Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Familia za Kikristo—Fuateni Mfano wa Yesu!

Familia za Kikristo—Fuateni Mfano wa Yesu!

Familia za Kikristo—Fuateni Mfano wa Yesu!

‘Kristo aliwaachia ninyi kielelezo ili mfuate hatua zake kwa ukaribu.’—1 PET. 2:21.

1. (a) Mwana wa Mungu alikuwa na daraka gani wakati wa uumbaji? (b) Yesu ana hisia gani kuelekea wanadamu?

MUNGU alipoumba mbingu na dunia, Mwana wake mzaliwa wa kwanza alikuwa kando yake ‘akiwa stadi wa kazi.’ Mwana huyo wa Mungu alishirikiana pia na Baba yake wakati Yehova alipobuni na kuumba aina mbalimbali za wanyama na mimea hapa duniani na wakati Alipotayarisha Paradiso ambayo ingekuwa makao ya wanadamu walioumbwa kwa mfano na sura ya Yehova. Mwana wa Mungu, ambaye baadaye alikuja kujulikana kuwa Yesu, aliwapenda sana wanadamu. “Vitu [alivyopenda] sana vilihusiana na wana wa binadamu.”—Met. 8:27-31; Mwa. 1:26, 27.

2. (a) Yehova amewapa nini wanadamu wasio wakamilifu? (b) Biblia inatoa mwongozo katika sehemu gani moja ya maisha?

2 Baada ya wanadamu wawili wa kwanza kutenda dhambi, ukombozi wa wanadamu wenye dhambi ulikuwa sehemu ya maana ya kusudi la Yehova. Yehova aliandaa fidia au dhabihu ya ukombozi ya Kristo ili kufanikisha ukombozi huo. (Rom. 5:8) Zaidi ya hayo, Yehova aliandaa Neno lake, Biblia, ambalo linawapa wanadamu mwongozo kuhusu jinsi ya kufanikiwa maishani ingawa wamerithi hali ya kutokamilika. (Zab. 119:105) Katika Neno lake, Yehova anatoa mwongozo ili kuwasaidia watu waendelee kuwa na familia zenye nguvu na furaha. Kuhusu ndoa, kitabu cha Mwanzo kinasema kwamba mwanamume anapaswa ‘kushikamana na mke wake na wanapaswa kuwa mwili mmoja.’—Mwa. 2:24.

3. (a) Yesu alifundisha nini kuhusu ndoa? (b) Tutachunguza nini katika habari hii?

3 Wakati wa huduma yake duniani, Yesu alikazia kwamba ndoa ilikusudiwa kudumu. Alifundisha kanuni ambazo ikiwa zingefuatwa, zingewasaidia washiriki wa familia kuepuka mitazamo na mwenendo ambao ulihatarisha ndoa zao au furaha yao ya familia. (Mt. 5:27-37; 7:12) Habari hii itazungumzia jinsi ambavyo mafundisho na mfano ambao Yesu aliweka alipokuwa duniani unavyoweza kuwasaidia waume, wake, wazazi, na watoto kuishi maisha yenye furaha na yenye kuridhisha.

Jinsi Mume Mkristo Anavyomheshimu Mke Wake

4. Kuna ulinganifu gani kati ya daraka la Yesu na lile la waume Wakristo?

4 Mungu alimweka rasmi mume kuwa kichwa cha familia kama vile tu Yesu alivyo Kichwa cha kutaniko. Mtume Paulo alisema hivi: “Mume ni kichwa cha mke wake kama vile Kristo pia alivyo kichwa cha kutaniko, yeye akiwa mwokozi wa mwili huu. Enyi waume, endeleeni kuwapenda wake zenu, kama vile Kristo pia alivyolipenda kutaniko na kujitoa mwenyewe kwa ajili yake.” (Efe. 5:23, 25) Kwa kweli, jinsi Yesu alivyowatendea wafuasi wake ni kielelezo kizuri cha jinsi wanaume Wakristo wanavyopaswa kuwatendea wake zao. Acheni tuchunguze njia fulani zinazoonyesha jinsi Yesu alivyotumia mamlaka aliyopewa na Mungu.

5. Yesu alitumia mamlaka yake juu ya wanafunzi wake jinsi gani?

5 Yesu alikuwa “mwenye tabia-pole na mnyenyekevu moyoni.” (Mt. 11:29) Alikuwa pia mtu wa matendo. Hakushindwa kamwe kutimiza madaraka yake. (Marko 6:34; Yoh. 2:14-17) Aliwashauri kwa fadhili wanafunzi wake, na hata ilipokuwa lazima alifanya hivyo tena na tena. (Mt. 20:21-28; Marko 9:33-37; Luka 22:24-27) Hata hivyo, Yesu hakuwashutumu kwa ukali au kuwafedhehesha, wala hakuwafanya wahisi kuwa wasiopendwa au wasioweza kutimiza mambo aliyokuwa akiwafundisha. Badala yake, aliwasifu na kuwatia moyo wanafunzi wake. (Luka 10:17-21) Haishangazi kwamba Yesu aliheshimiwa na wanafunzi wake kwa sababu aliwatendea kwa upendo na huruma!

