Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Tumfuate “Kristo”?

Kwa Nini Tumfuate “Kristo”?

Kwa Nini Tumfuate “Kristo”?

“Mtu yeyote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe . . . na kunifuata sikuzote.”—LUKA 9:23.

1, 2. Kwa nini ni jambo la maana kwetu kufikiria kwa nini tunapaswa kumfuata “Kristo”?

YEHOVA anafurahi kama nini kuona ninyi wapya na vijana mkiwa kati ya makundi yaliyokutanika ya waabudu wake duniani! Mnapoendelea kujifunza Biblia, kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida, na kupata ujuzi zaidi wa kweli yenye kuokoa uhai iliyo katika Neno la Mungu, mnahitaji kuchukua kwa uzito mwaliko huu wa Yesu: “Mtu yeyote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe na kuuchukua mti wake wa mateso siku baada ya siku na kunifuata sikuzote.” (Luka 9:23) Yesu anasema kwamba unapaswa kujikana mwenyewe na kuwa mfuasi wake. Basi, ni jambo la maana kwetu kufikiria kwa nini tunapaswa kumfuata “Kristo.”—Mt. 16:13-16.

2 Namna gani sisi ambao tayari tunafuata hatua za Yesu Kristo? Tunahimizwa ‘tuendelee kufanya hivyo kwa ukamili zaidi.’ (1 The. 4:1, 2) Iwe tulikubali ibada ya kweli hivi karibuni au miaka mingi iliyopita, kutafakari kwa nini tunapaswa kumfuata Kristo kutatusaidia kutumia himizo la Paulo na kumfuata Kristo kwa ukamili zaidi kila siku. Acheni tufikirie sababu tano zinazoonyesha kwa nini tunapaswa kumfuata Kristo.

Ili Tuwe na Uhusiano wa Karibu Zaidi na Yehova

3. Tunaweza kumjua Yehova kupitia njia gani mbili?

3 Alipokuwa akizungumza na Waathene akiwa ‘amesimama katikati ya Areopago,’ mtume Paulo alisema hivi: “[Mungu] aliamuru nyakati na mipaka ya makao ya watu, ili wao wamtafute Mungu, ikiwa wangeweza kupapasa-papasa wakimtafuta na kwa kweli wampate, ijapokuwa, kweli, hayuko mbali sana na kila mmoja wetu.” (Mdo. 17:22, 26, 27) Tunaweza kumtafuta Mungu na kumjua kikweli. Kwa mfano, uumbaji unatufundisha mengi kuhusu sifa za Mungu na uwezo wake. Kutafakari kwa uthamini kuhusu kazi zake za uumbaji kunaweza kutufundisha mengi kumhusu Muumba. (Rom. 1:20) Yehova pia amefunua mambo mengi kujihusu katika Neno lake lililoandikwa, Biblia. (2 Tim. 3:16, 17) Kadiri ‘tunavyotafakari utendaji wake wote,’ na ‘kujishughulisha na matendo yake’ ndivyo tutakavyomjua Yehova vizuri zaidi.—Zab. 77:12.

4. Kumfuata Kristo kunaweza kutusaidia kwa njia gani kumkaribia Yehova zaidi?

4 Njia nyingine bora ya kumkaribia Yehova zaidi ni kumfuata Kristo. Hebu fikiria utukufu ambao Yesu alikuwa nao kando ya Baba yake “kabla ya ulimwengu kuwako”! (Yoh. 17:5) Yeye ndiye “mwanzo wa uumbaji wa Mungu.” (Ufu. 3:14) Akiwa “mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote,” aliishi kwa muda mrefu sana mbinguni akiwa na Baba yake, Yehova. Kabla ya kuja duniani, Yesu hakukaa tu na Baba yake, alifanya mengi zaidi. Alikuwa rafiki wa karibu wa Mungu, akifanya kazi kwa furaha pamoja na Mweza-Yote, nao walikuwa na uhusiano wa karibu zaidi wa upendo ambao hauna kifani. Yesu alitazama jinsi Baba yake alivyofanya mambo, alichunguza hisia na sifa Zake, pia alikubali na kufuata mambo yote aliyojifunza kutoka kwa Baba yake. Hivyo, Mwana huyo mtiifu akawa kama Baba yake hivi kwamba Biblia inamtaja kuwa “mfano wa Mungu asiyeonekana.” (Kol. 1:15) Tukimfuata Kristo kwa ukaribu, tunaweza kumkaribia Yehova zaidi.

