Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Pokea kwa Shukrani Toa kwa Moyo Wote

Pokea kwa Shukrani Toa kwa Moyo Wote

Pokea kwa Shukrani Toa kwa Moyo Wote

YEHOVA, Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo anamjali kila mmoja wetu. Neno la Mungu linatuhakikishia kwamba anawajali sana watumishi wake wote. (1 Pet. 5:7) Njia moja ambayo Yehova anaonyesha kwamba anatujali ni kwa kutusaidia katika njia mbalimbali ili tumtumikie kwa uaminifu. (Isa. 48:17) Yehova anataka tutumie msaada ambao anatutolea hasa tunapokabili matatizo yanayosababisha mfadhaiko. Sheria ya Musa inaonyesha ukweli wa jambo hilo.

Chini ya mpango wa Sheria, Yehova alimsaidia kwa upendo mtu “mwenye kuteseka” kama vile yatima, mjane, na mkaaji mgeni. (Law. 19:9, 10; Kum. 14:29) Anajua kwamba huenda wengine kati ya watumishi wake wakahitaji kusaidiwa na waabudu wenzao. (Yak. 1:27) Hivyo, hakuna mtumishi hata mmoja wa Yehova ambaye anapaswa kusitasita kukubali msaada unaotolewa na wale wanaochochewa na Yehova kumsaidia. Hata hivyo, tunapokubali msaada, tungependa kufanya hivyo tukiwa na maoni mazuri.

Vilevile, Neno la Mungu linasema kwamba watu wa Mungu pia wana nafasi ya kutoa. Hebu kumbuka simulizi la ‘mjane fulani mwenye uhitaji’ ambaye Yesu alimwona katika hekalu huko Yerusalemu. (Luka 21:1-4) Inaelekea kwamba mjane huyo alifaidika kutokana na mipango yenye upendo ambayo Yehova alikuwa amefanya kwa ajili ya wajane kama Sheria ilivyosema. Ingawa alikuwa mwenye uhitaji, mjane huyo anakumbukwa kwa sababu alitoa, bali si kwa sababu alipokea. Bila shaka, mjane huyo alipata furaha kwa sababu ya mtazamo wake wa kutoa, kwa kuwa kama Yesu alivyosema, “kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.” (Mdo. 20:35) Ukitilia maanani ukweli huo, unaweza jinsi gani ‘kuwa na mazoea ya kuwapa watu’ na kupata furaha kwa kufanya hivyo?—Luka 6:38.

“Nitamlipa Yehova Nini?”

Mtunga-zaburi alijiuliza hivi: “Nitamlipa Yehova nini kwa ajili ya faida zake zote kwangu?” (Zab. 116:12) Alikuwa amepata faida gani? Yehova alimtegemeza alipokabiliana na “taabu na huzuni.” Zaidi ya hayo, Yehova alikuwa ‘ameiokoa nafsi yake kutokana na kifo.’ Hivyo basi, alitaka ‘kumlipa’ Yehova kwa njia fulani. Mtunga-zaburi angefanya nini? Alisema hivi: “Nadhiri zangu nitamtimizia Yehova.” (Zab. 116:3, 4, 8, 10-14) Aliazimia kutimiza nadhiri zote ambazo alikuwa ameweka kwa Yehova na pia kutimiza wajibu wake wote kumwelekea Yehova.

Wewe pia unaweza kufanya hivyo. Jinsi gani? Kwa kuishi kulingana na sheria na kanuni za Mungu nyakati zote. Basi, hakikisha kwamba jambo la maana zaidi maishani mwako ni kumwabudu Yehova na uruhusu roho ya Mungu ikuongoze katika kila jambo unalofanya. (Mhu. 12:13; Gal. 5:16-18) Bila shaka, ukweli ni kwamba huwezi kamwe kumlipa Yehova kikamili kwa ajili ya yote ambayo amekutendea. Hata hivyo, ‘moyo wa Yehova unashangilia’ anapoona kwamba unamtumikia kwa moyo wote. (Met. 27:11) Ni pendeleo la pekee sana kumfanya Yehova ashangilie tunapomtumikia kwa moyo wote.

