Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Uwe na Bidii kwa Ajili ya Nyumba ya Yehova!

Uwe na Bidii kwa Ajili ya Nyumba ya Yehova!

Uwe na Bidii kwa Ajili ya Nyumba ya Yehova!

“Bidii kwa ajili ya nyumba yako itanila.”—YOH. 2:17.

1, 2. Yesu alifanya nini hekaluni mwaka wa 30 W.K., na kwa nini?

FIKIRIA hali hii. Ni wakati wa Pasaka ya mwaka wa 30 W.K. Miezi sita iliyotangulia, Yesu alianza huduma yake duniani. Sasa yuko njiani kwenda Yerusalemu. Huko, akiwa hekaluni katika Ua wa Mataifa, Yesu anawakuta “wale waliokuwa wakiuza ng’ombe na kondoo na njiwa na waliokuwa wakivunja pesa wakiwa wameketi.” Anatumia mjeledi wa kamba, na kuwatoa wanyama wote nje, na bila shaka wafanyabiashara pia wanawafuata wanyama hao. Yesu anamwaga sarafu za wale ambao wanabadili pesa na kupindua meza zao. Anawaamuru wale wanaouza njiwa wachukue vitu vyao na kuondoka.—Yoh. 2:13-16.

2 Matendo ya Yesu yanaonyesha waziwazi kwamba anahangaikia hekalu. Anawaamuru hivi: “Acheni kuifanya nyumba ya Baba yangu kuwa nyumba ya biashara!” Wanafunzi wa Yesu wanapoangalia matukio hayo, wanakumbuka maneno yaliyoandikwa na mtunga-zaburi Daudi karne nyingi mapema: “Bidii kwa ajili ya nyumba yako itanila.”—Yoh. 2:16, 17; Zab. 69:9.

3. (a) Bidii ni nini? (b) Tunaweza kujiuliza swali gani?

3 Yesu alitenda kwa njia hiyo kwa sababu alichochewa na hangaiko na bidii kwa ajili ya nyumba ya Mungu. Bidii ni “hamu na shauku nyingi katika kufuatilia jambo fulani.” Katika karne hii ya 21, Wakristo zaidi ya milioni saba wanaonyesha bidii kwa ajili ya nyumba ya Mungu. Tukiwa mtu mmoja-mmoja, tunaweza tukajiuliza hivi: ‘Ninaweza kuongeza bidii yangu kwa ajili ya nyumba ya Yehova jinsi gani?’ Ili kutusaidia kujibu swali hilo, acheni kwanza tuchunguze nyumba ya Mungu leo ni nini. Kisha, tutachunguza mifano ya Biblia ya watu waaminifu ambao walionyesha bidii kwa ajili ya nyumba hiyo. Mifano yao iliandikwa “ili kutufundisha sisi” na inaweza kutuchochea kuwa na bidii kubwa hata zaidi.—Rom. 15:4.

Nyumba ya MunguZamani na Leo

4. Hekalu lililojengwa na Sulemani lilitimiza kusudi gani?

4 Katika Israeli la kale, hekalu huko Yerusalemu ndilo lililokuwa nyumba ya Mungu. Bila shaka, Yehova hakuwa akiishi kihalisi katika hekalu hilo. Alisema hivi: “Mbingu ni kiti changu cha ufalme, na dunia ni kiti cha miguu yangu. Iko wapi, basi, nyumba ambayo ninyi mnaweza kunijengea, na pako wapi, basi, mahali pa kupumzika kwa ajili yangu?” (Isa. 66:1) Hata hivyo, hekalu lililojengwa wakati wa utawala wa Sulemani lilikuwa kitovu cha ibada ya Yehova, mahali ambapo sala zilitolewa.—1 Fal. 8:27-30.

5. Ni mpango gani uliopo leo ambao ulifananishwa na ibada kwenye hekalu la Sulemani?

5 Leo, nyumba ya Yehova si jengo fulani la mawe huko Yerusalemu au mahali pengine popote pale. Badala yake, ni mpango unaotusaidia kumkaribia Mungu katika ibada kwa msingi wa fidia au dhabihu ya ukombozi ya Kristo. Watumishi wote waaminifu wa Mungu duniani wanamwabudu Yehova kwa umoja katika hekalu hilo la kiroho.—Isa. 60:4, 8, 13; Mdo. 17:24; Ebr. 8:5; 9:24.