6. (a) Mume anaweza kujifunza nini kutokana na jinsi Yesu alivyowatendea wanafunzi wake? (b) Ni himizo gani ambalo Petro anawapa waume?

6 Mfano wa Yesu unawafundisha waume kwamba ukichwa wa Kikristo si cheo cha kutawala kimabavu. Badala yake, ni cheo kinachotimizwa kwa heshima na upendo wa kujidhabihu. Mtume Petro anawahimiza waume waige njia za upendo za Yesu ‘wanapokaa na wake zao vivyo hivyo’ na ‘kuwapa heshima.’ (Soma 1 Petro 3:7.) Hivyo basi, mume anaweza kutumia mamlaka yake jinsi gani na wakati huohuo amtendee mke wake kama mtu anayestahili heshima?

7. Mume anaweza kumheshimu mke wake katika njia gani? Toa mfano.

7 Njia moja ambayo mume anaweza kuonyesha kwamba anamheshimu mke wake ni kufikiria kwa makini maoni na hisia za mke wake kabla ya kufanya maamuzi yanayohusisha familia. Labda wanahitaji kufanya uamuzi wa kuhamia mahali pengine au wa kubadili kazi au kuhusu mambo ya kila siku, kama vile mahali pa kwenda wakati wa likizo au jinsi ya kupunguza gharama za familia katika nyakati hizi zenye matatizo ya kiuchumi. Kwa kuwa maamuzi hayo yatahusisha familia, lingekuwa jambo la busara na fadhili kwa mume kufikiria maoni ya mke wake, na hivyo kufanya maamuzi yenye usawaziko ambayo yanaonyesha kwamba anajali sana. Akifanya hivyo itakuwa rahisi kwa mke wake kumuunga mkono. (Met. 15:22) Waume Wakristo ambao wanawaheshimu wake zao wanajipatia si upendo tu na heshima kutoka kwa wake zao, bali la maana hata zaidi, wanapata kibali cha Yehova.—Efe. 5:28, 29.

Jinsi Mke Anavyoonyesha Kwamba Anamheshimu Sana Mume Wake

8. Kwa nini wake wanapaswa kuepuka mfano wa Hawa?

8 Yesu anawawekea wake Wakristo kielelezo kikamilifu cha kujitiisha chini ya mamlaka. Mtazamo wa mke wa kwanza wa kibinadamu kuelekea mamlaka unatofautiana sana na mtazamo wa Yesu! Hawa alishindwa kuwawekea wake mfano mzuri wa kufuata. Alikuwa na mume aliyewekwa rasmi na Mungu kuwa kichwa chake na ambaye kupitia kwake Yehova alitoa maagizo. Hata hivyo, Hawa hakuheshimu mpango huo. Alikataa kukubali maagizo ambayo Adamu alimpa. (Mwa. 2:16, 17; 3:3; 1 Kor. 11:3) Ni kweli kwamba Hawa alidanganywa, hata hivyo, alipaswa kumuuliza kwanza mume wake ikiwa ilifaa kuiamini ile sauti iliyodai kwamba inaelewa mambo ambayo “Mungu anajua.” Badala yake, kwa kimbelembele alimwongoza mume wake.—Mwa. 3:5, 6; 1 Tim. 2: 14.

9. Yesu anaweka kielelezo gani katika kujitiisha?

9 Tofauti na Hawa, Yesu aliweka kielelezo kikamilifu cha kujitiisha chini ya yule ambaye ni Kichwa chake, yaani, Mungu. Mtazamo wake na maisha yake yanaonyesha kwamba “hakufikiria kufanya unyakuzi, yaani, kwamba yeye awe sawa na Mungu.” Badala yake, “alijiondolea mwenyewe hali yake na kuchukua umbo la mtumwa.” (Flp. 2:5-7) Leo, akiwa Mfalme anayetawala, Yesu ana mtazamo uleule. Anajitiisha kwa unyenyekevu kwa Baba yake katika mambo yote na anaunga mkono ukichwa wa Baba yake.—Mt. 20:23; Yoh. 5:30; 1 Kor. 15:28.

