Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Dini Nzuri Inawachochea Watu Kuwa na Viwango vya Juu vya Maadili

Dini Nzuri Inawachochea Watu Kuwa na Viwango vya Juu vya Maadili

DINI nzuri inatufundisha jinsi tunavyoweza kufikiria mambo mazuri, na pia inatuonyesha jinsi tunavyoweza kuboresha mwenendo wetu. Inatutegemeza tunapojitahidi kufanya yaliyo sawa na inatusaidia kuwa watu bora kabisa. Tunajua jinsi gani kwamba dini nzuri inafanya hivyo?

Ona mambo ambayo mtume Paulo aliwaandikia Wakristo wa karne ya kwanza walioishi huko Korintho, Ugiriki. Jiji hilo la kale lilijulikana sana kwa sababu ya maisha mapotovu ya wakaaji wake. Paulo aliwaonya hivi: “Waasherati hawataurithi ufalme wa Mungu, wala waabudu sanamu, wala wazinzi, wala wafiraji, wala walawiti, wala wevi, wala watamanio, wala walevi, wala watukanaji, wala wanyang’anyi.” Kisha Paulo akaongezea hivi: “Na baadhi yenu mlikuwa watu wa namna hii; lakini mlioshwa, lakini mlitakaswa, lakini mlihesabiwa haki katika jina la Bwana Yesu Kristo, na katika Roho wa Mungu wetu.” (1 Wakorintho 6:9-11, Union Version) Ona kwamba, dini nzuri iliwasaidia watu fulani ambao hapo zamani hawakufuata viwango vyovyote vya mema na mabaya ili wawe watumishi wa Mungu walio safi na waadilifu!

Kinyume na hilo, Biblia inaonya hivi: “Utakuja wakati ambapo watu hawatasikiliza mafundisho ya kweli, ila watafuata tamaa zao wenyewe na kujikusanyia waalimu tele watakaowaambia mambo yale tu ambayo masikio yao yako tayari kusikia.”—2 Timotheo 4:3, Biblia Habari Njema.

Dini ambazo unajua zinatenda jinsi gani kuhusu jambo hilo? Je, zinafuata viwango vya juu vya Biblia vya maadili? Au je, zinapunguza uzito wa mashauri yaliyo wazi ya Neno la Mungu, na kuwaambia watu “mambo yale tu ambayo masikio yao yako tayari kusikia”?

Ili kukusaidia uamue iwapo dini fulani inazaa matunda mazuri, kwa nini usichukue wakati kujibu maswali yafuatayo?

HABARI: Ndoa.

BIBLIA INAFUNDISHA HIVI: “Ndoa iheshimiwe na watu wote, na kitanda kisiwe na uchafu: kwa sababu Mungu atahukumu waasherati na wazini.”—Waebrania 13:4, Zaire Swahili Bible.

SWALI: Je, dini hiyo inawataka washiriki wake wanaoishi pamoja kama mume na mke wafunge ndoa kisheria?

HABARI: Talaka.

BIBLIA INAFUNDISHA HIVI: Yesu alipoulizwa kama kuna sababu yoyote halali ya kumpa talaka mwenzi wa ndoa, alisema: “Yeyote atakayemwacha mke wake isipokuwa kwa sababu ya uzinzi, akaoa mke mwingine, anazini.”—Mathayo 19:9, BHN.

SWALI: Je, dini hiyo inaheshimu mwongozo wa Yesu na kuruhusu talaka na kufunga ndoa tena kwa sababu tu ya uzinzi?

HABARI: Maadili ya kingono.

BIBLIA INAFUNDISHA HIVI: “Ikimbieni zinaa. Kila dhambi aitendayo mwanadamu ni nje ya mwili wake; ila yeye afanyaye zinaa hutenda dhambi juu ya mwili wake mwenyewe.”—1 Wakorintho 6:18, UV.

“Hata wanawake wakabadili matumizi ya asili kwa matumizi yasiyo ya asili; wanaume nao vivyo hivyo waliyaacha matumizi ya mke, ya asili, wakawakiana tamaa, wanaume wakiyatenda yasiyopasa, wakapata nafsini mwao malipo ya upotovu wao yaliyo haki yao.”—Warumi 1:26, 27, UV.

SWALI: Je, dini hiyo inafundisha kwamba upotovu wa maadili katika ngono iwe ni kati ya mwanamume na mwanamke au kati ya wenzi wa jinsia moja ni dhambi?

HABARI: Kutetea kwa ujasiri kwamba washiriki wa dini hiyo wafuate viwango vya Biblia.

BIBLIA INAFUNDISHA HIVI: “Msishirikiane na ndugu Mkristo aliye mzinzi, mchoyo, mwenye kuabudu sanamu, mchongezi, mlevi na mlaghai. Mtu wa namna hiyo, hata kula msile naye.” (1 Wakorintho 5:11, BHN) Watu ambao wanadai kwamba ni Wakristo lakini ni watenda-dhambi wasiotubu, wanapaswa kuchukuliwa hatua gani? “Mwondoe mutu yule mubaya katikati yenu,” linasema Neno la Mungu.—1 Wakorintho 5:13, ZSB.

SWALI: Je, dini hiyo inaondoa kwenye orodha yake jina la mshiriki yeyote ambaye anapuuza viwango vya Biblia na kukataa kutubu?

Ni dini gani ambayo inajulikana kwa kutetea viwango vya juu vya Biblia vya maadili?