Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Matukio Yote Maishani Mwetu Yameshaamuliwa?

Je, Matukio Yote Maishani Mwetu Yameshaamuliwa?

Wasomaji Wetu Wanauliza

Je, Matukio Yote Maishani Mwetu Yameshaamuliwa?

Watu fulani wanaamini kwamba siku ambayo tutakufa imekwisha amuliwa. Wengine wanasema kwamba Mungu mwenyewe ndiye anayeamua siku ambayo tutakufa. Isitoshe, watu hao wanaamini kwamba matukio yote muhimu maishani mwetu hayaepukiki. Maoni yako ni nini?

Jiulize maswali yafuatayo: ‘Ikiwa majaliwa au Mungu amekwisha amua jinsi ambavyo mambo yatakuwa, na hatuwezi kufanya lolote ili kubadili hali, kwa nini basi tunahimizwa kusali? Na kama matukio yote maishani mwetu yamekwisha amuliwa, kuna haja gani kuchukua hatua ya kujilinda? Kuna haja gani kujifunga kwa mshipi wakati wa kusafiri kwa gari, au kuepuka kuendesha gari baada ya kunywa kileo?’

Biblia haiungi mkono hata kidogo mwenendo huo wa kizembe. Badala ya kufundisha kwamba mambo yote yamekwisha amuliwa, Biblia iliwaamuru Waisraeli wafikirie hali ya usalama. Kwa mfano, waliagizwa wajenge ukuta mfupi ukingoni mwa paa bapa la nyumba zao ili mtu asianguke chini. Kwa nini Mungu aliwapa sheria hiyo ikiwa tayari ilikuwa imeamuliwa kwamba mtu angeanguka chini na kufa?—Kumbukumbu la Torati 22:8.

Namna gani watu wanaokufa kwa sababu ya misiba ya asili au mikasa mingine wasiyoweza kuizuia? Je, siku yao ya kufa inakuwa imeamuliwa mapema? La, mwandikaji wa Biblia Mfalme Sulemani anatuhakikishia kwamba ‘wakati na tukio lisilotazamiwa hutupata sote.’ (Mhubiri 9:11) Kwa hiyo, hata kama misiba inatokea katika hali zinazoonekana kuwa zisizo za kawaida, haimaanishi kwamba misiba hiyo imeamuliwa mapema.

Hata hivyo, watu fulani wanasema kwamba maneno hayo ya Sulemani yanapinga maneno haya aliyoandika mapema: “Kuna wakati uliowekwa wa kila kitu, hata kuna wakati wa kila jambo chini ya mbingu: wakati wa kuzaliwa na wakati wa kufa.” (Mhubiri 3:1, 2) Je, Sulemani aliunga mkono maoni ya kwamba matukio yote maishani mwetu yameamuliwa mapema? Tuchunguze maneno yake kwa makini.

Sulemani hakusema kwamba matukio ya kuzaliwa au kufa yameamuliwa mapema. Badala yake, alimaanisha kwamba matukio ya kuzaliwa na kufa, kama mambo mengine mengi maishani, yanaendelea daima. Bila shaka, kuna mazuri na mabaya katika panda-shuka za maisha. Sulemani anasema: “Kuna . . . wakati wa kulia na wakati wa kucheka.” Anaonyesha kwamba matukio yanayotarajiwa na mikasa isiyotarajiwa ni ya kawaida katika maisha—katika “kila jambo chini ya mbingu.” (Mhubiri 3:1-8; 9:11, 12) Kwa hiyo, anamalizia kwa kutuhimiza tusijiingize sana katika shughuli za kila siku hivi kwamba tunamsahau Muumba wetu.—Mhubiri 12:1, 13.

Ijapokuwa Muumba wetu ana mamlaka juu ya maisha na kifo, haamui matukio yote katika maisha yetu. Biblia inafundisha kwamba Mungu ametuandalia sisi sote tumaini la kuishi milele. Lakini hatulazimishi kulikubali. Badala yake, Neno lake linasema hivi: “Yeyote anayetaka achukue maji ya uzima bure.”—Ufunuo 22:17.

Naam, ni juu yetu kutaka ‘kuchukua maji ya uzima.’ Kwa hiyo, wakati wetu ujao haujaamuliwa mapema, bali unategemea kwa kadiri kubwa maamuzi yetu, mtazamo wetu, na mwenendo wetu.