Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

2. Soma Ukiwa na Maoni Mazuri

2. Soma Ukiwa na Maoni Mazuri

Jinsi Unavyoweza Kuielewa Biblia

2. Soma Ukiwa na Maoni Mazuri

Je, rafiki yako amewahi kukuambia mambo mabaya kumhusu mtu fulani ambaye hujawahi kukutana naye? Baadaye ulipokutana na mtu huyo, je, mambo ambayo ulikuwa umeambiwa na rafiki yako kumhusu yalikufanya usione vipawa na sifa zake nzuri? Inaweza kuwa hivyo pia kuhusu Biblia.

MTUME Paulo alitoa onyo kuhusu jambo linaloweza kutukia ikiwa tutasoma Biblia tukiwa na maoni yasiyofaa. Paulo aliandika hivi kuhusu Wayahudi fulani wa nyakati zake: “Nawatolea ushahidi kwamba wana bidii kwa ajili ya Mungu; lakini si kulingana na ujuzi sahihi.”—Waroma 10:2.

Wayahudi hao wa karne ya kwanza hawakuwa tayari kukubali ukweli fulani ambao ulifunuliwa waziwazi na Maandiko ya Kiebrania, yaani, utambulisho wa Masihi. Yesu wa Nazareti alitimiza kila takwa la Kimaandiko na alitimiza kila unabii uliomhusu Masihi. Hata hivyo, maoni yasiyofaa ambayo Wayahudi walikuwa wameshikilia yaliwazuia wengi wao wasielewe Neno la Mungu.

Tunaweza kujifunza nini kutokana na simulizi hilo la Biblia? Ni jambo la maana kuisoma Biblia tukiwa na maoni mazuri. Maoni yasiyofaa yanaweza kumzuia msomaji asielewe ukweli ulio katika Biblia.

Kwa mfano, profesa wa mambo ya kidini huko North Carolina, Marekani, anafafanua Biblia kuwa “kitabu ambacho kimejaa mawazo ya wanadamu na mengi ya mawazo hayo yanapingana na hayawezi kutupa mwongozo wenye kutegemeka maishani.” Ikiwa mtu angesoma Biblia akiwa na maoni ya kwamba ni “kitabu ambacho kimejaa mawazo ya wanadamu,” je, hatakuwa na mwelekeo wa kupuuza mwongozo au kanuni ambazo hapendi?

Kinyume cha hilo, Biblia inatutia moyo tuisome kwa bidii. Maandiko yanasema hivi kuhusu Waberoya ambao waliishi katika siku za Paulo: “Walilipokea neno kwa hamu kubwa zaidi ya akili, wakiyachunguza Maandiko kwa uangalifu kila siku ili kuona kama mambo hayo ndivyo yalivyo.” (Matendo 17:11) Kama wasomaji hao Waberoya, huenda ukahitaji kusoma Biblia ukiwa na maoni mazuri, na kuepuka maoni yoyote yasiyofaa ambayo yanaweza kukuzuia usiielewe. Soma Neno la Mungu ukiwa na maoni mazuri, na pia ukiwa na hamu ya kuelewa ujumbe wenye kusisimua kutoka kwa Mtungaji wake.