Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Waume, Igeni Upendo wa Kristo!

Waume, Igeni Upendo wa Kristo!

Waume, Igeni Upendo wa Kristo!

USIKU wa mwisho wa maisha yake duniani, Yesu aliwaambia mitume wake waaminifu hivi: “Ninawapa ninyi amri mpya, kwamba mpendane; kama vile ambavyo nimewapenda ninyi, ninyi nanyi mpendane vivyo hivyo. Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo kati yenu wenyewe.” (Yoh. 13:34, 35) Ndiyo, Wakristo wa kweli wanapaswa kupendana.

Akizungumza na waume ambao ni wafuasi wa Kristo, mtume Paulo aliandika hivi: “Enyi waume, endeleeni kuwapenda wake zenu, kama vile Kristo pia alivyolipenda kutaniko na kujitoa mwenyewe kwa ajili yake.” (Efe. 5:25) Mume Mkristo anaweza kutumia jinsi gani shauri hilo la Kimaandiko katika ndoa yake, hasa ikiwa mke wake ni mtumishi wa Yehova aliyejiweka wakfu?

Kristo Alilipenda Sana Kutaniko

Biblia inasema: “Waume wanapaswa kuwa wakiwapenda wake zao kama miili yao wenyewe. Yeye anayempenda mke wake anajipenda mwenyewe, kwa maana hakuna mtu anayeuchukia mwili wake kwa vyovyote; bali huulisha na kuutunza kwa upendo, kama vile Kristo pia anavyolitendea kutaniko.” (Efe. 5:28, 29) Yesu aliwapenda sana wanafunzi wake, naye aliwathamini sana. Hata ingawa hawakuwa wakamilifu, aliwatendea kwa upole na fadhili. Akitamani “kujipa mwenyewe kutaniko likiwa na fahari,” alikazia sifa nzuri za wanafunzi wake.—Efe. 5:27.

Kama vile Kristo alivyoonyesha kwamba analipenda kutaniko, ni lazima mume pia aonyeshe kwa maneno na kwa matendo kwamba anampenda mke wake. Mke akionyeshwa upendo kwa ukawaida na mume wake, atahisi kwamba anapendwa na atakuwa mwenye furaha. Lakini, mke aliye na nyumba nzuri na starehe zote za nyumbani anaweza kukosa furaha kabisa ikiwa mwenzi wake wa ndoa anampuuza au hamjali.

Mume anaweza kuonyesha jinsi gani kwamba anampenda mke wake? Anapokuwa mbele ya watu, anamtambulisha kwa wengine kwa heshima na anamsifu waziwazi kwa msaada wake. Ikiwa mke amefanya mengi ili familia yao ifanikiwe, mume wake hatasita kuwajulisha wengine jambo hilo. Wakiwa faraghani, mke anahitaji kuhisi kwamba mume wake anampenda. Huenda mambo kama vile kumgusa mkono, kumwonyesha tabasamu, kumkumbatia, na kumpongeza yakaonekana kuwa mambo madogo, lakini yanagusa sana moyo wa mwanamke.

“Haoni Aibu Kuwaita ‘Ndugu’”

Kristo Yesu ‘hakuona aibu kuwaita [wafuasi wake watiwa-mafuta] “ndugu.”’ (Ebr. 2:11, 12, 17) Ikiwa wewe ni mume Mkristo, kumbuka kwamba mke wako pia ni dada yako Mkristo. Wakfu wake kwa Yehova ndio unaochukua nafasi ya kwanza kabla ya nadhiri yake ya ndoa, iwe alibatizwa kabla au baada ya ninyi kufunga ndoa. Ndugu anayeongoza mkutano wa kutaniko anapomwomba mke wako atoe maelezo, anamwita “Dada fulani.” Yeye pia ni dada yako, si kwenye Jumba la Ufalme tu bali pia nyumbani. Ni jambo la maana kumtendea kwa fadhili na kwa upole nyumbani kama unavyomtendea kwenye Jumba la Ufalme.

