Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Mungu Anabadili Maoni Yake?

Je, Mungu Anabadili Maoni Yake?

Je, Mungu Anabadili Maoni Yake?

BIBLIA inasema hivi kumhusu Mungu: “Habadiliki, kama kugeuka kwa kivuli.” Naye Mungu mwenyewe alitoa uhakikisho huu: “Mimi ni Yehova; sikubadilika.” (Yakobo 1:17; Malaki 3:6) Yehova Mungu ni tofauti sana na watu ambao ni vigumu kuwapendeza na ambao hawawezi kuaminika kwa sababu maoni yao yanabadilika daima.

Hata hivyo, wasomaji fulani wa Biblia hujiuliza kama Mungu amebadili maoni yake. Kwa mfano, wakati mmoja Yehova Mungu aliwapa Wakristo uwezo wa kufanya miujiza, lakini sivyo ilivyo leo. Nyakati za kale, Mungu aliwavumilia watu wenye wake wengi, lakini sasa haruhusu jambo hilo. Chini ya Sheria ya Musa Yehova aliwataka Waisraeli washike Sabato, lakini sivyo ilivyo leo. Je, visa hivyo havionyeshi kwamba Mungu amebadilika?

Kwanza kabisa, tunaweza kuwa na hakika kwamba Mungu habadili viwango vyake vya upendo na haki. Pia, ‘kusudi lake la milele’ la kuwabariki wanadamu kupitia Ufalme wake halijabadilika kamwe. (Waefeso 3:11) Hata hivyo, kama vile unavyoweza kubadili maoni yako kumhusu mtu ambaye nyakati zote tabia zake zinakuudhi, Yehova pia hubadilika kulingana na hali.

Mungu pia hubadili maagizo yake kwa watu wake kupatana na hali na mahitaji yao. Hilo halipaswi kutushangaza. Fikiria jinsi ambavyo mwelekezi stadi angefanya anapoona hatari mbele. Angewaambia watu anaowatembeza wafuate barabara nyingine ili kuepuka hatari. Lakini hilo halimaanishi kwamba amebadili maoni yake kuhusu mahali wanapoenda, sivyo? Kwa hiyo, acheni tuchunguze vile visa vitatu vilivyotajwa ambavyo huwatatanisha watu fulani.

Kwa Nini Miujiza Iliisha?

Kwa nini Mungu aliwapa baadhi ya Wakristo wa karne ya kwanza uwezo wa kufanya miujiza? Huenda unajua kwamba wakati Israeli lilipokuwa taifa lililochaguliwa na Mungu, mara nyingi Mungu aliwaonyesha kupitia miujiza kwamba alikuwa pamoja nao. Kupitia Musa, Mungu alionyesha uwezo wake mkubwa kwa kuwakomboa Waisraeli kutoka Misri na kuwaongoza kupitia nyikani hadi Nchi ya Ahadi. Inasikitisha kwamba mara nyingi Waisraeli walikosa imani. Hatimaye Yehova alipolikataa taifa la Israeli na kuanzisha kutaniko la Kikristo, aliwapa mitume na wengineo uwezo wa kufanya miujiza. Kwa mfano, mtume Petro na Yohana walimponya mtu aliyekuwa kilema tangu kuzaliwa, naye Paulo akamfufua mtu fulani. (Matendo 3:2-8; 20:9-11) Miujiza waliyofanya ilisaidia kuanzisha Ukristo katika nchi nyingi. Kwa nini basi, miujiza iliisha?

Mtume Paulo alijibu swali hilo kupitia mfano: “Nilipokuwa mtoto, nilikuwa nikisema kama mtoto, nikifikiri kama mtoto, nikiwaza kama mtoto; lakini kwa kuwa sasa nimekuwa mtu mzima, nimeziondolea mbali tabia za mtoto.” (1 Wakorintho 13:11) Kama vile wazazi wanavyomtendea mtoto mdogo tofauti na mtoto ambaye ni mtu mzima, ndivyo njia ya Yehova ya kushughulika na kutaniko la Kikristo ilivyobadilika wakati lilipokomaa likaacha kuwa kama “mtoto.” Mtume Paulo alieleza kwamba zawadi hizo za kimuujiza kama vile uwezo wa kuzungumza katika lugha za kigeni au kutoa unabii “[zinge]ondolewa mbali.”—1 Wakorintho 13:8.

Kwa Nini Watu Waliruhusiwa Kuwa na Wake Wengi?

