Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Uwe na “Bidii kwa Ajili ya Kazi Njema”!

Uwe na “Bidii kwa Ajili ya Kazi Njema”!

Uwe na “Bidii kwa Ajili ya Kazi Njema”!

‘Yesu alijitoa mwenyewe kwa ajili yetu ili atukomboe sisi kutoka katika kila namna ya uasi-sheria na kujisafishia mwenyewe watu walio wake kwa njia ya pekee, walio na bidii kwa ajili ya kazi njema.’—TITO 2:14.

1. Kunatukia nini hekaluni Yesu anapofika mnamo Nisani 10, 33 W.K.?

NI NISANI 10, 33 W.K., siku chache tu kabla ya maadhimisho ya Pasaka. Umati mkubwa wa waabudu katika eneo la hekalu huko Yerusalemu umesisimuka. Ni nini kitakachotukia Yesu anapofika? Waandikaji watatu wa Injili, Mathayo, Marko, na Luka, wote wanathibitisha kwamba kwa mara ya pili, Yesu anawafukuza wale wanaouza na kununua hekaluni. Anapindua meza za wale wanaobadili pesa na viti vya wale ambao wanauza njiwa. (Mt. 21:12; Marko 11:15; Luka 19:45) Bidii ya Yesu haijapungua tangu alipochukua hatua kama hiyo miaka mitatu mapema.—Yoh. 2:13-17.

2, 3. Tunajua jinsi gani kwamba Yesu hakuwa na bidii tu ya kulisafisha hekalu?

2 Simulizi la Mathayo linaonyesha kwamba katika pindi hiyo, Yesu hakuwa na bidii tu ya kulisafisha hekalu. Aliwaponya pia vipofu na vilema ambao walimwendea hekaluni. (Mt. 21:14) Simulizi la Luka linazungumza kuhusu kazi nyingine ambazo Yesu alitimiza. ‘Yesu alikuwa akifundisha kila siku katika hekalu.’ (Luka 19:47; 20:1) Kwa hiyo, bidii ya Yesu ilionekana wazi katika huduma yake ya hadharani.

3 Baadaye, mtume Paulo alimwandikia Tito na akaeleza kwamba Yesu ‘alijitoa mwenyewe kwa ajili yetu ili atukomboe sisi kutoka katika kila namna ya uasi-sheria na kujisafishia mwenyewe watu walio wake kwa njia ya pekee, walio na bidii kwa ajili ya kazi njema.’ (Tito 2:14) Tunaweza kuwa wenye “bidii kwa ajili ya kazi njema” katika njia gani leo? Na mifano ya wafalme wazuri wa Yuda inaweza kututia moyo jinsi gani?

Bidii Katika Kuhubiri na Kufundisha

4, 5. Ni katika njia gani wafalme wanne wa Yuda walionyesha bidii kwa ajili ya kazi njema?

4 Asa, Yehoshafati, Hezekia, na Yosia walianzisha kampeni ya kuondoa kabisa ibada ya sanamu huko Yuda. Asa ‘aliondoa madhabahu za kigeni na mahali pa juu, akazivunja nguzo takatifu na kuikata miti mitakatifu.’ (2 Nya. 14:3) Yehoshafati, akichochewa na bidii kwa ajili ya ibada ya Yehova, ‘aliondoa mahali pa juu na miti mitakatifu katika Yuda.’—2 Nya. 17:6; 19:3. *

5 Baada ya sherehe ya siku saba ya Pasaka ambayo Hezekia alifanya huko Yerusalemu, “Waisraeli wote waliokuwa hapo wakaenda katika majiji ya Yuda, nao wakazivunja nguzo takatifu na kuikata miti mitakatifu na kupabomoa mahali pa juu na madhabahu kutoka katika Yuda yote na Benyamini na katika Efraimu na Manase mpaka walipomaliza.” (2 Nya. 31:1) Kijana Yosia alikuwa mfalme alipokuwa na umri wa miaka minane tu. Maandiko yanasema hivi: “Katika mwaka wa nane wa kutawala kwake, alipokuwa angali mvulana, akaanza kumtafuta Mungu wa Daudi babu yake; na katika mwaka wa kumi na mbili akaanza kutakasa Yuda na Yerusalemu kutokana na mahali pa juu na miti mitakatifu na sanamu za kuchongwa na sanamu za kuyeyushwa.” (2 Nya. 34:3) Hivyo, wafalme hao wote wanne walikuwa na bidii kwa ajili ya kazi njema.

