Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mwige Yesu—Fundisha Kwa Upendo

Mwige Yesu—Fundisha Kwa Upendo

Mwige Yesu—Fundisha Kwa Upendo

“Mtu mwingine hajapata kamwe kusema kama huyu.”—YOH. 7:46.

1. Watu walihisi jinsi gani kuhusu njia ya Yesu ya kufundisha?

HEBU wazia jinsi ilivyosisimua kumsikiliza Yesu akifundisha! Biblia inatuonyesha jinsi mafundisho ya Yesu yalivyowagusa moyo watu waliomsikiliza. Kwa mfano, Luka, mwandikaji wa Injili, akizungumza kumhusu Yesu, anasema kwamba watu wa Nazareti ‘walianza kustaajabia maneno yenye kuvutia sana yaliyokuwa yakitoka kinywani mwake.’ Mathayo anaripoti kwamba wale waliomsikiliza Yesu akifundisha katika Mahubiri ya Mlimani ‘walishangazwa na njia yake ya kufundisha.’ Naye Yohana anasema kwamba maofisa waliotumwa kumkamata Yesu walirudi mikono mitupu, wakisema: “Mtu mwingine hajapata kamwe kusema kama huyu.”—Luka 4:22; Mt. 7:28; Yoh. 7:46.

2. Yesu alitumia njia gani za kufundisha?

2 Maofisa hao hawakukosea. Hapana shaka kwamba Yesu alikuwa Mwalimu mkuu zaidi aliyepata kuishi. Alifundisha kwa njia rahisi na yenye kueleweka, na sababu alizotoa hazingeweza kupingwa. Alitumia kwa ustadi sana maswali na mifano. Alibadili njia yake ya kufundisha ikitegemea wale waliomsikiliza, iwe walikuwa watu mashuhuri au watu wa kawaida. Kweli alizofundisha zilieleweka kwa urahisi lakini zilikuwa na ujumbe mzito. Hata hivyo, si mambo hayo tu yaliyomfanya Yesu awe Mwalimu mkuu.

Sifa Kuu Zaidi Ni Upendo

3. Akiwa mwalimu, Yesu alikuwa tofauti jinsi gani na viongozi wa kidini wa siku zake?

3 Bila shaka, miongoni mwa waandishi na Mafarisayo kulikuwa na watu wenye akili ambao walikuwa na ujuzi na ustadi wa kufundisha. Kwa nini njia ya Yesu ya kufundisha ilikuwa tofauti sana na ya watu hao? Viongozi hao wa kidini hawakuwapenda watu wa kawaida. Badala yake, waliwadharau na kuwaona kuwa “watu waliolaaniwa.” (Yoh. 7:49) Tofauti na viongozi hao, Yesu aliwasikitikia watu, kwa kuwa walikuwa “wamechunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji.” (Mt. 9:36) Aliwatendea kwa upendo, huruma na fadhili. Zaidi ya hayo, viongozi wa kidini hawakumpenda Mungu kikweli. (Yoh. 5:42) Hata hivyo, Yesu alimpenda Baba yake na alifurahia kufanya mapenzi yake. Viongozi wa kidini waliyapotosha maneno ya Mungu kwa faida yao wenyewe, lakini Yesu alilipenda “neno la Mungu.” Alifundisha, alifafanua, alitetea, na kuishi kupatana na neno la Mungu. (Luka 11:28) Ndiyo, upendo ulikuwa sehemu ya utu wa Kristo, ulimwongoza katika mafundisho yake, katika njia aliyoshughulika na watu, na jinsi alivyowafundisha.

4, 5. (a) Kwa nini ni jambo la maana kufundisha kwa upendo? (b) Kwa nini ujuzi na ustadi ni mambo ya maana pia katika kufundisha?

