Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mwana wa Dada ya Paulo Amwokoa Asiuawe

Mwana wa Dada ya Paulo Amwokoa Asiuawe

Wafundishe Watoto Wako

Mwana wa Dada ya Paulo Amwokoa Asiuawe

JE, UNAJUA kwamba mtume Paulo alikuwa na watu wa familia waliokuwa wafuasi wa Yesu? *— Inaonekana dada ya Paulo na mwana wa dada huyo walikuwa wafuasi wa Yesu. Mwana huyo wa dada yake alimwokoa Paulo asiuawe! Hatujui jina la mwana huyo wala la mama yake, lakini tunajua mambo ambayo kijana huyo alifanya. Je, ungependa kujua alifanya nini?—

Paulo amerudi tu kutoka katika safari yake ya tatu ya umishonari na sasa yuko Yerusalemu. Yaelekea ni mwaka wa 56 W.K. Paulo amekamatwa na atapelekwa mahakamani. Lakini maadui wa Paulo hawataki ahukumiwe. Wanataka auawe! Kwa hiyo wamepanga wanaume 40 hivi wamngojee njiani wakiwa wamejificha ili wamuue Paulo.

Kwa njia fulani, mwana wa dada ya Paulo anajua mpango huo. Unajua anafanya nini?—Anaenda na kumwambia Paulo. Mara moja Paulo anamwambia ofisa wa jeshi hivi: “Mpeleke kijana huyu kwa kiongozi wa kijeshi, kwa maana ana jambo fulani la kumweleza.” Ofisa huyo anampeleka kwa kiongozi wa kijeshi, Klaudio Lisia, na kumweleza kwamba kijana huyo ana habari muhimu. Klaudio anaenda naye kando, na kijana huyo anamweleza kila kitu.

Klaudio anamwonya mwana huyo wa dada ya Paulo: “Usipayuke-payuke kwa yeyote kwamba umenieleza mambo hayo.” Kisha anawaita maofisa wawili wa jeshi na kuwaambia watayarishe askari-jeshi 200, wapanda-farasi 70, na watu 200 wachukua-mikuki ili waende moja kwa moja mpaka Kaisaria. Saa tatu ya usiku, wanaume 470 wanaondoka na kumpeleka Paulo salama kwa Gavana Mroma Feliksi jijini Kaisaria. Klaudio anamwandikia Feliksi barua na kumweleza kuhusu mpango wa kumuua Paulo.

Kwa hiyo, Wayahudi wanalazimika kukutana na Paulo katika mahakama jijini Kaisaria ili kutoa mashtaka yao. Lakini ni wazi kwamba hawawezi kuthibitisha kwamba Paulo amefanya jambo lolote baya. Hata hivyo, Paulo anafungwa bila sababu kwa miaka miwili. Kwa hiyo, anaomba kesi yake isikilizwe huko Roma, na anapelekwa huko.—Matendo 23:16–24:27; 25:8-12.

Tunaweza kujifunza nini kutokana na simulizi hili kuhusu mwana wa dada ya Paulo?— Tunahitaji kuwa na ujasiri ili kusema yaliyo sawa na tukifanya hivyo, tunaweza kuokoa maisha. Hata wakati Yesu alipojua kwamba maadui “walikuwa wakitafuta kumuua” aliendelea kuwaambia watu kuhusu Ufalme wa Mungu. Yesu alituambia tufanye vivyo hivyo. Je, tutafanya hivyo? Ndiyo, ikiwa tuna ujasiri kama ule wa mwana wa dada ya Paulo.—Yohana 7:1; 15:13; Mathayo 24:14; 28:18-20.

Paulo alimshauri hivi kijana Timotheo aliyekuwa rafiki yake: “Jiangalie daima wewe mwenyewe na kufundisha kwako. Kaa katika mambo haya, kwa maana kwa kufanya hivyo utajiokoa wewe mwenyewe na wale wanaokusikiliza pia.” (1 Timotheo 4:16) Kwa kweli, mwana wa dada ya Paulo alitenda kupatana na maneno hayo ya Paulo yanayotia moyo. Je, utafanya hivyo?

[Maelezo ya chini]

^ fu. 3 Kama unasoma sehemu hii pamoja na watoto, unapoona kistari kama hiki (—), tua na uwaruhusu watoe maoni yao.

Maswali:

○ Baadhi ya watu wa familia ya Paulo walikuwa akina nani, na tumejifunza nini kuwahusu?

○ Mwana wa dada ya Paulo alifanya nini ili amwokoe Paulo asiuawe?

○ Kwa kumtii Yesu, tunaweza kufanya jambo gani linaloweza kuokoa maisha ya watu leo?