Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Miaka 90 Iliyopita Nilianza ‘Kumkumbuka Muumba Wangu Mkuu’

Miaka 90 Iliyopita Nilianza ‘Kumkumbuka Muumba Wangu Mkuu’

Miaka 90 Iliyopita Nilianza ‘Kumkumbuka Muumba Wangu Mkuu’

Limesimuliwa na Edwin Ridgwell

WAKATI wa sikukuu ya mapatano ya kusimamisha vita kwa muda mnamo Novemba 11, 1918 (11/11/1918), kwa ghafula wanafunzi wote katika shule yetu waliombwa wakusanyike ili washerehekee mwisho wa vile Vita Vikuu, ambavyo baadaye viliitwa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu. Nilikuwa na umri wa miaka mitano tu na sikuelewa vizuri kabisa ni nini kilichokuwa kikisherehekewa. Hata hivyo, nilijua kutokana na mambo ambayo wazazi wangu walikuwa wamenifundisha kumhusu Mungu kwamba sikupaswa kushiriki katika sherehe hiyo. Nilisali kwa Mungu, lakini nililemewa na hisia nikaanza kulia. Hata hivyo, sikushiriki katika sherehe hiyo. Huo ndio wakati nilipoanza ‘kumkumbuka Muumba wangu Mkuu.’—Mhu. 12:1.

Miezi kadhaa kabla ya sherehe hiyo kufanyika shuleni, familia yetu ilikuwa imehamia karibu na Glasgow huko Scotland. Karibu wakati huo, Baba alikuwa amehudhuria hotuba ya watu wote yenye kichwa “Mamilioni Wanaoishi Sasa Hawatakufa Kamwe.” Hotuba hiyo ilibadili maisha yake. Baba na Mama walianza kujifunza Biblia na mara nyingi walizungumza pamoja kuhusu Ufalme wa Mungu na baraka zitakazokuja. Ninamshukuru Mungu kwa sababu tangu wakati huo na kuendelea wazazi wangu walinifundisha kumpenda na kumtegemea Mungu.—Met. 22:6.

Ninaanza Huduma ya Wakati Wote

Nilipokuwa na umri wa miaka 15, nilikuwa na nafasi ya kuendelea na masomo ya juu, lakini nilitaka sana kuwa mtumishi wa wakati wote. Baba alihisi kwamba sikuwa nimekomaa vya kutosha, kwa hiyo nilifanya kazi katika ofisi moja kwa muda fulani. Hata hivyo, nilitamani sana kumtumikia Yehova katika utumishi wa wakati wote hivi kwamba siku moja nilimwandikia barua J. F. Rutherford, ambaye alikuwa akisimamia kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote wakati huo. Nilimuuliza maoni yake kuhusu mipango yangu. Ndugu Rutherford aliniandikia hivi: “Ikiwa una umri wa kutosha kufanya kazi, basi una umri wa kutosha kushiriki katika utumishi wa Bwana. . . . Ninaamini kwamba Bwana atakubariki ukijitahidi kumtumikia kwa uaminifu.” Barua hiyo ambayo iliandikwa Machi 10, 1928 (10/3/1928), ilichochea sana familia yetu. Baada ya muda mfupi, mimi, Baba, Mama, na dada yangu mkubwa tulianza huduma ya wakati wote.

Mwaka wa 1931 kwenye kusanyiko huko London, Ndugu Rutherford aliomba wajitoleaji ili waeneze habari njema katika nchi za kigeni. Nilijitolea, na nikiwa na Andrew Jack, tulipewa mgawo wa kwenda Kaunas, ambao wakati huo ulikuwa mji mkuu wa Lithuania. Nilikuwa na umri wa miaka 18.