Ili Tumwige Yehova kwa Ukamili

5. Ni nini kitakachotusaidia kumwiga Yehova kwa ukamili zaidi, na kwa nini?

5 ‘Tumefanywa kwa mfano wa Mungu, kwa sura yake,’ hivyo tuna uwezo wa kuonyesha sifa kama zake. (Mwa. 1:26) Mtume Paulo aliwahimiza Wakristo wawe “waigaji wa Mungu, kama watoto wapendwa.” (Efe. 5:1) Kumfuata Kristo kunatusaidia kumwiga Baba yetu wa mbinguni, kwa sababu Yesu alikuwa na maoni, hisia, na sifa kama za Mungu na alifunua utu wa Mungu kwa ukamili kuliko mtu mwingine yeyote. Alipokuwa duniani, Yesu hakulitangaza tu jina la Yehova. Badala yake, alitufunulia jinsi Yehova alivyo. (Soma Mathayo 11:27.) Yesu alifanya hivyo kwa maneno, matendo, mafundisho, na mfano wake.

6. Mafundisho ya Yesu yanafunua nini kumhusu Yehova?

6 Kupitia mafundisho yake, Yesu alitufundisha mambo ambayo Mungu anataka tufanye na jinsi anavyohisi kuhusu waabudu wake. (Mt. 22:36-40; Luka 12:6, 7; 15:4-7) Kwa mfano, baada ya kunukuu moja ya zile Amri Kumi, ile iliyosema “usifanye uzinzi,” Yesu alieleza maoni ya Mungu kuhusu mambo yanayotukia katika moyo wa mtu muda mrefu kabla ya kufanya tendo hilo. Alisema hivi: “Kila mtu ambaye anaendelea kumtazama mwanamke na kumtamani tayari amefanya uzinzi pamoja naye moyoni mwake.” (Kut. 20:14; Mt. 5:27, 28) Baada ya kutaja jinsi Mafarisayo walivyofasiri maneno haya ya Sheria—“mpende jirani yako na kumchukia adui yako”—Yesu alieleza maoni ya Yehova, aliposema: “Endeleeni kuwapenda adui zenu na kusali kwa ajili ya wale wanaowatesa ninyi.” (Mt. 5:43, 44; Kut. 23:4; Law. 19:18) Kuelewa maoni ya Mungu, jinsi anavyohisi, na matakwa yake kunatusaidia kumwiga kwa ukamili.

7, 8. Tunajifunza nini kumhusu Yehova kupitia mfano wa Yesu?

7 Yesu pia alifunua utu wa Baba yake kupitia mfano wake. Tunaposoma katika Injili kwamba Yesu aliwahurumia wenye uhitaji na wale wanaoteseka, na kwamba alikasirika wanafunzi wake walipowakemea watoto wadogo, je, hatumwoni Baba akihisi vivyo hivyo? (Marko 1:40-42; 10:13, 14; Yoh. 11:32-35) Fikiria jinsi matendo ya Yesu yanavyotusaidia kutambua sifa kuu za Mungu. Miujiza ambayo Kristo alifanya inaonyesha kwamba alikuwa na nguvu nyingi. Hata hivyo, hakutumia nguvu hizo kujiletea faida au kuwaumiza wengine. (Luka 4:1-4) Tendo la kuwafukuza wafanyabiashara wenye pupa kutoka katika hekalu linaonyesha kwamba alipenda haki! (Marko 11:15-17; Yoh. 2:13-16) Mafundisho na maneno yenye kuvutia aliyotumia ili kugusa mioyo ya watu yanathibitisha kwamba alikuwa “mtu mkuu kuliko Sulemani” katika kuonyesha hekima. (Mt. 12:42) Upendo ambao Yesu alionyesha alipokufa kwa ajili ya wengine unatukumbusha kwamba “hakuna aliye na upendo mkuu kuliko huu”!—Yoh. 15:13.

8 Mwana wa Mungu alimwakilisha Yehova kwa ukamili sana katika kila jambo alilofanya hivi kwamba alisema hivi: “Yule ambaye ameniona mimi amemwona Baba pia.” (Soma Yohana 14:9-11.) Kumfuata Kristo ni sawa na kumwiga Yehova.

Yesu Ndiye Mtiwa-Mafuta wa Yehova

9. Ni wakati gani na jinsi gani Yesu alipata kuwa Mtiwa-Mafuta wa Mungu?

9 Fikiria mambo yaliyotukia mwaka wa 29 W.K. katika majira ya kupukutika kwa majani wakati ambapo Yesu, akiwa na umri wa miaka 30, alimwendea Yohana Mbatizaji. “Baada ya kubatizwa Yesu akapanda mara moja kutoka katika maji; na, tazama! mbingu zikafunguliwa, naye akaona roho ya Mungu ikishuka kama njiwa, ikija juu yake.” Wakati huo, akawa Kristo, au Masihi. Kisha, Yehova mwenyewe akatangaza kwamba Yesu ndiye Mtiwa-Mafuta wake, aliposema: “Huyu ni Mwanangu, mpendwa, ambaye nimemkubali.” (Mt. 3:13-17) Hiyo ni sababu nzuri kama nini inayotuchochea kumfuata Kristo!