6. Ni wafalme gani wa Yudea ambao walionyesha bidii ya pekee kwa ajili ya ibada ya kweli?

6 Baada ya Israeli kugawanyika katika falme mbili mwaka wa 997 K.W.K., wafalme 4 kati ya wale 19 waliotawala Yuda, sehemu ya kusini, walikuwa na bidii ya pekee kwa ajili ya ibada ya kweli. Wafalme hao walikuwa Asa, Yehoshafati, Hezekia, na Yosia. Ni masomo gani ya maana tunayoweza kujifunza kutokana na mifano yao?

Kumtumikia Mungu kwa Moyo Wote Kunaleta Baraka

7, 8. (a) Yehova anabariki utumishi wa aina gani? (b) Ni onyo gani tunaloweza kujifunza kutokana na mfano wa Mfalme Asa?

7 Wakati wa utawala wa Mfalme Asa, Yehova alitokeza manabii ili kuliongoza taifa Lake katika njia ya uaminifu. Kwa mfano, Biblia inatueleza kwamba Asa alimsikiliza nabii Azaria, mwana wa Odedi. (Soma 2 Mambo ya Nyakati 15:1-8.) Mabadiliko ambayo Asa alifanya yalileta umoja kati ya watu wa Yuda na kati ya hesabu kubwa ya watu kutoka katika ufalme wa Israeli ambao walienda kuhudhuria kusanyiko kubwa lililofanywa huko Yerusalemu. Wote pamoja walitangaza azimio lao la kumwabudu Yehova kwa ushikamanifu. Tunasoma hivi: “Wakamwapia Yehova kwa sauti kubwa na kwa sauti za shangwe na kwa tarumbeta na kwa baragumu. Na Yuda wote wakaanza kushangilia juu ya lile jambo waliloapa; kwa maana walikuwa wameapa kwa moyo wao wote nao walikuwa wamemtafuta kwa furaha kamili hivi kwamba yeye aliwaruhusu wampate; na Yehova akaendelea kuwapa pumziko kuzunguka pande zote.” (2 Nya. 15:9-15) Bila shaka, Yehova atatubariki vivyo hivyo tukimtumikia kwa moyo wetu wote.—Marko 12:30.

8 Inasikitisha kwamba baadaye Asa alikasirika sana aliporekebishwa na mwonaji Hanani. (2 Nya. 16:7-10) Tunaitikia jinsi gani Yehova anapotushauri au kututolea mwongozo kupitia wazee Wakristo? Je, tunakubali na kutumia haraka mashauri yao yanayotegemea Maandiko na hivyo kuepuka kuanguka katika mtego wa kuwa na kinyongo?

9. Ni tishio gani ambalo Yehoshafati na Yuda walikabili, na walitenda jinsi gani?

9 Yehoshafati alitawala akiwa mfalme huko Yuda katika karne ya kumi K.W.K. Yeye na wakaaji wote wa Yuda walikabili tishio la majeshi ya muungano ya Waamoni, Wamoabu, na watu wa eneo lenye milima la Seiri. Ingawa aliogopa, mfalme huyo alifanya nini? Yeye na watu wake, wakiwa pamoja na wake na watoto wao, walikusanyika kwenye nyumba ya Yehova ili kusali. (Soma 2 Mambo ya Nyakati 20:3-6.) Kupatana na maneno ambayo Sulemani alisema mapema wakati wa kuliweka wakfu hekalu, Yehoshafati alitoa dua akisema: “Ee Mungu wetu, je, hutafanya hukumu juu yao? Kwa maana hakuna nguvu ndani yetu mbele ya umati huu mkubwa unaokuja juu yetu; nasi wenyewe hatujui tunalopaswa kufanya, lakini macho yetu yanakuelekea wewe.” (2 Nya. 20:12, 13) Baada ya Yehoshafati kusali, hapo “katikati ya kutaniko,” roho ya Yehova ilimchochea Yahazieli, Mlawi, kusema maneno yenye kufariji ambayo yaliwapa watu tumaini.—Soma 2 Mambo ya Nyakati 20:14-17.

