Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehoashi Alimwacha Yehova kwa Sababu ya Marafiki Wabaya

Yehoashi Alimwacha Yehova kwa Sababu ya Marafiki Wabaya

Wafundishe Watoto Wako

Yehoashi Alimwacha Yehova kwa Sababu ya Marafiki Wabaya

HALI zilikuwa zenye kutisha sana katika jiji la Yerusalemu palipokuwa hekalu la Mungu. Mfalme Ahazia alikuwa ameuawa. Wazia yale ambayo mama ya Ahazia anayeitwa Athalia, alifanya muda mfupi tu baada ya Mfalme Ahazia kuuawa! Aliamuru wana wa Ahazia wauawe, yaani, alitaka wajukuu wake mwenyewe wauawe! Unajua kwa nini?— * Ni kwa sababu alitaka kuwa mtawala badala ya yeyote kati yao.

Hata hivyo, mjukuu mmoja wa Athalia, mtoto mchanga Yehoashi hakuuawa, lakini nyanya yake hakujua. Ungependa kujua jinsi alivyoepuka kuuawa?— Shangazi wa Yehoashi anayeitwa Yehosheba alimficha yule mtoto mchanga katika hekalu la Mungu. Aliweza kufanya hivyo kwa sababu Kuhani Mkuu Yehoyada alikuwa mume wake. Yehosheba na Yehoyada walihakikisha kwamba Yehoashi alikuwa salama salimini.

Yehoashi alifichwa hekaluni kwa miaka sita. Akiwa humo alifundishwa kumhusu Yehova Mungu na sheria zake. Hatimaye, Yehoashi alipokuwa na miaka saba, Yehoyada alichukua hatua ya kumfanya kuwa mfalme. Ungependa kujua jinsi Yehoyada alivyofanya jambo hili na yaliyompata nyanya ya Yehoashi, yule Malkia mwovu Athalia?—

Yehoyada aliwakusanya kisiri walinzi waliokuwa wakiwalinda wafalme huko Yerusalemu siku hizo. Aliwaeleza jinsi yeye na mkewe walivyokuwa wamemficha mtoto mchanga wa Mfalme Ahazia ili asiuawe. Halafu Yehoyada akamleta Yehoashi mbele ya walinzi hao ambao walitambua kwamba yeye ndiye anayepaswa kuwa mtawala. Kisha wakapanga yale ambayo wangefanya.

Yehoyada akamleta Yehoashi nje na kumtawaza, yaani, alimfanya kuwa mfalme. Alipofanya hivyo, watu “wakaanza kupiga makofi na kusema: ‘Mfalme na aishi!’” Wale walinzi wakamzunguka Yehoashi ili kumlinda. Athalia aliposikia kelele ya shangwe, alikimbia nje na kujaribu kuzuia jambo hilo. Lakini Yehoyada aliwaamuru wale walinzi wamuue Athalia.—2 Wafalme 11:1-16.

Kwa muda wote ambao Yehoyada aliishi, Yehoashi aliendelea kumsikiliza Yehoyada na kufanya mema. Hata Yehoashi alihakikisha kwamba watu walichanga pesa ili kukarabati hekalu la Mungu ambalo baba yake Ahazia na babu yake Yehoramu walikuwa wamelipuuza. Lakini namna gani baada ya Kuhani Mkuu Yehoyada kufa, unafikiri Yehoashi aliendelea kufanya mema?— Hebu tuone.—2 Wafalme 12:1-16.

Yehoashi alikuwa na miaka 40 hivi Yehoyada alipokufa. Badala ya kuendelea kushirikiana na wale waliomtumikia Yehova, Yehoashi alifanya urafiki na watu walioabudu miungu ya uwongo. Mwana wa Yehoyada anayeitwa Zekaria alikuwa kuhani wa Yehova wakati huo. Unafikiri Zekaria alifanya nini aliposikia mambo mabaya ambayo Yehoashi alikuwa akifanya?—

Zekaria alimwambia Yehoashi hivi: ‘Kwa sababu umemwacha Yehova, yeye naye atakuacha wewe.’ Maneno haya yalimkasirisha sana Yehoashi hivi kwamba aliamuru Zekaria auawe kwa kupigwa mawe. Wazia, Yehoashi aliyesaidiwa kuepuka muuaji, aliamuru Zekaria auawe!—2 Mambo ya Nyakati 24:1-3, 15-22.

Tunaweza kujifunza nini kutokana na masimulizi haya?— Hatutaki kamwe kuwa kama Athalia, aliyekuwa mwenye chuki na mkatili. Badala yake tunapaswa kuwapenda waabudu wenzetu na hata maadui wetu, kama Yesu alivyotufundisha. (Mathayo 5:44; Yohana 13:34, 35) Na kumbuka, tukianza kutenda mema, kama Yehoashi alivyofanya, ni lazima tuendelee kuwa marafiki wa watu wanaompenda Yehova, ambao watatusaidia kuendelea kufanya mema na kututia moyo tumtumikie Mungu.

[Maelezo ya chini]

^ fu. 3 Ikiwa unasoma pamoja na mtoto, kistari kirefu kinakukumbusha kwamba unapaswa kutua na kumtia mtoto moyo ajieleze.

Maswali:

○ Yehoashi aliepuka kuuawa jinsi gani, na ni nani aliyetaka kumuua?

○ Yehoashi alifanywa kuwa mfalme jinsi gani, na alitenda mambo gani mema?

○ Kwa nini Yehoashi aligeuka kuwa mbaya, na alimuua nani?

○ Tunajifunza nini kutokana na masimulizi haya ya Biblia?

[Picha katika ukurasa wa 25]

Yehoashi aliepuka kuuawa