Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kupata Hazina Ambazo “Zimefichwa Kwa Uangalifu Ndani Yake”

Kupata Hazina Ambazo “Zimefichwa Kwa Uangalifu Ndani Yake”

Kupata Hazina Ambazo “Zimefichwa Kwa Uangalifu Ndani Yake”

“Hazina zote za hekima na za ujuzi zimefichwa kwa uangalifu ndani yake.”—KOL. 2:3.

1, 2. (a) Ni vitu gani vya kale vilivyopatikana katika mwaka wa 1922, na vitu hivyo viko wapi sasa? (b) Neno la Mungu linamwalika kila mtu afanye nini?

MARA nyingi habari kuhusu kupatikana kwa hazina zilizofichwa zinakaziwa sana na vyombo vya habari. Kwa mfano, katika mwaka wa 1922, baada ya kufanya kazi ya jasho katika mazingira magumu sana, mtaalamu Mwingereza wa vitu vya kale, Howard Carter, alifanya uvumbuzi wenye kuvutia sana. Alipata kaburi la kifalme la Farao Tutankhamen likiwa katika hali nzuri, na ndani yake mlikuwa na vitu 5,000 hivi.

2 Ingawa uvumbuzi wa Carter ulikuwa wenye kuvutia sana, vitu vingi alivyopata vimewekwa sasa katika majumba ya makumbusho au ya kibinafsi. Huenda vikawa na thamani fulani ya kihistoria au ya kisanii, lakini vina thamani ndogo au havina thamani yoyote katika maisha yetu ya kila siku. Hata hivyo, Neno la Mungu linatualika tutafute hazina ambazo kwa kweli zina thamani kubwa katika maisha yetu. Kila mtu anaalikwa kufanya hivyo, na thawabu ni kubwa zaidi kuliko thamani ya hazina yoyote ile ya kimwili.—Soma Methali 2:1-6.

3. Hazina ambazo Yehova anawahimiza waabudu wake watafute ni zenye faida katika njia gani?

3 Fikiria thamani ya hazina ambazo Yehova anawahimiza waabudu wake watafute. Kati ya hazina hizo kuna “kumwogopa Yehova,” ambako kunaweza kutulinda katika nyakati hizi zenye msukosuko. (Zab. 19:9) Kupata “kumjua Mungu” kunaweza kutuletea heshima kubwa zaidi ambayo mwanadamu anaweza kupata, yaani, kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Aliye Juu Zaidi. Na tukiwa na hazina za ujuzi, utambuzi, na hekima tunayopewa na Mungu, tutaweza kupambana kwa mafanikio na matatizo na mahangaiko katika maisha yetu ya kila siku. (Met. 9:10, 11) Tunaweza kupata jinsi gani hazina hizo zenye thamani?

Kupata Hazina za Kiroho

4. Tunaweza kupata jinsi gani hazina za kiroho?

4 Tofauti na wataalamu wa vitu vya kale na wachunguzi ambao mara nyingi wanalazimika kutafuta hazina zao kila mahali, sisi tunajua mahali hususa ambapo hazina za kiroho zinaweza kupatikana. Kama ramani ya hazina, Neno la Mungu linatuonyesha mahali hususa ambapo tunaweza kupata hazina ambazo Mungu anaahidi. Akizungumza kumhusu Kristo, mtume Paulo aliandika hivi: “Hazina zote za hekima na za ujuzi zimefichwa kwa uangalifu ndani yake.” (Kol. 2:3) Tunaposoma maneno hayo, huenda tukajiuliza: ‘Kwa nini tunapaswa kuzitafuta hazina hizo? “Zimefichwa” ndani ya Kristo jinsi gani? Na tunazipata namna gani?’ Ili kujibu maswali hayo, acheni tuchunguze kwa uangalifu maneno ya mtume huyo.

