Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ninaweza Kumlipa Yehova Nini?

Ninaweza Kumlipa Yehova Nini?

Ninaweza Kumlipa Yehova Nini?

Limesimuliwa na Ruth Danner

Mama alizoea kusema kwa ucheshi kwamba mwaka wa 1933 ulikuwa mwaka wa misiba: Hitler alianza kutawala, papa aliutangaza mwaka huo kuwa Mwaka Mtakatifu, na nikazaliwa mwaka huohuo.

WAZAZI wangu waliishi katika mji wa Yutz, huko Lorraine, Ufaransa, eneo la kihistoria ambalo linapakana na Ujerumani. Mwaka wa 1921, Baba yangu ambaye ni Mprotestanti, alimwoa Mama, aliyekuwa Mkatoliki mwenye bidii. Dada yangu mkubwa, Helen, alizaliwa mwaka wa 1922, na akiwa mtoto mchanga wazazi wangu walimpeleka kubatizwa katika Kanisa Katoliki.

Siku moja mwaka wa 1925, Baba alipata kitabu The Harp of God (La Harpe de Dieu) cha Kijerumani. Aliposoma kitabu hicho alisadiki kwamba amepata kweli. Aliwaandikia wachapishaji wa kitabu hicho, wakamsaidia kuwapata Mashahidi wa Yehova au Bibelforscher, kama walivyoitwa wakati huo nchini Ujerumani. Mara moja, Baba alianza kuhubiri mambo aliyojifunza. Mama hakufurahia jambo hilo. Alimwambia hivi kwa Kijerumani: “Unaweza kufanya jambo lingine lolote unalotaka, lakini usijiunge na hao Bibelforscher!” Hata hivyo, Baba alikuwa ameamua kuendelea kushirikiana nao, na mwaka wa 1927 alibatizwa na kuwa Shahidi.

Kwa hiyo, nyanya yangu alianza kumchochea Mama atafute talaka na kumwacha Baba. Siku moja wakati wa Misa, kasisi aliwaonya waumini wa kanisa lake “wamwepuke kabisa Danner kwa kuwa ni nabii wa uwongo.” Nyanya yangu aliporudi kutoka katika Misa hiyo, alimwangushia Baba chungu cha ua kutoka ghorofa ya juu ya nyumba yetu. Chungu hicho kizito kilimgonga kwenye bega, karibu tu kimgonge kichwa. Kisa hicho kilimfanya Mama awazie hivi: ‘Dini ambayo inawafanya watu wawe wauaji si dini nzuri.’ Akaanza kusoma vichapo vya Mashahidi wa Yehova. Muda si muda, alisadiki kwamba alikuwa amepata kweli, akabatizwa mwaka wa 1929.

Wazazi wangu walijitahidi sana kunisaidia mimi na dada yangu kumwona Yehova kuwa halisi. Walitusomea hadithi za Biblia na kutuuliza kwa nini watu wanaotajwa katika Biblia walitenda kwa njia fulani. Wakati huo, Baba alikataa kufanya kazi usiku au jioni, hata ingawa uamuzi wake ulifanya apoteze pesa nyingi ambazo angetumia kuitunza familia. Alitaka kupata wakati wa kuhudhuria mikutano ya Kikristo, kushiriki katika huduma, na kujifunza pamoja na watoto wake.

Nyakati Zenye Misukosuko

Wazazi wangu waliwakaribisha kwa ukawaida waangalizi wanaosafiri na Wanabetheli kutoka Uswisi na Ufaransa. Walitueleza kuhusu matatizo ambayo waamini wenzetu walikuwa wakikabili huko Ujerumani, nchi iliyokuwa kilomita chache tu kutoka nyumbani kwetu. Serikali ya Wanazi ilikuwa ikiwahamisha Mashahidi wa Yehova na kuwapeleka katika kambi za mateso, na kuwatenganisha watoto na wazazi wao Mashahidi.

Mimi na Helen tulikuwa tumetayarishwa kukabiliana na hali ngumu ambazo zilikuwa mbele yetu. Wazazi wetu walitusaidia kushika akilini mistari ya Biblia ambayo ingetuongoza. Kwa mfano, walisema hivi: “Ikiwa hamjui jambo la kufanya, fikirieni Methali 3:5, 6. Ikiwa mnaogopa majaribu shuleni, tumieni 1 Wakorintho 10:13. Mkipelekwa mbali nasi, mrudie-rudie akilini Methali 18:10.” Nilijifunza Zaburi 23 na 91 kimoyomoyo na nikawa na hakika kwamba Yehova angenilinda sikuzote.

