Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Yesu alihubiri katika nchi yote ya Israeli. Basi kwa nini mtume Petro alisema kwamba Wayahudi na watawala wao ‘walitenda kwa kutojua’ walipoamuru Yesu auawe?—Mdo. 3:17.

Alipokuwa akihutubia kikundi cha Wayahudi kuhusu sehemu waliyotimiza katika kifo cha Masihi, mtume Petro alisema hivi: “Ninajua kwamba mlitenda kwa kutojua, kama vile watawala wenu pia walivyotenda.” (Mdo. 3:14-17) Huenda Wayahudi fulani hawakumwelewa Yesu na mafundisho yake. Lakini sababu zilizowafanya wengine watende kwa kutojua zilitia ndani kutokuwa na tamaa ya kumpendeza Mungu, ubaguzi, wivu, na chuki ya waziwazi.

Fikiria jinsi kutokuwa na tamaa ya kumpendeza Yehova kulivyowafanya wengi wawe na maoni mabaya kuhusu mafundisho ya Yesu. Mara nyingi Yesu alitumia mifano alipofundisha, na aliwafafanulia wote waliotaka kujifunza mengi zaidi. Hata hivyo, wengine wao walienda zao tu na hawakujitahidi hata kidogo kuelewa mifano hiyo. Pindi moja, hata wanafunzi fulani waliudhika kwa sababu ya lugha ya mfano ambayo Yesu alitumia. (Yoh. 6:52-66) Watu hao hawakutambua kwamba mifano ya Yesu ilifunua ikiwa walikuwa tayari kubadili maoni yao na matendo yao. (Isa. 6:9, 10; 44:18; Mt. 13:10-15) Pia, walipuuza unabii fulani uliosema kwamba Masihi angetumia mifano katika mafundisho yake.—Zab. 78:2.

Wengine walikataa mafundisho ya Yesu kwa sababu ya ubaguzi. Alipofundisha katika sinagogi la mji wao wa nyumbani, Nazareti, watu ‘walistaajabu.’ Lakini badala ya kumkubali Yesu kuwa Masihi, waliuliza maswali kuhusu malezi yake: “Mtu huyu alipata wapi mambo haya? . . . Je, huyu si yule seremala mwana wa Maria na ndugu ya Yakobo na Yosefu na Yuda na Simoni? Na dada zake wapo hapa pamoja nasi, sivyo?” (Marko 6:1-3) Watu wa Nazareti waliona mafundisho ya Yesu kuwa yasiyo ya maana kwa sababu alizaliwa katika familia maskini.

Namna gani viongozi wa kidini? Wengi wao hawakumsikiliza Yesu kwa makini kwa sababu kama hizo. (Yoh. 7:47-52) Walikataa pia mafundisho yake kwa sababu walimwonea wivu Yesu, ambaye alikuwa akiwavutia watu. (Marko 15:10) Na bila shaka watu wengi maarufu walikasirika sana alipowashutumu kwa sababu ya unafiki na udanganyifu wao. (Mt. 23:13-36) Yesu aliwashutumu kwa sababu ya hali yao ya kutojua ambayo walijiletea wenyewe. Alisema hivi: “Ole wenu ninyi wenye ujuzi mwingi wa Sheria, kwa sababu mliuondoa ufunguo wa ujuzi; ninyi wenyewe hamkuingia [katika Ufalme], na wale wanaoingia mliwazuia!”—Luka 11:37-52.

Kwa miaka mitatu na nusu, Yesu alihubiri habari njema katika nchi. Pia, aliwazoeza wengine wengi kufanya kazi hiyo. (Luka 9:1, 2; 10:1, 16, 17) Yesu na wanafunzi wake walipata matokeo mengi mazuri hivi kwamba Mafarisayo walilalamika hivi: “Oneni! Ulimwengu umemfuata.” (Yoh. 12:19) Kwa hiyo, si kwamba Wayahudi wengi hawakujua chochote kumhusu Yesu. Hata hivyo, wengi wao ‘hawakujua’ kuwa Yesu ni Masihi. Wangeongeza ujuzi wao na upendo wao kwa Masihi, lakini hawakufanya hivyo. Wengine wao walishiriki katika kumuua Yesu. Hivyo, mtume Petro aliwahimiza hivi wengi wao: “Kwa hiyo, tubuni na mgeuke ili dhambi zenu zipate kufutwa, ili majira ya kuburudisha yapate kuja kutoka kwa uso wa Yehova na kwamba apate kumtuma Kristo aliyewekwa rasmi kwa ajili yenu, Yesu.” (Mdo. 3:19, 20) Inapendeza kuona kwamba maelfu ya Wayahudi walianza kusikiliza, kutia ndani “umati mkubwa wa makuhani.” Hawakutenda tena kwa kutojua. Badala yake, walitubu na kupata kibali cha Yehova.—Mdo. 2:41; 4:4; 5:14; 6:7.