6. Kwa nini huduma yetu inaweza kulinganishwa na kampeni za wafalme waaminifu wa Yuda?

6 Vivyo hivyo leo, tunashiriki katika kampeni ya kuwasaidia watu waache mafundisho ya uwongo ya dini, kutia ndani ibada ya sanamu. Huduma yetu ya nyumba kwa nyumba inatuwezesha kukutana na watu wa kila aina. (1 Tim. 2:4) Msichana mmoja kutoka Asia anakumbuka jinsi mama yake alivyokuwa akifanya matambiko mbele ya sanamu nyingi nyumbani kwao. Kwa kuwa aliwaza kwamba sanamu zote haziwezi kumwakilisha Mungu wa kweli, mara nyingi msichana huyo alisali ili apate kumjua Mungu wa kweli. Aliposikia mlango ukigongwa alifungua na akakuta kwamba ni wanawake wawili Mashahidi ambao walikuwa tayari kumsaidia kujifunza kuhusu jina la pekee la Mungu wa kweli, Yehova. Alishukuru kama nini kujua ukweli kuhusu sanamu! Sasa anashiriki kwa bidii sana katika utumishi wa shambani, na hivyo anawasaidia watu wengine kiroho.—Zab. 83:18; 115:4-8; 1 Yoh. 5:21.

7. Tunaweza kufanya nini ili kuwaiga walimu waliotumwa kotekote nchini katika siku za Yehoshafati?

7 Tunaposhiriki katika huduma ya nyumba kwa nyumba, tunahubiri kikamilifu kadiri gani eneo ambalo tumegawiwa? Inapendeza kujua kwamba katika mwaka wa tatu wa utawala wake, Yehoshafati aliwatuma wakuu watano, Walawi tisa, na makuhani wawili. Aliwatuma katika majiji yote ili kuwafundisha watu sheria za Yehova. Kampeni yao ilikuwa na matokeo mazuri sana hivi kwamba watu wa mataifa jirani wakaanza kumwogopa Yehova. (Soma 2 Mambo ya Nyakati 17:9, 10) Tukiwatembelea watu nyumbani kwao nyakati na siku tofauti-tofauti, huenda tukafanikiwa kuzungumza na washiriki wengi wa familia moja.

8. Tunaweza kupanua utumishi wetu jinsi gani?

8 Watumishi wengi wa Mungu leo wamekuwa tayari kuacha nyumba zao na kuhama ili kutumika mahali ambapo pana uhitaji mkubwa zaidi wa Mashahidi wenye bidii. Je, unaweza kufanya hivyo? Wengine wetu ambao hatuwezi kuhama huenda tukajaribu kuwahubiria watu wanaoishi katika eneo letu ambao wanazungumza lugha tofauti. Kwa sababu ya watu wa mataifa mbalimbali ambao anakutana nao katika eneo lake, Ron aliye na umri wa miaka 81 alijifunza salamu katika lugha 32! Hivi karibuni alikutana barabarani na wenzi fulani wa ndoa kutoka Afrika na akawasalimu kwa lugha yao ya asili, Yoruba. Walimuuliza Ron ikiwa aliwahi kuwa Afrika. Aliposema hapana, walimuuliza alijua jinsi gani lugha yao. Hilo lilimpa nafasi ya kuwatolea ushahidi mzuri. Bila kusita, walikubali magazeti na hata wakampa anwani yao. Ron alituma anwani hiyo kwa kutaniko la eneo ambako watu hao waliishi ili ndugu wa huko wajifunze nao Biblia.

