Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mwige Yesu—Hubiri Kwa Ujasiri

Mwige Yesu—Hubiri Kwa Ujasiri

Mwige Yesu—Hubiri Kwa Ujasiri

“Tulijipa ujasiri . . . ili kuwaambia ninyi habari njema.”—1 THE. 2:2.

1. Kwa nini habari njema ya Ufalme inavutia sana?

INAFURAHISHA kama nini kusikia habari njema! Na habari bora kuliko zote ni habari njema ya Ufalme wa Mungu. Habari njema hiyo inatuhakikishia kwamba hakutakuwa tena na mateso, magonjwa, taabu, huzuni, na kifo. Inatupa tumaini la uzima wa milele, inafunua kusudi la Mungu, na inatuonyesha jinsi ya kuwa na uhusiano wenye upendo pamoja naye. Je, unafikiri kwamba kila mtu anafurahi kusikiliza habari hiyo ambayo Yesu aliwatangazia wanadamu? Inasikitisha kwamba sivyo ilivyo.

2. Eleza maana ya maneno haya ya Yesu: “Nilikuja kuleta mgawanyiko.”

2 Yesu aliwaambia wanafunzi wake: “Msifikiri nilikuja kuleta amani duniani; nilikuja kuleta, si amani, bali upanga. Kwa maana nilikuja kuleta mgawanyiko, mtu kumpinga baba yake, binti kumpinga mama yake, mke aliye mchanga kumpinga mama-mkwe wake. Kwa kweli, adui za mtu watakuwa watu wa nyumbani kwake mwenyewe.” (Mt. 10:34-36) Badala ya kukubali habari njema, watu wengi wanaikataa. Wengine hata wanajifanya kuwa maadui wa wale wanaohubiri habari njema hiyo, hata ikiwa ni watu wa familia yao.

3. Tunahitaji nini ili kutimiza kazi yetu ya kuhubiri?

3 Tunatangaza kweli zilezile ambazo Yesu alitangaza, na baada ya kuzisikia, watu wanaitikia kama tu walivyoitikia wakati wa Yesu. Tunatazamia jambo hilo. Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Mtumwa si mkuu kuliko bwana wake. Ikiwa wamenitesa mimi, watawatesa ninyi pia.” (Yoh. 15:20) Katika nchi nyingi hatukabili mateso ya moja kwa moja, lakini watu fulani wanadharau na kupuuza ujumbe wetu. Hivyo, tunahitaji imani na uhodari ili tuvumilie katika kazi yetu ya kuhubiri habari njema kwa ujasiri.—Soma 2 Petro 1:5-8.

4. Kwa nini Paulo alihitaji ‘kujipa ujasiri’ ili kuhubiri?

4 Labda nyakati nyingine unaona ni vigumu kushiriki katika huduma, au huenda ukaogopa kushiriki katika sehemu fulani ya huduma. Ikiwa ndivyo unavyohisi, basi kumbuka kwamba kuna wahubiri wengine wanaohisi hivyo. Ingawa mtume Paulo alikuwa mhubiri mwenye ujasiri na asiyeogopa ambaye alielewa kweli vizuri sana, nyakati nyingine alipambana ili kuhubiri. Paulo aliwaandikia hivi Wakristo wa huko Thesalonike: “Baada ya sisi kuwa tumeteseka kwanza na kutendewa kwa dharau (kama mnavyojua) katika Filipi, tulijipa ujasiri kwa njia ya Mungu wetu ili kuwaambia ninyi habari njema ya Mungu kwa kupambana sana.” (1 The. 2:2) Wenye mamlaka huko Filipi waliamuru Paulo na mwenzake Sila wapigwe kwa fimbo, watupwe gerezani, na kufungwa kwa mikatale. (Mdo. 16:16-24) Hata hivyo, Paulo na Sila ‘walijipa ujasiri’ wa kuendelea kuhubiri. Tunaweza jinsi gani kufanya vivyo hivyo? Ili kujibu swali hilo, acheni tuchunguze kilichowawezesha watumishi wa Mungu katika nyakati za Biblia kusema kwa ujasiri kweli kumhusu Yehova, na acheni tujifunze jinsi tunavyoweza kuiga mfano wao.