Changia Hali Njema ya Kutaniko

Bila shaka, utakubali kwamba umefaidika katika njia nyingi kwa sababu ya kushirikiana na kutaniko la Kikristo. Yehova ameandaa chakula kingi cha kiroho kupitia kutaniko. Ulipata kweli ambayo ilikuweka huru kutokana na uwongo wa kidini na giza la kiroho. (Yoh. 8:32) Katika mikutano ya Kikristo na makusanyiko yaliyotayarishwa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ulipata ujuzi ambao utakusaidia kupata uzima wa milele katika dunia paradiso ambayo haitakuwa na uchungu wala maumivu. (Mt. 24:45-47) Je, kweli unaweza kuhesabu faida zote ambazo umepata, na zile ambazo utapata kupitia kutaniko la Mungu? Unaweza kulishukuru kutaniko jinsi gani?

Mtume Paulo aliandika hivi: “Mwili wote, kwa kuunganishwa pamoja kwa upatano na kufanywa ushirikiane kupitia kila kiungo ambacho hutoa kile kinachohitajiwa, kulingana na utendaji wa kila kiungo kimoja-kimoja katika kipimo kinachofaa, hutokeza ukuzi wa mwili ili huo ujijenge wenyewe katika upendo.” (Efe. 4:15, 16) Ingawa andiko hilo linahusu hasa jamii ya Wakristo watiwa-mafuta, kanuni hiyo inaweza kutumiwa na Wakristo wote leo. Ndiyo, kila mshiriki wa kutaniko anaweza kuchangia hali njema na ukuzi wa kutaniko. Tunaweza kufanya hivyo katika njia gani?

Tunaweza kufanya hivyo kwa kujitahidi kabisa nyakati zote kuwatia moyo na kuwaburudisha wengine kiroho. (Rom. 14:19) Pia, tunaweza kuchangia katika “ukuzi wa mwili” kwa kusitawisha matunda ya roho ya Mungu katika shughuli zetu zote pamoja na waamini wenzetu. (Gal. 5:22, 23) Kwa kuongezea, tunaweza kutafuta nafasi za ‘kuwatendea wote mema, na hasa wale ambao katika imani ni jamaa zetu.’ (Gal. 6:10; Ebr. 13:16) Kila mtu kutanikoni, yaani, ndugu na dada, wachanga na wale ambao ni wazee kwa umri, wanaweza kushiriki katika ‘kuujenga mwili katika upendo.’

Zaidi ya hayo, tunaweza kutumia vipawa, nguvu na mali zetu katika kazi ya kuokoa uhai inayofanywa na kutaniko. Yesu Kristo alisema, “Mlipokea bure.” Nasi tunapaswa kutenda jinsi gani? “Toeni bure,” akasema. (Mt. 10:8) Kwa hiyo, shiriki kikamili katika kazi ya maana sana ya kuhubiri kuhusu Ufalme na kufanya wanafunzi. (Mt. 24:14; 28:19, 20) Je, kuna hali fulani zinazokuzuia usitimize mengi? Mkumbuke yule mjane mwenye uhitaji aliyetajwa na Yesu. Alitoa mchango mdogo sana. Hata hivyo, Yesu alisema kwamba alitoa zaidi ya wengine wote. Alitoa yote kulingana na hali zake.—2 Kor. 8:1-5, 12.