Kuhubiri Ujumbe wa Ufalme Katika Nchi ya Kigeni

Wakati huo, Lithuania ilikuwa nchi yenye wakulima wengi maskini sana, na haikuwa rahisi kuhubiri katika maeneo ya mashambani. Pia, haikuwa rahisi kupata mahali pa kuishi, na hatungeweza kamwe kusahau vyumba fulani tulimoishi. Kwa mfano, usiku mmoja mimi na Andrew tuliamka kwa sababu tulikuwa tukiumwa. Baada ya kuwasha taa, tuliona kwamba kitanda kilikuwa kimejaa mamia ya kunguni. Kunguni hao walituuma kila mahali mwilini! Kila asubuhi kwa muda wa juma moja, nililazimika kusimama mwili mzima kufikia shingoni ndani ya maji baridi ya mto uliokuwa karibu ili nipunguze maumivu. Hata hivyo, tuliazimia kuendelea na huduma. Muda mfupi baadaye, tatizo la kupata mahali pazuri pa kulala lilikwisha tulipokutana na wenzi wa ndoa vijana ambao walikuwa wamekubali kweli ya Biblia. Walitukaribisha katika nyumba yao ambayo ilikuwa ndogo sana lakini safi. Tulifurahi kulala kwenye sakafu badala ya kulala kwenye kitanda kilichojaa kunguni!

Wakati huo, Lithuania ilikuwa chini ya Kanisa Katoliki na makasisi wa Kanisa Othodoksi la Urusi. Matajiri tu ndio wangeweza kununua Biblia. Kusudi letu kuu lilikuwa kuhubiri eneo kubwa kadiri iwezekanavyo na kuwaachia watu waliopendezwa vichapo vingi vya Biblia. Kwanza tulipaswa kutafuta chumba cha kuishi mjini. Baada ya hapo tulihubiri kwa busara maeneo yaliyokuwa karibu, kisha tulihubiri haraka-haraka mji wote. Kwa kawaida, kwa kufanya hivyo tulifaulu kumaliza mahubiri yetu kabla kasisi wa eneo hilo hajachochea vurugu.

Vurugu Zinafanya Ujumbe Wetu Ujulikane

Mwaka wa 1934, Andrew alipewa mgawo wa kufanya kazi katika ofisi ya tawi huko Kaunas, na John Sempey akajiunga nami. Tukiwa pamoja, tulijionea mambo mengi ambayo hatuwezi kusahau. Siku moja nilitembelea ofisi ya wakili mmoja katika mji fulani mdogo. Mwanamume huyo alikasirika, akatoa bastola kwenye kabati, akaniamuru niondoke. Nilisali kimya-kimya na nikakumbuka shauri hili la Biblia: “Jibu, linapokuwa la upole, hugeuza ghadhabu.” (Met. 15:1) Basi nikamwambia, “Nilikuja hapa kama rafiki nikiwa na ujumbe wa habari njema, na ninashukuru kwamba hujanipiga risasi.” Mwanamume huyo aliulegeza mkono wake uliokuwa umeshika bastola, halafu nikaondoka polepole katika ofisi hiyo.

Tulipokutana na John, aliniambia kwamba yeye pia alikuwa amekabiliana na hali ngumu. Alikuwa amepelekwa kwenye kituo cha polisi kwa sababu alishtakiwa kwa uwongo kwamba alikuwa ameiba noti ya pesa nyingi kutoka kwa mwanamke ambaye alikuwa amekutana naye. Akiwa kwenye kituo hicho, John alivuliwa nguo zote alipokuwa akipekuliwa. Bila shaka, hakuwa na noti hiyo. Baadaye mwizi aliyeiba noti hiyo alikamatwa.

Visa hivyo viwili vilizua vurugu katika mji huo uliokuwa na utulivu na watu wengi sana wakasikia ujumbe wetu hata bila sisi kuwahubiria!

Utendaji wa Kisiri-Siri

Mgawo hatari ulikuwa ule wa kupeleka vichapo vya Biblia katika nchi jirani ya Latvia, ambako kazi yetu ya kuhubiri ilikuwa imepigwa marufuku. Karibu mara moja kwa mwezi, tulisafiri hadi Latvia kwa gari-moshi wakati wa usiku. Nyakati nyingine, baada ya kufikisha vichapo, tulisafiri hadi Estonia ili kuchukua vichapo vingine ambavyo tulipaswa kuacha Latvia wakati wa kurudi.