5. Kwa nini Paulo aliandika kuhusu hazina za kiroho?

5 Paulo aliwaandikia maneno hayo Wakristo wenzake huko Kolosai. Aliwaambia kwamba alikuwa anapambana kwa ajili yao ili kwamba “mioyo yao ifarijiwe [na] ili waunganishwe pamoja kwa upatano katika upendo.” (Soma Wakolosai 2:1, 2.) Kwa nini alikuwa na hangaiko hilo? Kwa wazi, Paulo alijua kwamba huenda akina ndugu huko walikuwa wameshawishiwa na watu fulani kati yao ambao walikuwa wakifundisha falsafa fulani za Kigiriki au walikuwa wakitetea kufuatwa tena kwa Sheria ya Musa. Aliwaonya ndugu hao kwa uthabiti hivi: “Mjihadhari: labda kuna mtu ambaye atawachukua ninyi kama windo lake kupitia falsafa na udanganyifu mtupu kulingana na pokeo la wanadamu, kulingana na mambo ya msingi ya ulimwengu na si kulingana na Kristo.”—Kol. 2:8.

6. Kwa nini tunapaswa kupendezwa na shauri la Paulo?

6 Leo, tunakabili uvutano huohuo kutoka kwa Shetani na mfumo wake mwovu. Falsafa za kilimwengu, kutia ndani elimu inayokazia ubinadamu badala ya mambo ya kidini, na pia fundisho la mageuzi, zina uvutano juu ya kufikiri kwa watu, maadili, miradi, na mtindo wao wa maisha. Dini ya uwongo inachangia sana maadhimisho ya sikukuu nyingi zinazopendwa na wengi. Maonyesho mengi kwenye televisheni, sinema, muziki, na aina nyingine za burudani zimekusudiwa kuchochea tamaa mbaya za mwili wenye dhambi, na mambo mengi yaliyo kwenye Intaneti ni hatari sana kwa vijana na wazee. Kutazama kwa ukawaida mambo hayo na pia uvutano wa mielekeo mingine ya ulimwengu unaweza kuharibu kwa urahisi hisia na mtazamo wetu kuelekea mwongozo ambao Yehova anatoa, na hivyo kutufanya tusiushike imara uzima ulio wa kweli. (Soma 1 Timotheo 6:17-19.) Kwa wazi, tunahitaji kuelewa maana ya maneno ya Paulo kwa Wakolosai na kuchukua shauri lake kwa uzito ikiwa hatutaki kuanguka katika mitego ya Shetani yenye hila.

7. Paulo alitaja mambo gani mawili ambayo yangewasaidia Wakolosai?

7 Tukichunguza tena maneno ya Paulo kwa Wakolosai, tunaona kwamba baada ya kueleza hangaiko lake, alitaja mambo mawili ambayo yangewasaidia kupata faraja na kuungana katika upendo. Kwanza, alitaja “uhakikisho kamili wa uelewaji wao.” Walihitaji kusadiki kabisa kwamba uelewaji wao wa Maandiko ulikuwa sahihi ili imani yao itegemee msingi ulio hakika. (Ebr. 11:1) Kisha, alitaja “ujuzi sahihi wa siri takatifu ya Mungu.” Badala ya kuwa tu na ujuzi wa msingi wa ile kweli, walihitaji kufanya maendeleo zaidi na kuwa na uelewaji ulio wazi wa mambo mazito ya Mungu. (Ebr. 5:13, 14) Hayo yalikuwa mashauri mazuri kama nini kwa Wakolosai na kwetu sote leo! Hata hivyo, tunaweza kupata jinsi gani uhakikisho huo na ujuzi sahihi? Paulo alijibu swali hilo katika maelezo yake mazito kuhusu Yesu Kristo: “Hazina zote za hekima na za ujuzi zimefichwa kwa uangalifu ndani yake.”