10, 11. (a) Jina “Kristo” linatumiwa kwa njia gani kuhusiana na Yesu? (b) Kwa nini tunapaswa kumfuata Yesu Kristo?

10 Katika Biblia, jina “Kristo” linatumiwa kumrejelea Yesu kwa njia mbalimbali, kama vile Yesu Kristo, Kristo Yesu, na Kristo. Yesu ndiye wa kwanza kutumia maneno “Yesu Kristo,” yaani, jina likifuatwa na cheo. Alipokuwa akisali kwa Baba yake, alisema hivi: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.” (Yoh. 17:3) Tunaposema “Yesu Kristo,” tunakazia yule aliyetumwa na Mungu na kuwa Mtiwa-Mafuta wake. Na tunaposema “Kristo Yesu,” tunakazia cheo chake badala ya mtu mwenyewe. (2 Kor. 4:5) Kutumia jina “Kristo,” ni njia nyingine ya kukazia cheo cha Yesu akiwa Masihi.—Mdo. 5:42.

11 Hata jina “Kristo” litumiwe namna gani kuhusiana na Yesu, linakazia ukweli huu wa maana: Hata ingawa Mwana wa Mungu alikuja duniani akiwa mwanadamu na kuwajulisha watu mapenzi ya Baba yake, hakuwa mtu wa kawaida tu wala nabii tu; alikuja kuwa Mtiwa-Mafuta wa Yehova. Tunapaswa kumfuata Mtiwa-Mafuta huyo.

Yesu Ndiye Njia Pekee ya Kupata Wokovu

12. Mtume Tomasi aliambiwa maneno gani ambayo yanatuhusu?

12 Sababu nyingine muhimu ya kuendelea kumfuata Masihi inaonyeshwa na maneno ambayo Yesu aliwaambia mitume wake waaminifu, saa chache tu kabla ya kifo chake. Wakati huo, Yesu alikuwa akijibu swali ambalo Tomasi aliuliza wakati Yesu aliposema anaenda kuwatayarishia mahali. Yesu alisema hivi: “Mimi ndiye njia na kweli na uzima. Hakuna anayekuja kwa Baba ila kupitia kwangu.” (Yoh. 14:1-6) Katika pindi hiyo, Yesu alikuwa akizungumza na mitume wake waaminifu 11. Aliwaahidi atawapa mahali mbinguni, lakini maneno yake yanawahusu pia wale walio na tumaini la kupata uzima wa milele duniani. (Ufu. 7:9, 10; 21:1-4) Jinsi gani?

13. Yesu ndiye “njia” katika maana gani?

13 Yesu Kristo ndiye “njia.” Hiyo inamaanisha kwamba ili tumfikie Mungu ni lazima tupitie kwa Yesu tu. Hilo ni kweli kuhusiana na sala, kwa sababu ni kwa kusali tu kupitia Yesu ndipo tunapoweza kuwa na uhakika wa kwamba Baba atatupa chochote tunachoomba kupatana na mapenzi Yake. (Yoh. 15:16) Hata hivyo, Yesu ndiye “njia” katika maana nyingine pia. Dhambi imewatenganisha wanadamu na Mungu. (Isa. 59:2) Yesu alitoa “nafsi yake kuwa fidia badala ya wengi.” (Mt. 20:28) Ndiyo sababu Biblia inaeleza hivi: “Damu ya Yesu . . . hutusafisha kutoka katika dhambi yote.” (1 Yoh. 1:7) Kwa hiyo, Mwana ametufungulia njia ya kupatanishwa na Mungu. (Rom. 5:8-10) Tunaweza kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Mungu ikiwa tutamwamini Yesu na kumtii.—Yoh. 3:36.