Walihitaji Ujasiri ili Kukabiliana na Uadui

5. Kwa nini sikuzote watumishi washikamanifu wa Yehova wamehitaji kuwa jasiri?

5 Bila shaka, Yesu Kristo aliweka mfano bora zaidi katika kuonyesha uhodari na ujasiri. Hata hivyo, tangu mwanzo wa historia ya wanadamu, watumishi washikamanifu wa Yehova wamehitaji sikuzote kuwa jasiri. Kwa nini? Baada ya uasi katika Edeni, Yehova alitabiri kwamba kungekuwa na uadui kati ya wale wanaomtumikia Mungu na wale wanaomtumikia Shetani. (Mwa. 3:15) Uadui huo ulionekana haraka wakati Abeli, mwanamume mwadilifu, alipouawa na ndugu yake. Baadaye, Enoko, mwanamume mwingine mwaminifu aliyeishi kabla ya Gharika alikabili uadui. Alitabiri kwamba Mungu angekuja na maelfu ya malaika Wake watakatifu kutekeleza hukumu juu ya watu wasiomwogopa Mungu. (Yuda 14, 15) Bila shaka, ujumbe huo haukupendwa na watu wengi. Watu walimchukia Enoko na ni wazi kwamba wangemuua ikiwa Yehova hangefupisha maisha yake. Enoko alikuwa jasiri sana.—Mwa. 5:21-24.

6. Kwa nini Musa alihitaji ujasiri ili kuzungumza na Farao?

6 Pia, fikiria ujasiri ambao Musa alionyesha alipozungumza na Farao, mtawala ambaye alionwa, si kama mwakilishi wa miungu tu, bali kama mungu mwenyewe, mwana wa mungu-jua, Ra. Huenda ikawa kwamba yeye, kama Mafarao wengine, aliabudu sanamu yake mwenyewe. Neno la Farao lilikuwa sheria; alitawala kwa amri. Farao alikuwa mwenye nguvu, mwenye kiburi, na mkaidi, naye hakuzoea kuambiwa na watu wengine jambo la kufanya. Musa, ambaye alikuwa mchungaji mnyenyekevu, alienda mara nyingi mbele ya mfalme huyo ambaye hakutaka kumwona. Musa alitabiri nini? Mapigo hatari sana. Na aliomba nini? Aliomba ruhusa ili mamilioni ya watumwa wa Farao waondoke nchini! Je, Musa alihitaji ujasiri? Bila shaka!—Hes. 12:3; Ebr. 11:27.

7, 8. (a) Ni majaribu gani ambayo yaliwapata waaminifu wa kale? (b) Ni nini kilichowawezesha waaminifu hao wa nyakati za kabla ya Ukristo kuunga mkono na kuendeleza ibada safi kwa ujasiri?

7 Kwa karne nyingi zilizofuata, manabii na watumishi wengine waaminifu wa Mungu waliendelea kutetea kwa ujasiri ibada safi. Ulimwengu wa Shetani haukuwatendea kwa fadhili. Paulo anasema: “Walipigwa kwa mawe, walijaribiwa, walikatwa vipande-vipande kwa msumeno, walikufa kwa kuuawa kwa upanga, walitembea huku na huku wakiwa wamevikwa ngozi za kondoo, wakiwa wamevikwa ngozi za mbuzi, wakiwa katika uhitaji, katika dhiki, wakitendewa vibaya.” (Ebr. 11:37) Ni nini kilichowasaidia watumishi hao washikamanifu wa Mungu kusimama imara? Katika mistari michache inayotangulia, mtume huyo alionyesha kile kilichompa Abeli, Abrahamu, Sara, na wengine nguvu za kuvumilia. Alisema hivi: “Hawakupata utimizo wa zile ahadi, bali [kwa imani] waliziona kwa mbali na kuzikaribisha.” (Ebr. 11:13) Bila shaka, manabii kama vile Eliya, Yeremia, na waaminifu wengine wa nyakati za kabla ya Ukristo ambao walitetea kwa ujasiri ibada ya kweli waliweza pia kuvumilia kwa kukazia macho ahadi za Yehova.—Tito 1:2.