4 Namna gani sisi? Tukiwa wafuasi wa Kristo, tunatamani kumwiga katika huduma yetu na katika maisha yetu. (1 Pet. 2:21) Hivyo, kusudi letu si kuwafundisha watu kuijua Biblia tu bali pia kuonyesha sifa za Yehova, hasa upendo wake. Iwe tunajua mengi au machache, iwe tuna ustadi mwingi wa kufundisha au hapana, upendo ambao tunaonyesha utagusa sana mioyo ya watu tunaowahubiria. Ili tupate matokeo mazuri zaidi katika kazi yetu ya kufanya wanafunzi, ni lazima tumwige Yesu kwa kufundisha kwa upendo.

5 Bila shaka, ili tuwe walimu wazuri, tunahitaji kuwa na ujuzi kuhusu habari tunayofundisha na pia ustadi au ufundi wa kufundisha habari hiyo. Yesu aliwasaidia wanafunzi wake kupata ujuzi na ustadi, na Yehova anatusaidia leo kupitia tengenezo lake kupata ujuzi na ustadi huo. (Soma Isaya 54:13; Luka 12:42.) Hata hivyo, tunapaswa kuwa na mradi wa kufundisha si kwa kutumia akili zetu tu bali pia mioyo yetu. Tukiwa na ujuzi, ustadi, na pia upendo, tunaweza kupata matokeo yenye kuridhisha sana. Kwa hiyo basi, ni katika njia gani tunaweza kuonyesha upendo tunapofundisha? Yesu na wanafunzi wake walifanya hivyo jinsi gani? Acheni tuone.

Ni Lazima Tumpende Yehova

6. Tunazungumza kwa njia gani kuhusu mtu tunayempenda?

6 Tunafurahia kuzungumza kuhusu mambo tunayopenda. Tunapozungumza kuhusu jambo tunalopenda kutoka moyoni, tunazungumza kwa msisimko mwingi na uso wetu unaonyesha uchangamfu na furaha. Ndivyo inavyokuwa hasa tunapozungumza kuhusu mtu tunayempenda. Kwa kawaida, tunakuwa na hamu ya kuwaambia wengine mambo tunayojua kuhusu mtu huyo. Tunamsifu, tunamheshimu, na kumtetea. Tunafanya hivyo kwa sababu tunataka watu wengine wavutiwe na mtu huyo na sifa zake kama tunavyovutiwa naye.

7. Upendo wa Yesu kumwelekea Mungu ulimchochea kufanya nini?

7 Kabla ya kuwasaidia wengine wasitawishe upendo kwa Yehova, ni lazima tumjue na kumpenda sisi wenyewe, kwa kuwa ibada ya kweli inategemea kumpenda Mungu. (Mt. 22:36-38) Yesu aliweka mfano mkamilifu. Alimpenda Yehova kwa moyo, akili, nafsi, na nguvu zake zote. Yesu alimjua vizuri Baba yake wa mbinguni kwa sababu alikaa naye mbinguni labda kwa mabilioni ya miaka. Matokeo yakawa nini? Yesu alisema: “Ninampenda Baba.” (Yoh. 14:31) Yesu alionyesha upendo huo katika kila jambo alilosema na kufanya. Sikuzote upendo huo ulimchochea kufanya mambo yaliyompendeza Mungu. (Yoh. 8:29) Ulimsukuma kuwashutumu viongozi wa kidini ambao walidai kwa unafiki kwamba walimwakilisha Mungu. Ulimchochea pia kuzungumza kumhusu Yehova na kuwasaidia wengine wamjue na kumpenda Mungu.

8. Kumpenda Mungu kuliwachochea wanafunzi wa Yesu wafanye nini?

8 Kama Yesu, wanafunzi wake wa karne ya kwanza walimpenda Yehova, na upendo huo uliwachochea kuhubiri habari njema kwa ujasiri na bidii. Walijaza Yerusalemu mafundisho yao, hata ingawa viongozi wa kidini wenye nguvu waliwapinga. Wanafunzi hao hawangeweza kuacha kusema juu ya mambo ambayo walikuwa wameona na kusikia. (Mdo. 4:20; 5:28) Walijua kwamba Yehova alikuwa pamoja nao na angewabariki, na kwa kweli aliwabariki! Miaka isiyozidi 30 baada ya kifo cha Yesu, mtume Paulo aliandika kwamba habari njema ilikuwa imehubiriwa “katika uumbaji wote ulio chini ya mbingu.”—Kol. 1:23.

