Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Vijana—Fanyeni Maendeleo Yenu Yawe Wazi

Vijana—Fanyeni Maendeleo Yenu Yawe Wazi

Vijana—Fanyeni Maendeleo Yenu Yawe Wazi

“Tafakari mambo haya; zama katika hayo, ili maendeleo yako yawe wazi kwa watu wote.”—1 TIM. 4:15.

1. Mungu anataka vijana wawe na nini?

“WEWE kijana, uufurahie ujana wako, na moyo wako ukuchangamshe siku za ujana wako.” (Mhu. 11:9, Union Version) Hivyo ndivyo alivyoandika Mfalme Sulemani mwenye hekima wa taifa la kale la Israeli. Bila shaka, Yehova Mungu ambaye ni Chanzo cha ujumbe huo, anataka ninyi vijana muwe na furaha. Kwa kuongezea, Yehova anataka mwendelee kuwa na shangwe hata mtakapozeeka. Hata hivyo, mara nyingi vijana wanafanya makosa mazito ambayo yanaweza kuharibu furaha yao ya wakati ujao. Hata Ayubu mwaminifu aliomboleza kwa sababu alipata ‘matokeo ya makosa ya ujana wake.’ (Ayu. 13:26) Wakati wa kubalehe na katika miaka inayofuata, mara nyingi kijana Mkristo anahitaji kufanya maamuzi mazito. Maamuzi mabaya yanaweza kumuumiza sana kihisia na kusababisha matatizo ambayo yanaweza kuharibu maisha yake yote.—Mhu. 11:10.

2. Vijana wanaweza kuepuka kufanya makosa mazito wakitumia shauri gani la Biblia?

2 Vijana wanapaswa kufanya maamuzi mazuri. Fikiria shauri ambalo mtume Paulo aliwapa Wakorintho. Aliandika hivi: “Msiwe watoto wachanga katika nguvu za uelewaji . . . Iweni watu wazima katika nguvu za uelewaji.” (1 Kor. 14:20) Kutii shauri la kujipatia uwezo wa kufikiri na kuchanganua mambo kama mtu mzima kutawasaidia vijana kuepuka kufanya makosa mazito.

3. Unaweza kufanya nini ili ukomae?

3 Ikiwa wewe ni kijana, kumbuka kwamba unahitaji kujitahidi ili kukomaa. Paulo alimwambia Timotheo hivi: “Usiache mtu yeyote audharau kamwe ujana wako. Badala yake, uwe kielelezo kwa waaminifu katika kusema, katika mwenendo, katika upendo, katika imani, katika usafi wa kiadili. . . . Endelea kufanya bidii katika kusoma mbele ya watu wote, katika kuhimiza, katika kufundisha. . . . Tafakari mambo haya; zama katika hayo, ili maendeleo yako yawe wazi kwa watu wote.” (1 Tim. 4:12-15) Vijana Wakristo wanahitaji kusonga mbele na kufanya maendeleo yao yawe wazi kwa wengine.

Maendeleo Ni Nini?

4. Kufanya maendeleo ya kiroho kunatia ndani nini?

4 Kufanya maendeleo ni “kusonga mbele, kuwa mtu bora zaidi.” Paulo alikuwa akimhimiza Timotheo aendelee kujitahidi ili afanye maendeleo katika kusema, katika mwenendo, katika upendo, katika imani, katika usafi wa kiadili, na pia katika kutimiza huduma yake. Alipaswa kujitahidi sana kuweka kielelezo kizuri kupitia njia yake ya maisha. Kwa hiyo, Timotheo alihitaji kuendelea kufanya maendeleo ya kiroho.

5, 6. (a) Maendeleo ya Timotheo yalionekana wazi wakati gani? (b) Vijana wanaweza kumwiga Timotheo jinsi gani leo katika kufanya maendeleo?

5 Paulo alipoandika shauri hilo kati ya mwaka wa 61 na 64 W.K., tayari Timotheo alikuwa mzee mwenye uzoefu. Hakuwa tu akianza kufanya maendeleo ya kiroho. Katika mwaka wa 49 au 50 W.K., Timotheo alipokuwa na umri wa miaka 20 hivi au mwishoni mwa miaka yake ya ujana, “alishuhudiwa vema na akina ndugu katika Listra na Ikoniamu,” ambao walikuwa wameona maendeleo yake ya kiroho. (Mdo. 16:1-5) Wakati huo, Paulo alienda na Timotheo katika safari yake ya umishonari. Baada ya kuona Timotheo akifanya maendeleo zaidi kwa miezi fulani, Paulo alimtuma huko Thesalonike ili awafariji na kuwaimarisha Wakristo waliokuwa katika jiji hilo. (Soma 1 Wathesalonike 3:1-3, 6.) Ni wazi kwamba Timotheo alianza kufanya maendeleo yake yawe wazi kwa wengine alipokuwa kijana.