10. (a) Yehoshafati na Yuda walipata mwongozo jinsi gani? (b) Tunaweza kuonyesha jinsi gani kwamba tunathamini mwongozo tunaopata kutoka kwa Yehova leo?

10 Ndiyo, wakati huo, Yehoshafati na ufalme wa Yuda walipata mwongozo kutoka kwa Yehova kupitia kwa Yahazieli. Leo, tunapata faraja na mwongozo kupitia jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara. Bila shaka, sikuzote tunapaswa kuwaheshimu na kushirikiana na wazee waliowekwa rasmi, ambao wanafanya kazi ya uchungaji kwa bidii na kuhakikisha kwamba miongozo ya “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” inafuatwa.—Mt. 24:45; 1 The. 5:12, 13.

11, 12. Ni somo gani tunaloweza kujifunza kutokana na hali ambayo Yehoshafati na Yuda walikabili?

11 Kama vile tu Yehoshafati na watu wake walivyokusanyika pamoja kutafuta mwongozo wa Yehova, basi tusipuuze kuhudhuria kwa ukawaida mikutano pamoja na ndugu na dada zetu. Ikiwa nyakati fulani tunajikuta katika hali ngumu, tusijue jambo la kufanya, acheni tufuate mfano mzuri wa Yehoshafati na watu wa Yuda na kusali kwa Yehova huku tukimtegemea kabisa. (Met. 3:5, 6; Flp. 4:6, 7) Hata ikiwa tunaishi mbali na waamini wenzetu, maombi yetu kwa Yehova yanatuunganisha na “ushirika mzima wa ndugu [zetu] ulimwenguni.”—1 Pet. 5:9.

12 Yehoshafati na watu wake walifuata mwongozo uliotolewa na Mungu kupitia Yahazieli. Walipata matokeo gani? Walishinda vita na wakarudi Yerusalemu ‘wakishangilia’ huku wakipiga “vinubi na tarumbeta, kwenye nyumba ya Yehova.” (2 Nya. 20:27, 28) Sisi pia tunaheshimu mwongozo unaotolewa na Yehova kupitia tengenezo lake na tunajiunga na wengine katika kumsifu.

Tutunze Vizuri Mahali Petu pa Mikutano

13. Ni kazi gani ambayo Hezekia alianzisha mwanzoni mwa utawala wake?

13 Katika mwezi wa kwanza wa utawala wake, Hezekia alionyesha kwamba alikuwa na bidii kwa ajili ya ibada ya Yehova kwa kufungua tena hekalu na kulirekebisha. Aliweka makuhani na Walawi ili waisafishe nyumba ya Mungu. Walifanya kazi hiyo kwa muda wa siku 16. (Soma 2 Mambo ya Nyakati 29:16-18.) Jitihada hizo zinatukumbusha kazi tunayofanya ya kutunza na kurekebisha mahali petu pa mikutano ili pawe safi, na hilo linaonyesha kwamba tuna bidii kwa ajili ya ibada ya Yehova. Je, hujawahi kusikia mambo yaliyoonwa yanayoonyesha kwamba watu wanavutiwa na bidii ya ndugu na dada zetu ambao wanashiriki katika kazi hiyo? Ndiyo, jitihada zao zinamletea Yehova sifa nyingi.

14, 15. Ni kazi gani leo ambayo imemletea Yehova sifa nyingi? Toa mifano.

14 Katika jiji fulani kaskazini mwa Uingereza, mwanamume mmoja alipinga kazi ya marekebisho iliyokusudiwa kufanywa kwenye Jumba la Ufalme lililopakana na nyumba yake. Ndugu wa eneo hilo walimtendea kwa fadhili mwanamume huyo. Kwa kuwa ukuta ulio kati ya Jumba la Ufalme na nyumba ya jirani huyo ulihitaji kurekebishwa, ndugu walijitolea kufanya kazi hiyo bila malipo. Walifanya kazi kwa bidii, na walijenga upya karibu ukuta wote. Walishughulikia hali hiyo vizuri sana hivi kwamba jirani huyo alibadili mtazamo wake. Sasa yeye ndiye anayesaidia kuangalia ikiwa uwanja wa Jumba la Ufalme uko salama.