9. Kwa nini ni jambo la maana katika huduma yetu kusoma maandiko moja kwa moja kutoka katika Biblia? Toa mfano.

9 Walimu waliotumwa na Yehoshafati kotekote nchini walikuwa na “kitabu cha sheria ya Yehova.” Ulimwenguni pote tunajitahidi kuwafundisha watu Biblia, kwa sababu Biblia ni Neno la Mungu. Tunaonyesha kwamba Biblia ni ya maana sana katika huduma yetu kwa kujitahidi kuwasomea watu moja kwa moja kutoka katika Biblia, ili wengine waone kuwa maneno yake ni ya kweli. Mwenye nyumba fulani alimweleza Shahidi mmoja anayeitwa Linda kwamba mume wake aliyepooza alihitaji msaada wake. Mwenye nyumba huyo alilalamika hivi: “Sijui nilifanya nini hivi kwamba Mungu akaruhusu jambo hili linipate.” Linda alimuuliza hivi: “Je, ninaweza kukuhakikishia jambo fulani?” Kisha, Linda akasoma maneno ya Yakobo 1:13 na kuongezea hivi: “Mateso yote ambayo sisi na wapendwa wetu tunapata si adhabu kutoka kwa Mungu.” Aliposikia maneno hayo, mwenye nyumba huyo akamkumbatia Linda kwa shauku. Linda anasema hivi: “Niliweza kumfariji kwa kutumia Biblia. Nyakati nyingine maandiko tunayosoma kutoka katika Biblia ni yale ambayo mwenye nyumba hajawahi kamwe kusikia.” Kwa sababu ya mazungumzo hayo, mwanamke huyo alikubali kujifunza Biblia.

Vijana Wanamtumikia Mungu kwa Bidii

10. Yosia aliwawekea jinsi gani mfano mzuri vijana Wakristo leo?

10 Tukirudia mfano wa Yosia, tunaona kwamba alifuatia ibada ya kweli akiwa kijana na alikuwa na umri wa miaka 20 hivi alipoanza kampeni yake kubwa ya kukomesha ibada ya sanamu. (Soma 2 Mambo ya Nyakati 34:1-3.) Vijana wengi leo wanaonyesha bidii kama hiyo katika utumishi wao wa Ufalme.

11-13. Ni mambo gani tunaweza kujifunza kutoka kwa vijana ambao wanamtumikia Yehova kwa bidii leo?

11 Hannah, ambaye anaishi huko Uingereza, alikuwa na umri wa miaka 13 na alikuwa akijifunza Kifaransa shuleni aliposikia kwamba kikundi cha Kifaransa kilikuwa kimeanzishwa katika mji jirani. Baba yake alikubali kumsindikiza kuhudhuria mikutano huko. Sasa akiwa na umri wa miaka 18, Hannah ambaye ni painia wa kawaida anahubiri kwa bidii katika Kifaransa. Je, wewe pia unaweza kujifunza lugha ya kigeni na hivyo kuwasaidia watu wengine wajifunze kumhusu Yehova?

12 Rachel alifurahia sana kutazama video moja (Pursue Goals That Honor God au Poursuivez Des Objectifs Qui Honorent Dieu katika Kifaransa). Anaeleza hivi kuhusu maoni aliyokuwa nayo alipoanza kumtumikia Yehova mwaka wa 1995: “Nilifikiri nilikuwa nikiendelea vizuri katika kweli.” Kisha anaongezea hivi: “Baada ya kutazama video hiyo, sasa ninatambua kwamba nilikuwa tu nikifanya mambo ya msingi kwa miaka mingi. Ni lazima nipiganie kweli, nijitahidi kabisa na kukazia akili funzo langu la kibinafsi na utumishi wangu.” Sasa Rachel anaona kwamba anamtumikia Yehova kwa bidii zaidi. Amepata matokeo gani? “Uhusiano wangu pamoja na Yehova umekuwa mzuri sana. Sala zangu ni zenye maana zaidi, funzo langu ni zuri na lenye kuridhisha zaidi, na masimulizi ya Biblia yamekuwa halisi zaidi kwangu. Kwa hiyo, ninafurahia sana huduma na ninapata uradhi wa kweli ninapoona maneno ya Yehova yakiwafariji wengine.”

