Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Biblia Iko Hai Hata Katika Lugha Iliyokufa

Biblia Iko Hai Hata Katika Lugha Iliyokufa

Biblia Iko Hai Hata Katika Lugha Iliyokufa

KATIKA karne chache zilizopita, angalau nusu ya lugha zimetoweka ulimwenguni. Lugha inasemekana kuwa imekufa wakati ambapo hakuna wenyeji wanaoizungumza. Kwa sababu hiyo, Kilatini kinatajwa kuwa “lugha iliyokufa,” ingawa bado watu wengi wanaijifunza na ni lugha rasmi ya Jiji la Vatikani.

Baadhi ya tafsiri muhimu za Biblia ni za Kilatini. Je, tafsiri za Biblia za lugha isiyotumiwa zinaweza kuwa na manufaa yoyote kwa wasomaji wa Biblia leo? Matukio yenye kusisimua kuhusu jinsi Biblia hizo zilivyotafsiriwa yanatusaidia kujibu swali hilo.

Tafsiri za Zamani Zaidi za Kilatini

Lugha ya kwanza ya Roma ilikuwa Kilatini. Hata hivyo, mtume Paulo alipowaandikia Wakristo katika jiji hilo alitumia Kigiriki. * Hilo halikuwa tatizo kwa sababu watu wengi walizungumza lugha zote mbili. Wakaaji wengi wa Roma walitoka katika maeneo ya Asia ambako Kigiriki kilizungumzwa, kwa hiyo ilisemekana kwamba Roma lilikuwa kama jiji la Ugiriki. Watu walizungumza lugha tofauti-tofauti katika maeneo mbalimbali ya Milki ya Roma, lakini kadiri milki hiyo ilivyopanuka, ndivyo Kilatini kilivyozidi kuwa lugha muhimu. Kwa sababu hiyo, Maandiko Matakatifu yaliyokuwapo katika Kigiriki yalianza kutafsiriwa katika Kilatini. Inaelekea kazi hiyo ilianza huko Afrika Kaskazini katika karne ya pili W.K.

Tafsiri hizo mbalimbali zinaitwa Vetus Latina, ama Tafsiri ya Kale ya Kilatini. Hakuna hati ya kale yenye Biblia nzima ya Kilatini ambayo imedumu mpaka leo. Yaelekea Vetus Latina hakikuwa kitabu kimoja kama inavyoonyeshwa na hati zinazopatikana na pia sehemu ambazo zimenukuliwa na waandishi wa kale. Badala yake, yaelekea kazi hiyo ya kutafsiri ilifanywa na watu kadhaa kutoka sehemu mbalimbali na wakati tofauti-tofauti. Kwa hiyo, Vetus Latina si kitabu kimoja bali ni mkusanyo wa tafsiri mbalimbali kutoka Kigiriki.

Watu waliochukua hatua ya kutafsiri sehemu za Maandiko katika Kilatini bila kushirikiana na watafsiri wengine, walisababisha mvurugo kwa kadiri fulani. Mwishoni mwa miaka ya 300 W.K., mwanatheolojia Mkatoliki Agostino alisema kwamba “mtu yeyote aliyeweza kupata hati ya Kigiriki na aliyefikiri kwamba anajua lugha hizo mbili, hata kwa kiwango kidogo tu, alianza kuitafsiri” katika Kilatini. Agostino na wengine waliona kwamba kulikuwa na tafsiri nyingi sana na walitilia shaka usahihi wa tafsiri hizo.

Tafsiri ya Jerome

Jerome ambaye mara kwa mara alitumika akiwa mwandishi wa askofu Damasusi wa Roma mwaka wa 382 W.K., alijaribu kukomesha mvurugo huo. Askofu huyo alimwomba Jerome asahihishe tafsiri ya Kilatini ya vitabu vya Injili, na Jerome alimaliza kazi hiyo baada ya miaka michache tu. Kisha akaanza kusahihisha tafsiri ya Kilatini ya vitabu vingine vya Biblia.