Pindi moja, ofisa wa forodha alikuwa ameambiwa kuhusu utendaji wetu na akatuamuru tushuke kutoka kwenye gari-moshi na tupeleke vichapo kwa ofisa aliyekuwa na cheo kikubwa kuliko chake. Mimi na John tulisali kwa Yehova ili atusaidie. Kwa kushangaza, ofisa yule hakumwambia mkubwa wake tulichokuwa tumebeba bali alimwambia tu kwamba, “Wanaume hawa wana ujumbe fulani.” Nilisema kwamba tulikuwa na vichapo ambavyo vingewasaidia watu katika shule na vyuo waelewe maana ya matukio yaliyokuwa yakiendelea katika ulimwengu wetu uliojaa msukosuko. Ofisa huyo wa forodha alitupungia mkono ili tupite na tukavipeleka vichapo hivyo bila matatizo.

Kadiri hali ya kisiasa ilivyoendelea kuharibika katika Nchi za Baltiki, ndivyo watu walivyowapinga zaidi Mashahidi na pia kazi yetu ikapigwa marufuku nchini Lithuania. Andrew na John walifukuzwa nchini, na Vita vya Pili vya Ulimwengu vilipokuwa vikikaribia kuanza, watu wote wa Uingereza walishauriwa waondoke Lithuania. Mimi pia niliondoka kwa huzuni.

Napata Mapendeleo na Baraka Huko Ireland ya Kaskazini

Wakati huo wazazi wangu walikuwa wamehamia Ireland ya Kaskazini, na mwaka wa 1937, nikajiunga nao huko. Kwa sababu ya wasiwasi wa vita, vichapo vyetu vilikuwa pia vimepigwa marufuku huko Ireland ya Kaskazini, lakini tuliendelea kuhubiri katika kipindi chote cha vita. Baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu, kazi yetu iliendelea bila vizuizi vya kisheria. Harold King, painia mwenye uzoefu ambaye baadaye alitumika akiwa mmishonari nchini China, aliongoza katika kufanya mipango ya kutoa hotuba za watu wote hadharani. Alisema hivi: “Jumamosi (Siku ya Posho) hii, nitatoa hotuba ya kwanza ya hadharani.” Kisha akanitazama na kuniambia, “Jumamosi ijayo wewe ndiye utakayetoa hotuba.” Nilishtuka.

Ninakumbuka vizuri hotuba yangu ya kwanza. Mamia ya watu walikuwa wamehudhuria. Niliitoa nikiwa nimesimama juu ya kisanduku huku nikizungumza bila kutumia kipaza-sauti chochote. Baada ya hotuba hiyo, mwanamume fulani alinijia na kunisalimu, kisha akaniambia kwamba jina lake ni Bill Smith. Alisema kwamba aliona umati akasimama ili aone jambo lililokuwa likiendelea. Bill alikuwa amehubiriwa na baba yangu mapema lakini hawakukutana tena baada ya Baba na mama yangu wa kambo kuhamia Dublin ili kutumika wakiwa mapainia huko. Nilianza kujifunza Biblia pamoja na Bill. Baada ya muda, watu tisa katika familia ya Bill wakawa watumishi wa Yehova.

Baadaye, nilihubiri katika eneo lenye nyumba kubwa za kifahari nje ya jiji la Belfast, ambako nilikutana na mwanamke Mrusi aliyewahi kuishi Lithuania. Nilipomwonyesha vitabu fulani, alinionyesha kwa kidole kitabu kimoja na kusema: “Nina kitabu hiki. Mjomba wangu ambaye ni profesa katika chuo kikuu huko Kaunas ndiye aliyenipa kitabu hicho.” Alinionyesha kitabu Creation, cha lugha ya Kipolishi. Kilikuwa kimejaa maandishi pambizoni. Alishangaa sana kujua kwamba mimi ndiye niliyekuwa nimempa mjomba wake kitabu hicho nilipokutana naye huko Kaunas!—Mhu. 11:1.

John Sempey aliposikia kwamba ninaenda Ireland ya Kaskazini, aliniomba nimtembelee dada yake mdogo, Nellie, kwa sababu alikuwa amependezwa na kweli ya Biblia. Mimi na dada yangu Connie tulijifunza Biblia pamoja naye. Nellie alifanya maendeleo haraka na akajiweka wakfu kwa Yehova. Baadaye, tulichumbiana na tukafunga ndoa.