14. Ni kwa njia gani Yesu ndiye “kweli”?

14 Yesu ndiye “kweli” si kwa sababu tu alisema na kuishi kupatana na kweli bali pia kwa sababu alitimiza unabii wote ulioandikwa kumhusu Masihi, ndiyo, unabii mwingi sana. Mtume Paulo aliandika hivi: “Hata ahadi za Mungu ziwe nyingi kadiri gani, zimekuwa Ndiyo kwa njia yake.” (2 Kor. 1:20) Hata “kivuli cha mambo mema yatakayokuja” kilichotajwa katika Sheria ya Musa kilikuwa halisi katika Kristo Yesu. (Ebr. 10:1; Kol. 2:17) Unabii wote unamhusu Yesu, na unabii huo unakazia daraka lake kuu katika kutimizwa kwa kusudi la Yehova. (Ufu. 19:10) Ili tunufaike na mambo ambayo Mungu amekusudia kwa ajili yetu, tunahitaji kumfuata Masihi.

15. Ni kwa njia gani Yesu ndiye “uzima”?

15 Yesu ndiye “uzima” kwa sababu aliwanunua wanadamu kwa damu yake, na uzima wa milele ni zawadi ambayo Mungu anatoa “kupitia Kristo Yesu Bwana wetu.” (Rom. 6:23) Yesu ndiye “uzima” hata kwa wale waliokufa. (Yoh. 5:28, 29) Zaidi ya hilo, fikiria mambo ambayo atafanya akiwa Kuhani Mkuu wakati wa Utawala wake wa Miaka Elfu. Atawakomboa milele raia wake walio duniani kutoka katika dhambi na kifo!—Ebr. 9:11, 12, 28.

16. Tuna sababu gani ya kumfuata Yesu?

16 Kwa hiyo, jibu la Yesu kwa Tomasi lina maana kubwa sana kwetu. Yesu ndiye njia na kweli na uzima. Yeye ndiye aliyetumwa na Mungu ulimwenguni ili ulimwengu uokolewe kupitia yeye. (Yoh. 3:17) Na hakuna anayekuja kwa Baba isipokuwa kupitia Yesu. Biblia inasema hivi waziwazi: “Hakuna wokovu katika mwingine yeyote, kwa maana hakuna jina lingine chini ya mbingu walilopewa wanadamu ambalo kupitia hilo lazima sisi tupate kuokolewa.” (Mdo. 4:12) Basi, hata iwe tuliamini nini zamani, ni jambo la hekima kumwamini Yesu, kumfuata, na hivyo kuongozwa kwenye uzima.—Yoh. 20:31.

Tunaamuriwa Tumsikilize Kristo

17. Kwa nini ni jambo la maana sana kumsikiliza Mwana wa Mungu?

17 Petro, Yohana, na Yakobo walishuhudia Yesu akigeuka sura. Wakati huo, walisikia sauti kutoka mbinguni ikisema: “Huyu ni Mwanangu, ambaye amechaguliwa. Msikilizeni.” (Luka 9:28, 29, 35) Ni jambo la maana sana tutii amri ya kumsikiliza Masihi.—Soma Matendo 3:22, 23.

18. Tunaweza kumsikiliza Yesu Kristo jinsi gani?

18 Kumsikiliza Yesu kunatia ndani ‘kumtazama kwa makini, kufikiria sana mfano wake.’ (Ebr. 12:2 3) Hivyo, tunapaswa ‘kukazia uangalifu zaidi kuliko ilivyo kawaida mambo’ tunayosoma kumhusu katika Biblia na vichapo vya “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” na vilevile mambo tunayosikia kumhusu katika mikutano ya Kikristo. (Ebr. 2:1; Mt. 24:45) Tukiwa kondoo zake, acheni tuwe na hamu ya kumsikiliza Yesu na kumfuata.—Yoh. 10:27.

19. Ni jambo gani litakalotusaidia kumfuata Kristo sikuzote?

19 Je, tunaweza kufaulu kumfuata Kristo sikuzote, hata tukabili matatizo gani? Ndiyo, tunaweza, ikiwa tu ‘tutaendelea kushika kielelezo cha maneno yenye afya’ kwa kutumia mambo tunayojifunza “pamoja na imani na upendo vinavyohusiana na Kristo Yesu.”—2 Tim. 1:13.

Umejifunza Nini?

• Kwa nini kumfuata “Kristo” kunaweza kutusaidia tuzidi kumkaribia Yehova?

• Kwa nini kumwiga Yesu ni sawa na kumwiga Yehova?

• Ni kwa njia gani Yesu ndiye “njia na kweli na uzima”?

• Kwa nini tunapaswa kumsikiliza Mtiwa-Mafuta wa Yehova?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 29]

Mafundisho ya Yesu yalifunua maoni yaliyotukuka ya Yehova

[Picha katika ukurasa wa 30]

Ni lazima tumfuate kwa uaminifu Mtiwa-Mafuta wa Yehova

[Picha katika ukurasa wa 32]

Yehova alitangaza hivi: “Huyu ni Mwanangu . . . msikilizeni”