Mwaka wa 1940, mji wa Alsace-Lorraine ulichukuliwa na Ujerumani ya Wanazi, na serikali hiyo mpya ikawaagiza watu wote wazima wajiunge na chama cha Nazi. Baba alikataa, na askari wa Gestapo wakamtisha kwamba wangemkamata. Mama alipokataa kushona mavazi ya kijeshi, askari wa Gestapo walianza kumtisha pia.

Nilikabili hali ngumu sana shuleni. Kila siku, darasa letu lilianza kwa kutoa sala kwa ajili ya Hitler, kisha tulitoa salamu ya “Heil Hitler,” halafu tuliimba wimbo wa taifa tukiwa tumenyoosha juu mkono wa kulia. Badala ya kunikataza nisitoe salamu ya Hitler, wazazi wangu walinisaidia kuizoeza dhamiri yangu. Kwa hiyo, niliamua mwenyewe kutotoa salamu ya Wanazi. Walimu walinipiga makofi na kunitisha kwamba wangenifukuza shuleni. Pindi moja nilipokuwa na umri wa miaka saba, nililazimishwa kusimama mbele ya walimu wote 12 shuleni. Walijaribu kunilazimisha kutoa salamu ya Hitler. Hata hivyo, nilisimama imara kwa msaada wa Yehova.

Mwalimu mmoja alianza kunishawishi kwa kucheza na hisia zangu. Aliniambia kwamba nilikuwa mwanafunzi mzuri, alinipenda sana, na kwamba angesikitika sana ikiwa ningefukuzwa shuleni. Alisema hivi: “Si lazima uunyooshe juu kabisa mkono wako. Unaweza kuuinua kidogo tu. Na si lazima useme, ‘Heil Hitler!’ Jifanye tu unaongea kwa kufumbua-fumbua mdomo.”

Nilipomwambia Mama mambo ambayo mwalimu huyo alikuwa akiniambia, alinikumbusha simulizi la Biblia la wale vijana watatu Waebrania wakiwa mbele ya sanamu iliyosimamishwa na mfalme wa Babiloni. Akaniuliza hivi: “Walipaswa kufanya nini?” Nikamjibu: “Kuinama.” Akasema: “Ikiwa wakati ambapo walipaswa kuiinamia sanamu hiyo, wangeinama na kufunga kamba za viatu vyao, je, ingekuwa sawa? Uamuzi ni wako; fanya jambo ambalo unafikiri linafaa.” Kama Shadraki, Meshaki, na Abednego, niliamua kubaki mwaminifu kwa Yehova peke yake.—Dan. 3:1, 13-18.

Walimu walinifukuza shuleni mara nyingi na kunitisha kwamba wangenitenganisha na wazazi wangu. Nilikuwa na wasiwasi sana, lakini wazazi wangu waliendelea kunitia moyo. Nilipokuwa nikitoka nyumbani ili kwenda shuleni, Mama alisali pamoja nami, na kumwomba Yehova anilinde. Nilijua kwamba Yehova angenitia nguvu ili nisimame imara kwa ajili ya kweli. (2 Kor. 4:7) Baba aliniambia kwamba ikiwa majaribu yangekuwa makali sana, nisiogope kurudi nyumbani. Alisema hivi: “Tunakupenda. Na sikuzote utakuwa binti yetu. Suala ni kati yako na Yehova.” Maneno hayo yaliitia nguvu tamaa yangu ya kuendelea kuwa mtimilifu.—Ayu. 27:5.

Askari wa Gestapo walikuja nyumbani kwetu mara nyingi ili kutafuta vichapo vya Mashahidi na kuwahoji wazazi wangu. Mara kwa mara, walimchukua Mama kwa saa nyingi na pia walimchukua baba na dada yangu kutoka kazini. Niliporudi kutoka shuleni, sikujua kamwe ikiwa ningemkuta Mama nyumbani. Nyakati nyingine jirani yetu aliniambia hivi: “Wamemchukua mama yako.” Halafu nilijificha ndani ya nyumba na kujiuliza: ‘Je, wanamtesa? Je, kweli nitamwona tena?’

