Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Vatikani Yajaribu Kuondoa Jina la Mungu Katika Ibada

Vatikani Yajaribu Kuondoa Jina la Mungu Katika Ibada

Vatikani Yajaribu Kuondoa Jina la Mungu Katika Ibada

VIONGOZI wa Kanisa Katoliki wanataka kukataza matumizi ya jina la Mungu katika ibada yao. Mwaka uliopita baraza la usimamizi la Kanisa Katoliki lilipeleka hati ya maagizo kuhusu jambo hili kwenye mikutano ya maaskofu wa Kanisa Katoliki iliyofanywa duniani kote. “Maagizo” hayo yalitoka kwa papa.

Hati hii ya maagizo iliyotolewa Juni 29, 2008 (29/6/2008), inalalamika kwamba ijapokuwa matumizi ya jina la Mungu yamekatazwa, “limekuwa jambo la kawaida katika miaka ya majuzi kutamka jina la Mungu wa Waisraeli, linalojulikana kama tetragramatoni takatifu, na ambalo linaandikwa kwa herufi nne za Kiebrania יהוה, zinazotafsiriwa YHWH.” Hati hii inataja kwamba jina la Mungu limeandikwa kwa njia kama vile “Yehova” na “Yahweh.” * Hata hivyo, kusudi la yale maagizo kutoka Vatikani ni kuimarisha msimamo wa awali wa Kanisa Katoliki, yaani, neno “Bwana” linapaswa kutumiwa badala ya Tetragramatoni. Isitoshe, Wakatoliki “hawapaswi kutumia au kutamka [jina la Mungu] YHWH” katika ibada, nyimbo, au sala zao.

Ile hati ya maagizo ya Vatikani inasema kwamba msimamo huu unategemea “mapokeo ya kale” ya Kanisa Katoliki. Hati hii inadai kwamba katika tafsiri ya Septuajinti ya Maandiko ya Kiebrania iliyotafsiriwa kabla ya Ukristo, neno la Kigiriki Kyʹri·os, linalotafsiriwa “Bwana,” lilitumiwa badala ya jina la Mungu. Kwa hiyo, ile hati inadai kwamba “kuanzia mwanzo, Wakristo pia hawakutamka kamwe jina la Mungu, au tetragramatoni.” Hata hivyo, kuna uthibitisho ulio wazi wa kwamba Wakristo walitumia jina la Mungu. Katika hati za kwanza-kwanza za Septuajinti, jina la Mungu liliandikwa kwa herufi za Kiebrania, yaani, יהוה. Neno Kyʹri·os halipatikani katika hati hizo. Wafuasi wa Kristo wa karne ya kwanza walijua na kulitamka jina la Mungu. Yesu mwenyewe alisema hivi aliposali kwa Baba yake: “Nimewajulisha jina lako.” (Yohana 17:26) Pia, alipowafundisha wanafunzi wake jinsi ya kusali, alisema hivi: “Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe.”—Mathayo 6:9.

Wakristo wote wanapaswa kutamani kuona jina la Mungu likitakaswa. Jitihada za Vatikani za kukataza matumizi ya jina la Mungu zinamshushia Yehova heshima, yule aliyesema: “Hili ndilo jina langu hata milele; nalo ni kumbukumbu langu hata vizazi vyote.”—Kutoka 3:15, The Jerusalem Bible.

[Maelezo ya chini]

^ fu. 3 Katika Kiswahili jina “Yehova” ndilo linalotumiwa kwa kawaida, nalo linapatikana katika tafsiri kadhaa za Biblia za Kiswahili.

[Blabu katika ukurasa wa 30]

“Hili ndilo jina langu hata milele.”—Kutoka 3:15, JB

[Picha katika ukurasa wa 30]

Kipande cha “Septuajinti” cha karne ya kwanza W.K. Jina la Mungu lililoandikwa kwa herufi nne za Kiebrania ambazo kwa kawaida zinatafsiriwa YHWH, limetiwa alama

[Hisani]

Courtesy of the Egypt Exploration Society