10. Mke anaweza kuunga mkono ukichwa wa mume wake jinsi gani?

10 Mke Mkristo anapaswa kumwiga Yesu kwa kuunga mkono ukichwa wa mume wake. (Soma 1 Petro 2:21; 3:1, 2.) Fikiria hali ifuatayo ambayo inampa mke nafasi ya kufanya hivyo. Mtoto anamwomba mama ruhusa ya kufanya jambo fulani ambalo anahitaji ruhusa ya wazazi wake. Kwa sababu wazazi hawajazungumzia jambo hilo, itakuwa vizuri kwa mama huyo kumuuliza, “Je, umezungumza na baba yako?” Ikiwa mtoto huyo hajafanya hivyo, mama anapaswa kuzungumzia jambo hilo pamoja na mume wake kabla ya kufanya uamuzi wowote. Zaidi ya hilo, bila shaka mke Mkristo anapaswa kuepuka kubishana na mume wake au kupinga maoni yake mbele ya watoto wao. Ikiwa hakubaliani na mume wake kuhusu jambo fulani, atazungumza naye faraghani.—Efe. 6:4.

Mfano Ambao Yesu Anawawekea Wazazi

11. Yesu aliwawekea wazazi mfano gani?

11 Hata ingawa Yesu hakuoa au kuzaa watoto, anawawekea wazazi Wakristo kielelezo bora. Jinsi gani? Aliwafundisha wanafunzi wake kwa upendo na subira kwa maneno na mfano wake. Aliwaonyesha jinsi ya kutimiza kazi aliyowapa. (Luka 8:1) Mtazamo wa Yesu na jinsi alivyowatendea wanafunzi wake kuliwafundisha jinsi ambavyo walipaswa kutendeana.—Soma Yohana 13:14-17.

12, 13. Wazazi wanahitaji kufanya nini ikiwa wanataka kuwalea watoto ambao wanamwogopa Mungu?

12 Watoto wana mwelekeo wa kuwaiga wazazi wao katika mambo mazuri au mabaya. Enyi wazazi, mnapaswa kujiuliza hivi: ‘Tunawafundisha watoto wetu nini kupitia mfano wetu kuhusu muda tunaotumia katika burudani na kutazama televisheni ukilinganishwa na muda tunaotumia kujifunza Biblia na kushiriki katika mahubiri? Ni mambo gani kwa kweli tunayotanguliza katika familia yetu? Je, tunaweka mfano mzuri kwa kuonyesha kwamba ibada ya kweli ndilo jambo la maana sana katika maamuzi na maisha yetu?’ Kwanza, sheria ya Mungu inapaswa kuwa ndani ya mioyo ya wazazi ikiwa wanataka kuwalea watoto ambao wanamwogopa Mungu.—Kum. 6:6.

13 Ikiwa wazazi wanajitahidi kufuata kanuni za Biblia katika shughuli za kila siku, bila shaka watoto wao watatambua hilo. Watoto watachukua kwa uzito maneno na mafundisho ya wazazi wao. Hata hivyo, ikiwa watoto wanaona kwamba wazazi wao hawafuati viwango ambavyo wanawawekea, watoto wanaweza kukata kauli kwamba kwa kweli kanuni za Biblia si za maana au hazina faida. Kwa sababu hiyo, huenda watoto wakashindwa na mikazo ya ulimwengu.

14, 15. Ni mambo gani yenye thamani ambayo wazazi wanapaswa kusitawisha ndani ya watoto wao, na ni njia gani moja ya kufanya hivyo?

14 Wazazi Wakristo wanatambua kwamba kumlea mtoto kunatia ndani mengi zaidi ya kutimiza mahitaji yake ya kimwili. Kwa hiyo, lingekuwa jambo lisilo la hekima hata kidogo kumfundisha mtoto kufuatia miradi ambayo ingetosheleza tu mahitaji yake ya kimwili. (Mhu. 7:12) Yesu aliwafundisha wanafunzi wake kutanguliza na kufuatia mambo ya kiroho katika maisha yao. (Mt. 6:33) Hivyo, kwa kumwiga Yesu, wazazi Wakristo wanapaswa pia kujitahidi kusitawisha ndani ya watoto wao tamaa ya kufuatia miradi ya kiroho.

15 Njia moja ambayo wazazi wanaweza kufanya hivyo ni kutafuta nafasi ili watoto wao waweze kushirikiana na ndugu na dada walio katika utumishi wa wakati wote. Fikiria jinsi vijana wanavyoweza kutiwa moyo wakifahamiana na mapainia au mwangalizi wa mzunguko na mke wake. Wamishonari, Wanabetheli, na wale wanaofanya kazi ya ujenzi wa kimataifa wanapowatembelea wanaweza kuzungumza kwa shauku kuhusu shangwe inayotokana na kumtumikia Yehova. Bila shaka, wageni hao watasimulia mambo yaliyoonwa yenye kupendeza. Huenda mfano wao wa utumishi wa kujidhabihu utawasaidia sana watoto wako kufanya maamuzi ya hekima, kuweka miradi ya kiroho, na kupata elimu itakayowawezesha kujitegemeza katika utumishi wa wakati wote.