Tunahamishwa

Mnamo Januari 28, 1943 (28/1/1943), askari wa Gestapo walituamsha saa tisa na nusu usiku. Walisema kwamba ikiwa mimi, wazazi wangu na dada yangu tutajiunga na chama cha Nazi, hatutahamishwa. Tulipewa muda wa saa tatu ili tujitayarishe. Mama alikuwa amejitayarisha kwa ajili ya hali hiyo na alikuwa ameweka ndani ya mifuko yetu mavazi ya kubadili na Biblia, hivyo tulitumia muda huo kusali na kutiana moyo. Baba alitukumbusha kwamba ‘hakuna kitu chochote ambacho kingeweza kututenga na upendo wa Mungu.’—Rom. 8:35-39.

Askari wa Gestapo walirudi. Sitamsahau kamwe Dada Anglade aliyezeeka ambaye alitupungia mkono na kutuaga huku akitokwa na machozi. Askari wa Gestapo walitupeleka kwenye kituo cha gari-moshi huko Metz. Baada ya kusafiri kwa siku tatu kwa gari-moshi, tulifika Kochlowice, kambi ndogo iliyokuwa chini ya kambi kubwa ya Auschwitz huko Poland. Baada ya miezi miwili, tulipelekwa Gliwice, makao ya watawa ambayo yalibadilishwa kuwa kambi ya kazi ngumu. Wanazi walituambia kwamba ikiwa kila mmoja wetu angetia sahihi cheti cha kuikana imani yetu, wangetuachilia huru na kuturudishia mali zetu. Baba na Mama walikataa, na askari waliotushika wakasema, “Hamtarudi kamwe nyumbani.”

Mwezi wa 6 tulihamishwa mpaka Swietochlowice, ambako nilianza kupata maumivu ya kichwa ambayo yangali yananisumbua. Vidole vyangu vilipata ugonjwa, na daktari akanifanyia upasuaji wa kung’oa kucha zangu kadhaa bila dawa ya kupunguza maumivu. Jambo moja zuri ni kwamba mara nyingi nilienda kwenye duka la kuoka mikate kwa sababu walinzi walinipa kazi ambazo zilinilazimu kwenda huko. Kwa kawaida, mwanamke fulani aliyefanya kazi katika duka hilo alinipa kitu cha chakula.

Kufikia wakati huo, familia yetu ilitenganishwa na wafungwa wengine. Mnamo Oktoba (Mwezi wa 10) 1943 tulipelekwa kwenye kambi ya Ząbkowice. Tulilala kwenye vitanda vya ghorofa katika chumba cha darini pamoja na watu wengine 60—wanaume, wanawake, na watoto. Askari wa SS walihakikisha kwamba chakula kilikuwa kibaya sana kisicholika kwa urahisi.

Ingawa tulikabili magumu, hatukukata tamaa. Tulikuwa tumesoma katika Mnara wa Mlinzi kuhusu kazi kubwa ya kuhubiri ambayo ingefanywa baada ya vita. Kwa hiyo, tulijua kwa nini tulikuwa tukiteseka na tulijua kwamba baada ya muda mfupi matatizo yetu yangekwisha.

Tuliposikia kwamba Majeshi ya Muungano yalikuwa yakikaribia, tulijua kwamba Wanazi walikuwa wanashindwa vitani. Mwanzoni mwa mwaka wa 1945, askari wa SS waliamua kuiacha kambi yetu. Mnamo Februari (Mwezi wa 2) 19, walitulazimisha kutembea umbali wa kilomita 240 hivi. Baada ya majuma manne hivi, tulifika huko Steinfels, Ujerumani, ambako walinzi waliwaingiza wafungwa wote ndani ya mgodi. Wengi walifikiri kwamba tungeuawa. Lakini siku hiyo Majeshi ya Muungano yalifika, askari wa SS wakakimbia, na matatizo yetu yakaisha.

Kufikia Miradi Yangu

Mnamo Mei 5, 1945 (5/5/1945), baada ya miaka miwili na nusu hivi, tulifika nyumbani kwetu huko Yutz, tukiwa wachafu na tukiwa tumejaa chawa. Hatukuwa tumebadili nguo zetu tangu Februari, kwa hiyo tuliamua kuchoma nguo hizo za zamani. Ninakumbuka mama akituambia hivi: “Acheni hii iwe siku nzuri zaidi ya maisha yenu. Hatuna chochote. Hata nguo ambazo tumevaa si zetu. Hata hivyo, sote wanne tumerudi tukiwa waaminifu. Hatukulegeza msimamo wetu.”

