Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mbegu za Ufalme Zafika Katika Maeneo ya Mbali Zaidi

Mbegu za Ufalme Zafika Katika Maeneo ya Mbali Zaidi

Mbegu za Ufalme Zafika Katika Maeneo ya Mbali Zaidi

JAMHURI ya Tuva, huko Urusi, iko kwenye ncha ya mbali zaidi kusini mwa Siberia na inapakana na Mongolia upande wa kusini na mashariki. Watu wengi huko Tuva wanaishi katika sehemu za mashambani ambazo ni vigumu kufikia na ujumbe wa Ufalme. Hata hivyo, muda fulani uliopita, kikundi cha watu kutoka maeneo mbalimbali ya Tuva walienda kwenye mji mkuu wa Kyzyl ili kuhudhuria mkutano fulani. Maria, painia anayeishi huko Kyzyl alipopata habari kwamba wamefika, alitambua kwamba hiyo ilikuwa nafasi ya pekee ya kuwahubiria watu ambao hawajawahi kusikia habari njema.

Maria anasimulia kilichotukia: “Shule ambako ninafanya kazi nikiwa mwalimu ilipanga mkutano wa kuzungumzia jinsi ya kuwatibu wale wanaotumia dawa za kulevya. Karibu watu 50 kutoka maeneo ya mbali zaidi ya Tuva walitarajiwa kuhudhuria. Kikundi hicho kilitia ndani walimu, wanasaikolojia, maofisa wanaoshughulikia mambo ya watoto, na watu wengine.” Mkutano huo ulimpa Maria nafasi nzuri ya kuhubiri, lakini haikuwa rahisi kufanya hivyo. Anaeleza hivi: “Mimi ni mtu mwenye haya, na ni vigumu kwangu kuhubiri isivyo rasmi. Hata hivyo, nilimwomba Yehova anipe ujasiri wa kushinda woga wangu ili niweze kutumia nafasi hiyo kutoa ushahidi.” Je, alifaulu?

Maria anaendelea kusema hivi: “Nilipata gazeti la Amkeni! lililozungumza kuhusu woga. Nilijiambia kwamba ‘huenda habari hii itamvutia mwanasaikolojia,’ hivyo nikabeba gazeti hilo na kwenda nalo shuleni. Siku hiyo, mmoja kati ya walimu waliokuwa wamehudhuria mkutano huo alikuja katika ofisi yangu nikampa gazeti hilo. Alilikubali kwa shangwe. Kwa kweli, aliniambia kwamba yeye mwenyewe alikuwa mwenye woga. Siku iliyofuata nilimletea kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 1. Vilevile, alikikubali kitabu hicho kwa shangwe. Kwa kuwa alikubali kuchukua kitabu hicho, nilifikiria kwamba huenda walimu wengine wangependezwa pia na kitabu hicho. Kwa hiyo, nilienda shuleni na katoni lililokuwa limejaa vitabu Vijana Huuliza na vichapo vingine.” Muda si muda, katoni hilo lilikuwa tupu. Maria anaeleza jambo lililotukia: “Baadhi ya marafiki wa walimu ambao nilikuwa nimewapa kitabu Vijana Huuliza walikuja katika ofisi yangu na kuniuliza: ‘Ni nani ambaye anawapa watu vitabu hivyo?’” Walikuja mahali panapofaa!

Jumamosi ndiyo iliyokuwa siku ya mwisho ya mkutano huo. Ilikuwa siku ya Maria ya kupumzika, kwa hiyo aliweka vichapo kwenye meza mbalimbali katika ofisi yake. Aliandika maneno haya kwenye ubao: “Walimu wapendwa! Mnaweza kuchukua vichapo kwa ajili yenu na marafiki wenu pia. Vichapo hivi bora vitawasaidia kufanikiwa kazini na vitasaidia familia zenu kuwa imara.” Waliitikia jinsi gani? “Nilienda katika ofisi yangu siku hiyo na nikaona kwamba vichapo vingi vilikuwa vimechukuliwa. Mara moja nilileta vitabu na magazeti zaidi.” Kufikia mwisho wa mkutano huo, Maria alikuwa amegawa magazeti 380, vitabu 173, na broshua 34. Wale waliohudhuria mkutano huo waliporudi katika maeneo yao ya mbali ambako waliishi na kufanya kazi, walienda na vichapo hivyo. Maria anasema hivi: “Ninafurahi sana kwa kuwa sasa mbegu za ufalme zimefika katika maeneo ya mbali zaidi ya Tuva!”—Mhu. 11:6.

[Ramani katika ukurasa wa 32]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

URUSI

JAMHURI YA TUVA