Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sema Kweli na Jirani Yako

Sema Kweli na Jirani Yako

Sema Kweli na Jirani Yako

“Sasa kwa kuwa mmeuondolea mbali uwongo, semeni kweli kila mmoja wenu na jirani yake.”—EFE. 4:25.

1, 2. Watu wengi wana maoni gani kuhusu kweli?

KWA miaka mingi watu wamekuwa wakibishana ikiwa wanadamu wanaweza kuwa wasema-kweli au kujua ukweli. Katika karne ya sita K.W.K., Alcaeus, mwandikaji wa mashairi Mgiriki alisema hivi: “Mna ukweli ndani ya divai.” Alimaanisha kwamba ukweli unaweza kujulikana tu baada ya mtu kulewa na labda kuanza kuropoka-ropoka maneno. Gavana Mroma wa karne ya kwanza Pontio Pilato alikuwa pia na maoni yaliyopotoka kuhusu kweli alipomuuliza Yesu kwa dhihaka: “Kweli ni nini?”—Yoh. 18:38.

2 Leo watu wana maoni mengi yanayopingana kuhusu kweli. Watu wengi wanasema kwamba neno “kweli” lina maana mbalimbali au kwamba kweli inategemea mtu mmoja-mmoja. Wengine wanasema kweli ikiwa tu watafaidika au wanapotaka kusuluhisha matatizo haraka. Kitabu kinachoitwa “Umuhimu wa Kusema Uwongo” (cha Kiingereza) kinasema hivi: “Unyoofu ni sifa inayofaa, lakini haina thamani kubwa katika mapambano ya maisha ya kufa na kupona na ya kutafuta usalama. Mwanadamu hana lingine la kufanya, ni lazima aseme uwongo ili aishi.”

3. Kwa nini Yesu aliweka mfano mzuri sana katika kusema kweli?

3 Wanafunzi wa Kristo wako tofauti kama nini! Yesu hakuwa na maoni kama hayo ya kifalsafa kuhusu kweli. Sikuzote alisema kweli. Hata maadui wake walikiri hivi: “Mwalimu, tunajua wewe una ukweli nawe hufundisha njia ya Mungu katika kweli.” (Mt. 22:16) Vivyo hivyo leo, Wakristo wa kweli wanaiga mfano wa Yesu. Hawasiti kusema kweli. Wanakubaliana kwa moyo wote na mtume Paulo, aliyewahimiza hivi waamini wenzake: “Sasa kwa kuwa mmeuondolea mbali uwongo, semeni kweli kila mmoja wenu na jirani yake.” (Efe. 4:25) Acheni tuzungumzie mambo matatu yanayotajwa na Paulo. Kwanza, jirani yetu ni nani? Pili, kusema kweli kunamaanisha nini? Na tatu, tunaweza kutumia himizo hilo jinsi gani katika maisha yetu ya kila siku?

Jirani Yetu Ni Nani?

4. Tofauti na viongozi Wayahudi wa karne ya kwanza, Yesu alionyesha jinsi gani maoni ya Yehova kuhusu jirani yetu?

4 Katika karne ya kwanza W.K., viongozi fulani Wayahudi walifundisha kwamba ni Wayahudi wenzao tu au marafiki wa karibu ndio waliostahili kuitwa “jirani.” Hata hivyo, Yesu aliiga kikamili utu na maoni ya Baba yake. (Yoh. 14:9) Aliwaonyesha wanafunzi wake kwamba Mungu hapendelei jamii moja au taifa moja na kudharau mataifa mengine. (Yoh. 4:5-26) Zaidi ya hayo, roho takatifu ilimfunulia mtume Petro kwamba “Mungu hana ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye anamwogopa na kutenda uadilifu anakubalika kwake.” (Mdo. 10:28, 34, 35) Kwa hiyo, tunapaswa kuwaona watu wote kuwa majirani wetu, na kuwapenda hata wale ambao wanatutendea kama maadui.—Mt. 5:43-45.