6 Ninyi vijana mlio kutanikoni, jitahidini sasa kusitawisha sifa za kiroho zinazohitajiwa, ili maendeleo yenu katika maisha ya Kikristo na katika uwezo wenu wa kufundisha kweli za Biblia yaonekane wazi. Kuanzia umri wa miaka 12, Yesu ‘alizidi kufanya maendeleo katika hekima.’ (Luka 2:52) Basi acheni tuchunguze jinsi unavyoweza kufanya maendeleo yako yawe wazi katika sehemu tatu za maisha yako: (1) unapokabili matatizo, (2) unapojitayarisha kwa ajili ya ndoa, na (3) unapojitahidi kuwa “mhudumu mzuri.”—1 Tim. 4:6.

Kabiliana na Matatizo kwa “Utimamu wa Akili”

7. Hali zenye kufadhaisha zinaweza kuwa na matokeo gani kwa vijana?

7 Mkristo mwenye umri wa miaka 17 anayeitwa Carol alisema, “Kuna nyakati ambazo nilichoka sana kihisia, kimwili, na kufadhaika kiakili hivi kwamba nilishindwa kuamka asubuhi.” * Kwa nini alifadhaika sana hivyo? Carol alipokuwa na umri wa miaka 10, familia yao ilivunjika baada ya talaka ya wazazi wake, akaanza kuishi na mama yake, ambaye alikataa kufuata viwango vya Biblia vya maadili. Huenda unakabili hali fulani zenye kufadhaisha kama Carol bila tumaini la kwamba hali itakuwa nzuri.

8. Timotheo alipambana na matatizo gani?

8 Timotheo pia alipambana na matatizo alipokuwa akifanya maendeleo ya kiroho. Kwa mfano, alipata ‘ugonjwa wa mara kwa mara’ kwa sababu ya tatizo la tumbo. (1 Tim. 5:23) Paulo alipomtuma Korintho kushughulikia matatizo fulani yaliyosababishwa na watu ambao walipinga mamlaka yake akiwa mtume, Paulo alilihimiza kutaniko lishirikiane naye ili Timotheo ‘asiogope’ akiwa kati yao. (1 Kor. 4:17; 16:10, 11) Inaonekana kwamba Timotheo alikuwa mtu mwenye haya, au mwoga.

9. Utimamu wa akili ni nini, na unatofautiana jinsi gani na roho ya woga?

9 Ili kumsaidia Timotheo, Paulo alimkumbusha hivi baadaye: “Mungu hakutupa sisi roho ya woga, bali ile ya nguvu na ya upendo na ya utimamu wa akili.” (2 Tim. 1:7) “Utimamu wa akili” unatia ndani kuweza kufikiri na kuchanganua mambo kwa busara. Kunatia ndani uwezo wa kuvumilia hali yoyote ile unayokabili hata kama haipendezi. Vijana fulani wasio wakomavu wanaonyesha roho ya woga na wanajaribu kuepuka hali zenye kufadhaisha kwa kulala kupita kiasi au kutazama sana televisheni, kutumia vibaya dawa za kulevya au vileo, kufanya karamu kila mara, au kuwa na maadili mapotovu ya kingono. Wakristo wanahimizwa ‘wakatae kabisa kutomwogopa Mungu na tamaa za kilimwengu na waishi kwa utimamu wa akili na uadilifu na ujitoaji-kimungu katikati ya mfumo wa mambo wa sasa.’—Tito 2:12.

10, 11. Utimamu wa akili unatusaidia jinsi gani kusitawisha nguvu za kiroho?

10 Biblia inawahimiza “wanaume vijana wawe na utimamu wa akili.” (Tito 2:6) Unapokabili matatizo, unaweza kutii shauri hilo kwa kusali na kutegemea nguvu kutoka kwa Mungu. (Soma 1 Petro 4:7.) Hivyo, utasitawisha uhakika wa kutoka moyoni katika “nguvu ambazo Mungu hutoa.”—1 Pet. 4:11.

11 Utimamu wa akili na sala ndiyo mambo yaliyomsaidia Carol. Alisema hivi: “Sijawahi kamwe kukabili jambo gumu zaidi kama kupinga maisha mapotovu ya mama yangu. Lakini sala ilinisaidia sana. Ninajua Yehova yupo pamoja nami, kwa hiyo siogopi tena.” Kumbuka, matatizo yanaweza kuboresha utu wako na kukutia nguvu. (Zab. 105:17-19; Omb. 3:27) Hata ukikabili hali gani, Mungu hatakuacha kamwe. ‘Atakusaidia kwelikweli.’—Isa. 41:10.