Hazina Ambazo ‘Zimefichwa Ndani’ ya Kristo

8. Eleza maana ya maneno ‘zimefichwa ndani’ ya Kristo.

8 Kusema kwamba hazina zote za hekima na za ujuzi ‘zimefichwa ndani’ ya Kristo hakumaanishi kwamba haziwezi kupatikana. Badala yake, kunamaanisha tu kwamba ili kupata hazina hizo, tunapaswa kufanya jitihada nyingi, na tunapaswa kumkazia fikira Yesu Kristo. Hilo linapatana na yale ambayo Yesu alisema kujihusu mwenyewe: “Mimi ndiye njia na kweli na uzima. Hakuna anayekuja kwa Baba ila kupitia kwangu.” (Yoh. 14:6) Ndiyo, ili kupata ujuzi wa Mungu, tunahitaji kutafuta msaada na mwongozo kutoka kwa Yesu.

9. Yesu amepewa madaraka gani?

9 Zaidi ya kuwa “njia,” Yesu alisema kwamba yeye ni “kweli na uzima.” Hilo linaonyesha kwamba daraka lake linatia ndani mengi zaidi ya kuwa tu njia ya kumkaribia Baba. Yesu pia ana madaraka ambayo ni ya maana sana katika kuelewa kweli ya Biblia na kupata uzima wa milele. Kwa kweli, hazina za kiroho ambazo zimefichwa ndani ya Yesu ni zenye thamani isiyo na kifani, na zinangoja kuvumbuliwa na wanafunzi wa Biblia walio makini. Acheni tuchunguze hazina fulani ambazo zinahusiana moja kwa moja na matarajio yetu ya wakati ujao na uhusiano wetu pamoja na Mungu.

10. Tunaweza kujifunza nini kumhusu Yesu kutokana na Wakolosai 1:19 na 2:9?

10 “Ni katika yeye kwamba ujazo wote wa sifa ya Mungu hukaa kimwili.” (Kol. 1:19; 2:9) Kwa kuwa aliishi na Baba yake wa mbinguni kwa miaka mingi, Yesu anajua vizuri zaidi utu na mapenzi ya Mungu kuliko mtu mwingine yeyote yule. Wakati wa huduma yake duniani, Yesu aliwafundisha wengine mambo ambayo Baba yake alimfundisha na alionyesha kwa matendo sifa ambazo Baba yake alimfundisha. Ndiyo sababu Yesu alisema hivi: “Yule ambaye ameniona mimi amemwona Baba pia.” (Yoh. 14:9) Hekima yote na ujuzi wa Mungu umefichwa au unakaa ndani ya Kristo, na hakuna njia nzuri zaidi ya kujifunza kumhusu Yehova isipokuwa kujifunza kwa makini mambo yote tunayoweza kumhusu Yesu.

11. Kuna uhusiano gani kati ya Yesu na unabii mbalimbali wa Biblia?

11 “Kutoa ushahidi kumhusu Yesu ndilo kusudi la unabii.” (Ufu. 19:10) Maneno hayo yanaonyesha kwamba Yesu anatimiza sehemu ya maana sana katika kutimizwa kwa unabii mwingi wa Biblia. Kuanzia unabii wa kwanza uliotolewa na Yehova katika Mwanzo 3:15, mpaka maono matukufu ya kitabu cha Ufunuo, tunaweza kuelewa kwa usahihi unabii mbalimbali wa Biblia ikiwa tu tutaelewa daraka ambalo Yesu anatimiza kuhusiana na Ufalme wa Kimasihi. Hilo linaonyesha kwa nini unabii mwingi ulio katika Maandiko ya Kiebrania unawatatanisha wale ambao hawamkubali Yesu kuwa Masihi aliyeahidiwa. Hilo linaonyesha pia kwa nini wale ambao hawathamini Maandiko ya Kiebrania ambayo yana unabii mwingi kumhusu Masihi wanamwona Yesu kuwa mtu mashuhuri tu. Ujuzi kumhusu Yesu unawasaidia watu wa Mungu kuelewa maana ya unabii mbalimbali wa Biblia ambao bado haujatimia.—2 Kor. 1:20.

12, 13. (a) Yesu ni “nuru ya ulimwengu” jinsi gani? (b) Kwa kuwa wamewekwa huru kutoka katika giza la kidini, wafuasi wa Kristo wako chini ya wajibu gani?