5. Kusema kweli na jirani yetu kunamaanisha nini?

5 Lakini Paulo alimaanisha nini aliposema kwamba tunapaswa kusema kweli na jirani yetu? Kusema kweli kunahusisha kusema mambo ya hakika, yasiyo na udanganyifu wowote. Wakristo wa kweli hawapotoshi au kuficha mambo ya hakika ili kuwadanganya wengine. ‘Wanachukia maovu’ na ‘kushikamana na mema.’ (Rom. 12:9) Ili kumwiga “Mungu wa ukweli,” tunapaswa kujitahidi kuwa wanyoofu na wasema-kweli katika shughuli zetu zote. (Zab. 15:1, 2; 31:5) Tukichagua maneno kwa uangalifu, tunaweza kutatua matatizo kwa busara na bila kutumia uwongo hata katika hali zinazoleta aibu.—Soma Wakolosai 3:9, 10.

6, 7. (a) Je, kuwa wasema-kweli kunamaanisha kwamba ni lazima tumfunulie mtu yeyote yule hata mambo ya kibinafsi? Eleza. (b) Ni nani tunayeweza kumtumaini na kumwambia kweli?

6 Je, kuwa msema-kweli kunamaanisha kwamba ni lazima tumfunulie mtu yeyote kila jambo analotaka kujua? Si lazima. Yesu alipokuwa duniani, alionyesha kwamba watu fulani hawastahili kupewa jibu la moja kwa moja au habari fulani. Viongozi wa kidini wanafiki walipomuuliza alifanya ishara na miujiza kwa nguvu au mamlaka ya nani, Yesu alisema hivi: “Nitawauliza ninyi swali moja. Nijibuni, nami pia nitawaambia ninyi ninafanya mambo haya kwa mamlaka gani.” Waandishi hao na wanaume wazee walipokataa kumjibu, Yesu alisema: “Wala mimi siwaambii ninyi ninafanya mambo haya kwa mamlaka gani.” (Marko 11:27-33) Kwa sababu ya mazoea yao ya ufisadi na ukosefu wao wa imani, Yesu hakuhisi kwamba alilazimika kujibu swali lao. (Mt. 12:10-13; 23:27, 28) Vivyo hivyo leo, watu wa Yehova wanahitaji kujilinda kutokana na waasi-imani na watu wengine waovu ambao wanatumia udanganyifu au hila kwa makusudi ya kichoyo.—Mt. 10:16; Efe. 4:14.

7 Paulo pia alionyesha kwamba huenda watu fulani hawastahili kupata jibu kamili. Alisema kwamba watu ‘wenye kupiga porojo na wenye kujiingiza katika mambo ya watu wengine, wanaongea juu ya mambo ambayo hawapaswi.’ (1 Tim. 5:13) Ndiyo, watu wanaojiingiza katika mambo ya wengine au wale ambao hawawezi kutumainiwa kuweka siri wataona kwamba wengine hawataki kuwaambia mambo yao ya kibinafsi. Ni vizuri zaidi kutii shauri hili la Paulo lililoongozwa na roho takatifu: ‘Ifanye iwe shabaha yako kuishi kwa utulivu na kukazia akili mambo yako mwenyewe.’ (1 The. 4:11) Hata hivyo, nyakati nyingine huenda wazee wa kutaniko wakalazimika kuuliza maswali kuhusu mambo ya kibinafsi ili watimize migawo yao. Katika hali kama hiyo, kushirikiana nao kwa kusema kweli ni jambo linalothaminiwa sana na lenye faida kubwa.—1 Pet. 5:2.

