Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Uwakabidhi Wengine Kazi—Unaweza Kufanya Hivyo Jinsi Gani?

Kwa Nini Uwakabidhi Wengine Kazi—Unaweza Kufanya Hivyo Jinsi Gani?

Kwa Nini Uwakabidhi Wengine Kazi—Unaweza Kufanya Hivyo Jinsi Gani?

YEHOVA alianza kuwakabidhi wengine madaraka au kazi muda mrefu kabla ya Dunia kuumbwa. Alimuumba Mwana wake mzaliwa-pekee kisha akaumba ulimwengu wote akimtumia Mwana huyo akiwa “stadi wa kazi.” (Met. 8:22, 23, 30; Yoh. 1:3) Mungu alipowaumba wenzi wawili wa kwanza, aliwaambia ‘wajaze dunia na kuitiisha.’ (Mwa. 1:28) Muumba aliwapa wanadamu kazi ya kupanua Paradiso ya Edeni mpaka ijaze dunia yote. Ndiyo, tangu mwanzo, tengenezo la Yehova limekuwa likiwakabidhi wengine kazi.

Kuwakabidhi wengine kazi kunatia ndani nini? Kwa nini wazee Wakristo wanapaswa kujifunza kuwakabidhi wengine kazi fulani kutanikoni, na wanaweza kufanya hivyo jinsi gani?

Kuwakabidhi Wengine Kazi Kunamaanisha Nini?

Neno “kabidhi” linamaanisha “kumpa mtu kazi; kumchagua mtu kuwa mwakilishi wako; kumpa madaraka au mamlaka.” Kwa hiyo, ili uwakabidhi wengine kazi unapaswa kuwahusisha katika kutimiza miradi fulani. Na hivyo ni lazima uwagawie mamlaka.

Wale wanaopewa kazi fulani katika kutaniko la Kikristo wanatazamiwa kutimiza mgawo waliopewa, kueleza jinsi wanavyotimiza mgawo huo, na kwa kawaida wanatazamiwa kuwasiliana na yule aliyewapa kazi hiyo. Hata hivyo, yule aliye na daraka la msingi la kuhakikisha kwamba kazi hiyo imefanywa ni ndugu aliyewakabidhi kazi hiyo. Anahitaji kuhakikisha kwamba kazi hiyo inafanywa ipasavyo na kutoa mashauri yanayohitajiwa. Lakini huenda wengine wakauliza, ‘Kwa nini uwakabidhi wengine kazi ikiwa unaweza kuifanya mwenyewe?’

Kwa Nini Uwakabidhi Wengine Kazi?

Fikiria jinsi Yehova alivyomuumba Mwana wake mzaliwa-pekee na kushiriki naye katika kazi iliyobaki ya uumbaji. Ndiyo, “kwa njia yake vitu vingine vyote viliumbwa mbinguni na duniani, vitu vinavyoonekana na vitu visivyoonekana.” (Kol. 1:16) Muumba angefanya kazi yote peke yake, lakini alitaka Mwana wake apate pia shangwe iliyotokana na kutimiza kazi hiyo nzuri. (Met. 8:31) Hilo lilimsaidia Mwana wake kujifunza mengi zaidi kuhusu sifa za Mungu. Kwa njia fulani, Baba alitumia nafasi hiyo kumzoeza Mwana wake mzaliwa-pekee.

Yesu Kristo alipokuwa duniani alimwiga Baba yake kwa kuwakabidhi wengine kazi. Aliwazoeza wanafunzi wake hatua kwa hatua. Aliwatuma mitume 12 na baadaye wanafunzi wengine 70 ili wamtangulie na kuongoza katika kazi ya kuhubiri. (Luka 9:1-6; 10:1-7) Yesu alipotembelea maeneo hayo baadaye, walikuwa wameweka msingi mzuri ambao angejenga juu yake. Alipoondoka duniani, Yesu aliwakabidhi wanafunzi wake waliozoezwa madaraka mazito zaidi, kutia ndani kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote.—Mt. 24:45-47; Mdo. 1:8.

Kutaniko la Kikristo lilikuwa na desturi ya kuwazoeza na kuwakabidhi wengine kazi. Mtume Paulo alimwambia Timotheo hivi: “Mambo hayo uwakabidhi watu waaminifu, ambao nao watakuwa na sifa za kustahili vya kutosha kufundisha wengine.” (2 Tim. 2:2) Ndiyo, watu wenye uzoefu wanapaswa kuwazoeza wale ambao pia watawazoeza wengine.

Mzee anapowakabidhi wengine kazi aliyogawiwa, anaweza kushiriki na wengine shangwe ya kufundisha na kufanya uchungaji. Kutambua kwamba uwezo wa wanadamu una mipaka, kunapaswa kuwachochea hata zaidi wazee wawaombe wengine wawasaidie kutimiza madaraka kutanikoni. Biblia inasema: “Wenye kiasi wana hekima.” (Met. 11:2) Mtu mwenye kiasi anatambua kwamba hawezi kufanya kila kitu. Ukijaribu kufanya kila kitu peke yako, huenda ukajichosha na kuinyima familia yako wakati ambao wanapaswa kuwa na wewe. Kwa hiyo, ni jambo la hekima kuwakabidhi wengine kazi au madaraka. Kwa mfano, mfikirie ndugu anayetumika akiwa mratibu wa baraza la wazee. Anaweza kuwaomba wazee wengine wakague hesabu za kutaniko. Wazee hao wanapokagua rekodi hizo wanaweza kuelewa hali ya kifedha ya kutaniko.