Kujitayarisha kwa Ajili ya Ndoa Yenye Mafanikio

12. Kwa nini Mkristo anayefikiria kufunga ndoa anapaswa kutumia kanuni iliyo katika Methali 20:25?

12 Vijana fulani wamekimbilia kufunga ndoa, wakifikiri kwamba ndoa ndiyo suluhisho la kupata furaha, kuepuka upweke, matatizo nyumbani, na maisha yenye kuchosha. Hata hivyo, kuweka nadhiri za ndoa ni jambo zito. Watu fulani katika nyakati za Biblia walikimbilia kuweka nadhiri takatifu bila kuchunguza kwa uangalifu mambo yaliyohusika. (Soma Methali 20:25.) Nyakati nyingine, vijana hawafikirii kwa uzito kuhusu madaraka ya ndoa. Baadaye, wanagundua kwamba hawakujua kuwa ndoa inahusisha mambo mengi zaidi.

13. Wale wanaofikiria kuanzisha uchumba wanapaswa kufikiria maswali gani, na wamepewa mashauri gani yenye faida?

13 Kwa hiyo, kabla ya kuanza uchumba, jiulize hivi: ‘Kwa nini ninataka kufunga ndoa? Ninatazamia nini? Je, huyu ni mwenzi anayenifaa? Je, niko tayari kutimiza madaraka yangu katika ndoa?’ Ili kukusaidia ujichunguze kwa busara, “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” amechapisha habari hususa kuhusu ndoa. * (Mt. 24:45-47) Ona habari hizo kuwa mashauri ambayo Yehova anakupa. Chunguza kwa uangalifu mambo hayo na uyatumie. Usijiruhusu kamwe uwe “kama farasi au nyumbu wasio na uelewaji.” (Zab. 32:8, 9) Uwe mkomavu katika uelewaji wako kuhusu madaraka ya ndoa. Ikiwa unahisi kwamba uko tayari kuanzisha uchumba, kumbuka sikuzote kwamba unapaswa kuwa “kielelezo . . . katika usafi wa kiadili.”—1 Tim. 4:12.

14. Maendeleo ya kiroho yatakusaidia jinsi gani ukifunga ndoa?

14 Ukomavu wa kiroho unamsaidia mtu kufanikiwa pia baada ya kufunga ndoa. Mkristo mkomavu anajitahidi sana kufikia “kipimo cha kimo ambacho ni cha ujazo wa Kristo.” (Efe. 4:11-14) Anafanya bidii kusitawisha utu kama wa Kristo. Akiwa Kielelezo chetu, “Kristo hakujipendeza mwenyewe.” (Rom. 15:3) Mume au mke akiendelea kutafuta, si faida yake mwenyewe tu, bali faida ya mwenzi wake, maisha ya familia yatakuwa yenye amani na yenye kuburudisha. (1 Kor. 10:24) Mume ataonyesha upendo wa kujidhabihu, na mke ataazimia kujitiisha kwa mume wake kama Yesu anavyojitiisha kwa Kichwa chake.—1 Kor. 11:3; Efe. 5:25.

“Timiza kwa Ukamili Huduma Yako”

15, 16. Unaweza kufanya nini ili maendeleo yako yawe wazi katika huduma?

15 Paulo aliandika hivi ili kukazia mgawo wa maana ambao Timotheo alikuwa nao: “Nakuagiza kwa uzito mbele za Mungu na Kristo Yesu, . . . lihubiri neno, fanya hivyo kwa bidii.” Akaongezea hivi: “Fanya kazi ya mweneza-injili, timiza kwa ukamili huduma yako.” (2 Tim. 4:1, 2, 5) Ili kutimiza mgawo huo, Timotheo alihitaji “kulishwa maneno ya imani.”—Soma 1 Timotheo 4:6.

16 Unaweza ‘kulishwa jinsi gani maneno ya imani’? Paulo aliandika hivi: “Endelea kufanya bidii katika kusoma mbele ya watu wote, katika kuhimiza, katika kufundisha. Tafakari mambo haya; zama katika hayo.” (1 Tim. 4:13, 15) Unahitaji kujifunza kibinafsi kwa bidii ili ufanye maendeleo. Neno “zama” linatoa wazo la kujishughulisha sana na utendaji fulani. Una mazoea gani ya kujifunza? Je, unazama katika “mambo mazito ya Mungu”? (1 Kor. 2:10) Au unajitahidi kwa kadiri ndogo tu? Kutafakari kuhusu mambo unayojifunza kutachochea moyo wako.—Soma Methali 2:1-5.

17, 18. (a) Unapaswa kujitahidi kusitawisha uwezo gani? (b) Kusitawisha mwelekeo kama wa Timotheo kunaweza kukusaidia jinsi gani katika huduma?