Sema Kweli Katika Mambo ya Familia

8. Kusema kweli kunawasaidia jinsi gani washiriki wa familia kuwa na uhusiano wa karibu zaidi?

8 Kwa kawaida tunakuwa na uhusiano wa karibu sana na washiriki wa familia yetu. Ili kutia nguvu uhusiano huo, ni jambo la maana kwa kila mshiriki kusema kweli na mwenzake. Matatizo mengi na kutoelewana kunaweza kupunguzwa au kuepukwa tukiwasiliana kwa uhuru, unyoofu, na kwa fadhili. Kwa mfano, tunapokosea, je, tunasita kukiri kosa hilo kwa mwenzi wetu, watoto wetu, au washiriki wengine wa karibu wa familia? Kuomba msamaha kutoka moyoni kunasaidia kudumisha amani na umoja katika familia.—Soma 1 Petro 3:8-10.

9. Kwa nini kusema kweli si sababu ya kuongea ovyoovyo au bila adabu?

9 Kusema kweli hakumaanishi kwamba tunapaswa kuongea ovyoovyo au bila busara. Watu hawapendezwi na maneno yanayosemwa na mtu asiye na adabu hata kama ni ya kweli. Paulo alisema hivi: “Uchungu wote wenye uovu na hasira na ghadhabu na kupiga kelele na matukano na viondolewe mbali kutoka kwenu pamoja na ubaya wote. Bali iweni wenye fadhili ninyi kwa ninyi, wenye huruma nyororo, mkisameheana kwa hiari kama vile Mungu pia kupitia Kristo alivyowasamehe ninyi kwa hiari.” (Efe. 4:31, 32) Tunapozungumza kwa njia ya fadhili na yenye adabu, tunafanya watu wapendezwe na ujumbe wetu na tunaonyesha kwamba tunawaheshimu wale tunaozungumza nao.—Mt. 23:12.

Sema Kweli Katika Mambo ya Kutaniko

10. Wazee Wakristo wanaweza kujifunza nini kutokana na mfano bora wa Yesu katika kusema kweli?

10 Yesu alizungumza na wanafunzi wake kwa njia rahisi na ya moja kwa moja. Sikuzote alitoa mashauri yenye upendo, lakini hakupunguza uzito wa ujumbe wake wa kweli ili awapendeze wale waliomsikiliza. (Yoh. 15:9-12) Kwa mfano, mitume wake walipobishana tena na tena kati yao kuhusu ni nani aliye mkuu zaidi, Yesu aliwasaidia kwa uthabiti lakini kwa subira kuelewa uhitaji wa kuwa wanyenyekevu. (Marko 9:33-37; Luka 9:46-48; 22:24-27; Yoh. 13:14) Vivyo hivyo, ingawa wazee Wakristo leo wanapaswa kutetea uadilifu kwa uthabiti, hawapigi ubwana juu ya kundi la Mungu. (Marko 10:42-44) Wanamwiga Kristo kwa kuwa “wenye fadhili” na “wenye huruma nyororo” wanaposhughulika na wengine.

11. Kuwapenda ndugu zetu kunapaswa kutuchochea kuutumia ulimi wetu kwa njia gani?

11 Tunaweza kuwaeleza ndugu zetu maoni yetu bila kuwaudhi, tukizungumza kwa unyoofu na bila kuwakosea adabu. Kwa kweli, hatutaki kamwe ulimi wetu uwe “umenolewa kama wembe,” na kuutumia kuwaumiza wengine kwa matusi au maneno machafu. (Zab. 52:2; Met. 12:18) Kuwapenda ndugu zetu kutatuchochea ‘kuulinda ulimi wetu na yaliyo mabaya, na midomo yetu isiseme udanganyifu.’ (Zab. 34:13) Katika njia hiyo, tunamheshimu Mungu na kudumisha umoja katika kutaniko.

