Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Betheli ya Brooklyn—Historia ya Miaka 100

Betheli ya Brooklyn—Historia ya Miaka 100

Betheli ya Brooklyn—Historia ya Miaka 100

MAMBO muhimu yalitukia katika Jiji la New York mwaka wa 1909. Daraja la Queensboro linalounganisha eneo la Queens na Manhattan lilifunguliwa, na vilevile Daraja la Manhattan linalounganisha eneo la Manhattan na Brooklyn.

Mambo muhimu pia yalitukia mwaka huo katika utendaji wa Mashahidi wa Yehova. Mapema, Charles Taze Russell, aliyekuwa msimamizi wa shirika la kisheria la Mashahidi wa Yehova (Watch Tower Bible and Tract Society), alikuwa ametambua uwezekano wa kupanua kazi ya kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu. (Mathayo 24:14) Aliona kwamba kuhamisha makao makuu ya Mashahidi wa Yehova kutoka Pittsburgh, Pennsylvania, hadi Brooklyn, New York, ingekuwa hatua muhimu sana ya kutimiza mradi huo. Matayarisho yalianza mwaka wa 1908, na mapema katika mwaka uliofuata makao makuu yakahamishwa.

Kwa Nini Makao Makuu Yalihamishiwa Brooklyn?

Ndugu waliosimamia kazi ya kuhubiri wakati huo walijua kwamba ujumbe wa Biblia uliochapwa katika magazeti ya ulimwengu ulisaidia sana kusambaza kweli za Biblia. Mwaka wa 1908, ujumbe wa Russell kuhusu Biblia ulitokea kila juma katika magazeti 11 ambayo kwa ujumla yalichapisha nakala 402,000.

Hata hivyo, Russell aliandika: “Ndugu wanaoelewa jinsi makala mbalimbali zinavyosambazwa kati ya magazeti ya ulimwengu . . . wanatuhakikishia kwamba ikiwa yale mahubiri ya kila juma yangeandikwa katika [jiji kubwa] huenda ikawa yangechapishwa kotekote Marekani, na wanakadiria kwamba katika muda wa mwaka mmoja yangekuwa yakichapishwa kwa ukawaida katika mamia ya magazeti.” Kwa hiyo, walianza kutafuta mahali bora kwa ajili ya kupanua kazi ya kuhubiri.

Kwa nini walichagua Brooklyn? Russell alisema: “Baada ya kusali kuhusu jambo hilo, sote tulikata kauli kwamba eneo la Brooklyn, New York, lenye watu wengi . . . na ambalo linaitwa ‘Mji wa Makanisa,’ linafaa sana kuwa kituo cha kazi ya mavuno.” Matokeo yanaonyesha kwamba uamuzi huo ulikuwa mzuri. Punde si punde, magazeti 2,000 yalikuwa yakichapisha ujumbe wa Biblia wa Russell.

Jiji la New York lilifaa kwa sababu nyingine pia. Mwaka wa 1909, ofisi za tawi zilikuwa zimefunguliwa nchini Uingereza, Ujerumani, na Australia, na nyingine zingefunguliwa muda mfupi baadaye. Kwa hiyo, lilikuwa jambo la hekima kuwa na makao makuu katika jiji lenye bandari ambalo lilikuwa na mfumo mzuri wa barabara na reli.

Kwa Nini Makao Makuu Yaliitwa Betheli?

Makao makuu ya kwanza ya shirika la Watch Tower Bible and Tract Society yalifunguliwa katika miaka ya 1880, huko Allegheny (sasa ni sehemu ya Pittsburgh), Pennsylvania. Wakati huo, makao makuu yaliitwa Nyumba ya Biblia. Katika mwaka wa 1896, watu 12 walikuwa wakifanya kazi huko.

Makao makuu yalipohamishwa kutoka Allegheny hadi Brooklyn mwaka wa 1909, makao mapya ya wafanyakazi yaliitwa Betheli. * Kwa nini yaliitwa Betheli? Majengo ambayo shirika la Watch Tower Society lilinunua kwenye 13-17 Hicks Street yalikuwa mali ya kasisi mashuhuri aliyeitwa Henry Ward Beecher, nayo yaliitwa Betheli ya Beecher. Makao ya zamani ya Beecher, 124 Columbia Heights, yalinunuliwa pia. Toleo la Mnara wa Mlinzi la Machi 1, 1909 (1/3/1909), lilisema: “Ni jambo la ajabu sana kwamba tulipata Betheli ya Beecher kisha bila kutarajia tukapata makao yake ya zamani. . . . Makao mapya yataitwa ‘Betheli,’ na ukumbi na ofisi mpya itaitwa ‘Maskani ya Brooklyn.’ Majina haya yatatumiwa badala ya jina ‘Nyumba ya Biblia.’”

Leo majengo ya Mashahidi yaliyopanuliwa sana huko Brooklyn na pia katika sehemu nyingine za Jimbo la New York, yaani, Wallkill na Patterson, yakiwemo makao, kiwanda cha uchapaji, na ofisi, yote yanaitwa Betheli. Kuna Betheli pia katika nchi nyingine 113. Katika Betheli hizo zote, wahudumu zaidi ya 19,000 wanafanya kazi ili kusaidia kusambaza ujumbe wa Biblia.

