Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Yesu Ni Mungu?

Je, Yesu Ni Mungu?

Je, Yesu Ni Mungu?

WATU wengi wanaona Utatu kuwa “fundisho kuu la dini ya Kikristo.” Kulingana na fundisho hilo, Baba, Mwana, na roho takatifu ni watu watatu katika Mungu mmoja. Kadinali John O’Connor alisema hivi kuhusu Utatu: “Tunajua kwamba Utatu ni fumbo lisiloweza kufumbuliwa kwa urahisi.” Kwa nini ni vigumu sana kuelewa Utatu?

Kamusi moja (The Illustrated Bible Dictionary) inasema hivi inapozungumzia Utatu: “Utatu si fundisho la Biblia kwa sababu hakuna andiko linaloeleza fundisho hilo.” Kwa kuwa Utatu “si fundisho la Biblia,” watu wanaoamini Utatu wametafuta juu chini maandiko ya Biblia yanayounga mkono fundisho hilo na hata wameyapotosha.

Je, Yohana 1:1 Linafundisha Utatu?

Andiko la Biblia linalopotoshwa mara nyingi ni Yohana 1:1. Katika tafsiri ya Union Version, mstari huo unasema hivi: “Hapo mwanzo kulikuwako Neno, naye Neno alikuwako kwa Mungu [Kigiriki, ton the·onʹ], naye Neno alikuwa Mungu [the·osʹ].” Katika mstari huo neno la Kigiriki the·osʹ (mungu) linapatikana katika miundo miwili. Mara ya kwanza linapoonekana, linatanguliwa na kibainishi wazi ton—neno linalotambulisha kitu au mtu hususa katika Kigiriki. Katika kisa hiki neno the·onʹ, linalotanguliwa na kibainishi wazi ton, linamrejelea Mungu Mweza-Yote. Hata hivyo, katika kisa cha pili, neno the·osʹ halina kibainishi wazi. Je, kibainishi hicho kiliachwa kimakosa?

Injili ya Yohana iliandikwa katika lugha ya Koine, au Kigiriki cha kawaida, ambayo ina sheria hususa kuhusu matumizi ya kibainishi wazi. Msomi wa Biblia A. T. Robertson anasema kwamba ikiwa sehemu zote mbili za sentensi (kiima, sehemu ya sentensi inayotaja mtu au kitu, na kiarifu, sehemu inayotoa maelezo kuhusu mtu huyo au kitu hicho) zina kibainishi wazi, inamaanisha kwamba “kiima na kiarifu zote ni hususa, sawa, na moja inaweza kuchukua mahali pa ile nyingine.” Robertson anatumia Mathayo 13:38 kueleza jambo hilo. Andiko hilo linasema: “Shamba [Kigiriki, ho a·grosʹ] ni ulimwengu [Kigiriki, ho koʹsmos].” Kabla ya neno “shamba” (a·grosʹ) na “ulimwengu” (koʹsmos) kuna kibainishi wazi (ho). Hivyo, sarufi ya Kigiriki inatusaidia kuelewa kwamba ulimwengu pia ni shamba.

Namna gani ikiwa kiima kina kibainishi wazi lakini kiarifu hakina, kama ilivyo katika Yohana 1:1? Msomi James Allen Hewett anasema hivi anapozungumzia mstari huohuo: “Katika sentensi kama hiyo [Yohana 1:1], kiima na kiarifu si sawa, yaani, hazilingani hata kidogo.”

Hewett anafafanua jambo hilo kwa kutumia andiko la 1 Yohana 1:5, ambalo linasema: “Mungu ni nuru.” Katika Kigiriki, “Mungu” ni ho the·osʹ, kwa hiyo neno hilo lina kibainishi wazi ho. Lakini neno phos linalomaanisha “nuru” halina kibainishi. Hewett anasema: “Mtu anaweza . . . kusema kwamba Mungu ni nuru; lakini hawezi kusema kwamba nuru ni Mungu.” Vilevile kuna sentensi kama hiyo kwenye Yohana 4:24, “Mungu ni Roho,” na 1 Yohana 4:16, “Mungu ni upendo.” Katika mistari hiyo miwili, kiima, “Mungu,” kina kibainishi wazi lakini viarifu, “Roho” na “upendo,” havina. Kwa hiyo, katika visa hivyo viima na viarifu si sawa. Mistari hiyo haiwezi kumaanisha “Roho ni Mungu” wala “upendo ni Mungu.”

“Neno” Ni Nani?

Wasomi wengi wa Kigiriki na watafsiri wa Biblia wanakubali kwamba andiko la Yohana 1:1 halielezi “Neno” ni nani, bali linafafanua jinsi alivyo. Mtafsiri wa Biblia, William Barclay, anasema: “Kwa sababu [mtume Yohana] hatumii kibainishi wazi (ho) kabla ya theos, neno hilo ni la ufafanuzi tu . . . Hapo Yohana hasemi Neno ni sawa na Mungu, yaani, hasemi kwamba Yesu ni Mungu.” Msomi Jason David BeDuhn pia anasema: ‘Katika Kigiriki, usipotumia kibainishi wazi kabla ya neno theos katika sentensi kama ile iliyo katika sehemu ya mwisho ya Yohana 1:1, basi wasomaji watafikiri kwamba unamaanisha mungu yeyote tu.’ BeDuhn anaongeza: “Katika Yohana 1:1, Neno si Mwenyezi Mungu, bali yeye ni . . . roho kama Mungu.” Msomi Joseph Henry Thayer aliyesaidia kutafsiri American Standard Version, alisema: “Logos [au, Neno] alikuwa kama Mungu, lakini si Mungu mwenyewe.”

Je, kujua jinsi Mungu alivyo ni jambo gumu kama kufumbua “fumbo lisiloweza kufumbuliwa kwa urahisi”? Yesu hakufikiri hivyo. Aliposali kwa Baba yake, Yesu alionyesha wazi kwamba yeye si sawa na Baba yake kwa kusema: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.” (Yohana 17:3) Ikiwa tunamwamini Yesu na kuelewa mafundisho rahisi ya Biblia, tutamheshimu kwa sababu yeye ni Mwana wa Mungu. Pia, tutamwabudu Yehova kwa sababu yeye ni “Mungu wa pekee wa kweli.”

[Blabu katika ukurasa wa 19]

Kwa nini ni vigumu sana kuelewa fundisho la Utatu?

[Blabu katika ukurasa wa 19]

Yesu alionyesha wazi kwamba yeye si sawa na Baba yake

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 19]

Church at Tagnon, France