12. Ni wakati gani mtu anayesema uwongo anastahili kuchukuliwa hatua ya kihukumu? Eleza.

12 Wazee wanajitahidi sana kulilinda kutaniko kutokana na wale wanaosema uwongo wenye kudhuru. (Soma Yakobo 3:14-16.) Uwongo wenye kudhuru unakusudiwa kumuumiza mtu mwingine; unakusudiwa kumfanya mtu huyo ateseke kwa njia fulani au kufadhaika. Kunahusisha mengi zaidi ya kusema mambo madogo ya uwongo au mambo ya kweli yaliyotiwa chumvi. Bila shaka, kusema uwongo wa aina yoyote ni kosa, lakini si kila uwongo unastahili kuchukuliwa hatua ya kihukumu. Hivyo, wazee wanahitaji kuwa na usawaziko na kutumia busara wanapoamua ikiwa mtu aliyesema mambo yasiyo ya kweli ana zoea la kusema kimakusudi uwongo wenye kudhuru na hivyo anastahili kuchukuliwa hatua ya kihukumu. Au je, shauri thabiti la Kimaandiko linalotolewa kwa upendo linatosha?

Sema Kweli Katika Shughuli za Kibiashara

13, 14. (a) Watu fulani wanakosa kuwa wanyoofu jinsi gani kwa wale waliowaajiri kazi? (b) Tunaweza kupata matokeo gani mazuri tukiwa wasema-kweli na wanyoofu kazini?

13 Ukosefu wa unyoofu umeenea sana katika nyakati tunamoishi, kwa hiyo, huenda ikawa vigumu kushinda kishawishi cha kutokuwa mnyoofu kwa mtu aliyetuajiri kazi. Watu wengi wanasema uwongo wa waziwazi wanapotafuta kazi. Kwa mfano, huenda wakatia chumvi habari kuhusu uzoefu au elimu yao ili wapate kazi nzuri zaidi au yenye mshahara mnono zaidi. Kwa upande mwingine, wafanyakazi wengi wanadai kwamba wanafanya kazi lakini wanafanya shughuli zao za kibinafsi, hata ingawa ni kinyume cha sheria za kazi. Huenda wakasoma mambo yasiyohusiana na kazi yao, kupiga simu za kibinafsi, kutuma ujumbe wa kibinafsi kwa simu au kompyuta, au kutumia Intaneti.

14 Ni lazima Wakristo wa kweli wawe wanyoofu na wasema-kweli. (Soma Methali 6:16-19.) Paulo alisema hivi: “Tunataka kujiendesha kwa unyoofu katika mambo yote.” (Ebr. 13:18) Hivyo, Wakristo wanafanya kazi kamili ya siku nzima kupatana na mshahara wanaopokea. (Efe. 6:5-8) Tukiwa wafanyakazi wenye bidii tunaweza pia kumletea sifa Baba yetu wa mbinguni. (1 Pet. 2:12) Kwa mfano, huko Hispania, mtu aliyemwajiri kazi Roberto alimpongeza kwa sababu ya kuwa mfanyakazi mnyoofu na mwenye kutegemeka. Kwa sababu ya mwenendo mzuri wa Roberto, kampuni hiyo iliwapa kazi Mashahidi wengine. Mashahidi hao pia walithibitika kuwa wafanyakazi wenye bidii. Kadiri miaka ilivyopita, Roberto aliwatafutia kazi ndugu 23 waliobatizwa na wanafunzi 8 wa Biblia!

15. Mfanyabiashara Mkristo anapaswa kuonyesha jinsi gani kwamba anasema kweli?

15 Ikiwa sisi ni wafanyabiashara, je, tunasema kweli katika shughuli zetu zote za kibiashara, au nyakati nyingine tunakosa kusema kweli na jirani yetu? Mfanyabiashara Mkristo hapaswi kusema uwongo kuhusu huduma fulani au vitu anavyouza ili vinunuliwe haraka; wala hapaswi kutoa au kukubali hongo. Tunapaswa kuwatendea wengine kama vile ambavyo tungependa sisi wenyewe tutendewe.—Met. 11:1; Luka 6:31.