Ikiwa una mapendeleo mengine ya utumishi katika kutaniko, huenda nyakati nyingine ikawa vigumu kusawazisha madaraka ya kutaniko na ya familia. Ushirikiano mzuri kati ya wazee na watumishi wa huduma na kuwakabidhi wengine madaraka kunaweza kukusaidia kupata wakati wa kuwa pamoja na dada anayekuhitaji zaidi, yaani, mke wako. Kumbuka kwamba ndugu mbalimbali wanaweza kutimiza madaraka uliyogawiwa katika kutaniko, lakini hakuna ndugu mwingine yeyote ambaye ameunganishwa na mke wako katika ndoa, isipokuwa wewe.

Zaidi ya hilo, wewe ndiye kichwa cha mke wako. Biblia inasema hivi: “Kichwa cha kila mwanamume ni Kristo; nacho kichwa cha mwanamke ni mwanamume.” (1 Kor. 11:3) Unapaswa kutumia ukichwa huo jinsi gani? Kwa njia ya upendo bali si kwa kutaja-taja andiko hilo na kudai uheshimiwe. Siri ya kutumia ukichwa kwa njia inayofaa ni kumwiga Yesu Kristo unaposhughulika na mke wako.—1 Pet. 2:21.

“Ninyi Ni Rafiki Zangu”

Yesu aliwaita wanafunzi wake rafiki zake. Aliwaambia hivi: “Siwaiti ninyi tena watumwa, kwa sababu mtumwa hajui yale ambayo bwana wake anafanya. Lakini nimewaita ninyi rafiki, kwa sababu mambo yote ambayo nimeyasikia kutoka kwa Baba yangu nimewajulisha ninyi.” (Yoh. 15:14, 15) Yesu na wanafunzi wake walikuwa na mawasiliano mazuri. Pia, walifanya mambo pamoja. “Yesu na wanafunzi wake” walialikwa kwenye karamu ya ndoa huko Kana. (Yoh. 2:2) Walipenda kwenda mahali mbalimbali, kama vile kwenye bustani ya Gethsemane. Biblia inasema kwamba “nyakati nyingi Yesu alikuwa amekutana hapo pamoja na wanafunzi wake.”—Yoh. 18:2.

Kwa hakika, mke anahitaji kuhisi kwamba yeye ndiye rafiki wa karibu zaidi wa mume wake. Enyi waume na wake, ni jambo la maana sana kwamba mfurahie maisha pamoja! Mtumikieni Mungu pamoja. Furahieni kujifunza Biblia pamoja. Tumieni wakati pamoja—mkitembea, mkiongea, na kula pamoja. Msiwe tu wenzi wa ndoa; mnapaswa pia kuwa marafiki wanaopendana.

‘Aliwapenda Mpaka Mwisho’

Yesu ‘aliwapenda wanafunzi wake mpaka mwisho.’ (Yoh. 13:1) Waume fulani wanashindwa kumwiga Kristo katika jambo hilo. Huenda hata wakamwacha ‘mke wa ujana wao,’ labda ili wamchukue mwanamke mchanga.—Mal. 2:14, 15.

Wengine, kama vile Willi, wanamwiga Kristo. Afya ya mke wa Willi, ilikuwa inadhoofika, kwa hivyo, alihitaji kutunzwa kwa miaka mingi. Willi alikuwa na maoni gani kuhusu hali hiyo? Alisema hivi: “Sikuzote ninamwona mke wangu kuwa zawadi kutoka kwa Mungu, nami ninamthamini kama zawadi. Zaidi ya hilo, miaka 60 iliyopita, nilimwahidi kwamba nitamtunza, katika hali nzuri au mbaya. Sitasahau kamwe ahadi hiyo.”

Waume Wakristo, igeni upendo wa Kristo. Mpende sana mke wako anayemwogopa Mungu. Yeye ni dada yako na rafiki yako.

[Picha katika ukurasa wa 20]

Je, mke wako ndiye rafiki yako wa karibu zaidi?

[Picha katika ukurasa wa 20]

‘Endelea kumpenda mke wako’