Watoto—Ni Nini Kitakachowasaidia Kufuata Mfano wa Yesu?

16. Yesu aliwaheshimu jinsi gani wazazi wake wa kidunia na Baba yake wa mbinguni?

16 Enyi watoto, Yesu anawawekea ninyi mfano bora pia. Yosefu na Maria walikabidhiwa daraka la kumtunza Yesu, naye aliwatii. (Soma Luka 2:51.) Yesu alitambua kwamba ingawa wazazi wake hawakuwa wakamilifu, walikabidhiwa na Mungu daraka la kumtunza. Kwa sababu hiyo, Yesu alipaswa kuwaheshimu. (Kum. 5:16; Mt. 15:4) Akiwa mtu mzima, sikuzote Yesu alifanya mambo yanayompendeza Baba yake wa mbinguni. Hilo lilimaanisha kwamba alipaswa kushinda vishawishi. (Mt. 4:1-10) Ninyi watoto huenda mkashawishiwa nyakati fulani kutowatii wazazi wenu. Basi, ni nini kinachoweza kuwasaidia kufuata mfano wa Yesu?

17, 18. (a) Vijana wanakabili mkazo wa aina gani shuleni? (b) Vijana wanaweza kushinda majaribu wakikumbuka nini?

17 Inaelekea kwamba wengi wa wanafunzi wenzako hawaheshimu viwango vya Biblia. Huenda wakajaribu kukuchochea ushiriki katika mambo mabaya na kukudhihaki unapokataa. Je, wanafunzi wenzako wanakubandika majina kwa sababu unakataa kushirikiana nao katika mambo fulani? Ikiwa ndivyo, unatenda jinsi gani? Unajua kwamba ukiogopa na kufuata umati, utawakatisha tamaa wazazi wako na Yehova pia. Utapatwa na nini ukiwafuata wanafunzi wenzako? Labda umejiwekea miradi fulani, kama vile kuwa painia, au mtumishi wa huduma, kutumikia katika eneo ambalo lina uhitaji mkubwa zaidi wa wahubiri wa Ufalme, au kuwa Mwanabetheli. Je, kushirikiana na wanafunzi wenzako kutakusaidia kufikia miradi yako?

18 Enyi vijana mlio katika kutaniko la Kikristo, je, mmewahi kujikuta katika hali ambazo zinajaribu imani yenu? Mnafanya nini? Fikirieni kielelezo chenu, Yesu. Hakushindwa na vishawishi naye alisimama imara kwa ajili ya mambo ambayo alijua kuwa ni sawa. Kukumbuka hilo kutawasaidia kupata nguvu za kuwaambia waziwazi wanafunzi wenzenu kwamba hamtaki kujiunga nao kufanya jambo ambalo mnajua kuwa ni kosa. Kama Yesu, kazieni akili zenu kwenye matarajio ya kuwa na maisha yenye shangwe ya kumtumikia na kumtii Yehova.—Ebr. 12:2.

Siri ya Kuwa na Maisha ya Familia Yenye Furaha

19. Ni nini kinacholeta furaha ya kweli maishani?

19 Yehova Mungu na Yesu Kristo wanataka wanadamu wawe na maisha bora kabisa. Hata katika hali yetu ya kutokamilika, tunaweza kwa kadiri fulani kuwa wenye furaha. (Isa. 48:17, 18; Mt. 5:3) Yesu alifundisha kweli za kidini ambazo ndizo chanzo cha furaha ya wanadamu, lakini si hayo tu aliyowafundisha wanafunzi wake. Yesu alifundisha pia njia bora zaidi ya maisha. Zaidi ya hayo, aliwawekea mfano mzuri wa jinsi ya kuwa na maisha na mtazamo wenye usawaziko. Sisi sote, hata tuwe na daraka gani katika familia, tunaweza kufaidika kwa kufuata mfano wake. Hivyo basi, waume, wake, wazazi, na watoto, fuateni mfano wa Yesu! Kukubali mafundisho ya Yesu na kuiga mfano wake kwa kweli ndiyo siri ya kuwa na maisha ya familia yenye kuridhisha na yenye furaha.

Ungesema Nini?

• Waume wanapaswa kutumia jinsi gani mamlaka waliyopewa na Mungu?

• Mke anaweza kuiga mfano wa Yesu jinsi gani?

• Wazazi wanaweza kujifunza nini kutokana na jinsi Yesu alivyowatendea wanafunzi wake?

• Vijana wanaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Yesu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 8]

Kabla ya kufanya uamuzi ambao unahusisha familia, mume mwenye upendo atafanya nini?

[Picha katika ukurasa wa 9]

Ni hali gani inayompa mke nafasi ya kuunga mkono ukichwa wa mume wake?

[Picha katika ukurasa wa 10]

Watoto wanaiga mazoea mazuri ya wazazi wao