8 Waaminifu hao wa nyakati za kabla ya Ukristo walikazia macho wakati ujao ulio mwangavu na wenye kuvutia. Baada ya kufufuliwa, mwishowe watafikia ukamilifu na ‘watawekwa huru kutoka katika utumwa wa uharibifu’ kupitia utumishi wa kikuhani wa Kristo Yesu na makuhani wenzake wasaidizi 144,000. (Rom. 8:21) Zaidi ya hayo, Yeremia na watumishi wengine jasiri wa Mungu katika nyakati za kale walikuwa na uhodari kwa sababu ya uhakikisho huu ambao Yehova alitoa katika ahadi yake kwa Yeremia: “Hakika watapigana nawe, lakini hawatakushinda, kwa maana ‘Mimi niko pamoja nawe,’ asema Yehova, ‘ili nikukomboe.’” (Yer. 1:19) Leo, tunapofikiria ahadi za Mungu kuhusu wakati wetu ujao na uhakikisho wa kwamba atatulinda kiroho, sisi pia tunatiwa nguvu.—Met. 2:7; soma 2 Wakorintho 4:17, 18.

Upendo Ulimchochea Yesu Kuhubiri kwa Ujasiri

9, 10. Ni katika njia gani Yesu alionyesha ujasiri mbele ya (a) viongozi wa kidini, (b) kikundi cha askari-jeshi, (c) kuhani mkuu, (d) Pilato?

9 Kielelezo chetu, Yesu, alionyesha ujasiri katika njia mbalimbali. Kwa mfano, ingawa alichukiwa na wakuu na wenye mamlaka, Yesu hakupunguza uzito wa ujumbe ambao Mungu alitaka watu wajue. Bila woga, aliwashutumu waziwazi viongozi wa kidini wenye nguvu kwa sababu ya kujiona kuwa waadilifu na pia kwa sababu ya mafundisho yao ya uwongo. Yesu aliwashutumu wanaume hao moja kwa moja na waziwazi. Pindi moja, alisema: “Ole wenu ninyi, waandishi na Mafarisayo, wanafiki! kwa sababu mnafanana na makaburi yaliyopakwa chokaa, ambayo kwa nje yanaonekana kwa kweli kuwa mazuri lakini ndani yamejaa mifupa ya wafu na kila namna ya ukosefu wa usafi. Katika njia hiyo ninyi pia, kwa kweli, mnaonekana kwa nje kuwa waadilifu kwa watu, lakini ndani mmejaa unafiki na uasi-sheria.”—Mt. 23:27, 28.

10 Alipokabiliwa na kikundi cha askari-jeshi katika bustani ya Gethsemane, Yesu alijitambulisha kwa ujasiri. (Yoh. 18:3-8) Baadaye alipelekwa mbele ya Sanhedrini na kuhojiwa na kuhani mkuu. Hata ingawa alijua kwamba kuhani mkuu alikuwa akitafuta kisingizio cha kumuua, Yesu alikubali bila woga kwamba Alikuwa Kristo na pia Mwana wa Mungu. Aliongeza kwamba wangemwona akiwa “ameketi kwenye mkono wa kuume wa nguvu akija pamoja na mawingu ya mbinguni.” (Marko 14:53, 57-65) Muda mfupi baadaye, Yesu alisimama akiwa amefungwa pingu mbele ya Pilato, ambaye alikuwa na uwezo wa kumweka huru. Lakini Yesu alinyamaza na hakujibu mashtaka yaliyokuwa yakitolewa juu yake. (Marko 15:1-5) Alihitaji ujasiri sana ili kufanya yote hayo.

11. Kuna uhusiano gani kati ya ujasiri na upendo?

11 Yesu alimwambia Pilato hivi: “Kwa ajili ya hili mimi nimezaliwa, na kwa ajili ya hili nimekuja ulimwenguni, ili nitoe ushahidi juu ya ile kweli.” (Yoh. 18:37) Yehova alimtuma Yesu kuhubiri habari njema, na Yesu alifurahi kufanya hivyo kwa sababu alimpenda Baba yake wa mbinguni. (Luka 4:18, 19) Yesu aliwapenda watu pia. Alijua kwamba maisha yao yalikuwa magumu. Sisi pia tunahubiri kwa ujasiri na bila woga kwa sababu tunampenda sana Yehova na majirani wetu.—Mt. 22:36-40.