Baada ya kupata matibabu kwa miezi mitatu huko Uswisi, nilirudi shuleni, lakini sikuogopa tena kufukuzwa shuleni. Sasa tuliweza kukutana na ndugu zetu wa kiroho na kuhubiri waziwazi. Mnamo Agosti 28, 1947, nikiwa na umri wa miaka 13, nilionyesha hadharani kwamba nilikuwa nimejiweka wakfu kwa Yehova miaka iliyopita. Baba yangu alinibatiza katika Mto Moselle. Nilitaka kuwa painia papo hapo, lakini Baba akasisitiza kwamba nijifunze kwanza kazi fulani. Kwa hiyo, nilijifunza kushona nguo. Mwaka wa 1951, nikiwa na umri wa miaka 17, niliwekwa rasmi kuwa painia na kutumwa katika mji uliokuwa karibu wa Thionville.

Mwaka huo, nilihudhuria kusanyiko huko Paris na nikajaza fomu ya kuomba utumishi wa umishonari. Sikuwa na umri wa kutosha, lakini Ndugu Nathan Knorr alisema kwamba angeweka fomu yangu “mpaka baadaye.” Katika Juni 1952, nilipokea mwaliko wa kuhudhuria darasa la 21 la Shule ya Gileadi (Watchtower Bible School of Gilead) huko South Lansing, New York, Marekani.

Kuhudhuria Gileadi na Maisha Yangu ya Baadaye

Shule ya Gileadi ilikuwa nzuri kama nini! Mara nyingi nilishindwa hata kuzungumza lugha yangu mbele ya watu. Sasa nililazimika kuzungumza Kiingereza. Hata hivyo, walimu walinisaidia kwa upendo. Ndugu mmoja alinibandika jina Tabasamu ya Ufalme kwa sababu kwa kawaida nilitabasamu nilipokuwa na haya.

Mnamo Julai 19, 1953 (19/7/1953), sherehe yetu ya kuhitimu ilifanyiwa katika Uwanja wa Yankee huko New York, na nilipewa mgawo wa kwenda Paris pamoja na Ida Candusso (baadaye aliitwa Seignobos). Niliogopa sana kuwahubiria wenyeji wa Paris waliokuwa matajiri, lakini nilifaulu kujifunza Biblia pamoja na watu wengi wanyenyekevu. Ida aliolewa kisha akaenda Afrika mwaka wa 1956, lakini mimi niliendelea kukaa Paris.

Mwaka wa 1960, niliolewa na ndugu mmoja wa Betheli, na tukatumika tukiwa mapainia wa pekee huko Chaumont na Vichy. Baada ya miaka mitano, nilipata ugonjwa wa kifua-kikuu na hivyo nikaacha upainia. Nilihisi vibaya sana kwa sababu tangu utotoni nilikuwa na mradi wa kuanza na kudumu katika utumishi wa wakati wote. Baada ya muda fulani, mume wangu aliniacha akachukua mwanamke mwingine. Ndugu na dada zangu wa kiroho walinisaidia katika miaka hiyo migumu sana, naye Yehova aliendelea kubeba mzigo wangu.—Zab. 68:19.

Sasa ninaishi huko Louviers, Normandy, karibu na ofisi ya tawi ya Ufaransa. Ingawa nina matatizo ya afya, ninafurahi kuona jinsi ambavyo Yehova amenisaidia katika maisha yangu. Malezi niliyopata nikiwa mtoto yananisaidia hata leo kuendelea kuwa na mtazamo unaofaa. Wazazi wangu walinifundisha kwamba Yehova ni Mtu halisi ambaye ninaweza kumpenda, kuzungumza naye, na anayejibu sala zangu. Kwa kweli, “nitamlipa Yehova nini kwa ajili ya faida zake zote kwangu?”—Zab. 116:12.

[Blabu katika ukurasa wa 6]

“Ninafurahi kuona jinsi ambavyo Yehova amenisaidia katika maisha yangu”

[Picha katika ukurasa wa 5]

Nikiwa na kifaa cha kuzuia gesi ya sumu nilipokuwa na umri wa miaka sita

[Picha katika ukurasa wa 5]

Nikiwa na wamishonari na mapainia huko Luxembourg kwa ajili ya kampeni ya pekee ya kuhubiri nilipokuwa na umri wa miaka 16

[Picha katika ukurasa wa 5]

Nikiwa na Baba na Mama katika kusanyiko mwaka wa 1953