Kuwakabidhi wengine kazi kunawapa nafasi ya kupata ustadi na uzoefu wanaohitaji, na pia yule anayewakabidhi wengine kazi anapata nafasi ya kuona uwezo wa wale ambao wamepewa kazi hiyo. Hivyo, kwa kuwakabidhi watumishi wa huduma wanaofikia pendeleo la kuwa wazee kazi fulani za kutaniko, wazee wanaweza kuwajaribu na kuona ‘ikiwa wanafaa.’—1 Tim. 3:10.

Mwishowe, wazee wanapowakabidhi wengine kazi wanaonyesha kwamba wanawaamini. Paulo alienda na Timotheo katika utumishi wa umishonari ili kumzoeza. Uhusiano wa karibu ulisitawi kati ya wanaume hao wawili. Paulo alimwita Timotheo ‘mtoto wake kwelikweli katika imani.’ (1 Tim. 1:2) Vivyo hivyo, Yehova na Yesu walisitawisha uhusiano wa karibu sana walipofanya pamoja kazi ya kuumba vitu vingine vyote. Wazee wanapowakabidhi wengine kazi, wanaweza kusitawisha uhusiano wa karibu sana pamoja nao.

Kwa Nini Wazee Fulani Wanasita Kuwakabidhi Wengine Kazi?

Ingawa wazee fulani wanajua faida za kuwakabidhi wengine kazi, wanaona vigumu kufanya hivyo, labda kwa sababu wanahisi kwamba watapoteza mamlaka yao. Huenda wakafikiri kwamba ni lazima sikuzote waongoze mambo wao wenyewe. Hata hivyo, kumbuka kwamba kabla ya kupanda mbinguni, Yesu aliwapa wanafunzi wake mamlaka ya kutimiza mgawo mzito, huku akijua kwamba wangetimiza kazi kubwa kuliko alizotimiza!—Mt. 28:19, 20; Yoh. 14:12.

Labda wazee fulani waliwakabidhi wengine kazi wakati uliopita lakini hawakupata matokeo mazuri. Huenda wakahisi kwamba wao wenyewe wanaweza kufanya kazi hiyo vizuri zaidi na haraka zaidi. Hata hivyo, fikiria mfano wa Paulo. Alijua faida za kuwakabidhi wengine kazi, lakini pia alitambua kwamba wale wanaozoezwa hawawezi sikuzote kutimiza kazi hizo kama inavyotazamiwa. Katika safari yake ya kwanza ya umishonari, Paulo alimzoeza Marko, kijana aliyesafiri pamoja naye. Paulo alivunjika moyo sana wakati Marko alipoacha mgawo wake na kurudi nyumbani. (Mdo. 13:13; 15:37, 38) Hata hivyo, jambo hilo halikumzuia Paulo asiwazoeze wengine. Kama ilivyotajwa mapema, alimwalika kijana Mkristo Timotheo asafiri pamoja naye. Timotheo alipokuwa tayari kubeba madaraka mazito zaidi, Paulo alimwacha Efeso, na kumpa mamlaka ya kuwaweka rasmi waangalizi wa kutaniko na watumishi wa huduma.—1 Tim. 1:3; 3:1-10, 12, 13; 5:22.

Vivyo hivyo leo, wazee hawapaswi kuacha kuwazoeza akina ndugu eti kwa sababu tu ndugu mmoja hafanyi vizuri. Ni jambo la hekima na la maana kujifunza kuwaamini wengine na kuwazoeza. Lakini ni mambo gani ambayo wazee wanapaswa kukumbuka wanapowakabidhi wengine kazi?

Jinsi ya Kuwakabidhi Wengine Kazi

Unapowakabidhi akina ndugu kazi, fikiria uwezo wa ndugu ambao unataka kuwakabidhi kazi. Kulipokuwa na uhitaji wa kushughulikia ugawaji wa kila siku wa chakula huko Yerusalemu, mitume waliwachagua ‘wanaume saba waliothibitishwa, wenye kujaa roho na hekima.’ (Mdo. 6:3) Ukimwomba mtu asiyetegemeka afanye kazi fulani, huenda akashindwa kuifanya. Kwa hiyo, mpe kazi ndogondogo kwanza. Mtu anapojithibitisha kuwa mwaminifu, anaweza kushughulikia madaraka zaidi.

Hata hivyo, mambo mengi yanahusika. Watu wana nyutu na uwezo tofauti-tofauti. Watu wana viwango mbalimbali vya uzoefu. Ndugu mwenye urafiki na mchangamfu anaweza kuwa mkaribishaji mzuri, naye ndugu anayefanya mambo kwa utaratibu na mpangilio mzuri anaweza kuwa msaidizi mzuri sana wa mwandishi wa kutaniko. Dada aliye na uwezo wa kurembesha vitu mbalimbali anaweza kukabidhiwa kazi ya kupanga maua wakati wa Ukumbusho.