Roho Takatifu Inatutia Nguvu ili Tuhubiri kwa Ujasiri

12. Ni nini kilichowaletea shangwe wanafunzi wa mapema?

12 Katika majuma yaliyofuata baada ya kifo cha Yesu, wanafunzi walifurahi sana kuona Yehova akiongeza hesabu ya wanafunzi wapya waliojiunga nao. Kwa siku moja tu, Wayahudi 3,000 hivi na watu waliogeuzwa imani kutoka katika nchi nyingi waliokuja Yerusalemu kusherehekea Pentekoste walibatizwa! Inaelekea kila mtu huko Yerusalemu alikuwa akizungumza kuhusu tukio hilo! Biblia inasema hivi: “Woga ukaanza kuwa juu ya kila nafsi, na mambo mengi ya ajabu na ishara nyingi zikaanza kutukia kupitia mitume.”—Mdo. 2:41, 43.

13. Kwa nini akina ndugu walisali ili wapewe ujasiri, kukawa na matokeo gani?

13 Kwa hasira, viongozi wa kidini waliwakamata Petro na Yohana, wakawafunga gerezani usiku wote, na kuwaamuru wasiseme kumhusu Yesu. Baada tu ya kuachiliwa huru, mitume hao wawili waliwaeleza akina ndugu kilichotukia, na wote wakasali kuhusu upinzani waliokuwa wakikabili, na kuomba hivi: ‘Yehova wawezeshe watumwa wako kuendelea kusema neno lako kwa ujasiri wote.’ Kukawa na matokeo gani? “Wote wakajazwa roho takatifu na wakawa wakisema neno la Mungu kwa ujasiri.”—Mdo. 4:24-31.

14. Roho takatifu inatusaidia jinsi gani katika kazi yetu ya kuhubiri?

14 Ona kwamba roho takatifu ya Yehova yenye nguvu ndiyo iliyowasaidia wanafunzi kusema neno la Mungu kwa ujasiri. Yehova ndiye anayetupa ujasiri wa kuwaambia wengine kweli, hata wale wanaopinga ujumbe wetu. Yehova anaweza kutupa na atatupa roho yake takatifu tukimwomba atupe roho hiyo. Kwa msaada wa Yehova, sisi pia tunaweza kuwa na ujasiri unaohitajika ili kushinda upinzani wowote.—Soma Zaburi 138:3.

Wakristo Wanahubiri kwa Ujasiri Leo

15. Kweli inawatenganisha watu jinsi gani leo?

15 Leo, kama ilivyokuwa katika nyakati za kale, kweli inaendelea kuwatenganisha watu. Watu fulani wanaitikia vizuri, lakini wengine hawaelewi wala kuthamini ibada yetu. Wengine wanatuchambua-chambua, wanatudhihaki, au hata kutuchukia, kama tu Yesu alivyotabiri. (Mt. 10:22) Nyakati nyingine, vyombo vya habari vinaeneza habari za uwongo na propaganda za chuki kutuhusu. (Zab. 109:1-3) Hata hivyo, watu wa Yehova wanatangaza kwa ujasiri habari njema duniani pote.

