Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Kwa nini vazi la ndani la Yesu liliwavutia sana askari-jeshi Waroma?

Askari-jeshi wanne waliosimamia kuuawa kwa Yesu waligawana mavazi yake. Andiko la Yohana 19:23 linasema hivi: “Lakini lile vazi la ndani [la Yesu] lilikuwa halina mshono, likiwa limefumwa kutoka juu mpaka urefu wake wote.” Askari-jeshi hao waliamua kwamba hawangelirarua vazi hilo, lakini wangepiga kura ili mmoja wao abaki nalo. Vazi kama hilo lilifumwa jinsi gani?

Inaelekea kwamba vazi hilo la ndani lilikuwa koti refu lisilo na mikono linalofanana na shati ambalo lilifika kwenye magoti au kwenye viwiko vya mguu na lilifumwa kutokana na kitani au sufu. Kwa kawaida mavazi hayo yalitengenezwa kwa kuunganisha pamoja vitambaa viwili vyenye umbo la mraba au mstatili, na kuvishona kwenye miisho yake mitatu. Mashimo yaliachwa kwa ajili ya kichwa na mikono.

Aina fulani ya koti refu lisilo na mikono lenye thamani ya juu zaidi lilitengenezwa kwa njia hiyohiyo lakini kwa kutumia “kitambaa kimoja tu kirefu, kilichokunjwa mara mbili, kikiwa kimetobolewa shimo katikati kwa ajili ya kichwa,” pia kilikuwa kimeshonwa kwenye pindo, kinasema kitabu kimoja (Jesus and His World). Koti refu kama hilo lilihitaji kushonwa kandokando.

Mavazi ambayo hayakuwa na mshono wowote, kama lile ambalo Yesu alivaa, yalipatikana Palestina tu. Yalifumwa kwa kitanda cha mfumi kilichotumia nyuzi mbili za mtande zilizo wima, uzi mmoja ulikuwa mbele na uzi wa pili ulikuwa upande wa nyuma wa ubao wa mfumi. Uzi wa kufuma uliolala ulishikiliwa na kipisha-uzi, na mfumaji alisukuma kipisha-uzi hicho kutoka nyuma ya kitanda cha mfumi kwenda mbele, “na kwa kufanya hivyo alifuma kitambaa chenye umbo la bomba,” kinasema kitabu kimoja. Inaelekea kwamba haikuwa rahisi kupata koti lililofumwa bila mshono, kwa hiyo kila askari-jeshi alitamani koti hilo.

Je, kulikuwa na wafugaji wa nyuki katika Israeli la kale?

Kulingana na Maandiko ya Kiebrania, Mungu alikuwa ameahidi kwamba angewaleta Waisraeli wa kale katika “nchi inayotiririka maziwa na asali.” (Kutoka 3:8) Inaonekana kwamba mara nyingi Maandiko yanapotaja asali, yanarejelea chakula kinachotokezwa na nyuki wa mwituni. Biblia haitaji kuhusu ufugaji wa nyuki katika Israeli la kale. Hata hivyo, kulingana na uvumbuzi ambao umefanywa hivi karibuni katika Bonde la Bet She’an huko Israel, inaonekana kwamba siku za kale wakaaji wa eneo hilo “walijishughulisha na ufugaji wa nyuki kwa kiwango kikubwa.”

Huko Tel Rehov, watafiti wa Chuo Kikuu kimoja (Hebrew University of Jerusalem’s Institute of Archaeology) wamefukua eneo lililokuwa na mizinga ambalo linakadiriwa kwamba lilikuwapo kati ya karne ya kumi na mwanzoni mwa karne ya tisa K.W.K. ambacho ni kipindi cha kale sana katika ufalme wa Israeli. Hii ndiyo mara ya kwanza kwa mizinga ya kale kupatikana huko Mashariki ya Kati. Inakadiriwa kwamba eneo hilo la kufuga nyuki lilikuwa na mizinga 100 hivi ya nyuki iliyokuwa imepangwa katika safu na angalau katika matabaka matatu kwenda juu.

Kulingana na ripoti ya chuo hicho, kila mzinga wa nyuki ulikuwa “silinda iliyotengenezwa kwa udongo . . . yenye urefu wa karibu sentimita 80 [inchi 30] na kipenyo cha karibu sentimita 40 [inchi 15]. . . . Wafugaji stadi wa nyuki na wasomi ambao walitembelea eneo hilo walikadiria kwamba asali yenye uzito wa karibu nusu tani ingeweza kukusanywa kila mwaka kutoka kwenye mizinga hiyo.”

[Picha katika ukurasa wa 22]

Eneo Hilo Huko Tel Rehov

[Hisani]

Institute of Archaeology/Hebrew University © Tel Rehov Excavations