9. Tunaweza jinsi gani kutia nguvu upendo wetu kumwelekea Mungu?

9 Ikiwa tunataka kuwa walimu wenye matokeo mazuri kwelikweli, sisi pia tunahitaji kuhakikisha kwamba tunaendelea kutia nguvu upendo wetu kwa Mungu. Tunaweza kufanya hivyo jinsi gani? Kwa kuwasiliana na Mungu mara nyingi katika sala. Pia, tunatia nguvu upendo wetu kwa Mungu kwa kujifunza Neno lake, kusoma vitabu vinavyotegemea Biblia, na kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Kadiri ujuzi wetu kumhusu Mungu unavyoongezeka, ndivyo mioyo yetu itakavyojaa upendo kumwelekea. Kisha, tunapoonyesha upendo wetu kumwelekea Mungu kwa maneno na matendo, wengine wataona hilo na huenda wakavutwa kwa Yehova.—Soma Zaburi 104:33, 34.

Ni Lazima Tupende Mambo Tunayofundisha

10. Mwalimu mzuri ana sifa gani kuu?

10 Sifa kuu ya mwalimu mzuri ni kwamba anapenda mambo anayofundisha. Ni lazima aamini kwamba mambo anayofundisha ni ya kweli, ni ya maana, na ni yenye thamani. Ikiwa mwalimu anapenda mambo anayofundisha, uchangamfu wake utaonekana, na utakuwa na uvutano mkubwa sana kwa wale anaowafundisha. Kwa upande mwingine, ikiwa mwalimu hathamini kikweli mambo anayofundisha, hawezi kutazamia wanafunzi wake wathamini yale wanayosikia. Usipuuze kamwe umuhimu wa kuweka mfano mzuri ukiwa mwalimu wa Neno la Mungu. Yesu alisema hivi: “Kila mwanafunzi aliyezoezwa vizuri atakuwa kama mwalimu wake.”—Luka 6:40, The New Berkeley Version in Modern English.

11. Kwa nini Yesu alipenda mambo aliyofundisha?

11 Yesu alipenda mambo aliyofundisha. Alijua kwamba alikuwa na kitu fulani chenye thamani cha kuwapa wengine, yaani, kweli kumhusu Baba yake wa mbinguni, “maneno ya Mungu” mwenyewe na “maneno ya uzima wa milele.” (Yoh. 3:34; 6:68) Kama nuru nyangavu, kweli ambazo Yesu alifundisha zilifunua mambo mabaya na kukazia mambo mazuri. Kweli hizo ziliwafariji na kuwapa tumaini watu wanyenyekevu ambao walikuwa wamekandamizwa na Ibilisi na kudanganywa na viongozi wa kidini wa uwongo. (Mdo. 10:38) Yesu alionyesha kwamba alipenda kweli si katika mafundisho yake tu bali pia katika mambo yote aliyofanya.

12. Mtume Paulo alikuwa na maoni gani kuhusu habari njema?

12 Kama Yesu, wanafunzi wake walipenda na walithamini sana kweli kumhusu Yehova na Kristo hivi kwamba wapinzani hawangeweza kuwazuia wasiwaambie wengine kweli hizo. Paulo aliwaandikia hivi Wakristo wenzake huko Roma: “Nina hamu ya kuitangaza habari njema . . . Kwa maana siionei aibu habari njema; kwa kweli, hiyo ni nguvu za Mungu kwa ajili ya wokovu kwa kila mtu aliye na imani.” (Rom. 1:15, 16) Paulo aliona kuwa ni heshima kutangaza kweli. Aliandika hivi: “Mimi, . . . nilipewa fadhili hizi zisizostahiliwa, ili niwatangazie mataifa habari njema juu ya utajiri usiopimika wa Kristo.” (Efe. 3:8) Si vigumu kuwazia shauku ambayo Paulo alikuwa nayo alipowafundisha wengine kumhusu Yehova na makusudi Yake.