16. Ni jambo gani lililoonwa linaloonyesha kwamba ujasiri unaweza kubadili maoni ya wale tunaowahubiria?

16 Ujasiri wetu unaweza kuwafanya watu wabadili maoni yao kuhusu ujumbe wa Ufalme. Dada mmoja huko Kyrgyzstan anasema: “Nilipokuwa nikihubiri, mwenye nyumba mmoja aliniambia hivi: ‘Ninamwamini Mungu lakini si Mungu wa Wakristo. Ukirudi tena kwenye mlango huu, nitaamuru mbwa wangu akushambulie!’ Mbwa huyo mkubwa na mwenye nguvu alikuwa nyuma yake akiwa amefungwa kwa mnyororo. Lakini wakati wa kampeni ya kugawa trakti Habari za Ufalme Na. 37, yenye kichwa, ‘Mwisho wa Dini ya Uwongo Unakaribia!,’ niliamua kurudi kwenye nyumba ileile nikitazamia kumkuta mshiriki mwingine wa familia ya mwanamume huyo. Hata hivyo, mwanamume yuleyule alifungua mlango. Nilisali haraka kwa Yehova kisha nikasema: ‘Hujambo, ninakumbuka mazungumzo yetu siku tatu zilizopita, na ninamkumbuka pia mbwa wako. Lakini singepita bila kukuachia trakti hii kwa sababu ninamwamini yule Mungu mmoja tu wa kweli kama wewe unavyomwamini. Hivi karibuni Mungu ataadhibu dini ambazo zinamvunjia heshima. Unaweza kujifunza mengi zaidi kuhusu hilo kwa kusoma trakti hii.’ Nilishangaa sana kuona mwanamume huyo akikubali trakti hiyo ya Habari za Ufalme. Kisha nikaenda kwenye nyumba nyingine. Dakika chache baadaye, mwanamume huyo alinifuata akikimbia huku akiwa amebeba trakti hiyo. Akasema: ‘Nimeisoma. Ninahitaji kufanya nini ili niepuke hasira ya Mungu?’” Mwanamume huyo alianza kujifunza Biblia na pia akaanza kuhudhuria mikutano ya Kikristo.

17. Ujasiri wa dada mmoja ulimtia nguvu jinsi gani mwanafunzi fulani wa Biblia ambaye alikuwa mwoga?

17 Ujasiri wetu unaweza pia kuwatia wengine moyo kuwa jasiri. Huko Urusi dada mmoja aliyekuwa akisafiri kwa basi alimwonyesha msafiri mwenzake gazeti. Kwa ghafula, mwanamume mmoja aliinuka kutoka kwenye kiti chake, akamnyang’anya dada huyo gazeti hilo kwa nguvu, akalikunja-kunja, na kulitupa chini. Alimtukana dada huyo kwa sauti kubwa, akamwamuru ampe anwani yake na kumwonya asihubiri katika kijiji chao. Dada huyo alisali kwa Yehova na kumwomba msaada, akajikumbusha maneno haya ya Yesu: “Msiwaogope wale ambao wanaua mwili.” (Mt. 10:28) Kwa utulivu, dada huyo alisimama na kumwambia mwanamume huyo, “Sitakupa anwani yangu, na nitaendelea kuhubiri kijijini.” Kisha akashuka basi hilo. Dada huyo hakujua kwamba mmoja wa wanafunzi wake wa Biblia alikuwa ndani ya basi hilo. Mwanafunzi huyo aliacha kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwa sababu ya kuwaogopa wanadamu. Hata hivyo, baada ya kuona ujasiri wa dada yetu, mwanafunzi huyo wa Biblia aliamua kwamba angeanza tena kuhudhuria mikutano.

18. Ni nini kitakachokusaidia kuhubiri kwa ujasiri kama Yesu alivyofanya?

18 Katika ulimwengu huu uliotengwa mbali na Mungu, unahitaji ujasiri ili uhubiri kama Yesu alivyofanya. Ni nini kitakachokusaidia kufanya hivyo? Kazia macho wakati ujao. Endelea kuutia nguvu upendo wako kwa Mungu na kwa jirani. Sali kwa Yehova ili akupe ujasiri. Sikuzote kumbuka kwamba hujaachwa peke yako, Yesu yupo pamoja nawe. (Mt. 28:20) Roho takatifu itakutia nguvu. Na Yehova atakubariki na kukutegemeza. Kwa hiyo, na tuwe hodari na kusema: “Yehova ni msaidizi wangu; sitaogopa. Mwanadamu anaweza kunitenda nini?”—Ebr. 13:6.

Ungesema Nini?

• Kwa nini watumishi wa Mungu wanahitaji ujasiri?

• Kuhusu kuwa na ujasiri, tunajifunza nini kutokana na . . .

waaminifu walioishi kabla ya Kristo?

Yesu Kristo?

Wakristo wa mapema?

Wakristo wenzetu leo?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 21]

Yesu aliwashutumu bila woga viongozi wa kidini

[Picha katika ukurasa wa 23]

Yehova anatupa ujasiri wa kuhubiri