13 Luke ni kijana mwingine aliyetiwa moyo na video moja (Young People AskWhat Will I Do With My Life? au Les jeunes s’interrogentQue vais-je faire de ma vie? ya Kifaransa). Baada ya kuitazama, Luke anaandika hivi: “Ninahisi nimechochewa kuchunguza upya maisha yangu.” Anakiri hivi: “Zamani, nilisukumwa kufuatilia usalama wa kifedha kwa kutanguliza elimu ya juu na kisha kukazia fikira miradi ya kiroho. Mikazo kama hiyo haimsaidii mtu kufanya maendeleo ya kiroho; badala yake inamdhoofisha.” Enyi akina ndugu na dada vijana, kwa nini msijaribu kuona ikiwa mnaweza kutumia mambo mliyojifunza shuleni ili kupanua huduma yenu kama alivyofanya Hannah? Na kwa nini msiige mfano wa Rachel kwa kufuatilia kwa bidii miradi ambayo kwa kweli inamheshimu Mungu? Fuateni mfano wa Luke, epukeni hatari ambazo zimekuwa mtego kwa vijana wengi.

Tii Maonyo kwa Bidii

14. Yehova anakubali ibada ya aina gani, na kwa nini si rahisi kudumisha ibada hiyo leo?

14 Watu wa Yehova wanahitaji kuwa safi ili Yehova akubali ibada yao. Isaya anaonya hivi: “Geukeni, geukeni, tokeni humo, msiguse kitu chochote kilicho najisi; tokeni katikati yake [Babiloni], jiwekeni safi, ninyi mnaovichukua vyombo vya Yehova.” (Isa. 52:11) Miaka mingi kabla ya Isaya kuandika maneno hayo, Mfalme mzuri Asa aliendelea kwa bidii na kampeni ya kuondoa kabisa upotovu wa maadili katika Yuda. (Soma 1 Wafalme 15:11-13) Na karne nyingi baadaye, mtume Paulo alimwambia Tito kwamba Yesu alijitoa mwenyewe kuwasafisha wafuasi wake na kuwafanya wawe “watu walio wake kwa njia ya pekee, walio na bidii kwa ajili ya kazi njema.” (Tito 2:14) Leo katika jamii hii iliyopotoka, si jambo rahisi kubaki safi kiadili, hasa kwa vijana. Kwa mfano, watumishi wote wa Mungu, vijana kwa wazee, wanapaswa kupambana ili kuepuka kabisa kuchafuliwa na ponografia (picha au habari za ngono) inayoonyeshwa kwenye vibao vya matangazo, televisheni, sinema, na hasa kwenye Intaneti.

15. Ni nini kinachoweza kutusaidia kuchukia mambo mabaya?

15 Bidii yetu katika kutii maonyo ya Mungu inaweza kutusaidia kuchukia mambo mabaya. (Zab. 97:10; Rom. 12:9) Tunapaswa kuchukia kabisa ponografia ili “tuepuke uvutano wake wenye nguvu sana kama sumaku,” kama alivyosema Mkristo mmoja. Ili kutenganisha vipande vya chuma ambavyo vimeshikanishwa na sumaku, mtu anahitaji kutumia nguvu zaidi kuliko nguvu ambazo zinaunganisha vipande hivyo. Vivyo hivyo, tunahitaji jitihada kubwa ili kukataa kushawishiwa na ponografia. Lakini kuelewa madhara makubwa ambayo ponografia inaweza kutuletea kutatusaidia tuichukie kabisa. Ndugu mmoja alijitahidi sana kuacha zoea lake la kutazama ponografia kwenye Intaneti. Alihamisha kompyuta yake na kuiweka mahali ambapo washiriki wote wa familia wangeweza kuiona. Pamoja na hayo, yeye mwenyewe aliazimia zaidi kuwa safi kiadili na kuwa na bidii kwa ajili ya kazi njema. Hata alichukua hatua nyingine. Kwa kuwa alihitaji kutumia Intaneti katika shughuli zake, aliamua kutumia Intaneti wakati tu alipokuwa na mke wake.