13. Ni sababu gani zinazotufanya tupende habari njema?

13 Habari njema iliyo katika Neno la Mungu inatuwezesha kumjua Muumba na kuwa na uhusiano wenye upendo pamoja naye. Habari hiyo njema inajibu kwa njia yenye kuridhisha maswali ya maana sana kuhusu maisha na ina nguvu za kubadili maisha yetu, kutupa tumaini, na kutuimarisha katika nyakati za taabu. Kwa kuongezea, habari hiyo inatuwezesha kuwa na maisha yenye kusudi ambayo yataendelea milele. Hakuna ujuzi wa aina yoyote ambao una thamani au ni wa maana kuliko habari njema. Ni zawadi isiyo na kifani ambayo tumepewa, inayotuletea shangwe kubwa sana. Na tunapata shangwe zaidi tunapowapa wengine zawadi hiyo.—Mdo. 20:35.

14. Tunaweza kufanya nini ili upendo wetu kwa ajili ya mambo tunayofundisha uwe wenye nguvu zaidi?

14 Unaweza kufanya nini ili upendo wako kwa ajili ya habari njema uwe wenye nguvu zaidi? Unaposoma Neno la Mungu, tua mara kwa mara na utafakari mambo unayosoma. Kwa mfano, jiwazie ukiambatana pamoja na Yesu katika huduma yake duniani au ukisafiri pamoja na mtume Paulo. Jiwazie ukiwa katika ulimwengu mpya, na ufikirie jinsi maisha yatakavyokuwa tofauti kabisa. Tafakari kuhusu baraka ambazo umepata kwa sababu ya kutii habari njema. Ukiendelea kudumisha upendo wenye nguvu kwa ajili ya habari njema, wale unaowafundisha wataona upendo huo. Hivyo basi, tuna sababu nzuri za kutafakari kwa uangalifu mambo ambayo tumejifunza na kufikiria kwa uzito yale tunayofundisha.—Soma 1 Timotheo 4:15, 16.

Ni Lazima Tuwapende Watu

15. Kwa nini mwalimu anapaswa kuwapenda wanafunzi wake?

15 Mwalimu mzuri anawafanya wanafunzi wake wajihisi wamestarehe hivi kwamba wanakuwa na hamu ya kujifunza kwa makini na wanafurahia kutoa maoni yao. Mwalimu mwenye upendo anawasaidia wanafunzi wake kupata ujuzi kwa sababu anawajali kikweli. Anabadili ufundi wake wa kufundisha kulingana na mahitaji yao na uwezo wao wa kuelewa mambo. Anatilia maanani uwezo na hali ya wanafunzi wake. Mwalimu akiwa na upendo wa aina hiyo wanafunzi watatambua hilo, na mwalimu atafurahia kufundisha nao wanafunzi watafurahia kujifunza.

16. Yesu aliwaonyesha watu upendo kwa njia gani?

16 Yesu alionyesha upendo wa aina hiyo. Alionyesha upendo kwa njia kubwa kupita zote alipodhabihu uhai wake mkamilifu wa kibinadamu ili wengine waokolewe. (Yoh. 15:13) Wakati wa huduma yake, Yesu hakuchoka kuwasaidia watu kimwili na hasa kiroho. Badala ya kuwangojea watu waje kwake, alisafiri mamia ya kilomita kwa miguu ili awahubirie habari njema. (Mt. 4:23-25; Luka 8:1) Alikuwa mwenye subira na alielewa hali za wanafunzi wake. Walipohitaji kurekebishwa, aliwarekebisha kwa upendo. (Marko 9:33-37) Aliwatia moyo kwa kuwahakikishia kwamba wangekuwa wahubiri wa habari njema wenye matokeo mazuri. Yesu ndiye mwalimu mwenye upendo zaidi kuliko walimu wengine wote. Upendo ambao aliwaonyesha wanafunzi wake uliwachochea wampende na kushika amri zake.—Soma Yohana 14:15.

