Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Anafikiria Kupungukiwa Kwetu

Anafikiria Kupungukiwa Kwetu

Mkaribie Mungu

Anafikiria Kupungukiwa Kwetu

Mambo ya Walawi 5:2-11

“NILIJARIBU sana, lakini sikuridhika.” Akasema mwanamke mmoja kuhusu jitihada zake za kumpendeza Mungu. Je, Yehova Mungu anakubali jitihada za waabudu wake? Je, anafikiria uwezo na hali zinazoweza kuwazuia wasitimize wanachotaka? Ili kujibu maswali hayo, itafaa kuchunguza kinachosemwa katika Sheria ya Musa kuhusu matoleo fulani, kama yanavyoelezwa katika Mambo ya Walawi 5:2-11.

Chini ya Sheria, Mungu alitaka watu watoe dhabihu mbalimbali, au matoleo, ili kufanya upatanisho wa dhambi. Katika visa vilivyotajwa katika simulizi hili, mtu alikuwa amefanya dhambi bila kukusudia au bila kufikiri. (Mstari wa 2-4) Alipojulishwa kuhusu jambo hilo, alipaswa kuungama dhambi yake na kutoa toleo la hatia—“mwana-kondoo jike au mwana-mbuzi jike.” (Mstari wa 5, 6) Lakini namna gani ikiwa alikuwa maskini na hakuwa na mwana-kondoo au mbuzi wa kutoa? Je, Sheria ilidai kwamba akope mnyama huyo na hivyo kujiingiza katika deni? Je, alipaswa kufanya kazi ili aweze kununua mnyama huyo, na hivyo kufanya dhambi zake zisipatanishwe upesi?

Kwa kuwa Sheria ilitegemea huruma za Yehova, ilisema hivi: “Ikiwa hana uwezo wa kutoa kondoo, basi atamletea Yehova njiwa-tetere wawili au hua wawili wachanga wawe toleo lake la hatia kwa ajili ya dhambi ambayo ametenda, mmoja kwa ajili ya toleo la dhambi na mmoja kwa ajili ya toleo la kuteketezwa.” (Mstari wa 7) Maneno “ikiwa hana uwezo” yanaweza pia kusemwa “ikiwa mkono wake haungeweza kufikia.” Ikiwa Mwisraeli alikuwa maskini hivi kwamba hangeweza kununua kondoo, basi Mungu alifurahi kupokea kitu ambacho mtoaji angeweza kufikia—njiwa-tetere wawili au hua wawili.

Lakini namna gani ikiwa mtu huyo hangeweza hata kununua ndege hao wawili? “Basi ataleta sehemu ya kumi ya efa [vikombe nane au tisa] ya unga laini kwa ajili ya toleo la dhambi,” Sheria ilisema. (Mstari wa 11) Kwa ajili ya maskini, Yehova alikubali kwamba toleo la dhambi litolewe bila damu. * Katika Israeli, umaskini haukumzuia mtu yeyote asipate baraka ya kupatanishwa au pendeleo la kurudisha amani kati yake na Mungu.

Tunajifunza nini kumhusu Yehova kutokana na sheria iliyohusu matoleo ya hatia? Yeye ni Mungu mwenye huruma, na mwenye kukubali sababu ambaye anafikiria kupungukiwa kwa waabudu wake. (Zaburi 103:14) Anataka tumkaribie na kusitawisha uhusiano mzuri pamoja naye hata ikiwa tunakabili hali ngumu, kama vile ikiwa tunazeeka, tuna afya mbaya, au madaraka ya familia au ya aina nyingine. Tunaweza kufarijika kujua kwamba Yehova Mungu anafurahi tunapofanya yote tunayoweza kulingana na hali zetu.

[Maelezo ya chini]

^ fu. 4 Uwezo wa kupatanisha wa mnyama aliyetolewa dhabihu ulikuwa katika damu yake, ambayo Mungu aliiona kuwa takatifu. (Mambo ya Walawi 17:11) Je, hilo lilimaanisha kwamba matoleo ya maskini ya unga hayakuwa na thamani? La. Yehova alithamini matoleo kama hayo yaliyotolewa kwa unyenyekevu na hiari. Isitoshe, dhambi za taifa lote—kutia ndani za maskini—zilifunikwa na damu ya wanyama waliotolewa kwa Mungu katika Siku ya Upatanisho ya kila mwaka.—Mambo ya Walawi 16:29, 30.