Wageni Wakaribishwa kwa Uchangamfu

Majengo hayo yaliwekwa wakfu Januari 31, 1909 (31/1/1909). Jumatatu (Siku ya 1), Septemba 6, 1909 (6/9/1909), ilikuwa siku ya wageni huko Betheli. Mamia ya Wanafunzi wa Biblia, kama Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo, walitembelea Betheli siku hiyo. Wengi wao walikuwa wamehudhuria kusanyiko la Kikristo huko Saratoga Springs, umbali wa kilomita 320 hivi kaskazini ya Jiji la New York. Ndugu Charles Taze Russell mwenyewe aliwakaribisha wageni hao. *

Wageni wanakaribishwa kutembelea Betheli hata leo. Kila mwaka watu zaidi ya 40,000 wanatembelea Betheli ya Brooklyn, ambayo bado ni muhimu katika upanuzi wa kazi ya kuhubiri Ufalme wa Yehova, kwa manufaa ya mamilioni ya watu.

[Maelezo ya chini]

^ fu. 11 Neno la Kiebrania “Betheli” linamaanisha “Nyumba ya Mungu.” Jiji la Betheli linalozungumziwa katika Biblia lilikuwa jiji maarufu la Waisraeli. Katika Biblia jiji la Yerusalemu tu ndilo linalotajwa mara nyingi zaidi kuliko jiji la Betheli.

^ fu. 14 Ili kupata habari zaidi, ona kitabu Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu, ukurasa wa 718-723, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 25]

Unajua Nini Kuhusu Shirika la Watch Tower Bible and Tract Society?

Shirika linaloitwa Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania liliandikishwa kisheria mwaka wa 1884 kama Zion’s Watch Tower Tract Society. Lilianzishwa kwa kusudi la kueneza kweli za Biblia kotekote duniani, hasa kwa njia ya vitabu na magazeti. Shirika la Watch Tower Bible and Tract Society ni mojawapo ya mashirika ya kisheria ambayo Mashahidi wa Yehova wanayatumia duniani kote mpaka leo. *Wafilipi 1:7.

Shirika la Watch Tower Bible and Tract Society limechapisha Biblia na vitabu vya Biblia katika lugha 473. Limechapisha nakala milioni 150 za Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya, ikiwa nzima au kwa sehemu, katika lugha 72. Zaidi ya kuchapa Tafsiri ya Ulimwengu Mpya, shirika hili limechapa au kuagiza uchapaji wa tafsiri zifuatazo za Biblia: American Standard Version, The Bible in Living English, The Emphatic Diaglott, King James Version (na vilevile Chapa ya Wanafunzi wa Biblia), Linear Parallel Edition ya Holman, na The New Testament Newly Translated and Critically Emphasized, Chapa ya Pili.

Isitoshe, katika miaka kumi iliyopita, Mashahidi wa Yehova wamechapa vitabu, magazeti na trakti, na kutengeneza CD, DVD, na vitu vinginevyo bilioni 20, ili kueneza ujumbe wa Biblia. * Idadi kubwa ya vitu hivyo vimechapwa, kupakiwa, na kusafirishwa kutoka katika Betheli za nchi kama vile Afrika Kusini, Argentina, Australia, Brazili, Filipino, Finland, Hispania, India, Italia, Japani, Kanada, Kolombia, Korea, Marekani, Mexico, Myanmar, Nigeria, Uingereza, na Ujerumani.

[Maelezo ya chini]

^ fu. 21 Katika mwaka wa 2008, idadi ya Mashahidi wa Yehova ilikuwa 7,124,443 katika nchi 236, na idadi ya makutaniko yao ilikuwa 103,267.

^ fu. 23 Vitu hivyo haviuzwi. Kazi ya Mashahidi wa Yehova ya kuwafundisha watu Biblia inaendelezwa kwa michango ya hiari.

[Chati]

UZALISHAJI 1998-2008

Vitabu 458,230,708

Magazeti 11,292,413,199

Trakti 7,996,906,376

Broshua 862,050,233

CD/MP3 34,621,130

DVD 13,500,125

Vitu vingine 129,083,031

Jumla 20,786,804,802

[Picha katika ukurasa wa 22]

Makao ya Betheli 122-124 Columbia Heights

[Picha katika ukurasa wa 22]

13-17 Hicks Street (1909-1918)

[Picha katika ukurasa wa 22]

Ujumbe wa Biblia wa Russell uliochapwa katika magazeti

[Picha katika ukurasa wa 22]

35 Myrtle Avenue (1920-1922)

[Picha katika ukurasa wa 23]

18 Concord Street (1922-1927)

[Picha katika ukurasa wa 23]

117 Adams Street (tangu 1927 hadi leo)

[Picha katika ukurasa wa 24]

25-30 Columbia Heights

[Picha katika ukurasa wa 24]

Kiwanda cha uchapaji huko Wallkill

[Picha katika ukurasa wa 24]

Kituo cha Elimu cha Patterson