo mtoto alijifunza. Yesu alitumia neno hilo alipomsihi sana Baba yake katika sala. Katika bustani ya Gethsemane, saa chache kabla ya kifo chake, Yesu alitumia maneno “Abba, Baba,” aliposali kwa Yehova.—Marko 14:36.

Kitabu kilichotajwa hapo juu kinasema: “Vitabu vya Wayahudi vya kipindi cha milki za Wagiriki na Waroma, havitumii sana neno ʼabbāʼ vinapozungumzia sala kwa Mungu, yaelekea kwa sababu lingeonekana kuwa jambo lisilo la heshima kutumia neno hilo la kirafiki katika kumwomba Mungu.” Hata hivyo, “matumizi ya Yesu . . . ya neno hili katika sala yanathibitisha kwa njia isiyo ya moja kwa moja dai Lake kwamba alikuwa na uhusiano wa karibu sana na Mungu.” Katika maandishi ya Paulo tunapata maandiko mawili yaliyo na neno “Abba” yanayoonyesha kwamba Wakristo wa karne ya kwanza pia walilitumia katika sala zao.—Waroma 8:15; Wagalatia 4:6.

Kwa nini sehemu ya Biblia iliandikwa katika Kigiriki?

Mtume Paulo alisema kwamba Wayahudi “walikabidhiwa maneno matakatifu ya Mungu.” (Waroma 3:1, 2) Hivyo, sehemu ya kwanza ya Biblia iliandikwa hasa katika Kiebrania, lugha ya Wayahudi. Lakini, Maandiko ya Kikristo yaliandikwa katika Kigiriki. * Kwa nini?

Katika miaka ya 300 K.W.K., askari-jeshi wa Aleksanda Mkuu walizungumza lahaja kadhaa za Kigiriki, ambazo pole kwa pole zilichanganyika na kuwa Koine, au Kigiriki cha kawaida. Aleksanda alipoteka nchi mbalimbali, Koine ilienea na kuwa lugha ya kimataifa ya siku hizo. Wakati huo, Wayahudi walikuwa wametawanyika sana. Walikuwa wamepelekwa uhamishoni Babiloni mwaka wa 607 K.W.K. na wengi wao hawakurudi Palestina baada ya kuachiliwa. Kwa sababu hiyo, mwishowe Wayahudi wengi hawakujua Kiebrania sanifu na badala yake walianza kuzungumza Kigiriki. (Matendo 6:1) Ili kuwasaidia, Maandiko ya Kiebrania yalitafsiriwa katika Kigiriki cha kawaida, au Koine. Maandiko hayo yanaitwa Septuajinti.

Kamusi moja (Dictionnaire de la Bible) inasema kwamba hakuna lugha nyingine iliyokuwa na “maneno mengi, ilikuwa rahisi kuitumia kueleza mambo, na iliyowapendeza watu wa mataifa mbalimbali kama lugha ya Kigiriki.” Lugha hiyo ilikuwa na msamiati hususa, sarufi bora, na vitenzi vilivyoeleza maana kwa undani, na “watu wengi katika milki hii waliongea na kuelewa Kigiriki, kwa hiyo ilifaa sana kwa kuwasiliana na kueneza habari. Ilikuwa lugha iliyofaa sana kwa kueneza Ukristo.” Hivyo, ni jambo linalofaa kwamba Maandiko ya Kikristo yaliandikwa katika Kigiriki.

[Maelezo ya chini]

^ fu. 7 Sehemu ndogo ya Maandiko ya Kiebrania iliandikwa katika Kiaramu. Inaonekana kwamba Injili ya Mathayo iliandikwa kwanza katika Kiebrania, kisha huenda Mathayo mwenyewe aliitafsiri katika Kigiriki.

[Picha katika ukurasa wa 13]

Kipande cha Hati ya Kigiriki ya Septuajinti

[Hisani]

Courtesy of Israel Antiquities Authority