Uwe na Mtazamo Mzuri Unapokubali Msaada

Hata hivyo, huenda nyakati nyingine ukahitaji msaada wa kutaniko. Unapopambana na mikazo inayosababishwa na mfumo huu, usisite kamwe kukubali msaada wowote ambao kutaniko linaweza kukupa. Yehova ameandaa wanaume wanaojali na wanaostahili ili ‘walichunge kutaniko,’ yaani, wakusaidie unapokabili majaribu na mateso. (Mdo. 20:28) Wazee na wengine katika kutaniko wanataka kukufariji, kukutegemeza, na kukulinda nyakati za magumu.—Gal. 6:2; 1 The. 5:14.

Lakini, hakikisha kwamba unapopewa msaada ambao unahitaji, unaupokea ukiwa na mtazamo unaofaa. Sikuzote pokea kwa shukrani msaada unaopewa. Ona msaada huo kutoka kwa waamini wenzako kuwa wonyesho wa fadhili zisizostahiliwa za Mungu. (1 Pet. 4:10) Kwa nini ni jambo la maana kufanya hivyo? Kwa sababu tunataka kuwa tofauti na watu wa ulimwengu ambao wanapokea bila kuonyesha shukrani hata kidogo.

Uwe na Usawaziko

Katika barua yake kwa kutaniko la Filipi, Paulo aliandika hivi kumhusu Timotheo: “Sina mtu mwingine yeyote aliye na mwelekeo kama wake atakayejali kwa unyoofu mambo yenu.” Hata hivyo, Paulo aliongezea hivi: “Wengine wote wanatafuta faida zao wenyewe, wala si zile za Kristo Yesu.” (Flp. 2:20, 21) Tunapofikiria maneno hayo mazito ya Paulo, tunaweza jinsi gani kuepuka kuhangaikia sana ‘faida zetu wenyewe’?

Hatupaswi kamwe kuwashurutisha wengine katika kutaniko watumie wakati wao ili kutusaidia au kutuhangaikia sana tunapokuwa na matatizo. Kwa nini tusifanye hivyo? Fikiria jambo hili: Bila shaka, tungethamini sana ikiwa ndugu angetusaidia kimwili tunapokabiliana na hali ya dharura. Lakini je, tunaweza kumshurutisha atusaidie? Bila shaka hapana. Vivyo hivyo, ingawa sikuzote ndugu zetu wenye upendo wanafurahi kutusaidia, tunahitaji kuwa na usawaziko kuhusu msaada tunaotarajia watupe ikitegemea muda wanaoweza kupata. Kwa kweli, tunapokabiliana na hali ngumu, tunataka waamini wenzetu watusaidie kwa njia yoyote ile kwa kupenda.

Bila shaka, sikuzote ndugu na dada zako Wakristo watakuwa tayari kukusaidia kutoka moyoni unapohitaji msaada. Hata hivyo, huenda nyakati nyingine wakashindwa kukupa msaada wote ambao unahitaji. Jambo kama hilo linapotokea, uwe na hakika kwamba Yehova atakutegemeza unapokabili majaribu yoyote yale, kama alivyomtegemeza mtunga-zaburi.—Zab. 116:1, 2; Flp. 4:10-13.

Hivyo basi, usisitesite kukubali kwa shukrani msaada wowote ambao Yehova anakupa, hasa unapokabiliana na mfadhaiko na matatizo. (Zab. 55:22) Anataka ukubali msaada wake. Hata hivyo, anataka pia uwe “mtoaji uchangamfu.” Kwa hiyo, ‘azimia kabisa moyoni mwako’ kutoa kulingana na hali zako katika kuitegemeza ibada ya kweli. (2 Kor. 9:6, 7) Kwa kufanya hivyo, utafanikiwa kupokea msaada kwa shukrani, na wakati huohuo utatoa kwa moyo wote.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 31]

“Nitamlipa Yehova nini kwa ajili ya faida zake zote kwangu?”—Zab. 116:12

▪ Tafuta nafasi za ‘kuwatendea wote mema’

▪ Watie moyo na kuwaburudisha wengine kiroho

▪ Shiriki kikamili katika kazi ya kufanya wanafunzi kadiri hali zako zinavyokuruhusu