17 Kijana mmoja painia anayeitwa Michelle alisema hivi: “Ili nipate matokeo mazuri kabisa katika huduma, nina ratiba nzuri ya kujifunza kibinafsi, na ninahudhuria mikutano kwa ukawaida. Kwa sababu hiyo, ninaendelea kukua kiroho.” Bila shaka, kutumika ukiwa painia kutakusaidia kuboresha uwezo wako wa kutumia Biblia katika huduma na kufanya maendeleo ya kiroho. Jitahidi kuwa msomaji mzuri na kutoa maelezo yenye maana katika mikutano ya Kikristo. Ukiwa kijana aliyekomaa kiroho, bila shaka utajitahidi kutayarisha na kutoa hotuba zenye kujenga katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, na kushikamana na habari uliyopewa.

18 ‘Kufanya kazi ya mweneza-injili’ kunamaanisha kuboresha zaidi huduma yako na kuwasaidia wengine wapate wokovu. Ili ufanye hivyo unapaswa kusitawisha “ufundi wa kufundisha.” (2 Tim. 4:2) Ukipanga kuhubiri pamoja na wale wenye uzoefu katika kazi hiyo, utajifunza njia zao za kufundisha, kama vile Timotheo alivyojifunza kwa kuhubiri pamoja na Paulo. (1 Kor. 4:17) Kuhusu wale ambao aliwasaidia, Paulo alisema kwamba hakuwahubiria tu habari njema, bali pia alitoa ‘nafsi yake,’ au alitumia maisha yake kuwasaidia, kwa sababu walikuwa wapendwa wake. (1 The. 2:8) Ili ufuate mfano wa Paulo katika huduma, unahitaji kuwa na mwelekeo kama wa Timotheo, ambaye aliwajali wengine kwa unyoofu na ‘kutumika katika kuendeleza habari njema.’ (Soma Wafilipi 2:19-23.) Je, unaonyesha roho hiyo ya kujidhabihu katika huduma yako?

Utaridhika Kikweli Unapofanya Maendeleo

19, 20. Kwa nini kufanya maendeleo ya kiroho kunaleta shangwe?

19 Unahitaji kujitahidi ili ufanye maendeleo ya kiroho. Lakini ukisitawisha kwa subira ustadi wako wa kufundisha, baada ya muda utakuwa na pendeleo la “kuwatajirisha wengi” kiroho, nao watakuwa ‘shangwe au taji lako la furaha.’ (2 Kor. 6:10; 1 The. 2:19) Fred, ambaye ni mhudumu wa wakati wote anasema hivi: “Ninatumia wakati wangu kuwasaidia wengine sasa kuliko nilivyofanya wakati uliopita. Ni kweli kwamba kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.”

20 Kuhusu shangwe na uradhi aliopata kwa sababu ya kukua kiroho, kijana mmoja painia anayeitwa Daphne alisema: “Nilisitawisha uhusiano wa karibu zaidi pamoja na Yehova nilipoanza kujifunza mambo mengi kumhusu na kuthamini utu wake. Unapompendeza Yehova kwa uwezo wako wote, unahisi vizuri sana, unaridhika kwelikweli!” Ingawa nyakati nyingine huenda wanadamu wasione maendeleo yetu ya kiroho, sikuzote Yehova anayaona, naye anayathamini. (Ebr. 4:13) Hakuna shaka yoyote kwamba ninyi vijana Wakristo mnaweza kumletea utukufu na sifa Baba yetu wa mbinguni. Endeleeni kuufanya moyo wake ushangilie mnapojitahidi kwa unyoofu kufanya maendeleo yenu yawe wazi.—Met. 27:11.

[Maelezo ya chini]

^ fu. 7 Majina fulani yamebadilishwa.

^ fu. 13 “Je, Ananifaa?” katika kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2; “Mwongozo wa Mungu Katika Kuchagua Mwenzi wa Ndoa,” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Mei 15, 2001 (15/5/2001); na “Je, Ni Hekima kwa Matineja Kufunga Ndoa?” katika gazeti la Amkeni! la Septemba 22, 1983 (22/9/1983), la Kiingereza au gazeti la Kifaransa la Desemba 22, 1983 (22/12/1983).

Umejifunza Nini?

• Kufanya maendeleo ya kiroho kunatia ndani nini?

• Unaweza kufanya nini ili maendeleo yako yawe wazi . . .

unapokabili matatizo?

unapojitayarisha kwa ajili ya ndoa?

katika huduma?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 15]

Sala inaweza kukusaidia kukabiliana na matatizo

[Picha katika ukurasa wa 16]

Wahubiri vijana wanaweza kusitawisha jinsi gani njia bora za kufundisha?