Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuhusu “Mwisho”

Kuhusu “Mwisho”

Tunayojifunza Kutoka kwa Yesu

Kuhusu “Mwisho”

Mwisho wa nini?

Wanafunzi wa Yesu walimuuliza: “Ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?” (Mathayo 24:3) Alipojibu swali hilo, Yesu hakusema kwamba dunia halisi itaharibiwa. Awali alikuwa amezungumza kuhusu “mfumo wa mambo,” na alitumia usemi huo kurejelea mfumo wa siasa, biashara, na dini unaoongozwa na Shetani. (Mathayo 13:22, 40, 49) Kwa hiyo, alikuwa akifikiria mfumo huo aliposema kwamba ‘mwisho utakuja.’—Mathayo 24:14.

Yesu aliufafanua mwisho jinsi gani?

Mwisho wa mfumo huu usiofuata haki ni “habari njema.” Yesu alisema: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” Yesu aliufafanua mwisho wa mfumo huu wa mambo hivi: “[Kutakuwa] na dhiki kuu ya namna ambayo haijapata kutukia tangu mwanzo wa ulimwengu mpaka sasa, hapana, wala haitatukia tena. Kwa kweli, kama siku hizo hazingefupishwa, hakuna chochote chenye mwili ambacho kingeokolewa.”—Mathayo 24:14, 21, 22.

Ni nani watakaoharibiwa?

Watu wasiompenda na kumtumikia Yehova na Yesu ndio watakaoharibiwa. Watu hao hawamtii Mungu. Yesu alisema: “Kama vile siku za Noa zilivyokuwa, ndivyo kuwapo kwa Mwana wa binadamu kutakavyokuwa.” Kisha akasema kwamba watu walioishi siku hizo “hawakujali mpaka gharika ikaja na kuwafagilia mbali wote.” (Mathayo 24:36-39) Yesu alisema wengi wanapitia barabara inayoelekea kwenye uharibifu. Lakini alitoa uhakikisho kwamba kuna ‘barabara yenye nafasi ndogo inayoongoza kwenye uzima.’—Mathayo 7:13, 14.

Mfumo huu wa mambo utaharibiwa wakati gani?

Alipoulizwa kuhusu ishara ya kuwapo kwake “na ya umalizio wa mfumo wa mambo,” Yesu alijibu: “Taifa litasimama kupigana na taifa na ufalme kupigana na ufalme, kutakuwa na upungufu wa chakula na matetemeko ya nchi . . . na kwa sababu ya kuongezeka kwa uasi-sheria upendo wa walio wengi zaidi utapoa.” (Mathayo 24:3-12) Hivyo, habari zote zenye kuhuzunisha leo zinatia moyo, kwa kuwa zinaonyesha kwamba hivi karibuni Ufalme wa Mungu utawaletea amani wanadamu watiifu. Yesu alisema: “Wakati mnapoona mambo hayo yakitukia, jueni kwamba ufalme wa Mungu uko karibu.”—Luka 21:31.

Unapaswa kufanya nini?

Yesu alisema kwamba Mungu “[alimtoa] Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:16) Ili uwe na imani katika Mungu na Mwana wake, unahitaji kuwajua vizuri. Kwa hiyo, Yesu alisema: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.”—Yohana 17:3.

Uwe macho na usiruhusu mahangaiko na matatizo yakuzuie usisitawishe upendo kwa Mungu. Yesu alisema: “Jiangalieni ninyi wenyewe kwamba mioyo yenu isilemewe kamwe . . . na mahangaiko ya maisha, na kwa ghafula siku hiyo iwe juu yenu mara moja kama mtego. Kwa maana itakuja” hakika. Ikiwa unatii maneno ya Yesu utapata “kufanikiwa kuponyoka mambo yote hayo yaliyokusudiwa kutukia.”—Luka 21:34-36.

Ili upate habari zaidi ona sura ya 9, “Je, Tunaishi Katika ‘Siku za Mwisho’?,” ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? *

[Maelezo ya chini]

^ fu. 14 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.