Mimi na Nellie tulimtumikia Yehova pamoja kwa miaka 56 na tulipata pendeleo la kuwasaidia watu zaidi ya 100 kupata ujuzi wa kweli ya Biblia. Tulitumaini kwamba tungeona Har–Magedoni na kuingia katika ulimwengu mpya wa Yehova tukiwa pamoja, lakini alikufa mwaka wa 1998. Hilo lilikuwa pigo kubwa, ni mojawapo ya majaribu makali zaidi ambayo nimewahi kupata.

Kurudi Katika Nchi za Baltiki

Mwaka mmoja hivi baada ya kifo cha Nellie, nilipata baraka nzuri ajabu. Nilialikwa kutembelea ofisi ya tawi huko Tallinn, Estonia. Barua kutoka kwa akina ndugu huko Estonia ilisema: “Kati ya ndugu 10 waliopewa migawo katika Nchi za Baltiki mwishoni mwa miaka ya 1920 na mwanzoni mwa miaka ya 1930, ni wewe tu ungali hai.” Barua hiyo iliendelea kusema kwamba ofisi ya tawi ilikuwa ikitayarisha historia kuhusu kazi ya kuhubiri nchini Estonia, Latvia, na Lithuania, kisha ikauliza hivi: “Je, unaweza kuja?”

Lilikuwa pendeleo kubwa kama nini kusimulia mambo ambayo mimi na wenzangu tulijionea katika miaka hiyo ya zamani! Huko Latvia niliwaonyesha ndugu nyumba ya kwanza ambayo ilitumiwa kama ofisi ya tawi na sehemu ambayo tulificha vichapo katika paa, na havikupatikana kamwe na polisi. Huko Lithuania nilipelekwa kwenye mji mdogo unaoitwa Šiauliai, ambako nilitumika nikiwa painia. Tukiwa huko katika mkutano fulani, ndugu mmoja aliniambia hivi: “Miaka mingi iliyopita mimi na mama yangu tulinunua nyumba mjini. Tulipokuwa tukiondoa takataka kwenye dari, nilipata vitabu The Divine Plan of the Ages na The Harp of God (Le Divin Plan des Âges na La Harpe de Dieu katika Kifaransa). Nilipovisoma nilitambua kwamba nilikuwa nimepata kweli. Lazima iwe ni wewe uliyeviacha vitabu hivyo katika nyumba hiyo miaka mingi iliyopita!”

Pia nilihudhuria kusanyiko la mzunguko katika mji ambako nilitumikia nikiwa painia zamani. Nilikuwa nimehudhuria kusanyiko huko miaka 65 iliyopita. Wakati huo, watu 35 tu ndio waliohudhuria. Lakini sasa tulifurahi sana kuona hudhurio la watu 1,500! Kwa kweli, Yehova amebariki sana kazi ya kuhubiri!

‘Yehova Hakuniacha’

Hivi karibuni nilipokea baraka ambayo sikutarajia kamwe. Dada mmoja Mkristo anayeitwa Bee alikubali kuwa mke wangu. Tulifunga ndoa mnamo Novemba 2006.

Ninaweza kumhakikishia kijana yeyote ambaye hajui jinsi atakavyotumia maisha yake kwamba ni jambo la hekima sana kutii maneno haya yaliyoongozwa na roho takatifu: ‘Mkumbuke Muumba wako Mkuu katika siku za ujana wako.’ Sasa ninaweza kushangilia kama mtunga-zaburi wa Biblia aliyesema: “Mungu, umenifundisha tangu ujana wangu, na mpaka sasa ninaendelea kutangaza kazi zako za ajabu. Na mpaka wakati wa uzee na wa kuwa na kichwa chenye mvi, Ee Mungu, usiniache, mpaka nikitangazie kizazi habari za mkono wako, habari za nguvu zako, kwa wale wote watakaokuja.”—Zab. 71:17, 18.

[Ramani katika ukurasa wa 25]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Mgawo hatari tuliopewa ulikuwa kupeleka vichapo vya Biblia nchini Latvia

ESTONIA

TALLINN

Ghuba ya Riga

LATVIA

RIGA

LITHUANIA

VILNIUS

Kaunas

[Picha katika ukurasa wa 26]

Nilianza kutumika nikiwa kolpota (painia) nikiwa na umri wa miaka 15 huko Scotland

[Picha katika ukurasa wa 26]

Nikiwa na Nellie siku yetu ya arusi, 1942