15 Watu wa Yehova wanashiriki katika kazi ya ulimwenguni pote ya ujenzi. Wajitoleaji wenyeji wanajiunga na watumishi wa wakati wote wa kimataifa kujenga Majumba ya Ufalme na pia Majumba ya Makusanyiko na makao ya Betheli. Sam ni injinia wa vyombo vya kusambaza joto, hewa, na mashini zinazopoza hewa. Yeye na mke wake, Ruth, wamesafiri katika nchi nyingi za Ulaya na Afrika kusaidia katika miradi ya ujenzi. Popote pale wanapoenda, wanafurahia pia kuhubiri pamoja na makutaniko ya maeneo hayo. Sam anaeleza kilichomchochea kushiriki katika miradi hiyo ya kimataifa: “Nilitiwa moyo na wengine ambao walitumikia hapa katika makao ya Betheli na katika nchi za kigeni. Kuona bidii na shangwe yao kulinichochea kabisa kutaka kuingia katika utumishi huo.”

Tii Maagizo ya Mungu

16, 17. Watu wa Mungu wameshiriki kwa bidii katika utendaji gani wa pekee, na kumekuwa na matokeo gani?

16 Zaidi ya kurekebisha hekalu, Hezekia alirudisha maadhimisho ya kila mwaka ya Pasaka ambayo Yehova alikuwa ameamuru. (Soma 2 Mambo ya Nyakati 30:1, 4, 5.) Hezekia na wakaaji wa Yerusalemu walialika taifa lote, na hata wakaaji wa ufalme wa kaskazini kuhudhuria maadhimisho hayo. Wakimbiaji walipeleka barua za mwaliko kotekote nchini.—2 Nya. 30:6-9.

17 Katika miaka ya hivi karibuni, tumeshiriki katika jitihada zinazofanana kidogo na hizo. Tumetumia mialiko iliyochapishwa yenye kuvutia ili kuwaalika watu wa maeneo yetu kukusanyika nasi ili kuadhimisha Mlo wa Jioni wa Bwana, na hivyo kutii amri ya Yesu. (Luka 22:19, 20) Baada ya kupokea maagizo kwenye Mikutano yetu ya Utumishi, tumeshiriki kwa bidii katika kazi hiyo. Na Yehova ametubariki sana. Mwaka jana, Mashahidi wa Yehova milioni saba hivi waligawa mialiko hiyo, na jumla ya watu 17,790,631 walihudhuria!

18. Kwa nini ni jambo la maana sana kwetu kuwa na bidii kwa ajili ya ibada ya kweli?

18 Ilisemwa hivi kumhusu Hezekia: “Alimtegemea Yehova Mungu wa Israeli; na baada yake hapakuwa na yeyote kama yeye kati ya wafalme wote wa Yuda, hata wale waliomtangulia. Naye akaendelea kushikamana na Yehova. Hakugeuka kando na kuacha kumfuata, bali aliendelea kuzishika amri zake ambazo Yehova alimwamuru Musa.” (2 Fal. 18:5, 6) Na tufuate mfano wake. Bidii yetu kwa ajili ya nyumba ya Mungu itatusaidia ‘kuendelea kushikamana na Yehova’ huku tukitazamia uzima wa milele.—Kum. 30:16.

Fuata Haraka Mwongozo

19. Ni jitihada gani za pekee zinazofanywa wakati wa Ukumbusho?

19 Yosia alipotawala akiwa mfalme, yeye pia alifanya matayarisho makubwa ya kuadhimisha Pasaka. (2 Fal. 23:21-23; 2 Nya. 35:1-19) Sisi pia tunafanya matayarisho ya pekee kwa ajili ya makusanyiko ya wilaya, ya mzunguko, na ya pekee, na pia Ukumbusho. Katika nchi fulani ndugu zetu wanahatarisha hata maisha yao ili kukusanyika pamoja kuadhimisha kifo cha Kristo. Wazee wenye bidii wanahakikisha kwamba hakuna mtu anayesahauliwa katika kutaniko. Wale waliozeeka na wagonjwa wanasaidiwa ili wawepo wakati wa tukio hilo.