12 “Mimi ndiye nuru ya ulimwengu.” (Soma Yohana 8:12; 9:5.) Miaka mingi kabla Yesu hajazaliwa duniani, nabii Isaya alitabiri hivi: “Watu waliokuwa wakitembea katika giza wameona nuru kuu. Kwa habari ya wale wanaokaa katika nchi yenye kivuli kizito, nuru imewaangazia.” (Isa. 9:2) Mtume Mathayo alieleza kwamba Yesu alitimiza unabii huo wakati Alipoanza kuhubiri na kusema: “Tubuni, kwa maana ufalme wa mbinguni umekaribia.” (Mt. 4:16, 17) Huduma ya Yesu iliwaletea watu nuru ya kiroho na uhuru kutokana na utumwa wa mafundisho ya dini ya uwongo. Yesu alisema hivi: “Nimekuja nikiwa nuru ulimwenguni, ili kila mtu anayeniamini asipate kukaa katika giza.”—Yoh. 1:3-5; 12:46.

13 Miaka mingi baadaye, mtume Paulo aliwaambia hivi Wakristo wenzake: “Wakati mmoja ninyi mlikuwa giza, bali sasa ninyi ni nuru kuhusiana na Bwana. Endeleeni kutembea kama watoto wa nuru.” (Efe. 5:8) Kwa kuwa wamewekwa huru kutoka katika utumwa wa giza la kidini, Wakristo wako chini ya wajibu wa kutembea kama watoto wa nuru. Hilo linapatana na yale ambayo Yesu aliwaambia wafuasi wake katika Mahubiri ya Mlimani: “Acheni nuru yenu iangaze mbele ya watu, ili wapate kuona matendo yenu mazuri na kumpa utukufu Baba yenu aliye mbinguni.” (Mt. 5:16) Je, unathamini hazina za kiroho ambazo umepata ndani ya Yesu hivi kwamba ungezipendekeza kwa wengine kwa kuwaambia kuzihusu na kwa mwenendo wako mzuri wa Kikristo?

14, 15. (a) Katika nyakati za Biblia, kondoo na wanyama wengine walitumiwa jinsi gani katika ibada ya kweli? (b) Kwa nini Yesu ni hazina isiyolinganishwa katika daraka lake akiwa “Mwana-Kondoo wa Mungu”?

14 Yesu ni “Mwana-Kondoo wa Mungu.” (Yoh. 1:29, 36) Katika Biblia, kondoo alitimiza daraka la maana katika msamaha wa dhambi na kuwawezesha watu kumkaribia Mungu. Kwa mfano, baada ya Abrahamu kuonyesha kwamba alikuwa tayari kumtoa mwana wake Isaka, aliambiwa asimuumize Isaka, na badala ya kumdhabihu Isaka akapewa kondoo-dume. (Mwa. 22:12, 13) Waisraeli walipokombolewa kutoka Misri, kwa mara nyingine tena kondoo alitimiza daraka la maana sana akiwa sehemu ya “pasaka ya Yehova.” (Kut. 12:1-13) Zaidi ya hayo, chini ya Sheria ya Musa kulikuwa na mpango wa kutoa dhabihu mbalimbali za wanyama, kutia ndani kondoo na mbuzi.—Kut. 29:38-42; Law. 5:6, 7.

15 Kwa kweli, hakuna hata moja kati ya dhabihu hizo zilizotolewa na wanadamu ambayo ingeondoa dhambi na kifo milele. (Ebr. 10:1-4) Kwa upande mwingine, Yesu ni “Mwana-Kondoo wa Mungu ambaye huondolea mbali dhambi ya ulimwengu.” Uhakika huo peke yake unamfanya Yesu kuwa hazina ambayo haiwezi kulinganishwa na hazina yoyote ile ya kimwili ambayo imewahi kupatikana. Kwa hiyo, ni vizuri tuchukue wakati wa kujifunza kwa uangalifu habari kuhusu fidia au dhabihu ya ukombozi na kuwa na imani katika mpango huo mzuri ajabu. Tukifanya hivyo, tutakuwa na tumaini la kupata baraka kubwa na thawabu, yaani, utukufu na heshima pamoja na Kristo mbinguni kwa wale wa “kundi dogo” na uzima wa milele katika Paradiso duniani kwa wale wa “kondoo wengine.”—Luka 12:32; Yoh. 6:40, 47; 10:16.