Unapogawa kazi, eleza waziwazi jinsi kazi hiyo inavyopaswa kutimizwa. Kabla ya Yohana Mbatizaji kuwatuma wajumbe kwa Yesu, aliwaeleza mambo ambayo alitaka kujua na swali ambalo wangeuliza. (Luka 7:18-20) Kwa upande mwingine, Yesu alipowaagiza wanafunzi wake wakusanye masalio ya chakula kilichoandaliwa kimuujiza, aliwaambia mambo hususa ya kufanya. (Yoh. 6:12, 13) Kuwakabidhi wengine kazi kunategemea hasa kazi yenyewe na uwezo wa yule anayesaidia. Yule anayemkabidhi mwingine kazi na yule anayeombwa afanye kazi hiyo wanapaswa kuelewa jinsi kazi hiyo inavyopaswa kufanywa na ripoti kuhusu kazi hiyo zinapaswa kutolewa mara ngapi. Wote wawili wanapaswa kujua yule anayefanya kazi hiyo ana uhuru wa kutumia busara katika mambo gani. Ikiwa kazi hiyo inapaswa kukamilishwa kufikia tarehe fulani, itakuwa vizuri zaidi ikiwa watazungumzia tarehe ya kumaliza kazi hiyo na kukubaliana badala tu ya kuamuru kazi hiyo imalizwe tarehe fulani.

Mtu anayekabidhiwa kazi fulani anapaswa kupewa pesa, vifaa, na msaada anaohitaji. Huenda likawa jambo linalofaa kuwajulisha wengine mpango huo. Yesu alipomkabidhi Petro “funguo za ufalme wa mbinguni,” alimpa mbele ya wanafunzi wengine. (Mt. 16:13-19) Vivyo hivyo, katika hali fulani huenda ikawa vizuri kulitangazia kutaniko ni nani aliye na daraka la kufanya kazi fulani.

Ni vizuri pia kuwa mwangalifu. Ikiwa utaendelea kufanya kazi ambayo umemkabidhi mtu mwingine, ni kana kwamba unamwambia, “Sikuamini sana.” Ni kweli kwamba nyakati nyingine huenda kazi isifanywe kama ulivyotazamia. Hata hivyo, ikiwa ndugu ambaye amekabidhiwa daraka fulani anapewa kiasi fulani cha uhuru, inaelekea kwamba atapata ujasiri na uzoefu. Bila shaka, hilo halimaanishi kwamba hupaswi kuangalia jinsi anavyofanya kazi uliyompa. Hata ingawa Yehova alimkabidhi Mwana wake daraka fulani katika kazi ya uumbaji, bado Yehova mwenyewe alishiriki katika kazi hiyo. Alimwambia hivi Stadi huyo wa Kazi: “Na tufanye mtu kwa mfano wetu.” (Mwa. 1:26) Kwa hiyo, kwa maneno na matendo yako, unga mkono kazi inayofanywa na umpongeze mtu huyo kwa jitihada zake. Kuzungumza naye kwa ufupi kuhusu matokeo ya kazi anayofanya kunaweza kumsaidia. Ikiwa kazi hiyo haifanywi kwa njia inayofaa, usisite kutoa mashauri au msaada zaidi. Kumbuka kwamba unapomkabidhi mtu kazi wewe ndiye utakayetoa hesabu ya matokeo ya kazi hiyo.—Luka 12:48.

Wengi wamefaidika kwa sababu ya kukabidhiwa kazi kutanikoni na wazee ambao walipendezwa nao kutoka moyoni. Kwa kweli, wazee wote wanahitaji kujifunza sababu za kuwakabidhi wengine kazi na jinsi ya kufanya hivyo kwa kumwiga Yehova.

[Sanduku katika ukurasa wa 29]

KUWAKABIDHI WENGINE KAZI NI

• njia ya kuwafanya wengine wapate shangwe inayotokana na kutimiza kazi fulani

• njia ya kutimiza mengi zaidi

• uthibitisho wa kwamba mtu ana hekima na kiasi

• njia ya kuwazoeza wengine

• njia ya kuonyesha kwamba unawaamini wengine

[Sanduku katika ukurasa wa 30]

JINSI YA KUWAKABIDHI WENGINE KAZI

• Chagua watu ambao wanaweza kufanya kazi hiyo

• Eleza waziwazi kuhusu kazi hiyo/zungumza nao

• Fafanua jambo linalopaswa kutimizwa

• Wape vifaa wanavyohitaji

• Onyesha kwamba unapendezwa na kazi hiyo, na kwamba unawaamini

• Uwe tayari kutoa hesabu ya matokeo ya kazi hiyo

[Picha katika ukurasa wa 31]

Kuwakabidhi wengine kazi kunatia ndani kuwapa kazi na kuangalia jinsi wanavyoitimiza