Jerome alitumia tafsiri kadhaa kama msingi wa tafsiri yake ambayo baadaye ilikuja kuitwa Vulgate. Alipotafsiri kitabu cha Zaburi, Jerome alitumia Septuajinti, tafsiri ya Kigiriki ya Maandiko ya Kiebrania iliyotafsiriwa katika miaka ya 100 K.W.K. Alisahihisha vitabu vya Injili, na pia akatafsiri sehemu kubwa ya Maandiko ya Kiebrania yaliyokuwa yameandikwa katika Kiebrania cha awali. Sehemu nyingine za Maandiko huenda zilisahihishwa na wengine. Hatimaye, sehemu mbalimbali za Vetus Latina ziliunganishwa na Vulgate ya Jerome.

Mwanzoni watu wengi hawakupenda tafsiri ya Jerome. Hata Agostino aliichambua. Lakini, muda si muda ilikuja kuonwa kuwa chapa bora kati ya Biblia zilizochapwa zikiwa na vitabu vyote katika kitabu kimoja. Katika miaka ya 700 na 800, wasomi kama Alcuin na Theodulf walianza kusahihisha makosa ya sarufi na ya uandishi katika tafsiri ya Jerome. Makosa hayo yalikuwa yametokea kwa sababu ya kuinakili mara nyingi. Watu wengine waligawanya Maandiko katika sura ili iwe rahisi kuyarejelea. Mashini za kuchapa zilipoundwa, tafsiri ya Jerome ilikuwa Biblia ya kwanza kuchapishwa.

Tafsiri ya Jerome ilipewa jina Vulgate na Kanisa Katoliki katika Baraza la Trent la mwaka wa 1546. Baraza hilo liliamua kwamba Biblia ya Jerome ni “sahihi,” na hivyo ingefaa kutumiwa katika ibada ya Kanisa Katoliki. Wakati huohuo, baraza hilo lilisema kwamba tafsiri hiyo inapaswa kusahihishwa. Kazi hiyo ingesimamiwa na halmashauri za pekee, lakini Papa Sixtus wa Tano alitaka ifanywe haraka, na yaelekea alijiamini mno kwa sababu aliamua kuifanya mwenyewe. Uchapaji wa tafsiri iliyosahihishwa na papa huyo ulikuwa umeanza tu alipokufa mwaka wa 1590. Mara alipokufa, makadinali walikataa tafsiri hiyo ambayo walisema ina makosa mengi nao wakasimamisha uchapaji.

Tafsiri mpya ilichapishwa mwaka wa 1592 wakati wa Papa Klementi wa Nane na hatimaye iliitwa chapa ya Sixtus ya Klementi. Kwa muda mrefu tafsiri hiyo ilikuwa tafsiri rasmi ya Kanisa Katoliki. Vulgate ya Sixtus ya Klementi pia ilitumiwa kutafsiri Biblia za Kanisa Katoliki katika lugha za kienyeji, kama vile tafsiri ya Kiitaliano ya Antonio Martini ya mwaka wa 1781.

Biblia ya Kisasa ya Kilatini

Wachunguzi wa maandishi wa miaka ya 1900 walitambua kwamba Vulgate, kama tafsiri nyingine, ilihitaji kusahihishwa. Kwa hiyo, katika mwaka wa 1965 Kanisa Katoliki liliweka Halmashauri ya Vulgate Mpya na likaiagiza isahihishe tafsiri ya Kilatini kupatana na ujuzi mpya. Tafsiri hiyo mpya ingetumiwa katika ibada ya Kilatini ya Kanisa Katoliki.

Sehemu ya kwanza ya tafsiri hiyo mpya inayoitwa Nova Vulgata ilianza kutumiwa mwaka wa 1969, na Papa Yohana Paulo wa Pili aliiidhinisha mwaka wa 1979. Chapa ya kwanza ilikuwa na jina la Mungu, Iahveh, katika mistari kadhaa, kama vile Kutoka 3:15 na 6:3. Lakini, mtu mmoja katika halmashauri hiyo alisema kwamba watafsiri “walitubu . . . na neno Dominus [‘Bwana’] liliwekwa tena mahali pa Iahveh,” katika chapa rasmi ya pili, iliyochapishwa 1986.

