Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

1. Mwombe Mtungaji wa Biblia Akusaidie

1. Mwombe Mtungaji wa Biblia Akusaidie

Jinsi Unavyoweza Kuielewa Biblia

1. Mwombe Mtungaji wa Biblia Akusaidie

“Kuna wakati ambapo nilikuwa nikisoma Biblia usiku kabla ya kulala,” anasema Ninfa, anayeishi huko Italia. “Nilifanya hivyo kwa kuwa nilitambua kwamba ni Neno la Mungu, na hata ingawa sikufurahia kuisoma, nilitaka kujua mambo ambayo Mungu aliandika katika Biblia. Nilitaka kuisoma Biblia nzima. Mwanzoni niliona ni jambo rahisi, lakini nilipofika kwenye sehemu ngumu, nikaacha kuisoma.”

JE, WEWE pia una maoni kama ya Ninfa? Watu wengi wana maoni kama hayo. Ingawa hivyo, kama tulivyoona katika habari iliyotangulia, Mtungaji wa Biblia, Yehova Mungu, anataka ulielewe Neno lake. Lakini, unaweza kupata uelewaji huo jinsi gani? Hatua ya kwanza ni kumwomba Mtungaji wa Biblia akusaidie.

Mitume wa Yesu walionwa kuwa “watu wasio na elimu na wa kawaida tu” kwa sababu hawakuwa wamehudhuria shule za kirabi ili wapate elimu ya kidini. (Matendo 4:13) Hata hivyo, Yesu aliwahakikishia kwamba wangeweza kuelewa Neno la Mungu. Jinsi gani? Yesu alieleza hivi: “Msaidizi, roho takatifu, ambayo Baba atatuma katika jina langu, hiyo itawafundisha ninyi mambo yote.” (Yohana 14:26) Mungu alitumia roho hiyo takatifu, au nguvu za utendaji, kuumba dunia na uhai wote uliomo. (Mwanzo 1:2) Pia, aliitumia kuwaongoza waandikaji 40 hivi ili waandike mawazo yake katika Biblia. (2 Petro 1:20, 21) Roho hiyohiyo inaweza kuwasaidia watu wanaotaka kuielewa Biblia.

Unaweza kuipokea roho takatifu ya Mungu jinsi gani? Ni lazima uombe kwa imani ili Mungu akupe roho takatifu. Kwa kweli, huenda ukahitaji kuendelea kuomba ili upewe roho hiyo. “Endeleeni kuomba, nanyi mtapewa,” akasema Yesu. “Ikiwa ninyi . . . mnajua jinsi ya kuwapa watoto wenu zawadi zilizo njema, je, Baba aliye mbinguni hatawapa hata zaidi roho takatifu wale wanaomwomba!” (Luka 11:9, 13) Yehova yuko tayari kuwapa kwa ukarimu roho takatifu wale wanaomwomba kwa unyoofu. Nguvu hizo za utendaji zinaweza kukusaidia kuelewa maneno yaliyoongozwa kwa roho ambayo yaliandikwa katika Biblia maelfu ya miaka iliyopita. Pia, roho ya Mungu inaweza kukupa hekima inayohitajika ili uishi kupatana na ujumbe wenye nguvu ulio katika Biblia.—Waebrania 4:12; Yakobo 1:5, 6.

Hivyo basi, kila mara kabla hujaanza kusoma Biblia, sali kwa Mungu na umwombe akupe roho takatifu ili ikusaidie kulielewa Neno lake.