16, 17. Kwa nini ni jambo la maana kwetu kuelewa daraka la Yesu akiwa “Wakili Mkuu na Mkamilishaji wa imani yetu”?

16 Yesu ni “Wakili Mkuu na Mkamilishaji wa imani yetu.” (Soma Waebrania 12:1, 2.) Katika Waebrania sura ya 11, tunapata maelezo mazito ya Paulo kuhusu imani. Maelezo hayo yanatia ndani ufafanuzi wa neno imani na orodha ya wanaume na wanawake ambao ni vielelezo vizuri vya imani kama vile Noa, Abrahamu, Sara, na Rahabu. Akiwa na yote hayo akilini, Paulo aliwahimiza Wakristo wenzake ‘wamtazame kwa makini Wakili Mkuu na Mkamilishaji wa imani yetu, Yesu.’ Kwa nini?

17 Ingawa wanaume na wanawake hao waaminifu ambao wanaorodheshwa katika kitabu cha Waebrania sura ya  11 walikuwa na imani yenye nguvu katika ahadi ya Mungu, hawakujua mambo yote kuhusu jinsi ambavyo Mungu angetimiza ahadi yake kupitia Masihi na Ufalme. Katika njia hiyo, imani yao haikuwa kamili. Kwa kweli, hata wale ambao walitumiwa na Yehova kuandika unabii mwingi kuhusu Masihi hawakuelewa kikamili maana ya mambo waliyoandika. (1 Pet. 1:10-12) Imani inaweza kukamilishwa, au kukamilika kupitia Yesu tu. Ni jambo la maana sana kwetu kuelewa waziwazi na kutambua daraka la Yesu akiwa “Wakili Mkuu na Mkamilishaji wa imani yetu.”

Endelea Kutafuta

18, 19. (a) Taja hazina nyingine za kiroho zilizofichwa ndani ya Kristo. (b) Kwa nini tunapaswa kuendelea kutafuta hazina za kiroho zilizofichwa ndani ya Yesu?

18 Tumechunguza madaraka machache tu yenye thamani ambayo Yesu anatimiza katika kusudi la Mungu kwa ajili ya wokovu wa wanadamu. Bado kuna hazina nyingine za kiroho ambazo zimefichwa ndani ya Kristo. Tukipata hazina hizo tutakuwa wenye furaha na tutafaidika sana. Kwa mfano, mtume Petro alimwita Yesu “Wakili Mkuu wa uzima” na “nyota ya mchana” inayochomoza. (Mdo. 3:15; 5:31; 2 Pet. 1:19) Na Biblia ilitumia neno “Amina” kumhusu Yesu. (Ufu. 3:14) Je, unajua maana na umuhimu wa madaraka hayo ya Yesu? Kama Yesu alivyosema, “endeleeni kutafuta, nanyi mtapata.”—Mt. 7:7.

19 Hakuna mtu yeyote aliye kama Yesu katika historia yote ambaye maisha yake yana maana kubwa sana na yanahusiana sana na hali yetu njema ya milele. Ndani ya Yesu mna hazina za kiroho ambazo mtu yeyote anayezitafuta kwa moyo wote anaweza kuzipata kwa urahisi. Na iwe shangwe na baraka kwako kuzipata hazina ambazo “zimefichwa kwa uangalifu ndani yake.”

Je, Unakumbuka?

• Wakristo wanahimizwa watafute hazina gani?

• Kwa nini bado shauri la Paulo kwa Wakolosai linatufaa leo?

• Taja na ueleze hazina fulani za kiroho ambazo ‘zimefichwa ndani’ ya Kristo.

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 5]

Biblia ni kama ramani ya hazina inayotuelekeza kwenye utajiri ambao ‘umefichwa kwa uangalifu ndani’ ya Kristo