20. (a) Ni nini kilichotukia wakati wa utawala wa Mfalme Yosia, na alitenda jinsi gani? (b) Tunapaswa kuchukua kwa uzito somo gani?

20 Wakati wa kazi ya kurudisha ibada safi ambayo Mfalme Yosia alianzisha, Kuhani Mkuu Hilkia ‘alikipata kile kitabu cha sheria ya Yehova kupitia mkono wa Musa.’ Hilkia alimpa Shafani, mwandishi wa mfalme kitabu hicho, naye Shafani akaanza kumsomea Yosia ujumbe wa kitabu hicho. (Soma 2 Mambo ya Nyakati 34:14-18.) Kulikuwa na matokeo gani? Papo hapo mfalme alirarua mavazi yake kwa huzuni naye akawaamuru watu wamtafute Yehova. Kupitia nabii wa kike Hulda, Mungu alitoa ujumbe ambao ulishutumu mazoea fulani ya kidini yaliyokuwa yakifanywa huko Yuda. Hata hivyo, jitihada nzuri za Yosia za kuondoa ibada ya sanamu zilionekana wazi, naye aliendelea kuwa na kibali cha Yehova ingawa ilitabiriwa kwamba misiba ingepata taifa hilo. (2 Nya. 34:19-28) Tunaweza kujifunza nini kutokana na hilo? Bila shaka, tamaa yetu ni kama ile ya Yosia. Tunataka kufuata haraka mwongozo wa Yehova na kuchukua kwa uzito onyo kuhusu hatari ya kuruhusu uasi-imani na ukosefu wa uaminifu uchafue ibada yetu. Na tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova ataona na kuthamini bidii yetu kwa ajili ya ibada safi, kama tu alivyofanya katika kisa cha Yosia.

21, 22. (a) Kwa nini tunapaswa kuonyesha bidii kwa ajili ya nyumba ya Yehova? (b) Tutachunguza nini katika habari inayofuata?

21 Wale wafalme wanne wa Yuda, yaani, Asa, Yehoshafati, Hezekia, na Yosia, walituwekea mifano mizuri katika kuwa na bidii kwa ajili ya ibada na nyumba ya Mungu. Bidii yetu inapaswa pia kutuchochea tumtegemee Yehova na kujitahidi kwa ajili ya ibada yake. Bila shaka, ni jambo la hekima na linaloleta furaha kutii maagizo ya Mungu na kuitikia upendo wake na kukubali nidhamu tunayopewa kupitia kutaniko na wazee.

22 Katika habari inayofuata tutakazia uangalifu jinsi ya kuwa na bidii kwa ajili ya huduma ya shambani na itawatia moyo vijana wamtumikie kwa bidii Baba yetu mwenye upendo. Pia, tutachunguza jinsi tunavyoweza kuepuka moja ya mambo yenye uvutano mwovu sana wa Shetani. Tukitii kwa bidii vikumbusho hivyo vyote kutoka kwa Yehova, tutakuwa tukifuata mfano wa Mwana wa Yehova mwenyewe, Yesu, ambaye ilisemwa hivi kumhusu: “Bidii nyingi kwa ajili ya nyumba yako imenila.”—Zab. 69:9; 119:111, 129; 1 Pet. 2:21.

Je, Unakumbuka?

• Yehova anabariki utumishi wa aina gani, na kwa nini?

• Tunaweza kuonyesha jinsi gani kwamba tunamtumaini Yehova?

• Bidii inaweza kutuchochea jinsi gani kutii maagizo ya Mungu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 9]

Asa, Yehoshafati, Hezekia, na Yosia, walionyesha jinsi gani bidii kwa ajili ya nyumba ya Yehova?