Faida ya Kuwa na Mwenendo Mzuri

16, 17. Mwenendo wetu mzuri wa Kikristo unaweza kuwa na matokeo gani juu ya wale wanaotutazama? Toa mfano.

16 Vijana wa kiume na wa kike wanaonyesha mtazamo mzuri katika utumishi wa Yehova, na hilo linawavutia kama nini watazamaji! (Soma 1 Petro 2:12.) Mtu mmoja alibadili mtazamo wake kuelekea Mashahidi wa Yehova baada ya kufanya kazi kwa siku nzima akirekebisha mashini ya kuchapisha katika Betheli ya London. Mke wake, ambaye alikuwa akijifunza Biblia pamoja na Shahidi mmoja, alitambua jinsi mtazamo wa mume wake ulivyobadilika. Kabla ya hapo, mwanamume huyo hakutaka Mashahidi wafike nyumbani kwake. Lakini aliporudi kutoka Betheli alisema mambo mengi mazuri kuhusu jinsi alivyotendewa kwa fadhili. Alisema kwamba hakusikia mtu yeyote akitumia lugha chafu. Kila mtu alikuwa mwenye subira, na mazingira yalikuwa ya amani. Alivutiwa hasa na ndugu na dada vijana ambao walifanya kazi kwa bidii bila mshahara, na ambao wamejitolea kutumia wakati na nguvu zao ili kusaidia kueneza habari njema.

17 Vivyo hivyo, ndugu na dada ambao wanafanya kazi za kimwili ili kutunza familia zao wanafanya hivyo kwa nafsi yao yote. (Kol. 3:23, 24) Mara nyingi, hilo linafanya waajiri wao wathamini bidii yao ya kutoka moyoni na hawataki kuwapoteza.

18. Tunaweza kuwa wenye “bidii kwa ajili ya kazi njema” jinsi gani?

18 Kumtegemea Yehova, kutii maagizo yake, na kutunza mahali petu pa mikutano ni kati ya mambo yanayoonyesha kwamba tuna bidii kwa ajili ya nyumba ya Yehova. Zaidi ya hayo, tunataka kushiriki kikamilifu kadiri tunavyoweza katika kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme na kufanya wanafunzi. Iwe sisi ni vijana au wazee, tutapata baraka nyingi ikiwa tutafanya yote tunayoweza ili kuishi kulingana na viwango vya usafi ambavyo vinahusianishwa na ibada yetu. Na tutaendelea kujulikana kuwa watu wenye “bidii kwa ajili ya kazi njema.”—Tito 2:14.

[Maelezo ya chini]

^ fu. 4 Huenda Asa aliondoa mahali pa juu ambapo palitumiwa kwa ajili ya ibada ya miungu ya uwongo lakini si mahali ambapo watu walimwabudu Yehova. Au huenda ikawa kwamba mahali pa juu palijengwa tena katika kipindi cha mwisho cha utawala wa Asa na kwamba paliondolewa na mwana wake Yehoshafati.—1 Fal. 15:14; 2 Nya. 15:17.

Ulijifunza nini kutokana na mifano ya Biblia na ile ya leo

• kuhusu jinsi ya kuonyesha bidii katika kuhubiri na kufundisha?

• kuhusu jinsi vijana Wakristo wanavyoweza kuwa wenye “bidii kwa ajili ya kazi njema”?

• kuhusu jinsi ya kuacha mazoea mapotovu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 13]

Je, unatumia Biblia kwa ukawaida katika huduma yako?

[Picha katika ukurasa wa 15]

Kujifunza kuzungumza lugha nyingine unapokuwa shuleni kunaweza kukusaidia kupanua huduma yako