17. Wanafunzi wa Yesu waliwaonyesha wengine upendo jinsi gani?

17 Wanafunzi wa Yesu walimwiga kwa kuwapenda sana watu ambao walihubiria. Waliwahudumia wengine na kufanikiwa kuhubiri habari njema ingawa walivumilia mateso na kuhatarisha uhai wao. Waliwapenda sana watu ambao walikubali habari njema. Maneno haya ambayo mtume Paulo aliandika yanagusa moyo sana: “Tulikuwa wapole katikati yenu, kama mama mwenye kunyonyesha anavyowatunza kwa upendo watoto wake mwenyewe. Kwa hiyo, tukiwa na upendo mwororo kwa ajili yenu, tulipendezwa vema kuwapa ninyi, si habari njema ya Mungu tu, bali pia nafsi zetu wenyewe, kwa sababu ninyi mlikuwa wapendwa kwetu.”—1 The. 2:7, 8.

18, 19. (a) Kwa nini tuko tayari kujidhabihu ili kufanya kazi ya kuhubiri? (b) Toa mfano unaothibitisha kwamba wengine wanaona upendo ambao tunaonyesha.

18 Vivyo hivyo leo, Mashahidi wa Yehova wanahubiri duniani pote wakiwatafuta watu ambao wanatamani sana kumjua Mungu na kumtumikia. Kwa kweli, kwa muda wa miaka 17 mfululizo, tumetumia muda wa saa zaidi ya bilioni moja kila mwaka katika kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi, nasi tunaendelea na kazi hiyo. Tunafanya hivyo kwa kupenda, hata ingawa kazi ya kuhubiri inatulazimu kudhabihu wakati, nguvu, na mali zetu. Kama Yesu, tunaelewa kwamba Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo anatamani kuona watu wakipata ujuzi ambao unaongoza kwenye uzima wa milele. (Yoh. 17:3; 1 Tim. 2:3, 4) Upendo unatuchochea kuwasaidia watu wenye mioyo minyoofu wapate kumjua na kumpenda Yehova kama tunavyomjua na kumpenda.

19 Wengine wanaona upendo ambao tunaonyesha. Kwa mfano, dada mmoja painia huko Marekani anaandika barua za kuwafariji watu ambao wamefiwa na wapendwa wao. Mwanamume mmoja alimjibu hivi katika barua aliyomwandikia: “Kwanza, nilishangaa kwamba mtu anaweza kufanya jitihada hizo za kumwandikia barua mtu asiyemjua ili amsaidie kuvumilia hali ngumu. Ninaweza kusema tu kwamba unawapenda wanadamu wenzako na unampenda Mungu ambaye anawaongoza watu kwenye njia ya uzima.”

20. Kufundisha kwa upendo ni jambo la maana kadiri gani?

20 Mwandishi mmoja alisema kwamba mtu anapofanya kazi kwa upendo na pia kwa ustadi, anapata matokeo bora sana. Tunapofundisha, tunajitahidi kuwasaidia wanafunzi wamjue na kumpenda Yehova kwa akili na moyo wao wote. Ndiyo, ili tuwe walimu wenye matokeo mazuri, tunahitaji kuonyesha upendo katika njia tatu—kumpenda Mungu, kupenda kweli, na kuwapenda watu. Tunapositawisha upendo wa aina hiyo na kuuonyesha katika huduma yetu, tunapata shangwe inayotokana na kutoa na pia tunapata uradhi kwa sababu tunajua kwamba tunamwiga Yesu na tunampendeza Yehova.

Ungesema Nini?

• Tunapowafundisha wengine habari njema, kwa nini ni jambo la maana . . .

kumpenda Mungu?

kupenda mambo tunayofundisha?

kuwapenda watu tunaofundisha?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 15]

Kwa nini njia ya Yesu ya kufundisha ilikuwa tofauti na ya waandishi na Mafarisayo?

[Picha katika ukurasa wa 18]

Ili mtu afundishe vizuri anahitaji ujuzi, ustadi, na zaidi ya yote, upendo