Yesu alionyesha kwamba Mungu aliweka kiwango cha ndoa alipowaambia wanadamu wa kwanza wawili hivi: “Mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye atashikamana na mke wake, na hao wawili watakuwa mwili mmoja.” (Mathayo 19:5) Ndoa ilipaswa kuwa muungano wa kudumu kati ya watu wawili. Hata hivyo, kufikia wakati Mungu alipowafanya Waisraeli kuwa taifa na kuwapa Sheria, lilikuwa jambo la kawaida mtu kuwa na mke zaidi ya mmoja. Kwa hiyo, ingawa Mungu hakuanzisha wala kuwatia moyo watu wawe na mke zaidi ya mmoja, alitoa sheria zilizowapa mwongozo kuhusiana na jambo hilo. Kutaniko la Kikristo lilipoanzishwa, Neno la Mungu lilikataza waziwazi mtu kuwa na mke zaidi ya mmoja.—1 Timotheo 3:2.

Yehova Mungu huvumilia mambo fulani hadi wakati wake wa kuyarekebisha unapofika. (Waroma 9:22-24) Yesu alionyesha kwamba Yehova alikuwa amevumilia kwa muda tu desturi zisizofaa kuhusu ndoa kati ya Waisraeli kana kwamba amewapa “ruhusa” kwa sababu ya ‘ugumu wao wa moyo.’—Mathayo 19:8; Methali 4:18.

Kwa Nini Sheria ya Kushika Sabato Ilikuwa ya Muda Tu?

Mungu aliwapa Waisraeli sheria ya kushika Sabato ya kila juma baada ya kuwakomboa kutoka Misri. Baadaye aliifanya kuwa sehemu ya Sheria yao ya taifa. (Kutoka 16:22-30; 20:8-10) Mtume Paulo alieleza kwamba Yesu alijitoa kuwa dhabihu na ‘kufuta ile Sheria ya amri zilizofanyizwa kwa maagizo’ na pia “kuifuta kabisa ile hati iliyoandikwa kwa mkono.” (Waefeso 2:15; Wakolosai 2:14) Sheria ‘zilizofutwa’ zilitia ndani sheria ya Sabato, kwa kuwa Biblia inaendelea kusema: “Kwa hiyo mtu yeyote asiwahukumu ninyi katika kula na kunywa au kuhusu sherehe au kuhusu kushika mwezi mpya au sabato.” (Wakolosai 2:16) Kwa nini basi Mungu alitoa Sheria, kutia ndani sheria ya kushika Sabato?

Mtume Paulo aliandika: “Sheria imekuwa mtunzaji wetu kutuongoza kwa Kristo.” Kisha akaongeza: “Lakini sasa kwa kuwa imani imefika, sisi hatuko tena chini ya mtunzaji.” (Wagalatia 3:24, 25) Badala ya kubadili maoni yake, Mungu alitumia Sabato kama mpango wa muda ili kuwafundisha watu kwamba wanapaswa kutenga wakati kwa ukawaida ili kutafakari mambo ya kiroho. Ingawa sheria ya Sabato ilikuwa ya muda, ilionyesha wakati ujao ambapo matatizo ya kimwili na ya kiroho ya wanadamu yangeisha.—Waebrania 4:10; Ufunuo 21:1-4.

Mungu Mwenye Kutegemeka na Mwenye Upendo

Mifano ya Biblia ambayo imetajwa hapo juu inaonyesha kwamba Yehova Mungu alitoa maagizo na miongozo tofauti-tofauti nyakati tofauti-tofauti. Lakini hiyo haimaanishi kwamba alibadili maoni yake. Badala yake, alishughulikia mahitaji ya watu wake chini ya hali zilizo tofauti, na alifanya hivyo kwa faida yao. Anafanya vivyo hivyo leo.

Kwa kuwa Yehova habadili viwango vyake, tunaweza kujua tunachopaswa kufanya ili kumpendeza. Isitoshe, tunaweza kuwa na hakika kwamba ahadi zote za Mungu zitatimia. Yehova anasema: “Kila jambo ambalo ni mapenzi yangu nitafanya . . . Nimelifanyiza, pia nitalitenda.”—Isaya 46:10, 11.

[Blabu katika ukurasa wa 21]

Mungu habadili viwango vyake vya upendo na haki

[Blabu katika ukurasa wa 22]

Paulo alieleza kwamba zawadi za kimuujiza “[zinge]ondolewa mbali”

[Blabu katika ukurasa wa 23]

Ndoa ilipaswa kuwa muungano wa kudumu kati ya watu wawili