Sema Kweli Unaposhughulika na Wenye Mamlaka Katika Serikali

16. Wakristo (a) wanawapa nini wenye mamlaka katika serikali? (b) wanampa Yehova nini?

16 Yesu alisema hivi: “Basi, mlipeni Kaisari vitu vya Kaisari, lakini Mungu vitu vya Mungu.” (Mt. 22:21) Kaisari, yaani, wenye mamlaka katika serikali, wanatudai “vitu” gani? Yesu aliposema maneno hayo, alikuwa akizungumza kuhusu kodi. Kwa hiyo, ili kuwa na dhamiri safi mbele za Mungu na wanadamu, Wakristo wanapaswa kutii sheria za nchi, kutia ndani sheria za kulipa kodi. (Rom. 13:5, 6) Lakini tunatambua kwamba Yehova ndiye Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote, Mungu wa pekee wa kweli, ambaye tunapaswa kumpenda kwa moyo, nafsi, akili, na nguvu zetu zote. (Marko 12:30; Ufu. 4:11) Kwa hiyo, tunajitiisha kwa Yehova Mungu bila masharti.—Soma Zaburi 86:11, 12.

17. Watu wa Yehova wana maoni gani kuhusu kupokea misaada ya kijamii?

17 Nchi nyingi zina programu au huduma za kijamii za kuwasaidia wale wanaohitaji msaada wa kimwili. Hakuna kosa lolote kwa Mkristo kupokea msaada kama huo ikiwa anastahili. Ikiwa tunasema kweli na jirani yetu, hatutawapa wenye mamlaka katika serikali habari za uwongo au zenye kupotosha ili tupokee msaada huo.

Baraka Tunazopata kwa Sababu ya Kusema Kweli

18-20. Tunapata baraka gani tunaposema kweli na jirani yetu?

18 Tunapata baraka nyingi tunaposema kweli. Tunakuwa na dhamiri safi, ambayo inatusaidia kuwa na amani ya akili na utulivu wa moyo. (Met. 14:30; Flp. 4:6, 7) Kuwa na dhamiri safi kuna thamani kubwa machoni pa Mungu. Pia, tunaposema kweli katika mambo yote, hatuhitaji kuwa na wasiwasi kwamba tutagunduliwa au kufunuliwa na wanadamu.—1 Tim. 5:24.

19 Fikiria baraka nyingine. Paulo alisema hivi: “Katika kila njia tunajipendekeza kuwa wahudumu wa Mungu, . . . kwa kusema maneno ya kweli.” (2 Kor. 6:4, 7) Ndivyo ilivyokuwa kwa Shahidi mmoja anayeishi Uingereza. Alitaka kuuza gari lake kwa mtu fulani aliyetaka kulinunua, hivyo, alimweleza mambo yote mazuri na kasoro zote za gari hilo, kutia ndani kasoro ambazo hazingeonekana. Baada ya kuliendesha gari hilo ili aone jinsi lilivyo, mtu huyo alimuuliza ndugu huyo ikiwa alikuwa Shahidi wa Yehova. Kwa nini alikata kauli hiyo? Mtu huyo alitambua unyoofu wa ndugu huyo na kuona jinsi alivyokuwa safi. Ndugu huyo alizungumza naye na kumtolea ushahidi mzuri.

20 Je, sisi pia tunamletea sifa Muumba wetu kwa kuwa wanyoofu na kusema kweli sikuzote? Paulo alisema hivi: “Tumeyakataa mambo ya kichinichini ambayo ni ya kuonea aibu, si kutembea kwa ujanja.” (2 Kor. 4:2) Hivyo, acheni tujitahidi kabisa kusema kweli na jirani yetu. Tukifanya hivyo, tutamletea utukufu Baba yetu wa mbinguni na watu wake.

Ungesema Nini?

• Jirani yetu ni nani?

• Kusema kweli na jirani yetu kunamaanisha nini?

• Kusema kweli kunaweza kumletea Mungu utukufu jinsi gani?

• Tunapata baraka gani tunapokuwa wasema-kweli?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 17]

Je, unakiri haraka makosa madogo unayofanya?

[Picha katika ukurasa wa 18]

Je, unasema kweli unapotafuta kazi?