Nova Vulgata ilichambuliwa kama Vulgate ilivyokuwa imechambuliwa miaka mingi kabla ya hapo. Hata wasomi Wakatoliki waliichambua. Mwanzoni ilisemekana kuwa tafsiri ambayo ingeleta umoja kati ya watafsiri wa makanisa mbalimbali. Lakini wengi waliiona kuwa kizuizi cha umoja hasa kwa sababu papa aliitangaza kuwa msingi wa tafsiri za sasa badala ya maandishi ya awali. Nchini Ujerumani, Nova Vulgata ilibishaniwa na Waprotestanti na Wakatoliki wakati wa kusahihisha tafsiri ambayo ingetumiwa na dini zote mbili. Waprotestanti waliwashutumu Wakatoliki kwa sababu walisisitiza kwamba Nova Vulgata iwe msingi wa tafsiri hiyo mpya.

Ijapokuwa watu hawazungumzi Kilatini tena, Biblia ya Kilatini imewanufaisha mamilioni ya wasomaji. Maneno yanayohusiana na mambo ya dini katika lugha nyingi yametokana na Biblia hiyo. Neno la Mungu katika lugha yoyote ile lina nguvu ya kubadili maisha ya mamilioni ya watu wanaojitahidi kuishi kupatana na mafundisho yake bora.—Waebrania 4:12.

[Maelezo ya chini]

^ fu. 5 Kwa habari zaidi kuhusu kile kilichofanya Maandiko ya Kikristo yaandikwe katika Kigiriki, ona makala “Je, Wajua?” kwenye ukurasa wa 13.

[Blabu katika ukurasa wa 23]

Papa Yohana Paulo wa Pili aliidhinisha Nova Vulgata. Chapa ya kwanza ina jina la Mungu, Iahveh

[Sanduku katika ukurasa wa 21]

MANENO YANAYOENDELEA KUTUMIWA

Katika Vetus Latina kulikuwa na maneno mengi yaliyotafsiriwa kutoka katika Kigiriki ambayo yanaendelea kutumiwa. Mojawapo ya maneno hayo ni di·a·theʹke, linalotafsiriwa “agano.” (2 Wakorintho 3:14) Kwa sababu hiyo, katika lugha nyingi Maandiko ya Kiebrania na ya Kigiriki yanaitwa Agano la Kale na Agano Jipya.

[Sanduku katika ukurasa wa 23]

MAAGIZO YALIYOCHAMBULIWA

Mnamo 2001, baada ya kufanya kazi kwa miaka minne, baraza la usimamizi la Kanisa Katoliki lilichapisha maagizo kuhusu kawaida inayokubalika ya ushirika mtakatifu (Liturgiam authenticam). Maagizo hayo yamechambuliwa sana na wasomi wengi Wakatoliki.

Kulingana na maagizo hayo, Nova Vulgata ndiyo Biblia rasmi ya kanisa hilo, hivyo inapaswa kutumiwa kutafsiri Biblia katika lugha nyingine zote, hata ikiwa inapotosha maana ya kinachosemwa na maandishi ya awali. Biblia itakubaliwa na wasimamizi wa Kanisa Katoliki ikiwa tu inapatana na maagizo hayo. Maagizo hayo yanasema kwamba katika tafsiri za Kikatoliki, “jina la Mungu mweza-yote linalowakilishwa na tetragramatoni ya Kiebrania (YHWH)” linapaswa kutafsiriwa “katika lugha zote kwa kutumia neno” Dominus linalomaanisha “Bwana,” kama ilivyo katika chapa ya pili ya Nova Vulgata—hata ingawa chapa ya kwanza ilitumia “Iahveh.” *

[Maelezo ya chini]

[Picha katika ukurasa wa 22]

Tafsiri ya Alcuin ya Biblia ya Kilatini, 800 W.K.

[Hisani]

From Paléographìe latine, by F. Steffens (www.archivi.beniculturali.it)

[Picha katika ukurasa wa 22]

Vulgate ya Sixtus ya Klementi, 1592

[Picha katika ukurasa wa 23]

Kutoka 3:15, Nova Vulgata, 1979

[Hisani]

© 2008 Libreria Editrice Vaticana